Ikiwa Mtu wa Ukoo Ametengwa na Ushirika...
1, 2. (a) Kusudi la Mungu lilikuwa nini juu ya dini ya kijamaa? (b) Jamaa fulani zilikabili uamuzi gani wakati wa Kora?
ADAMU alipokwisha kukaa peke yake kwa muda fulani, Mungu alisema: “Si vema huyo mtu awe peke yake.” Ndipo alipomwumba Hawa na kuanzisha ndoa ya kibinadamu. (Mwa. 2:18, 21, 22) Baada ya hapo, idadi ya watu duniani ilipasa iongezeke. Kwa hiyo kila mtu angekuwa na watu wengi wa ukoo wake. Hata kama washiriki fulani wa jamaa, kama vile watoto, wasingeishi karibu-karibu wangeweza kutembelewa na kufurahishana.—Mwa. 1:28; Ayubu 1:1-5.
2 Mungu alikuwa amekusudia jamaa ziwe zimeungana katika ibada ya kweli, kwa hiyo imani za kidini zisingetokeza migawanyiko yo yote. Lakini kulitukia visa vilivyofanya dini iwe jambo la kijamaa. Kisa kimoja ni wakati Kora, Dathani na Abiramu walipoasi wakakataa kutii. Yehova alihakikisha kwamba alikuwa akishughulika na watu kwa kuwatumia Musa na Haruni, wala si kwa kuwatumia waasi hao wa kidini. Halafu Musa akawaambia watu waondoke wawe mbali na hema za waasi hao. Watoto na jamaa za Kora, Dathani na Abiramu wangefanya nini? Je! wangetanguliza ushikamanifu wao kwa jamaa zao mbele ya ushikamanifu wao kwa Yehova na kundi lake? Wengi wa wale waliokuwa na uhusiano wa ukoo na waasi hao walitanguliza jamaa mbele ya Mungu. Yehova aliwaua watu hao wa ukoo pamoja na waasi hao.—Hes. 16:16-33.
3. Wengine katika jamaa ya Kora walifanya uchaguzi gani wenye hekima?
3 Walakini, wana fulani wa Kora walibaki wakiwa washikamanifu kwa Mungu na watu Wake. Wao hawakuuawa pamoja na watu wale wengine wa jamaa ya Kora na jamaa za Dathani na Abiramu. (Hes. 26:9-11) Kwa kweli, baadaye wazao wa watu hao wa Kora walibarikiwa kwa kupewa utumishi wa pekee kwenye hekalu na kutajwa kwa heshima katika Biblia.—2 Nya. 20:14-19; Zab. 42, 44-49, 84, 85, 87.
4. Ni kwa njia gani nyingine ushikamanifu kwa jamaa ungaliweza kutokeza jaribu katika Israeli?
4 Watu walikabili uamuzi kama uo huo wa kuwa washikamanifu ama kwa jamaa ama kwa Mungu wakati Mwisraeli alipopata kuwa mwasi-imani. Je! jamaa yake ingejaribu kumkinga asikatiliwe mbali (asiuawe) kwa sababu ya kuongozwa na maoni ya moyoni ya kibinadamu au uhusiano wa damu? Au hata ndugu yake, mwanawe au bintiye angetambua kwamba mwendo wa haki na wenye hekima ungekuwa kuonyesha ushikamanifu kwa Mungu na kundi? (Angalia Kumbukumbu la Torati 13:6-11.) Siku hizi mtenda dhambi katika mpango wa Kikristo hakatiliwi mbali kwa kuuawa, lakini huenda Wakristo wakapatwa na majaribu kwa sababu ya mtu wa ukoo wao kutiwa adabu.
HUENDA WATU WA UKOO WAKATOKEZA MATATIZO
5, 6. (a) Mgawanyiko wa kijamaa unaweza kutokeaje kwa sababu ya dini? (b) Kwa sababu gani lazima Wakristo waepuke kuuacha msimamo wao katika hali hii? (Zab. 109:2-5)
5 Miungano na shauku za kijamaa zinaweza kuwa zenye nguvu sana. Hilo ni jambo la asili nalo linapatana na mpango wa Mungu. (Yohana 16:21) Lakini uhusiano huo wenye nguvu unaweza pia kuletea Wakristo jaribu gumu. Yesu alieleza kwamba tokeo moja la kuwa Mkristo lingekuwa kwamba watu wa ukoo wangeweza kumpinga mtu. Yesu alisema: “La! sikuja kuleta amani, bali upanga. Kwa maana nalikuja kumfitini mtu na babaye, na binti na mamaye, na mkwe na mkwe mtu; na adui za mtu ni wale wa nyumbani mwake. Apendaye baba au mama kuliko mimi, hanistahili.”—Mt. 10:34-38.
6 Wakristo hawataki kuwe na uadui huo. Na hakuna sababu ya kuwafanya watu wa ukoo wawapinge au wawachukie kwa sababu wao wamekuwa watumishi wa Mungu walio safi, wenye adili na unyofu. Hata hivyo Wakristo wa kweli wanajua kwamba hawawezi kutanguliza jamaa mbele ya Mungu. Baadaye matokeo huja kuwa kwamba kuendelea kuwa waaminifu kwa Mungu ndiko kunakomfaidi kila Mkristo. Baada ya muda fulani huenda wakaweza kuwavuta watu wa ukoo wao watembee katika njia inayoongoza kwenye wokovu.—Rum. 9:1-3; 1 Kor. 7:12-16.
7, 8. Ni nani wa kulaumiwa juu ya matatizo ya kijamaa yanayoweza kuletwa na hatua ya kutengwa na ushirika? (Kum. 32:4)
7 Huenda watu wa ukoo wakawaletea Wakristo wa kweli matatizo kwa njia nyingine pia. Jambo hilo linaweza kusitawi wakati mtu wa ukoo anapotengwa na ushirika. Kama ilivyozungumzwa katika makala zilizotangulia, ikiwa mtu kundini anazoea dhambi nzito bila kutubu, Mungu anataka huyo atengwe na ushirika. (1 Kor. 5:11-13) Mwenendo wa mkosaji huyo umebadili uhusiano wake na Yehova na kwa hiyo umebadili pia uhusiano wake na washiriki wa jamaa ambao ni Mashahidi wa Yehova. Mungu siye wa kulaumiwa kwa matokeo hayo, kwa sababu kanuni zake ni za haki ya adili na haki ya hukumu. (Ayubu 34:10, 12) Wala kosa si la watu waaminifu wa ukoo ambao ni Wakristo. Huyo aliyetengwa na ushirika ndiye amejiletea matatizo mwenyewe na kuwaletea watu wa ukoo wake, kama walivyofanya Kora, Dathani na Abiramu.
8 Tunahitaji kuchunguza hali mbili zinazotofautiana. Hali ya kwanza ni wakati inapokuwa kwamba Mkristo anaishi katika nyumba moja na mshiriki wa jamaa aliyetengwa au aliyejitenga mwenyewe na ushirika. Hali ya pili ni wakati mtu huyo wa ukoo anapokuwa si mshiriki wa jamaa hiyo ya karibu.
KATIKA JAMAA IYO HIYO YA KARIBU
9. Inakuwaje kuhusu wajibu wa kijamaa ikiwa mwenzi wa ndoa wa mtu si Mkristo au ametengwa na ushirika?
9 Huenda mtu akawa Mkristo bila ya wengine katika jamaa yao kuikubali imani. Kwa mfano, huenda mke akawa anamtumikia Yehova, lakini mumewe asiwe. Ijapokuwa hivyo, bado mke ni “mwili mmoja” na mumewe na ana wajibu wa kumpenda na kumheshimu. (Mwa. 2:24; 1 Pet. 3:1-6) Au huenda akawa aliolewa na mwanamume aliyekuwa Mkristo aliye wakf lakini baadaye huyo akaondoshwa kundini. Hata hivyo jambo hilo lisingekomesha uhusiano wao wa ndoa; kifo peke yacho au talaka inayopatana na Maandiko ndiyo mambo ambayo yangeweza kuukomesha uhusiano huo.—1 Kor. 7:39; Mt. 19:9.
10, 11. Hatua ya kutenga na ushirika inabadili uhusiano wa kiroho nyumbani kwa njia gani?
10 Vivyo hivyo, ikiwa mtu wa ukoo, kama mzazi, mwana au binti, ametengwa au amejitenga mwenyewe na ushirika, bado uhusiano wa damu na wa kijamaa unaendelea kuwapo. Basi, je! hiyo inamaanisha kwamba katika jamaa hiyo kila jambo litaendelea kufanywa sawasawa na lilivyokuwa hapo kwanza ikiwa mshiriki mmoja ametengwa na ushirika? Sivyo kabisa.
11 Mtu aliyetengwa na ushirika amekatiliwa mbali kiroho atoke kwenye kundi; ule uhusiano wa kiroho uliokuwapo umezuiwa kabisa. Ndivyo ilivyo hata kuhusiana na watu wa ukoo wake, kutia na wale walio ndani ya jamaa iyo hiyo ya karibu. Hivyo, ingawa washiriki wa jamaa watatambua kwamba wangali na uhusiano wa kijamaa na mtu huyo, hawatakuwa tena na ushirika wo wote wa kiroho pamoja naye.—1 Sam. 28:6; Mit. 15:8, 9.
12. Kwa habari ya ushirika wa kiroho, ni mabadiliko gani yanayoweza kutokea ikiwa mshiriki wa jamaa ametengwa na ushirika?
12 Hiyo itamaanisha wafanye mabadiliko katika ushirika wa kiroho ambao huenda ulikuwa katika jamaa hiyo. Kwa mfano, mume akitengwa na ushirika, mkewe na watoto hawatafurahia kumwacha awaongoze katika funzo la jamaa la Biblia wala katika usomaji wa Biblia na sala. Ikiwa yeye anataka kutoa sala, kama vile wakati wa kula, yeye ana haki ya kufanya hivyo katika nyumba yake mwenyewe. Lakini wao wanaweza kumtolea Mungu kwa kimya sala zao wenyewe. (Mit. 28:9; Zab. 199:145, 146) Namna gani ikiwa mtu aliyetengwa na ushirika katika nyumba hiyo anataka kuwapo wakati jamaa inaposoma Biblia pamoja au inapokuwa na funzo la Biblia? Wale wengine wanaweza kumwacha awepo asikilize ikiwa hatajaribu kuwafundisha au kuwatolea maoni yake ya kidini.
13. Wazazi wangeshughulikaje nyumbani na mtoto aliyetengwa na ushirika?
13 Ikiwa mtoto mdogo ametengwa na ushirika, bado wazazi wataendelea kumtimizia mahitaji yake ya kimwili na kumpa mazoezi ya adili na kumtia adabu. Wao wasingemfundisha mtoto huyo moja kwa moja katika funzo la Biblia, huku yeye akishiriki. Lakini hiyo haimaanishi kwamba angekataliwa asiwe kwenye funzo la jamaa. Nao wanaweza kutaja-taja sehemu za Biblia au za vitabu vya Kikristo zilizo na mashauri anayohitaji. (Mit. 1:8-19; 6:20-22; 29:17; Efe. 6:4) Wanaweza kumwacha aende pamoja nao na kuketi pamoja nao kwenye mikutano ya Kikristo, wakitumaini kwamba yeye atayathamini mashauri ya Biblia.
14, 15. Jambo gani lifanywe juu ya kumrudisha nyumbani mzazi aliyetengwa na ushirika?
14 Lakini namna gani ikiwa mtu wa ukoo wa karibu, kama vile mwana au mzazi asiyeishi katika nyumba hiyo, ametengwa na ushirika na baada ya hapo anataka kurudi aishi pamoja nao? Jamaa hiyo inaweza kuamua jambo la kufanya kwa kutegemea ni hali gani iliyopo.a
15 Kwa mfano, huenda aliyetengwa na ushirika akawa ni mgonjwa au hawezi tena kujitunza mwenyewe kwa upande wa pesa au kimwili. Watoto Wakristo wana wajibu wa Maandiko na wa adili kumsaidia. (1 Tim. 5:8) Labda inaelekea kuna uhitaji wa lazima kumleta mzazi huyo nyumbani, kwa muda au daima. Au huenda ikafaa kufanya mipango ya kumtunza mzazi huyo akiwa mahali palipo na watu wa utabibu (madaktari) lakini mahali anapoweza kutembelewa. Jambo la kufanya huenda likategemea mambo kama mahitaji ya kweli ya mzazi huyo, nia yake na heshima ambayo kichwa cha jamaa kinayo kwa hali ya kiroho ya jamaa.
16, 17. (a) Wazazi wanaweza kuamuaje uwezekano wa kurudi nyumbani kwa mtoto aliyetengwa na ushirika? (b) Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa mwana mpotevu?
16 Ingeweza kuwa ivyo hivyo kwa habari ya mtoto aliyekuwa ameondoka nyumbani lakini sasa ametengwa au amejitenga mwenyewe na ushirika. Nyakati nyingine wazazi Wakristo wamemkubali arudi nyumbani kwa muda fulani mtoto aliyetengwa na ushirika ambaye amekuwa mgonjwa sana kimwili au katika mawazo yake ya moyoni. Lakini katika kila kisa wazazi wanaweza kuzipima hali za mtu huyo waone ziko namna gani. Je! mwana aliyetengwa na ushirika amekuwa akiishi kwa kujitegemea mwenyewe, na je! sasa hawezi kufanya hivyo? Au yeye anataka kurudi nyumbani kwa sababu hasa akirudi maisha yatakuwa mepesi zaidi? Nazo tabia zake na nia yake iko namna gani? Je! ataingiza “chachu” nyumbani?—Gal. 5:9.
17 Katika mfano wa Yesu wa mwana mpotevu, baba ndiye aliyekimbia kumlaki kisha akamkubali mwanawe mwenye kurudi. Kwa kuiona hali yenye kusikitisha sana ya kivulana wake, baba alimsikitikia kwa huruma iliyo asili ya mzazi. Ingawa hivyo, tunaweza kuona kwamba mwana huyo hakuja nyumbani akiwa na makahaba (malaya) wala hakuja akiwa na nia ya kuendeleza maisha yake yenye dhambi katika nyumba ya baba yake. Sivyo, yeye alionyesha toba ya moyoni na kwa wazi alikuwa amepiga moyo konde (ameamua kabisa) arudi aishi maisha safi.—Luka 15:11-32.
WATU WA UKOO WALIOTENGWA NA USHIRIKA WASIOISHI NYUMBANI
18, 19. (a) Inawapasa Wakristo wawe na maoni gani juu ya kushirikiana na watu wa ukoo waliotengwa na ushirika ambao wako nje ya jamaa ya karibu? (b) Kwa sababu gani msimamo huo unafaa? (2 Tim. 2:19)
18 Hali ya pili tunayohitaji kufikiria ni ile inayohusu mtu wa ukoo aliyetengwa au aliyejitenga mwenyewe na ushirika ambaye hayumo katika jamaa hiyo ya karibu wala haishi katika nyumba ya mshiriki wa jamaa. Bado mtu huyo ana uhusiano wa damu au wa ndoa, na kwa hiyo huenda kukawa na uhitaji wa kiasi kidogo kumtimizia mambo ya kijamaa ambayo yanahitajiwa kabisa. Hata hivyo, hangetendewa kama kwamba anaishi katika nyumba moja na watu wa ukoo ambamo kuonana na kuzungumza naye kusingeweza kuepukwa. Inatupasa tuliweke waziwazi akilini agizo hili la Biblia lililoongozwa na Mungu: “Acheni kuchangamana katika ushirika pamoja na mtu ye yote aitwaye ndugu ambaye ni mwasherati au mtu mwenye pupa . . . , wala hata kula pamoja na mwanamume kama huyo.”—1 Kor. 5:11, NW.
19 Kwa hiyo, Wakristo wenye ukoo na mtu huyo aliyetengwa na ushirika ambaye anaishi nje ya nyumba hiyo wangejitahidi kuepuka kushirikiana naye kusipokuwa na uhitaji, hata kupunguza sana shughuli zao za kazi pamoja naye. Kufaa kwa mwendo huu kunaonekana wazi kutokana na habari zinazoeleza mambo ambayo yametukia wakati watu wa ukoo walipofuata maoni yenye makosa ya kusema, ‘Ingawa ametengwa na ushirika, yeye ni mtu wa ukoo wetu na kwa hiyo tunaweza kumtendea kama tulivyokuwa tukimtendea hapo kwanza.’ Kutoka eneo moja yaja habari hii:
“Mtu mmoja aliyetengwa na ushirika alikuwa wa ukoo mmoja na karibu sehemu moja kwa tatu ya kundi hilo. Watu wote wa ukoo wake waliendelea kushirikiana naye.”
Na mzee mmoja Mkristo mwenye kuheshimiwa sana aandika hivi:
“Katika eneo letu kuna nyakati ambazo watu fulani waliotengwa na ushirika wenye jamaa kubwa-kubwa wamekwenda kulakiwa, wanapoingia katika ukumbi wa Jumba la Ufalme, huku wakipigwa-pigwa mgongoni kwa furaha ya ajabu na kusalimiwa kwa mikono (ingawa wenye kumsalimu walijua kwamba huyo aliyetengwa na ushirika alikuwa bado akiishi maisha ya uasherati). Mimi najisikia sana kwamba wale ambao wametengwa na ushirika wanahitaji kuona kwamba mwendo wao unachukiwa na Yehova na watu wake na kwamba inawapasa wajisikie wakiwa na uhitaji mkubwa sana wa kutubu kwa njia ya kweli. Ni jambo gani litakalowasaidia hawa waliotengwa na ushirika wabadilike na huku wanaendelea kusalimiwa na wote walio katika jamaa zao kubwa-kubwa wanaoyajua mazoea yao?”
20, 21. Kwa habari ya watu wa ukoo waliotengwa na ushirika, kwa sababu gani tunahitaji kuwa waangalifu? (2 Tim. 2:22)
20 Bila shaka katika karne ya kwanza kulikuwa na makundi ambako watu wengi walikuwa wa ukoo mmoja. Lakini wakati mtu fulani alipotengwa na ushirika, je! iliwapasa watu wote wa ukoo wake waendelee kumtendea kama kawaida maadamu hawakuzungumza mambo ya Maandiko pamoja na huyo aliyetengwa na ushirika? Sivyo. Kama ingalikuwa hivyo kundi lisingalikuwa likiifuata kwa kweli amri hii: “Ninyi mwondoeni yule mbaya miongoni mwenu.”—1 Kor. 5:13.
21 Uangalifu mkubwa unahitaji kutumiwa ili hali ya mtenda dhambi aliyetengwa na ushirika isije ikaachiliwa au kuonekana kama jambo dogo tu. Kama vile wana wa Kora walivyoonyesha kwa njia nzuri, lazima tuonyeshe ushikamanifu wetu wa kwanza kwa Yehova na mpango wake wa kitheokrasi. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba tunapozitetea kanuni zake na kupendelea kushirikiana na watu wake walio katika mpango wa tengenezo, badala ya kushirikiana na wakosaji, tutapata ulinzi na baraka yake.—Zab. 84:10-12.
VIKUSANYIKO VYA URAFIKI NA WATU WA UKOO WALIOTENGWA NA USHIRIKA
22. Kwa sababu gani vikusanyiko vya kijamaa vinaweza kutokeza matatizo ya pekee kuhusu watu wa ukoo waliotengwa na ushirika?
22 Mara nyingi ni jambo la kawaida watu wa ukoo kuwa pamoja nyakati za kula, kwenye pikniki, kwenye vikusanyiko vya jamaa vya kufurahiana wakati mtu alikuwa katika safari ya mbali arudipo au kwenye vikusanyiko vingine vya urafiki. Lakini wakati mtu amefuatia dhambi bila kutubu ikawa lazima atengwe na ushirika, huenda akawaletea magumu Wakristo wa ukoo wake kuhusiana na vikusanyiko hivyo. Ingawa wanajua kwamba bado wao ni wa ukoo mmoja naye, hawapaswi walipuze shauri la Paulo linalosema Wakristo waaminifu ‘waache kuchangamana katika ushirika’ pamoja na mtenda dhambi aliyeondoshwa kundini.
23. Hali ya mtu wa ukoo aliyetengwa na ushirika ingekuwa nini kuhusiana na arusi ya Kikristo?
23 Hakuna sababu ya kutafuta sheria fulani ya kuamulia washiriki wa jamaa kama watakuwa kwenye vikusanyiko ambako mtu wa ukoo aliyetengwa na ushirika yuko. Hilo ni jambo la kuamuliwa na wale wanaohusika, kupatana na shauri la Paulo. (1 Kor. 5:11) Hata hivyo inapasa ifahamike kwamba ikiwa mtu aliyetengwa na ushirika atakuwa kwenye kikusanyiko ambako Mashahidi wasio wa ukoo huo wamekaribishwa, jambo hilo linaweza kubadili mambo yanayofanywa na wengine. Kwa mfano, huenda Wakristo wawili wakawa wakioana kwenye Jumba la Ufalme. Mtu wa ukoo aliyetengwa na ushirika akija kwenye Jumba la Ufalme kuhudhuria arusi hiyo, ni wazi asingeweza kuwa kati ya wale wenye kumleta bibi-arusi wala asingeweza kuwa ndiye wa kumpokeza bibi-arusi kwa bwana-arusi. Namna gani ikiwa kuna karamu ya arusi au chai? Huo unaweza kuwa wakati wenye furaha, kama ulivyokuwa katika Kana wakati Yesu alipohudhuria. (Yohana 2:1, 2) Lakini je! mtu wa ukoo aliyetengwa na ushirika ataruhusiwa kuja au hata kukaribishwa? Ikiwa atahudhuria, huenda Wakristo wengi, wawe ni wa ukoo huo au wasiwe, wakaamua kwamba haiwapasi kuwapo, kula wala kushirikiana naye, kupatana na maagizo ya Paulo kwenye 1 Wakorintho 5:11.
24. Wakristo washikamanifu wanaweza kufurahia zaidi sana ushirika gani? (Mit. 18:24)
24 Hivyo, huenda nyakati nyingine Wakristo wakajisikia hawawezi kumwacha mtu aliyetengwa au aliyejitenga mwenyewe na ushirika ahudhurie kikusanyiko ambacho kwa kawaida kingekuwa na washiriki wa jamaa. Hata hivyo, Wakristo wanaweza kuufurahia ushirika wa washiriki washikamanifu wa kundi, wakiyakumbuka maneno ya Yesu: “Mtu ye yote atakayeyafanya mapenzi ya Mungu, huyo ndiye ndugu yangu, na umbu [ndugu wa kiume au wa kike] langu, na mama yangu.”—Marko 3:35.
25, 26. Mtu wa ukoo aliyetengwa na ushirika akifa, ni jambo gani lingefanywa kuhusu maziko?
25 Jambo la uhakika ni kwamba wakati Mkristo anapojiacha atende dhambi kisha inakuwa lazima atengwe na ushirika, yeye anapoteza mambo mengi: msimamo wake wenye kukubaliwa na Mungu; ushirika katika kundi lenye furaha la Wakristo; ushirika mtamu pamoja na kina ndugu, kutia na mwingi wa ushirika aliokuwa nao pamoja na watu wa ukoo wake walio Wakristo. (1 Pet. 2:17) Huenda maumivu aliyoleta yakaendelea kuwapo hata baada ya yeye kufa.
26 Akifa akiwa bado katika hali ya kutengwa na ushirika, mipango ya maziko yake inaweza kuwa tatizo. Huenda Wakristo wa ukoo wake wakawa walitaka hotuba itolewe kwenye Jumba la Ufalme, ikiwa hiyo ndiyo desturi ya mahali hapo. Lakini jambo hilo lisingefaa kufanywa kwa ajili ya mtu aliyeondoshwa kundini. Ikiwa yeye alikuwa amekuwa akionyesha ushuhuda wa toba na kutaka msamaha wa Mungu, kama vile kwa kuacha kuzoea dhambi na kuhudhuria mikutano ya Kikristo, huenda dhamiri ya ndugu fulani ikamruhusu atoe hotuba ya Biblia kwenye sehemu ya nyumbani ambako atazikwa au kwenye makaburi. Maelezo hayo ya Biblia juu ya hali ya wafu yanatolea wasioamini ushuhuda au kuwafariji watu wa ukoo. Walakini, ikiwa mtu aliyetengwa na ushirika alikuwa amekuwa akiunga mkono mafundisho ya uongo au mwenendo usio wa kimungu, hata hotuba kama hiyo isingefaa kutolewa.—2 Yohana 9-11.
MASOMO AMBAYO SISI SOTE TUNAPASWA KUJIFUNZA
27. Imetupasa tuwe na maoni gani juu ya hukumu za Mungu?
27 Sisi sote tunahitaji kuthamini kwamba uamuzi wa Yehova ndio wa maana zaidi. (Mit. 29:26) Ndivyo ilivyo kuhusu mazoea yenye kuchukiza, kwa maana Biblia inaonyesha kwamba hayo ni mambo anayoyachukia sana Mungu. (Mit. 6:16-19) Ndivyo ilivyo pia juu ya uamuzi wake unaohusu watu mmoja mmoja. Neno la Yehova linasema waziwazi kwamba “wadhalimu,” wale wanaoendesha “matendo ya mwili,” hawatarithi ufalme wake. (1 Kor. 6:9, 10; Gal. 5:19-21) Watu kama hao hawana nafasi mbinguni, wala hakuna mahali patakapowafaa katika makao ya kidunia ya ule Ufalme. Kwa hiyo, mtu ye yote anayetaka kubaki katika kundi safi la Mungu leo lazima azitimize kanuni Zake. Mungu hataruhusu kamwe “chachu” ibaki kati ya watu wake watakatifu ili kuwachafua.—1 Kor. 5:6-13.
28. Shauri hili la kutenga na ushirika linaweza kuujaribuje ushikamanifu wetu?
28 Ni wazi kwamba mtu wa ukoo wa karibu akitengwa na ushirika, maoni ya moyo wa kibinadamu yanaweza kutuletea jaribu kubwa. Misisimuko ya moyo na uhusiano wa jamaa unakuwa wenye nguvu hasa kati ya wazazi na watoto wao, na unakuwa wenye nguvu pia wakati mwenzi wa ndoa anapotengwa na ushirika. Hata hivyo, lazima tutambue kwamba, mwishowe kabisa, hatutamfaidi mtu ye yote wala kumpendeza Mungu tukiacha maoni ya moyoni yatuongoze kupuza shauri Lake lenye hekima na uongozi wake. Tunahitaji kuonyesha tunaamini kwa ukamili kwamba njia za Mungu, kutia na mpango wake wa kutenga na ushirika wakosaji wasiotubu, ni zenye haki kabisa kabisa. Tukiendelea kuwa washikamanifu kwa Mungu na kwa kundi, huenda baadaye mkosaji akapata somo kutokana na jambo hilo, atubu kisha arudishwe kundini. Hata hivyo, kama atafanya hivyo au hatafanya, sisi tunaweza kupata faraja na nguvu kutokana na maneno aliyoyasema Daudi katika maisha yake ya uzee:
“Maamuzi yote ya hukumu [ya Mungu] yako mbele yangu; . . . Na acha Yehova anilipe mimi kulingana na haki yangu ya adili, kulingana na usafi wangu mbele ya macho yake. Kwa mtu mshikamanifu wewe utatenda kwa ushikamanifu; kwa mtu asiye na kosa, aliye hodari wewe utashughulika bila kosa; kwa mtu anayeendelea kuwa safi wewe utajionyesha mwenyewe kuwa safi . . . Nao watu wanyenyekevu wewe utawaokoa.”—2 Sam. 22:23-28, NW.—Kutoka The Watchtower, September 15, 1981.
[Maelezo ya Chini]
a Maelezo juu ya hali ya wazee na watumishi wa huduma yameonyeshwa katika “Maswali Kutoka kwa Wasomaji’’ katika Mnara wa Mlinzi wa Agosti 1, 1978.
[Picha katika ukurasa wa 20]
Huenda mzazi aliyetengwa na ushirika akahitaji kutunzwa katika makao ya watoto Wakristo
[Picha katika ukurasa wa 21]
Mwana mpotevu hakurudi nyumbani akiwa na kusudi la kuendeleza maisha yake yenye dhambi, bali alitubu. Baba yake alikubali arudi