Nufaika na Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ya 1996—Sehemu ya 2
1 Muda mfupi baada ya kuanzishwa kwa Shule ya Huduma ya Kitheokrasi mnamo 1943, mojawapo ofisi za tawi za Sosaiti iliripoti: “Mpango huu mzuri sana ulifaulu kwa muda mfupi katika kusaidia ndugu wengi ambao walifikiri hawangekuwa kamwe wasemaji wa hadharani, kuwa wenye matokeo sana jukwaani na wenye matokeo zaidi shambani.” Shule hii yaendelea kuandaa mazoezi bora, ambayo sisi sote twahitaji.
2 Usomaji wa Biblia: Si wale wanaopewa sehemu za kusema peke yao wanaonufaika na shule. Kwa kweli, sisi sote tuna mgawo—usomaji wa Biblia kila juma. Ratiba ya shule huonyesha ni sura zipi za Biblia zinazopaswa kusomwa kila juma. Kuna vikumbusha vingi vya Kimaandiko vinavyokazia umaana wa kusoma Biblia kila siku. (Yos. 1:8; Zab. 1:2; Mdo. 17:11) Usomaji wa Biblia ni muhimu kwa afya ya kiroho; hulisha akili na moyo. Tukisoma Biblia kwa angalau dakika tano kila siku, tutaweza kudumisha ratiba. Mwishoni mwa mwaka, tutakuwa tumesoma sura 150 za Neno la Mungu. Tukiwa na Biblia karibu, twaweza kusoma sehemu yayo kila siku.
3 Hotuba ya Maagizo: Ili kuchochea akina ndugu kwa utumishi wenye uaminifu-mshikamanifu na wenye bidii, msemaji anayetoa hotuba ya maagizo ahitaji kutumia njia nzuri za kufundisha, atoe uelewevu, na kujenga uthamini kwa Yehova, Neno lake, na tengenezo lake. Wazee na watumishi wa huduma wanaweza kutimiza haya kwa kujitayarisha vizuri, wakikazia kichwa cha hotuba yao, wakisema kwa usadikisho, na kuifanya habari iwe ya kuchangamsha. (Ebr. 4:12) Ni jambo la maana msemaji atunze wakati wake uliowekwa. Kitabu “Kila Andiko” kimejaa maandiko ya Biblia nacho hutoa habari nyingi zenye kusisimua za Kimaandiko zinazoweza kutunufaisha kiroho. Kitabu Proclaimers kina historia ya siku ya kisasa ya tengenezo la Yehova lionekanalo na husimulia matukio katika maisha ya watu halisi walioonyesha imani, bidii, ujitoaji, na upendo. Kuna mengi ya kujifunza juu ya urithi wa kitheokrasi na njia ambayo Yehova amebariki watu wake wa nyakati za kisasa.
4 Mambo Makuu ya Biblia: Ndugu wanaopewa mgawo huu wanapaswa kuteua mistari hususa ambayo yaweza kutumiwa katika njia yenye kutumika kwa manufaa ya kutaniko. Kufanya hivi kwahitaji kusoma sura walizopewa mgawo, kuzitafakari, na kufanyia utafiti mistari iliyoteuliwa ili kupata mambo makuu ambayo yatafafanua maana ya maandiko hayo. Nyuma ya Watch Tower Publications Index, kuna “Scripture Index,” (Faharisi ya Maandiko) inayoweza kusaidia katika kutafuta habari juu ya mistari hususa ya Biblia. Ndugu wanaoshughulikia sehemu hii wapaswa kutumia ufahamu na kuepuka kuongeza habari isiyohusika. Hawapaswi kutayarisha habari nyingi zaidi ya ile inayoweza kushughulikiwa kwa dakika sita.
5 Sisi sote twaweza kunufaika na Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Inaweza kutusaidia kuboresha usemaji wetu na uwezo wetu wa kufundisha. Kutumia kwa manufaa kamili uandalizi huu kwa hakika kutatusaidia tufanye ‘kuendelea kwetu kuwe dhahiri kwa watu wote.’—1 Tim. 4:15.