Nufaika na Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ya 1996—Sehemu ya 3
1 Mtume Paulo alitaka ndugu zake wamwombee ili aweze kupata uwezo wa kusema habari njema kwa ujasiri. (Efe. 6:18-20) Twatamani kusitawisha uwezo huohuo. Ili kuufikia, twathamini msaada unaoandaliwa na Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, ambayo wahudhuriaji wanaostahili wanatiwa moyo kujiandikisha.
2 Tukiwa wanafunzi, twapokea shauri la kibinafsi la kutusaidia tufanyie maendeleo usemaji wetu na uwezo wetu wa kufundisha. (Mit. 9:9) Pia twaweza kunufaika kwa kusikiliza shauri wanalopokea wanafunzi wengine, kwa kutumia tunayojifunza sisi wenyewe. Tunapotayarisha mgawo, twapaswa kusoma chanzo cha habari kwa uangalifu ili kuhakikisha kwamba tunaieleza habari hiyo kwa usahihi. Mambo makuu na maandiko tunayotumia yapaswa kufaana na uendelezaji wa kichwa chote. Ikiwa mgawo watia ndani mtu mwingine, wapaswa kufanyiwa mazoezi mapema kabla ya kutolewa kwenye shule. Tunapofanya maendeleo, jitihada yapaswa kufanywa ili kusema bila kutazamia, kwa kutumia habari fupi badala ya hati ya hotuba.
3 Wote walio na mgawo katika shule wapaswa kufika mapema, wampe mwangalizi wa shule kikaratasi cha Shauri la Usemi, na wakae karibu na mbele ya jumba. Akina dada wanapaswa kumjulisha mwangalizi wa shule mapema kuhusu kikao chao na kama wataketi au watasimama katika sehemu yao. Kushirikiana kwa njia hizi huchangia programu nzuri na husaidia wale wanaotunza jukwaa kuweka kila kitu tayari mapema.
4 Kutayarisha Mgawo Na. 2: Kusudi moja la usomaji wa Biblia ni kusaidia mwanafunzi afanyie maendeleo uwezo wake wa kusoma. Hili laweza kufikiwa vizuri jinsi gani? Kusoma habari kwa sauti kwa kurudia-rudia ndiyo njia bora ya kuufikia. Ili kujifunza maana na utamkaji mzuri wa maneno yoyote asiyofahamu, mwanafunzi apaswa kuyaangalia katika kamusi. Kufanya hivi pia kwataka kujua maana ya alama za matamshi yanayotumiwa katika kamusi.
5 New World Translation hutoa msaada katika kutamka maneno maalumu ya Kiingereza yanayopatikana katika Biblia. Hiyo hufanya hivyo kwa kuyaweka katika silabi na kuandaa alama za lafudhi. (Ona “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa,” kurasa 325-326, mafungu 27-28.) Kanuni ni kwamba, silabi inayotangulia lafudhi huwa na mkazo mkubwa. Ikiwa silabi inaishia na irabu, irabu hiyo ni ndefu kwa matamshi yayo. Ikiwa silabi inaishia na konsonanti, irabu iliyo katika silabi hiyo ni fupi. (Linganisha Saʹlu na Salʹlu.) Ili wajitayarishe kwa migawo yao ya usomaji wa Biblia, ndugu wengine husikiliza kaseti za Sosaiti.
6 Wazazi wanaweza kusaidia watoto wao wachanga watayarishe mgawo wa usomaji. Huku kwaweza kutia ndani kusikiliza mtoto ajizoezapo kisha kumpa madokezo yanayosaidia kufanya maendeleo. Wakati uliowekwa huruhusu utangulizi mfupi na umalizio ufaao ambao huonyesha matumizi ya mambo ya msingi. Hivyo mwanafunzi husitawisha uwezo wake wa kusema bila kutazamia.
7 Mtunga-zaburi aliomba kwa sala hivi: “Ee Bwana, uifumbue midomo yangu, na kinywa changu kitazinena sifa zako.” (Zab. 51:15) Ushiriki wetu katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na utusaidie kutimiza tamaa hiyohiyo.