“Hii Yamaanisha Uhai Udumuo Milele”
1 Maneno ya Yesu yaliyorekodiwa kwenye Yohana 17:3 (NW) yanapaswa kueleweka kwa uzito. Yeye alimaanisha alichosema—kutwaa ujuzi juu ya Mungu na Kristo kwamaanisha uhai! Lakini je, ni kupata kwetu tu ujuzi juu ya Yehova na Yesu kutakakotuthawabisha na uhai wa milele? Sivyo. Waisraeli walijua kwamba Yehova alikuwa Mungu wao, lakini mwendo wa maisha yao haukuonyesha itikadi hiyo. Likiwa tokeo, walipoteza upendeleo wake. (Hos. 4:1, 2, 6) Leo mamilioni ya watu huenda wakawa “wana juhudi kwa ajili ya Mungu, lakini si katika maarifa [“ujuzi sahihi,” NW].” (Rum. 10:2) Wanahitaji kumjua Yehova, “Mungu wa pekee wa kweli,” na kujifunza jinsi ya kumtumikia kwa njia inayofaa. Kwa kusudi hilo, wakati wa Novemba tutakuwa tukitoa kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele. Utatumia mfikio gani katika kutoa kitabu Ujuzi? Hapa pana madokezo kadhaa yanayoweza kukusaidia.
2 Kwa kuwa wazo la kuishi milele duniani ni jipya kwa watu walio wengi, utangulizi huu waweza kunasa upendezi wao:
◼ “Tunauliza jirani zetu swali. Ikiwa ungealikwa kuishi milele katika ulimwengu kama huu, je, ungekubali mwaliko huo? [Onyesha picha kwenye kurasa 4-5 katika kitabu Ujuzi. Ruhusu itikio.] Hili laweza kuwa ono lako lenye furaha maishani. Lakini unafikiri ungepaswa kufanya nini ili kufanya hilo liwe halisi kwako? [Ruhusu itikio.] Ona ni hatua gani inayohitajiwa kulingana na Yohana 17:3. [Soma.] Kitabu hiki chasaidia wengi wapate aina hiyo ya ujuzi wa pekee. Je, ungependa kuwa na nakala ya kibinafsi ya kusoma? [Ruhusu itikio na utoe kitabu kwa mchango wa kawaida.] Katika ziara yangu itakayofuata, twaweza kuzungumza kwa nini ni jambo lenye kusababu vizuri kuamini kwamba twaweza kupata uhai udumuo milele hapahapa duniani.”
3 Unaporudi kuzuru wale uliozungumza nao kuhusu Yohana 17:3, unaweza kuendelea kwa njia hii:
◼ “Wakati wa ziara yangu ya mwisho, nilikusomea maneno ya Yesu yenye kuchochea yapatikanayo kwenye Yohana 17:3, ambapo alituhakikishia kwamba kutwaa ujuzi juu ya Mungu na juu yake yeye humaanisha uhai udumuo milele. Lakini watu wengi huamini kwamba uhai ulio bora zaidi waweza kupatikana tu mbinguni. Wahisije kuhusu hilo? [Ruhusu itikio.] Ikiwa kile kitabu nilichokuachia kiko karibu, ningependa kukuonyesha mistari kadhaa ya Biblia inayothibitisha kwamba Paradiso itarudishwa duniani. [Zungumzia mafungu 11-16 kwenye kurasa 9-10 katika kitabu Ujuzi.] Katika ziara yangu itakayofuata, ningependa kukuonyesha kwa nini unaweza kuitibari ahadi hizi zinazopatikana katika Biblia. Hadi wakati huo, labda unaweza kusoma sura ya 2 katika nakala yako ya hicho kitabu.”
4 Huu ni utoaji ambao huenda ukataka kutumia kwa watu walio na mwelekeo wa kidini:
◼ “Tumekuwa tukiongea na jirani zetu kuhusu kwa nini kuna dini tofauti nyingi sana ulimwenguni. Karibu dini 1,200 zinapatikana Marekani pekee, na zaidi ya 10,000 ulimwenguni pote. Lakini kuna Biblia moja tu. Kwa maoni yako, kwa nini vurugu hii ya dini ipo? [Ruhusu itikio. Fungua kitabu Ujuzi sura ya 5, na usome fungu la 1.] Utapata majibu yenye kuridhisha ya maswali hayo kwa kusoma sura hii. Nitafurahi kukuachia kitabu hiki ikiwa utajali kukichunguza kwa mchango kidogo wa __________________.” Kikikubaliwa, fanya mipango hususa ya kurudi, na useme: “Nitakaporudi, labda tunaweza kuzungumza kama dini zote ni barabara tofauti tu ziongozazo mahali pamoja.”
5 Unaporudi kuendeleza mazungumzo juu ya kwa nini kuna dini nyingi sana, unaweza kusema hivi:
◼ “Nilipoongea na wewe wakati uliopita, nilitokeza swali kama dini zote ni barabara tofauti tu ziongozazo mahali pamoja. Unafikirije kuhusu hilo? [Ruhusu itikio.] Ningependa kukuonyesha katika kitabu nilichokuachia yale ambayo Yesu alisema kuhusu habari hiyo. [Fungua sura ya 5 katika kitabu Ujuzi, na usome mafungu 6-7, kutia ndani Mathayo 7:21-23.] Huenda ukashangaa ni kwa nini ni muhimu sana kujua mapenzi ya Mungu ni nini hasa. Utaona kwamba mafungu yafuatayo ni yenye kuarifu sana. Tafadhali soma sehemu iliyobaki ya sura hiyo. Wakati ujao nikija, nitafurahi kukuonyesha thamani ya kuwa na ujuzi sahihi wa Biblia.”
6 Mfikio wa moja kwa moja mara nyingi ni wenye mafanikio katika kuanzisha mafunzo ya Biblia. Hapa pana utangulizi uliodokezwa ambao wapatikana kwenye ukurasa wa 12 wa kitabu “Kutoa Sababu”:
◼ “Nazuru ili kukutolea mtaala wa Biblia nyumbani bila malipo. Ukiniruhusu, ningependa kuchukua dakika chache nikuonyeshe jinsi watu katika nchi zipatazo 200 huzungumzia Biblia nyumbani wakiwa vikundi vya familia. Twaweza kutumia yoyote ya masomo haya kwa mazungumzo. [Onyesha yaliyomo katika kitabu Ujuzi.] Ni lipi linalokupendeza hasa?” Ngoja mtu afanye uchaguzi. Fungua sura inayochaguliwa, na uanzishe funzo katika fungu la kwanza.
7 Hapa pana mfikio mwingine wa moja kwa moja wenye mafanikio ambao ungependa kujaribu ili kuanzisha mafunzo:
◼ “Mimi hutoa masomo ya Biblia bila malipo na nina wakati katika ratiba yangu kwa ajili ya wanafunzi zaidi. Huu msaada wa kujifunza Biblia ndio sisi hutumia. [Onyesha kitabu Ujuzi.] Mtaala humalizika kwa miezi michache tu na huandaa majibu kwa maswali kama vile: Kwa nini Mungu ameruhusu kuteseka? Kwa nini tunazeeka na kufa? Ni nini huwapata wapendwa wetu waliokufa? Na twaweza kumkaribiaje Mungu?” Kisha uliza, “Naweza kukuonyesha jinsi ya kufanya funzo?” Toleo la funzo likikataliwa, muulize mtu huyo kama angependa kuwa na kitabu Ujuzi ili akisome mwenyewe kwa mchango wa kawaida.
8 Ujuzi sahihi juu ya Mungu na Kristo ni hazina iliyoje kwa kila mtu aliye nao! Kuutwaa kwa kweli kwamaanisha uhai udumuo milele katika hali kamilifu. Na tutumie kila fursa wakati wa Novemba kushiriki na wengine ujuzi uongozao kwenye uhai udumuo milele.