Kuonyesha Uthamini Kwa Ajili ya Fidia
1 Tamaa ya kuonyesha uthamini kwa rafiki au mtu wa ukoo ambaye amekufa ni ya kawaida katika tamaduni zote. Tamaa hiyo yaweza kuwa yenye nguvu hasa ikiwa yule mpendwa alikufa akiwa katika shughuli ya kuokoa uhai wa wengine. Wote wanaoshiriki tumaini la uhai wa milele wana sababu kuu zaidi za kuonyesha uthamini kwa ajili ya fidia kwa kuhudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo mnamo Aprili 6.—2 Kor. 5:14; 1 Yoh. 2:2.
2 Thamini Upendo wa Yehova: Inafaa kama nini tuonyeshe uthamini wetu wenye kina kirefu kwa Mfadhili wetu mkuu zaidi, Yehova Mungu, aliyeandaa fidia! (1 Yoh. 4:9, 10) Kina cha upendo wa Yehova kinadhihirishwa katika zawadi isiyo na kifani aliyoandaa ikiwa fidia yetu, si tu mmojawapo mamilioni ya malaika waadilifu, bali Mwana wake mpendwa aliye mzaliwa pekee. (Mit. 8:22, 30) Mwana huyo anayemjua Yehova vizuri zaidi, Yesu Kristo, alitukumbusha: “Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.”—Yn. 3:16.
3 Thamini Upendo wa Yesu Kristo: Vivyo hivyo, inafaa kwamba tuonyeshe uthamini wa kina kwa Yesu Kristo, aliyetoa nafsi yake kuwa fidia kwa ajili ya wengi. (Mt. 20:28) Upendo wake unadhihirishwa katika kujitoa kwake kwa hiari ili kufanya mapenzi ya Yehova kuhusu fidia. Fikiria jinsi alivyoacha hali zenye kupendeleka za ushirikiano na Baba yake na maelfu ya malaika waadilifu ili awe fidia yetu. Wala ugumu wa kuishi miongoni mwa wanadamu wasio wakamilifu na kutiishwa chini yao wala ufahamu kwamba kutoa fidia kulimaanisha kifo chake haukumzuia. Badala yake, ‘alitwaa namna ya mtumwa, akawa ana mfano wa wanadamu, tena, . . . alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti, naam, mauti juu ya mti wa mateso.’—Flp. 2:5-8.
4 Tuonyesheje Uthamini Kwa Ajili ya Fidia?: Uthamini wetu kwa ajili ya fidia lazima uwe zaidi ya kusema tu asante. Tunahitaji kujifunza kuhusu maandalizi ya Mungu kwa ajili ya wokovu kupitia Yesu Kristo. (Yn. 17:3) Kisha ni lazima tujizoeze imani katika fidia. (Mdo. 3:19) Halafu, ni lazima tuchochewe kujitoa kwa Yehova Mungu kwa kujiweka wakfu na kubatizwa. (Mt. 16:24) Huku tukiishi kupatana na wakfu wetu, twapaswa kununua kila fursa ya kuwaambia wengine kuhusu uandalizi wa fidia ulio mzuri ajabu kwa ajili ya wokovu.—Rum. 10:10.
5 Kutimiza matakwa hayo hakupiti uwezo wa yeyote kati yetu. Mika 6:8 hutuhakikishia hivi: “[Yehova, NW] anataka nini kwako, ila kutenda haki, na kupenda rehema, na kwenda kwa unyenyekevu na Mungu wako?” Vivyo hivyo, Daudi alimwambia Yehova: “Vitu vyote vyatoka kwako, na katika vitu vyako mwenyewe tumekutolea.”—1 Nya. 29:14.
6 Ili kuongeza kina cha uthamini wetu kwa ajili ya uandalizi mzuri ajabu wa Yehova, kwa nini msisome na kuzungumzia sura 112 hadi 126 za kitabu Mtu Mkuu Zaidi mkiwa familia kabla ya tarehe ya Ukumbusho? Kwa njia hiyo, sisi sote twaweza kujiandaa wenyewe kiakili ili kuonyesha uthamini kwa ajili ya fidia kwenye mwadhimisho wa Ukumbusho utakaofanywa mnamo Aprili 6, 1993.