Kutoa Utumishi Mtakatifu Kama Jamaa
“Nawasihi . . . mtoe miili yenu dhabihu iliyo hai, takatifu, yenye kukubalika kwa Mungu, utumishi mtakatifu.”—Rum. 12:1, NW.
1, 2. (a) Ili kutimiza “utumishi mtakatifu” unaokubalika, ni lazima jamaa ya Kikristo itimize matakwa gani? (b) Taja baadhi ya matatizo yanayoweza kuzuia “utumishi mtakatifu” wa jamaa ya Kikristo.
KATIKA kundi la Kikristo jamaa inatambuliwa kuwa ndiyo sehemu ya msingi. Kukiwako upendo, amani na umoja katika jamaa na kutambua umaana wa kufanya “utumishi mtakatifu’’ kwa Yehova, basi jamaa yaweza kulifaa sana kundi la Kikristo. (Rum. 12:1, NW) Jambo la kuona kuwa shindano, ni kujenga na kuendeleza jamaa ya namna hiyo.
2 Kuna mambo mengi yanayozuia jamaa nyingi za Kikristo katika siku zetu zisifaulu. Kwa mfano, mume na mke mara nyingi wanaona ni lazima waajiriwe kazi ili wachume fedha za kutosha kuweza kutegemeza jamaa. Katika hali hiyo, huenda jamaa zikaelekea kutengana. Nyakati nyingine, kwa sababu ya uvutano usiolingana wa hii taratibu ya mambo, huenda jamaa ikavunjwa-vunjwa na tamaa ya kuishi zaidi ya ulivyo uwezo wayo. Mahali pa kutii shauri la Biblia la kuridhika na “chakula na nguo” zao. (1 Tim. 6:8) Roho ya kujitegemea na tamaa ya kila mmoja kufanya anavyotaka, mahali pa kufanya kazi pamoja, vilevile ni mambo yanayotenganisha jamaa mahali pa kuzileta pamoja katika umoja. Hata uvutano uwe nini, kuna mwendo ambao, ukifuatwa, unaweza kusaidia sana sana jamaa ya Kikristo.
3. Ni mwendo gani unaopendekezwa?
3 Mwendo huo umeandikwa katika usemi uliotamkwa katika Mahubiri ya Mlimani. Bwana Yesu alisema: “Basi, endeleeni, kuutafuta kwanza ufalme na haki yake, na mambo hayo mengine yote mtaongezewa.” (Mt. 6:33, NW) Mazungumzo haya yatahusu mwendo huo. Hayatashughulika na sehemu za nyumbani za maisha ya jamaa bali yatashughulika na hatua zinazofaa ambazo jamaa inaweza kufuata katika kutafuta kwanza Ufalme na kuendeleza mambo yale yanayotokeza jamaa ya Kikristo yenye furaha na yenye upendo, ambayo inaweza kutoa “utumishi mtakatifu” kwa Mungu kwa njia inayofaa.
‘KUUTAFUTA KWANZA UFALME’
4. Tunapaswa kufundishwa juu ya namna ya kumpendeza Yehova kwa sababu ya hali gani tuliyorithi? (Yer. 10:23)
4 Ikiwa jambo ndilo la kwanza katika maisha ya mtu, basi linachukua mahali pa kwanza, ndilo namba 1 kwa umaana. Yesu alisema: “Mtu ye yote akitaka kunifuata, na ajikane na kuuchukua mti wake wa mateso siku baada ya siku na kunifuata wakati wote.” (Luka 9:23, NW) Ili kuwa mfuasi wa kweli wa Yesu na kujikana mwenyewe inahitaji mtu ‘atafute kwanza kweli kweli Ufalme.’ Kwa sababu ya maelekeo yetu yasiyokamilika ya akili na moyo tangu kuzaliwa na kuendelea kwa ajili ya dhambi tuliyoirithi, lazima sote tufundishwe juu ya yanayotazamiwa kwetu ili kumpendeza Mungu. (Mwa. 8:21; Rum. 5:12) Lazima tufundishwe ‘kuutafuta kwanza Ufalme,’ kwa sababu, tukiachwa peke yetu, siku zetu tungetafuta tamaa na mambo ya kibinafsi tunayotaka wenyewe. Kwa hiyo Yehova ametoa maagizo tunayoyapata kupitia Neno lake naye anatupa uongozi unaofaa.
5. Katika Kumbukumbu la Torati 6:6-9 programu ya kuzoeza iliyotolewa na Yehova kwa Waisraeli wa kale ilikuwa kubwa kadiri gani?
5 Yehova aliwaamuru watu wake waliochaguliwa, Waisraeli wa kale, wafundishe watoto wao sheria na amri zake. Walipaswa kuyarudia mafundisho hayo nyumbani, walipokuwa mbali na nyumbani, walipokuwa wakipumzika, na walipokuwa wakifanya kazi. (Kum. 6:6-9) Maagizo hayo hayo yanafaa kwa jamaa katika kutoa “utumishi mtakatifu” kwa Mungu. Tunapofundishwa ‘kuutafuta kwanza Ufalme,’ tunajifunza kuchukua madaraka. Mojalapo la madaraka hayo ni kushiriki na wengine.
KUSHIRIKI NA WENGINE
6. (a) Sana-sana hapa tunafikiria kushiriki na wengine kwa namna gani? (b) Daraka la wazazi katika habari hiyo ya kushiriki na wengine ni kubwa namna gani? (c) Mtume Paulo aliandika juu ya kizuizi gani katika 2 Wakorintho 2:14-16, na jambo hilo linaweza kutokeza hali gani katika wengine?
6 Hatutaki kuzungumza sana juu ya maana ya kushiriki na wengine katika njia ya kimwili, ambako, bila shaka, ni kwa lazima pia ili kuwa na furaha ya kweli. (Matendo 20:35) Tunahangaikia kushiriki na wengine katika kuwapa nafasi ya kuwa na tumaini walilo nalo Wakristo katika ufalme wa Mungu. Mojayapo ya sifa njema sana ambayo mzazi anaweza kutia katika mtoto wake ni tamaa ya kushiriki “habari njema” za Ufalme pamoja na wengine. Tangu umri mchanga watoto wanaweza kufundishwa kushiriki kusema na wengine juu ya “habari njema za ufalme.” (Mt. 24:14, NW) Jambo hilo linachukua wakati mwingi kwa upande wa wazazi kwa sababu jinsi ujumbe huo wa Ufalme ulivyo ni kwamba haukubaliwi mara moja au hautamanwi na wengi wa wale tunaowapa. Kwa sababu Shetani, “mungu wa taratibu hii ya mambo,” amepofusha akili za watu zisione “habari njema zenye utukufu juu ya Kristo.” (2 Kor. 4:4, NW) Mtume Paulo alitoa usemi juu ya kutimiza kwetu daraka hilo na matokeo yake. Yeye alisema: “Mungu hututumia kueneza maarifa juu ya Kristo kila mahali kama harufu tamu. Kwa maana sisi ni kama ubani unaonukia vitamu unaotolewa kupitia Kristo kwa Mungu, ambao unaenea kati ya wale wanaookolewa na wale wanaopotea. Kwa wale wanaopotea huo ni uvundo mbaya sana unaoua; bali kwa wale wanaookolewa, huo ni harufu nzuri inayoleta uzima.” (2 Kor. 2:14-16, Today’s English Version) Tatizo ni kwamba wengi wa wanadamu wanauona ujumbe huo wenye maana kuwa jambo lenye kuua, jambo lisilokubalika kwao. Kushiriki kueneza ujumbe huo kwa watu hao kwaweza kuwa kugumu na kwenye kuvunja moyo.
7. Watoto wanahitaji kitia-moyo gani ili waendelee kufuata yale wanayojifunza?
7 Jambo hilo linafanya sehemu ya wazazi Wakristo iwe ya maana sana katika kuzoeza watoto wao wawe washiriki katika huu “utumishi mtakatifu.” Utumishi huo unaeneza “maarifa juu ya Kristo,” ambayo ni sababu ya kuleta furaha kuu kwa wachache, bali yanakataliwa kabisa na wengine. Wazazi wana nafasi na daraka la kuanza kuwazoeza watoto wao tangu uchanga wao katika maisha ili wawe tayari na kushiriki katika huu “utumishi mtakatifu,” kwa kueneza kwa wengine ujumbe juu ya Kristo na Ufalme. Watoto wanahitaji msaada mwingi kuthamini kwamba, ingawa wengi wanauona ujumbe huo mtukufu kutoka kwa Mungu kuwa wenye kuua, watangazaji wachanga wa “habari njema” hawapaswi kupoteza furaha na juhudi yao. Wala hawapaswi kulegea na kuacha kushiriki katika kutoa “utumishi mtakatifu” kwa Yehova.—1 Kor. 9:16, 17.
8. (a) Mfano wa wazazi ni wa maana kadiri gani katika kufanya “utumishi mtakatifu”? (b) Kwa sababu gani ni vizuri wazazi watimize sehemu ya moja kwa moja katika mazoezi hayo?
8 Basi, ni wazi kabisa, kwamba wazazi wana daraka kubwa na lenye kuwahusu sana la kuonyesha katika maisha zao juhudi na kujitoa kwa kushiriki kwa ukawaida katika kazi ya kutangaza Ufalme. Wanapaswa kufanya iwe kawaida yao ya maisha kuwa pamoja na watoto wao katika utumishi wa Ufalme, wala si kuwatuma vijana waende zao wakaangaliwe na wengine nyakati zote. Hakuna mwingine anayeweza kuchukua daraka hilo kwa ajili yao. Kuweka mfano mwema ndiyo njia bora zaidi ya kusisitiza miradi inayofaa na nia katika watoto. Kumbuka shauri la Maandiko: “Mlee mtoto katika njia impasayo, naye hataiacha, hata atakapokuwa mzee.” (Mit. 22:6) Ili kutoa mazoezi yanayofaa, baba au mama, au wote wawili inapowezekana, wanapaswa kuwa pamoja na watoto wao. Wanapaswa kushiriki katika “utumishi mtakatifu” kama jamaa.
9. Taja matokeo mawili yenye faida ya kushiriki katika utumishi mtakatifu wa Ufalme.
9 Kushiriki huko katika “habari njema” na wengine kuna matokeo yenye faida, licha ya kumpa mtu uradhi wa kujua kwamba anafanya yale Yehova ameamuru. Kunawapa watoto miradi inayofaa ya kufikia maishani. Kufuatia miradi ya ubatili kwa vijana wengi hakuwaletei furaha ya kweli na yenye kudumu. Kufuatia mradi unaompendeza Yehova kunaleta utawa pamoja na uradhi ambayo ndiyo miradi inayofaa zaidi. Ingawa ulimwengu kwa ujumla unatafuta uradhi, jamaa zenye kumwogopa Mungu katika kundi la Kikristo zinaweza kuupata, ikiwa tu zitanyosha mkono kuuchukua. Kuna njia nyingi za uradhi unaoweza kupatikana.—Efe. 5:15, 16.
UTUMISHI WA PAINIA
10. Jamaa ya Kikristo inawezaje kutiwa moyo ichukue utumishi wa painia, na kufanya hivyo kutaleta faida gani?
10 Ulimwenguni pote wakati wa mwaka wa utumishi wa 1980 kulikuwako Mashahidi wa Yehova 137,000 walioshiriki katika namna fulani ya huduma ya wakati wote, utumishi wa painia. Watu hao walipata uradhi mwingi katika kushiriki kikamilifu katika kuutangaza Ufalme. Namna hiyo ya “utumishi mtakatifu” iliwaletea baraka nyingi kutoka kwa Yehova. Nyakati nyingine, washiriki wa jamaa wanaweza kupanga mmoja wao aingie katika utumishi wa wakati wote wa painia. Huenda ikahitaji kila mmoja ajinyime kwa kadiri fulani, walakini thawabu zake zinastahilisha. Je! mmepata kufikiria uwezekano wa mmoja wa washiriki wenu wa jamaa kushiriki katika sehemu hiyo ya “utumishi mtakatifu”? Waseja wengi (watu ambao hawajaoa au kuolewa) na watu waliooana wanaoanza utumishi wa painia kwanza wakiwa mapainia wasaidizi, kisha kama mapainia wa kawaida au wa pekee, wanaona wako katika hali ya kuweza kupanua huduma yao katika sehemu nyingine za “utumishi mtakatifu.”
UTUMISHI WA MISIONARI
11. (a) Wengi wameingia katika sehemu gani nyingine ya “utumishi mtakatifu”? (b) Jambo hilo limekuwa na ubora gani katika kutimiza “utumishi mtakatifu”?
11 Kwa miaka zaidi ya 38 Shule ya Biblia ya Gileadi ya Sosaiti imekuwa ikifanya kazi kwa kuzoeza na kutayarisha watu waende kwenye nchi za ugenini ambapo wameweza ‘kuutafuta kwanza Ufalme.’ Baba na mama wengi Wakristo wamekuwa na nia ya kujinyima furaha ya kuwa na watoto wao karibu, na wamewatia moyo wapanue huduma yao na hivyo wasaidie wengine katika nchi za ugenini. Maelfu ya ndugu na dada waseja, pamoja na watu waliooana, wamebarikiwa kwa pendeleo la kuchukua utumishi wa misionari katika nchi za ugenini. Wamebarikiwa sana sana katika namna hiyo ya “utumishi mtakatifu” nao wametumika kama chombo cha kueneza “habari njema” kwa sehemu zilizo mbali za dunia. Mpaka siku hii kuna watu waliohitimu katika madarasa ya kwanza ya Shule ya Gileadi wanaotumikia katika nchi za ugenini, na katika visa vingi wao ndio msingi thabiti wa kazi iliyoanzishwa miongo mingi ya miaka iliyopita. Katika kuutimiza “utumishi mtakatifu” wenu kama jamaa, je! ninyi mko katika hali ya kutia ye yote wa watoto wenu fikira ya kuchukua sehemu hiyo ya utendaji?—Mal. 3:10.
UTUMISHI WA BETHELI
12. Betheli inaweza kutimiza sehemu gani katika “utumishi mtakatifu” wa jamaa fulani?
12 Duniani pote kwenye afisi za tawi za Sosaiti kuna makao ya Betheli yanayoendeshwa ambamo vijana wanaume na wanawake waliojiweka wakf kabisa wanaweza kumtumikia Muumba wao katika siku za ujana wao. (Mhu. 12:1) Namna hiyo ya “utumishi mtakatifu” vilevile inaleta furaha nyingi kwa wale wanaoistahili, kwa kuwa wanaweza kutoa utumishi kwa ajili ya ndugu na dada zao wanaofanya huduma ya kuhubiri na kufundisha. Jamaa nyingi zinabarikiwa na pendeleo la kuwa na watoto au watu wa ukoo wanaotumikia katika makao ya Betheli. Ingawa sehemu hiyo ya utendaji wa wakati wote haimruhusu mtu ashiriki kutoa huduma kwa watu wote kwa kadiri ile ile ambayo kazi ya upainia au ya umisionari inaruhusu bado wale wanaotumikia katika Betheli wanashiriki kuhubiri nyumba kwa nyumba na kueneza ujumbe wa Ufalme. (Matendo 20:20) Zaidi ya hayo, wanatoa utumishi wa lazima unaosaidia huduma ya ulimwenguni pote iendelee kusonga mbele.
WEWE UTAFANYA NINI?
13. Ni nafasi gani inayoendelea kupatikana kwa jamaa za Kikristo?
13 Paulo, katika barua yake aliyoliandikia kundi la Kikristo, aliandika kwamba alikuwa akibaki Efeso kwa muda fulani kwa sababu ‘alikuwa amefunguliwa mlango mkubwa unaoongoza kwenye utendaji.’ (1 Kor. 16:9, NW) Mbele ya watu wa Yehova leo kungali na mlango mkubwa wa utendaji, “utumishi mtakatifu,” ulio wazi. Tunaishi katika siku za utimizo wa mwisho wa unabii mwingi wa Biblia unaohusu “wakati wa mwisho” wakati ambapo habari njema za Ufalme lazima zihubiriwe katika ulimwengu wote kwa ushuhuda. (Dan. 12:4; Mt. 24:14) Jamaa za Kikristo za Mashahidi wa Yehova zitafanya nini? Kuna uharaka, kwa kuwa wakati umewekewa kipimo. Misaada ipo, kwa maana Yehova ametoa Neno lake Biblia na vitabu vinavyotolewa na “mtumwa mwaminifu mwenye akili” kwa faida ya watu wanaomwogopa Mungu. (Mt. 24:45-47) Jamaa zipo, na Yehova ameendelea kuongeza maelfu kati ya wale wanaoshiriki katika kutangaza Ufalme.—Linganisha Isaya 60:22.
14. (a) Ni maulizo gani yanayofaa ambayo jamaa zinaweza kujiuliza? (b) Ni kwa njia gani tunayoweza kufikiriwa kuwa wanaostahili kushiriki katika “utumishi mtakatifu”?
14 Kwa hiyo maulizo ni haya: Ninyi mnafanya nini? Je! mnatumia nafasi mliyo nayo, kama jamaa na kama mtu mmoja mmoja, kutoa “utumishi mtakatifu” kwa Muumba? Je! mnatia wengine moyo wafanye hivyo? Je! jamaa yenu ni mojayapo kati ya zile katika kundi zinazotoa ushuhuda kuwa zina msingi imara, wenye kutaka kuzaa matunda ya Ufalme? Alipokuwa akisema juu ya uvumba unaonukia vitamu na kuenea kati ya wale wanaookolewa na wale wanaopotea, Paulo aliendelea kusema hivi: “Basi, ni nani awezaye kazi hiyo ngumu? Sisi si kama wengine wengi, wanaochukua ujumbe wa Mungu kama kwamba ni bidhaa ya bei ndogo; bali kwa sababu Mungu ametutuma tunasema kwa unyofu katika kuwapo kwake tukiwa watumishi wa Kristo.”—2 Kor. 2:16, 17, TEV.
15, 16. (a) Wengine wanawezaje kuongeza sehemu yao katika kushiriki kuendeleza faida za Ufalme? (b) “Utumishi mtakatifu” ukiongezwa ni baraka gani zinazopatikana?
15 Kwa kuusitawisha upendo, amani na umoja katika jamaa, kwa kuona umaana wa kwanza wa ‘kutafuta kwanza Ufalme,’ kwa kuketi na kuhesabu gharama, jamaa za Kikristo zinaweza kuona kwamba kweli kweli zitaweza kuongeza sehemu yazo katika kusogeza mbele ujumbe wenye maana zaidi kupita mwingine wo wote uliopata kutangazwa katika dunia hii, zile “habari njema” za ufalme wa Mungu uliosimamishwa. Kwa ajili ya jitihada zao za unyofu na umoja baraka ya Yehova itakuwa yao, naye haongezi uchungu wo wote pamoja na baraka anazotoa.—Mit. 10:22.
16 Mbona msiketi pamoja kama jamaa na mfikirie mnayofanya na mnayoweza kufanya? Bila shaka unyofu utalazimisha wengine wetu tukubali kwamba kwa kujitahidi zaidi kidogo tunaweza kupanua sehemu ya jamaa yetu ya kushiriki katika “utumishi mtakatifu” wa Yehova. Kumbukeni kwamba Yehova haombi tufanye mengi kupita kiasi. Upendo wetu kwake, kwa jamaa yetu na kwa wanadamu kwa ujumla unapasa kutusukuma tujichunguze na kuamua tunayoweza kufanya. Kufikiria juu ya sehemu mbalimbali za “utumishi mtakatifu” wako, huduma tukufu yako ukiwa mwanafunzi wa Kristo (2 Kor. 4:7) Mpelekee Yehova jambo hilo katika sala, ukimwomba uongozi na msaada kuhusiana na jitihada unazofanya. Baraka ni nyingi sasa pamoja na uradhi wa kimungu, na wakati ujao kuna ahadi ya uzima ambao ni uzima kweli kweli katika taratibu mpya ya mambo ya Mungu.—Mt. 25:34; 1 Tim. 6:6, l7-19.—Kutoka The Watchtower, October 15 1981.
MAMBO MAKUU YA KUZUNGUMZA MKIWA JAMAA
• Zaidi ya mtu binafsi kutimiza maneno ya Yesu katika Mathayo 6:33, kwa sababu gani jamaa zapasa kuhangaikia kutimiza maneno hayo kwa umoja?
• Unawezaje kushiriki zaidi katika programu ya jamaa ya kufundisha watoto washiriki na wengine ujumbe wa Ufalme?
• Ni marekebisho gani yanayofaa unayoweza kufikiria ambayo kwayo watoto wanaweza kushiriki kikamilifu katika kazi hiyo?
• Ni sehemu gani za pekee za “utumishi mtakatifu” zinazoweza kuwa mradi unaofaa kwako wewe au kwa mshiriki fulani wa jamaa yenu?
• Jamaa yenu inawezaje kufanya kazi pamoja ili angaa mmoja wenu aweze kufikia mradi kama huo?
[Picha katika ukurasa wa 14]
Vijana wanaweza kujifunza masomo ya maana juu ya kushiriki wanapokwenda pamoja na mzazi mmoja ambaye anashiriki na wengine ujumbe wa Kikristo
[Picha katika ukurasa wa 15]
Vijana wengi waliofurahia “utumishi mtakatifu” pamoja na jamaa zao wamepata furaha katika kutumikia wakiwa wahudumu mapainia wa wakati wote
[Picha katika ukurasa wa 17]
Kutumikia katika makao ya Betheli kwaweza kuwa chanzo cha uradhi mwingi sana. Ni sehemu ya lazima ya “utumishi mtakatifu” duniani pote