Je, Umejaribu Kutoa Ushahidi Katika Maeneo Yasiyogawiwa Mtu?
1 Sisi sote hufurahia kuwa wenye matokeo katika kazi yetu. Kwa upande ule mwingine, tunapokosa kuona matokeo mazuri, kazi yaweza kuwa yenye kuchosha na isiyo ya kuridhisha. Kazi yenye umaana inathawabisha kibinafsi, nayo ni baraka. (Linganisha Mhubiri 3:10-13.) Twaweza kutumia kanuni hii katika kazi yetu ya kuhubiri. Twajua kutokana na uzoefu kwamba tunapoenda mlango hadi mlango na kuweza kuzungumza na watu juu ya Biblia, sisi hurudi nyumbani tukiwa tumeburudishwa kiroho. Twahisi kwamba kweli tumetimiza jambo fulani.
2 Hisia kama hiyo ya kutimiza jambo fulani ilifurahiwa na wengi walioshiriki kutoa ushahidi katika maeneo yasiyogawiwa mtu mwaka uliopita. Kwa sababu ya jitihada zao makutaniko mapya yanatokezwa katika maeneo kama vile Ol Donyo Sabuk, na Shianda katika Kenya; Bulembia na Kajjansi katika Uganda; na Kinyori na Magomeni katika Tanzania, kuongezea sehemu nyinginezo katika nchi nyinginezo. Mwaka huu idadi fulani ya mapainia wa pekee wa muda imegawiwa tena maeneo ya mbali. Makutaniko pia, yatapokea migawo ya kuwaomba watangazaji wafikie eneo fulani la “Makedonia” wawezalo kufikia. Twajua kwamba mtafanya jitihada za pamoja kushiriki katika kampeni ya mwaka huu ya “Makedonia.”
3 Ni kweli kwamba maeneo mengine yametawanyika au ni vigumu kufikia na ongezeko la gharama ya usafiri laweza kufanya iwe vigumu kuyafikia. Ni kweli pia kwamba maeneo fulani ni yenye matokeo zaidi ya mengine. (Linganisha Mathayo 13:3-8.) Lakini twataka kumpa kila mtu fursa ya kusikia “habari njema” kwa kupanda mbegu ya Ufalme kadiri tuwezavyo.
4 Ukikumbuka hili bila shaka tayari umefikiria kuweka akiba kiasi fulani cha fedha kwa ajili ya gharama za usafiri za Julai na Agosti. Uwe tayari na ugavi mwingi wa vichapo vyetu hasa katika lugha ya hilo eneo. Ingawa kuna gharama za ziada za kibinafsi, wale ambao wamehubiri eneo kama hilo wakati uliopita wanajua kwamba kazi hiyo ni yenye kuthawabisha sana. Kuna msisimko wa pekee kukuta watu ambao hawajapata kamwe kupokea ushahidi kamili wa kweli hapo mbeleni. Hiyo ndiyo sababu mtume Paulo alilifanya kuwa lengo lake ‘kutangaza habari njema mahali ambapo Kristo hakuwa ametajwa bado.’ (Rum. 15:20, NW) Fanya liwe lengo lako kushiriki kutoa ushahidi katika eneo lisilogawiwa mtu mwaka huu.
5 Kama kawaida Mwangalizi wa Utumishi, pamoja na ndugu aliyegawiwa kuangalia rekodi za eneo, watapangia maeneo haya yasiyohubiriwa kwa ukawaida yashughulikiwe vizuri. Jitayarishe kuandika wanaopendezwa kwa njia ya kipekee. Labda mmoja au zaidi katika kikundi anaweza kuombwa aende huko pindi kwa pindi kutunza wanaopendezwa waliopatikana na watangazaji mbalimbali. Labda baadhi ya mafunzo yanaweza kuongozwa kwa njia ya barua. Tayarisha vizuri, uwe na mradi, tafuta baraka na mwelekezo wa Yehova unaposhiriki katika kazi hii yenye kuthawabisha zaidi.
6 Kuongezea sehemu hizi zisizogawiwa mtu, zilizo mbali, tutajaribu kukazia uangalifu wa pekee kwa sehemu zisizohubiriwa kwa ukawaida za eneo la kutaniko. Iwe tunahubiri katika eneo lisilogawiwa mtu au sehemu zisizohubiriwa kwa ukawaida twahakikishiwa kwamba tunapomtolea Mungu “[“utumishi mtakatifu,” NW] mchana na usiku,” kwa hakika Yehova atabariki jitihada zetu.—Ufu. 7:15.