Jipe Ujasiri wa Kufanya Ziara za Kurudia
1 Je, wewe hufurahia kufanya ziara za kurudia? Watangazaji wengi hufurahia. Huenda ikawa ulikuwa mwenye wasiwasi mara ya kwanza, hasa uliporudi kwa wenye nyumba ambao walipendezwa kidogo walipofikiwa mara ya kwanza. Lakini kadiri ‘ujipatiavyo ujasiri wa kusema habari njema kupitia Mungu wetu’ katika kufanya ziara za kurudia, huenda ukashangazwa kuona jinsi kazi hii iwezavyo kuwa rahisi na yenye kuthawabisha. (1 The. 2:2) Jinsi gani?
2 Kwa kweli, kuna tofauti yenye maana kati ya ziara ya kurudia na ziara ya kwanza. Ziara ya kurudia yafanywa kwa mjuani, si mtu asiyejulikana, na kwa ujumla ni rahisi kuongea na mjuani kuliko mtu asiyejulikana. Kwa habari ya matokeo yenye kuridhisha yatokanayo na kushiriki kazi hii, ziara za kurudia zaweza kuongoza kwenye mafunzo ya Biblia nyumbani yenye matokeo.
3 Tunapohubiri nyumba hadi nyumba, twazuru mara kwa mara watu ambao hawakupendezwa tulipowatembelea wakati uliopita. Basi, kwa nini twaendelea kuzuru? Twatambua kwamba hali za watu hubadilika na kwamba mtu aliyeonekana kuwa mwenye ubaridi au hata mwenye kupinga katika ziara iliyopita huenda akapendezwa wakati mwingine tuzurupo. Tukiwa na hilo akilini, twajitayarisha vizuri na kuomba baraka za Yehova ili jambo tusemalo wakati huu litokeze itikio zuri.
4 Ikiwa, katika mahubiri yetu ya nyumba hadi nyumba, kwa hiari twahubiria watu walioonyesha kupendezwa, je, hatupaswi hata zaidi kurudia yeyote anayeonyesha kupendezwa na ujumbe wa Ufalme?—Mdo. 10:34, 35.
5 Wengi wetu tuko katika kweli leo kwa sababu mtangazaji alitufanyia ziara za kurudia kwa subira. Ikiwa wewe ni mmoja wao, huenda ukajiuliza: ‘Nilitoa wazo gani mara ya kwanza kwa mtangazaji huyo? Je, niliitikia ujumbe wa Ufalme mara moja nilipousikia kwa mara ya kwanza? Inawezekana kwamba nilionekana kuwa mwenye ubaridi?’ Twapaswa kuwa wenye furaha kwamba mtangazaji aliyeturudia alituona kuwa wenye kustahili kurudiwa, ‘akajipa ujasiri kwa njia ya Mungu,’ akafanya ziara hiyo, na kuendelea kutufunza kweli. Vipi wale watu wanaoonyesha kupendezwa mara ya kwanza lakini baadaye wanaonekana kuwa wanatuepuka? Mtazamo chanya ni wa muhimu, kama jambo lililoonwa lifuatalo linavyoonyesha.
6 Walipokuwa wakitoa ushahidi barabarani asubuhi moja, watangazaji wawili walimkuta bibi mchanga akisukuma mtoto katika kigari cha kutembezea mtoto. Mwanamke huyo alikubali magazeti na akawaalika akina dada hao kwenda nyumbani kwake Jumapili iliyofuata. Walifika kwa wakati uliowekwa, lakini mwenye nyumba aliwaambia hakuwa na wakati wa kuongea. Hata hivyo, aliwaahidi kuwapo juma lililofuata. Akina dada walitia shaka kama kweli angetimiza miadi hiyo, lakini yule bibi alikuwa akiwangoja waliporudi. Funzo lilianzishwa, na maendeleo ya mwanamke huyo yalikuwa yenye kustaajabisha. Kwa muda mfupi tu, alianza kuhudhuria mikutano kwa ukawaida na kushiriki katika utumishi wa shambani. Yeye sasa amebatizwa.
7 Weka Msingi Kwenye Ziara ya Kwanza: Msingi wa ziara ya kurudia yenye mafanikio mara nyingi huwekwa kwenye ziara ya kwanza. Sikiliza kwa uangalifu maelezo ya mwenye nyumba. Yanakueleza nini? Yeye ni mwenye mbetuko wa kidini? Anahangaishwa na masuala ya kijamii? Je, anapendezwa na sayansi? historia? mazingira? Mwishoni mwa ziara, unaweza kutokeza swali lenye kuvuta fikira na uahidi kuzungumzia jibu la Biblia unaporudi.
8 Kwa kielelezo, ikiwa mwenye nyumba anaitikia ahadi ya Biblia kuhusu dunia iliyo paradiso, mazungumzo ya ziada ya habari hiyo yanaweza kufaa. Kabla tu ya kuondoka, waweza kuuliza: “Twawezaje kuwa na uhakika kwamba Mungu atatimiza ahadi hii?” Kisha uongezee: “Labda naweza kufika hapa familia nzima ikiwa nyumbani, kisha naweza kukuonyesha jibu la Biblia kwa swali hili.”
9 Ikiwa mwenye nyumba hajaonyesha kupendezwa katika somo lolote hususa, unaweza kutokeza mojawapo ya maswali ambayo yamekaziwa katika utoaji mbalimbali kwenye ukurasa wa nyuma wa Huduma ya Ufalme Yetu na ulitumie kuwa msingi wa mazungumzo yako yafuatayo.
10 Weka Rekodi Sahihi Iliyoandikwa: Rekodi yako ya nyumba hadi nyumba yapaswa kuwa sahihi na kamili. Andika jina na anwani ya mwenye nyumba mara uondokapo katika hiyo nyumba. Usikisie nambari ya nyumba au jina la barabara—angalia habari uhakikishe kwamba ni sahihi. Andika habari yenye kusimulia aina ya mtu huyo. Andika habari mliyozungumzia, maandiko mliyosoma, fasihi yoyote uliyoacha, na swali utakalojibu unaporudi. Tia ndani siku na saa ya ziara ya kwanza na wakati uliosema ungerudi. Sasa kwa kuwa rekodi yako imekamilika, usiipoteze! Iweke mahali salama ili uweze kuirejezea baadaye. Endelea kumfikiria mtu huyo na jinsi utakavyoshughulika na ziara wakati ufuatao.
11 Yajue Malengo Yako: Kwanza kwa kuwa mwenye uchangamfu na mwenye urafiki, fanya uwezavyo ili umfanye mwenye nyumba astarehe. Onyesha kwamba unapendezwa naye akiwa mtu, bila kuwa mwenye udadisi mno. Kisha, mkumbushe swali lolote ulilotokeza kwenye ziara ya kwanza. Sikiliza kwa uangalifu kauli yake, na umwonyeshe uthamini wa moyo mweupe kwa maelezo yake. Kisha, onyesha kwa nini maoni ya Biblia yanafaa. Ikiwezekana, mwelekeze kwenye wazo linalofanana na hilo kwenye kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele. Kumbuka kwamba lengo lako kubwa kwenye ziara za kurudia ni kuanzisha funzo la Biblia.
12 Habari ya moja kwa moja inayotumiwa katika kitabu Ujuzi imechochea wengi ‘kujipatia ujasiri’ kwenye mafunzo ya Biblia ili kutia moyo wanafunzi wahudhurie mikutano na kushiriki na tengenezo la Yehova. Wakati uliopita, tulielekea kungoja hadi watu wajifunze kwa muda fulani kabla ya kuwaalika washirikiane nasi. Sasa, wanafunzi wengi wanahudhuria mikutano upesi waanzapo kujifunza, nao wanafanya maendeleo haraka zaidi.
13 Wenzi waliooana walimtolea ushahidi vivi hivi mfanyakazi mwenzao. Alipopendezwa na kweli, walimwalika awe na funzo la Biblia kwa kutumia kitabu Ujuzi. Kwa wakati uleule, walimwambia alipaswa kuhudhuria mikutano, ambapo maswali yake mengi yangejibiwa. Mtu huyo hakukubali kwa hiari tu mwaliko wa kujifunza bali pia alijifunza mara mbili kwa juma na akaanza kuhudhuria mikutano kwa ukawaida kwenye Jumba la Ufalme.
14 Tumia Broshua Mungu Anataka Tufanye Nini?: Kwenye Mikusanyiko ya Wilaya ya “Wajumbe wa Amani ya Kimungu,” tulipokea broshua Mungu Anataka Tufanye Nini? Broshua hii ni yenye mafaa katika kuanzisha mafunzo ya Biblia na watu wenye kumhofu Mungu bila kujali wana elimu kiasi gani. Ina mtaala wa funzo wenye mapana, ukishughulikia mafundisho ya msingi ya Biblia. Kichapo hicho kitakuwa chombo chenye matokeo zaidi kwa kuwapa ujuzi wa Mungu. Chaeleza kweli waziwazi na kwa usahili hivi kwamba karibu kila mmoja wetu ataweza kukitumia kufundishia wengine matakwa ya Mungu. Yamkini, watangazaji wengi watakuwa na pendeleo la kuongoza funzo la Biblia katika broshua hii.
15 Watu fulani ambao huhisi kwamba hawana wakati wa kujifunza kitabu Ujuzi huenda wakawa tayari kuwa na vipindi vifupi vya kujifunza broshua Anataka. Watasisimuliwa na yale wanayojifunza! Katika kurasa mbili au tatu tu, watapata majibu kwa maswali ambayo watu wametafakari kwa karne nyingi: Mungu ni nani? Ibilisi ni Nani? Ni nini kusudi la Mungu kwa dunia? Ufalme wa Mungu ni nini? Unaweza kupataje dini ya kweli? Ijapokuwa broshua hiyo yatoa kweli kwa maneno sahili, ujumbe wayo ni wenye nguvu sana. Hushughulikia mambo makuu ambayo wazee watapitia na wataka kubatizwa na yaweza kuwa chombo cha kwanza kwa ajili ya funzo lenye kina katika kitabu Ujuzi.
16 Ili kutoa funzo kwenye ziara ya kurudia, unaweza tu kusema hivi: “Je, ulipata kujua kwamba kwa kuchukua tu dakika chake, unaweza kupata jibu la swali lenye maana la Biblia?” Kisha, tokeza swali linalopatikana mwanzoni mwa mojawapo ya masomo yaliyo katika broshua. Kwa kielelezo, ikiwa unamzuru mtu mzee, waweza kusema: “Twajua kwamba zamani Yesu aliponya watu. Lakini wakati ujao, Yesu atafanyia nini wagonjwa? wazee-wazee? wafu?” Majibu yapatikana katika somo la 5. Mtu mwenye maelekeo ya kidini huenda akaamshwa kupendezwa na swali: “Je, Mungu husikiliza sala zote?” Linajibiwa katika somo la 7. Washiriki wa familia watataka kujua: “Mungu hutaka wazazi na watoto wafanye nini?” Watapata majibu wanapojifunza somo la 8. Maswali mengine ni haya: “Je, wafu waweza kuwadhuru walio hai?” linaloelezewa katika somo la 11; “Kwa nini kuna dini nyingi sana zinazodai kuwa za Kikristo?” linalozungumziwa katika somo la 13; na “Ni lazima ufanye nini ili kuwa rafiki ya Mungu?” linaloshughulikiwa katika somo la 16.
17 Fanya Ziara za Kurudia Bila Kukawia: Je, ungoje hata lini ili ufanye ziara ya kurudia? Watangazaji kadhaa hurudi baada ya siku moja au siku mbili baada ya ziara ya kwanza. Wengine hurudi baadaye siku hiyohiyo! Je, hiyo ni haraka sana? Kwa ujumla, wenye nyumba hawapingi. Mara nyingi ni mtangazaji anayerudi ambaye huhitaji kusitawisha mtazamo chanya zaidi, pamoja na ujasiri zaidi. Angalia mambo yaliyoonwa yafuatayo.
18 Mtangazaji mwenye umri wa miaka 13 alikuwa akihubiri nyumba hadi nyumba siku moja alipoona wanawake wawili wakitembea pamoja. Akikumbuka kitia moyo cha kuwahubiria watu popote tuwapatapo, aliwafikia wanawake hao barabarani. Walionyesha kupendezwa na ujumbe wa Ufalme, na kila mmoja wao alikubali kitabu Ujuzi. Ndugu huyo mchanga alichukua anwani yao, akarudi siku mbili baadaye, na kuanzisha funzo la Biblia na kila mmoja wao.
19 Dada mmoja hufanya mipango ya kurudi juma lifuatalo. Lakini siku moja au mbili baada ya ziara ya kwanza, yeye humfikia mwenye nyumba na kumpa gazeti juu ya somo walilozungumzia wakati uliopita. Yeye humwambia mwenye nyumba: “Niliona makala hii na nikafikiria ungependa kuisoma. Siwezi kuongea kwa sasa, lakini nitarudi Jumatano alasiri kama tulivyopanga. Bado wakati huo ni sawa kwako?”
20 Mtu akionyesha kupendezwa na kweli, twaweza kuwa na uhakika kwamba atapata upinzani kwa njia moja au nyingine. Kurudi kwetu upesi baada ya ziara ya kwanza kutamwimarisha kuuweza msongo wowote anaopata kutoka jamaa, marafiki wa karibu, na wengine.
21 Sitawisha Kupendezwa kwa Wale Wanaopatikana Mahali pa Umma: Wengi wetu hufurahia kuhubiri barabarani, kwenye maegesho ya magari, kwenye usafiri wa umma, madukani, kwenye bustani, na kadhalika. Zaidi ya kuangusha fasihi, twahitaji kusitawisha kupendezwa. Tukiwa na lengo hilo, jitihada yapaswa kufanywa kupata jina, anwani na ikiwezekana, namba ya simu ya kila mtu anayependezwa tunayekutana naye. Si vigumu kupata habari hii kama vile huenda ukafikiri. Mazungumzo yakaribiapo kumalizika, chukua kitabu chako cha kuandikia na uulize: “Kuna njia nyingine tunayoweza kuendeleza mazungumzo haya wakati mwingine?” Au sema: “Ningependa usome makala ambayo nina hakika itakupendeza. Je, niilete nyumbani kwako au ofisini?” Ndugu mmoja huuliza tu: “Waweza kufikiwa kwa kutumia namba gani ya simu?” Yeye aripoti kwamba kwa miezi mitatu watu wote walifurahia kumpa namba yao ya simu isipokuwa watatu.
22 Tumia Simu Panapowezekana Upate na Kusitawisha Kupendezwa: Dada mmoja painia hutumia simu kufikia watu wanaoishi katika majengo yenye ulinzi mkali. Pia yeye hufanya ziara za kurudia kwa njia ileile. Kwenye ziara ya kwanza, yeye husema: “Najua kwamba hunijui. Nafanya jitihada ya pekee kufikia watu kwenye eneo lako kushiriki wazo moja kutoka Biblia. Ikiwa una dakika, ningependa kukusomea ahadi ipatikanayo kwenye . . . ” Baada ya kusoma andiko, yeye husema: “Je, haingekuwa vizuri ikiwa tungeweza kuona wakati huo umekuja? Nimefurahia kukusomea hili. Ikiwa umefurahia pia, ningependa kurudi tena, tuzungumzie andiko jingine.”
23 Anapopiga simu ya kurudia, humkumbusha mwenye nyumba mazungumzo yao ya wakati uliopita na kusema angependa kusoma kutoka Biblia hali zitakuwaje uovu utakapoondolewa. Kisha huwa na mazungumzo mafupi ya Biblia pamoja na mwenye nyumba. Katika mazungumzo mengi ya simu, watu 35 wamemwalika nyumbani kwao na mafunzo ya Biblia nyumbani saba yameanzishwa!
24 Fuatia Kupendezwa Kunakoonyeshwa Mahali pa Biashara: Mengi yanahusika katika kuhubiri duka hadi duka kuliko kutoa tu magazeti. Wenye duka wengi wanapendezwa na kweli kwa moyo mweupe, na kupendezwa huko lazima kusitawishwe. Katika visa fulani, huenda ikawezekana kuwa na mazungumzo ya Biblia au hata funzo mahali hapohapo pa biashara. Katika visa vingine, wewe na mwenye kupendezwa huenda mkaweza kukutana wakati wa mapumziko ya mchana au mahali pengine pafaapo.
25 Mwangalizi asafiriye alimzuru mwenye duka dogo la vyakula, akajitolea kumwonyesha funzo la Biblia. Mwangalizi asafiriye alipoulizwa lingechukua muda gani, alimwambia kwamba lingechukua dakika 15 tu. Mwenye duka aliweka ishara mlangoni isemayo: “Nitarudi Baada ya Dakika 20,” akatoa viti viwili nao wakazungumzia mafungu ya kwanza tano ya kitabu Ujuzi. Mtu huyo mwenye moyo mweupe alipendezwa sana na yale aliyojifunza hivi kwamba alihudhuria Mkutano wa Watu Wote na Funzo la Mnara wa Mlinzi Jumapili hiyo na akakubali kuendelea kujifunza juma lililofuata.
26 Ili kutoa funzo mahali pa biashara, waweza kusema hivi: “Programu yetu ya funzo la Biblia huchukua dakika 15 kulifanya. Ikifaa, nitafurahi kukuonyesha jinsi linavyofanywa.” Kisha, tunza wakati. Ikiwa haiwezekani kuwa na mazungumzo marefu mahali pa biashara, huenda ikafaa zaidi kumwendea mwenye duka nyumbani kwake.
27 Rudi Hata Kama Hakuna Fasihi Ambayo Imeangushwa: Kupendezwa kokote kwastahili ziara ya kurudia, iwe fasihi imeangushwa au haijaangushwa. Bila shaka, ikiwa wazi kwamba mwenye nyumba hapendezwi kikweli na ujumbe wa Ufalme, ni vizuri kuelekeza jitihada zako kwingine.
28 Katika mahubiri ya mlango hadi mlango, dada mmoja alimkuta bibi aliyekuwa mwenye urafiki sana lakini akakataa katakata magazeti. Mtangazaji huyo aandika: “Nilimfikiria kwa siku kadhaa na nikaamua nataka kuongea naye tena.” Hatimaye, dada huyo alisali, akajipa moyo mkuu, akagonga mlango wa yule bibi. Kwa furaha yake yule mwenye nyumba akamkaribisha ndani. Funzo la Biblia lilianzishwa, nalo likaongozwa siku iliyofuata. Baada ya muda fulani, mwenye nyumba alikuja katika kweli.
29 Panga Kimbele Kutimiza Mengi Zaidi: Inapendekezwa kwamba wakati fulani utumiwe kila juma kufanya ziara za kurudia. Mengi yanaweza kutimizwa kukiwa na mpango mzuri. Panga ziara zilizo mahali ambako utakuwa unahubiri nyumba hadi nyumba. Mnapohubiri mkiwa na gari, kikundi chapaswa kuwa kidogo ili kila mtu awe na fursa kamili ya kufanya ziara za kurudia. Dereva apaswa kujua kimbele mahali ambako ziara za kurudia zitafanywa ili kuendesha kusiko kwa lazima kuepukwe.
30 Wale ambao wana mafanikio katika kufanya ziara za kurudia na kuanzisha mafunzo ya Biblia nyumbani wanasema kwamba ni muhimu kuonyesha kupendezwa kwa moyo mweupe katika watu na kuendelea kuwafikiria hata baada ya kuwazuru. Pia ni lazima kuwe na somo la Biblia linalopendeza la kuzungumzia na kuweka msingi wa ziara ya kurudia kabla ya kuondoka kwenye ziara ya kwanza. Zaidi ya hayo, ni jambo la maana kurudi bila kukawia ili kufuatia kupendezwa huko. Lengo la kuanzisha funzo la Biblia lapaswa kukumbukwa sikuzote.
31 Sifa muhimu ya mafanikio katika kazi ya ziara ya kurudia ni ujasiri. Huo wapatwaje? Mtume Paulo ajibu kwa kusema kwamba lazima ‘tujipatie ujasiri’ wa kutangazia wengine habari njema “kwa njia ya Mungu wetu.” Ikiwa wataka kukua katika sehemu hii, sali kwa Yehova upate msaada. Kisha, kupatana na sala zako, fuatia kupendezwa kwote. Kwa hakika Yehova atabariki jitihada zako!
[Sanduku katika ukurasa wa 3]
Jinsi ya Kuwa Mwenye Mafanikio Katika Kufanya Ziara za Kurudia
■ Onyesha kupendezwa na watu kwa moyo mweupe.
■ Chagua somo la Biblia lenye kupendeza la kuzungumzia.
■ Weka msingi kwa kila ziara yenye mafanikio.
■ Endelea kumfikiria mtu huyo baada ya kuondoka.
■ Rudi baada ya siku moja au mbili ili kufuatia kupendezwa.
■ Kumbuka lengo lako ni kuanzisha funzo la Biblia.
■ Sali upate msaada wa kujipatia ujasiri kwa kazi hii.