Fuliza Kufuatia Utendaji wa Kitheokrasi Wakati wa Desemba
1 Desemba hutoa fursa za kushiriki utendaji mbalimbali. Wengi wetu hupenda kutumia kwa manufaa hali nzuri ya hewa kwa kufanya jambo tofauti na kustarehe. Hata hivyo, twapaswa kulinda dhidi ya kuruhusu kawaida yetu ya kitheokrasi kuvurugwa.—Flp. 3:16.
2 Twatazamia sana mkusanyiko wa wilaya kila mwaka. Je, umefanya mipango kamili ya kuhudhuria, ukipanga usafiri na mahali pa kulala kama ihitajiwavyo? Je, umefikiria juu ya kutia ndani mtu fulani katika kutaniko lenu ambaye huenda akahitaji msaada wa kibinafsi? Wonyesho mzuri kama huo wa fadhili waweza kuleta baraka kwenu nyote.
3 Ikiwa utakuwa na wakati, kama vile likizo ya shule, je, umefikiri juu ya kufikia ushiriki mkubwa zaidi katika huduma? Wengi wameona huu kuwa wakati mzuri kujiandikisha wawe mapainia-wasaidizi. Mara nyingi kufanya hivi kumefungua mlango mkubwa wa mapendeleo zaidi ya utumishi. Familia zaweza kupata shangwe halisi kwa kutumia siku kamili zikiwa pamoja katika huduma. Vyovyote vile, je, unaweza kuongeza wakati ambao umekuwa ukitumia katika utumishi?
4 Vipi juu ya kusaidia kutaniko lililo na uhitaji wa msaada katika kutimiza eneo? Huenda kukawa na wengine katika kutaniko lako ambao wangetaka kujiunga nawe katika kutumikia kwa juma moja au mawili mahali ambapo kuna uhitaji mkubwa zaidi. Watu fulani wanaoishi mijini wameweza kutoa ushahidi katika maeneo ya mashambani hivyo wakifanyiza vikundi kwa ajili ya makutaniko mapya. Wameona shangwe iliyoje!—Mdo. 20:35.
5 Je, unapangia likizo mbali na nyumbani? Ikiwa ndivyo, je, unafanya mipango kuhudhuria mikutano kule utakuwa ukizuru? Vipi juu ya kuhubiri katika utumishi wa shambani pamoja na akina ndugu huko? Kutia ndani jambo hili katika likizo yako kwaweza kukuthawabisha na wengine. (Rum. 1:11, 12) Pia, je, waweza kutoa ushahidi wa vivi hivi unaposafiri? Hakikisha unabeba Biblia yako na ugavi wa fasihi. Tumia sehemu fulani ya wakati wako usio wenye shughuli ili ufikie usomaji na funzo lako la Biblia. Kumbuka kwamba ijapokuwa twahitaji likizo kutoka ufuatiaji wa kimwili, hatutaki kuchukua pumziko la kumtumikia Yehova.
6 Wazee wanapaswa kuwa chonjo kufanya mipango ya utendaji wa kutaniko ikiwa mizuri. Ikiwa wazee au watumishi wa huduma wowote hawatakuwepo, mipango yapaswa kufanywa kwa wengine ili watunze madaraka yao. Kumjulisha mwangalizi-msimamizi mapema kuhusu tarehe ambazo akina ndugu hao hawatakuwepo kutamsaidia aone kwamba marekebisho ya lazima yamefanywa.
7 Naam, Desemba waweza kuwa wakati ulio na shughuli nyingi sana. Lakini vikengeusha-fikira vyaweza kuvuruga kwa urahisi kawaida yako nzuri ya utumishi wa Ufalme. Tumia vizuri fursa zako zote. Azimia mambo yako ya kiroho ya kwanza, na uyashikilie.—Flp. 1:10.