Mengi ya Kufanya Sikuzote
1 Watu wa Yehova ni watu wenye shughuli. Tuna wajibu mwingi kuhusiana na familia yetu, kazi ya kuajiriwa, na shule. Na zaidi ya yote, sikuzote kuna ‘mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.’ (1 Kor. 15:58, NW) Lazima tujitayarishe na kuhudhuria mikutano ya kutaniko ya kila juma. Twatiwa moyo tusiache juma lipite bila ushiriki fulani kwenye huduma ya shambani. Wakati wa kutosha lazima uwekwe kando kwa ukawaida kwa ajili ya funzo la Biblia la kibinafsi na la familia. Wazee na watumishi wa huduma wana migawo mingi ya kutaniko. Wakati mwingine sisi huombwa tuwasaidie wenye uhitaji.
2 Pindi kwa pindi, baadhi yetu huenda tukahisi tumelemewa na yote tupaswayo kufanya. Lakini, watu wenye shughuli zaidi waweza kuwa miongoni mwa wenye furaha zaidi ikiwa usawaziko na busara inayofaa vyadumishwa.—Mhu. 3:12, 13.
3 Mtume Paulo alikuwa mtu aliyekuwa na mengi ya kufanya. Alipokuwa akitunza mahitaji yake mwenyewe ya kibinafsi kwa kufanya kazi ya kimwili akiwa mtengeneza-mahema, alifanya kazi nyingi kuzidi mitume wale wengine. Alifanya kazi bila kuchoka akiwa mweneza-evanjeli, akihubiri peupe na nyumba kwa nyumba, wakati uleule hakupuuza madaraka yake akiwa mchungaji wa kondoo. (Mdo. 20:20, 21, 31, 34, 35) Ijapokuwa ratiba yake hii yenye shughuli, Paulo alitamani sikuzote kufanya mengi katika utumishi wa Yehova.—Linganisha Warumi 1:13-15.
4 Paulo alidumisha usawaziko wake na moyo wenye furaha kwa kumtegemea Yehova ili apate nguvu. Aliona huduma yake kuwa yenye kuthawabisha na kuridhisha. (Flp. 4:13) Alijua kwamba Mungu hangesahau kazi yake. (Ebr. 6:10) Shangwe ya kusaidia wengine wamjue Yehova ilimtia nishati. (1 The. 2:19, 20) Uhakikisho wa kutambua tumaini lake lililotegemea Biblia ulimsukuma aendelee kuwa mwenye bidii ya kazi.—Ebr. 6:11.
5 Twapaswa pia kufikiria uzuri utokanao na kazi zetu. Kuwapo na kushiriki kwetu katika mikutano ya kila juma hujenga na kutia moyo wengine. (Ebr. 10:24, 25) Jitihada zetu zenye bidii za kuwafikia wote na habari njema huchangia maendeleo ya kutaniko kadiri kupendezwa kunapositawishwa na wapya wanapojiunga nasi. (Yn. 15:8) Kuwasaidia wengine walio na uhitaji huchochea roho ya ukaribiano, iliyo ya kifamilia katika kutaniko. (Yak. 1:27) Zaidi ya hilo, kama vile Paulo, hatupaswi kusahau kamwe kwamba kuwa wenye shughuli katika kazi zenye faida kwampendeza Yehova Mungu. Twaliona kuwa pendeleo tukufu kumtumikia. Kwetu sisi hakuna njia nyingine bora zaidi ya maisha!
6 Kuna manufaa iliyoongezeka tukiwa na mengi ya kufanya. Tunapokuwa wenye shughuli nyingi kufuatia kawaida yenye afya ya kiroho, wakati huonekana ukipita haraka sana. Tukitambua kwamba kila siku inayopita hutuleta karibu zaidi na ulimwengu mpya, twakubali kwa furaha maisha yenye kujaa tunayofurahia sasa. Pia twatambua hekima ya kuwa wenye shughuli, kwa kuwa tunakuwa na wakati mchache wa kujiingiza kwenye ufuatiaji wa kilimwengu ulio duni.—Efe. 5:15, 16.
7 Kwa kweli, kuna mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana. Lakini twaweza kubaki tukiwa wenye furaha ikiwa twaendelea kumtegemea Yehova Mungu na Yesu Kristo, wanaofanya utumishi wetu uwe wenye kuburudisha na kuthawabisha.—Mt. 11:28-30; 1 Yoh. 5:3.