“Toka Katika Bara Lako na Kutoka kwa Watu wa Ukoo Wako”
KATIKA Novemba 1981 Tony na mke wake, Margaret, pamoja na watoto wao wawili, wenye umri wa miaka 9 na 11, walihama Uingereza kwenda magharibi ya Ailandi. Kwa nini? Ili kusaidia katika kazi ya kufundisha peupe ya Mashahidi wa Yehova. Majuma machache tu baadaye, wao walikuwa wakielekeana na magumu. Kilikuwa kipupwe chenye baridi kali sana. Matarajio ya kazi hayakuwa yametimia, kwa hiyo Tony akawa ameanza biashara ya kusafisha mabomba ya kutolea moshi ndani ya nyumba. Kwa kuwa alikuwa bado si stadi sana, yeye alirudi kwenye maskani yao akiwa na masizi baada ya kazi ngumu ya siku. Wazia fadhaa yake alipokuta kwamba mifereji yote ya maji ilikuwa imegandamana kwa barafu, na maji ya kuogea aliyokuwa nayo yalikuwa ya kiasi cha birika moja ndogo tu! “Kwa dakika moja nikaanza kujiuliza ni kwa nini sisi tulihama kutoka kwenye maskani yetu na kutoka kwa watu wa ukoo wetu,” yeye akakiri.
Kuhama kutoka kwenye jamaa na marafiki ili kutumikia Mungu kwa ukamili zaidi, halafu kufuliza mwendo yajapokuwako magumu, kunahitaji imani halisi. Mtu mmoja aliyeonyesha imani kama hiyo karibu miaka 4,000 iliyopita alikuwa Abrahamu mzee wa ukoo. Mwanafunzi Stefano alisema hivi juu yake: “Yule Mungu wa utukufu alitokea kwa Abrahamu baba yetu wa zamani wakati yeye alipokuwa katika Mesopotamia, kabla ya yeye kuanza kukaa katika Harani, na [Mungu] akasema kwake, ‘Toka katika bara lako na kutoka kwa watu wa ukoo wako na uje mpaka uingie ndani ya bara ambalo mimi nitakuonyesha wewe.’”—Matendo 7:2, 3, NW.
Bila shaka, hakuna mmoja leo aliye na amri ya wazi hivyo kutoka kwa Mungu kwamba ahame kutoka kwenye bara la maskani yao. Hata hivyo, maelfu ya Wakristo katika karne hii ya 20 wamepanga mambo yao ili watende alilotenda Abrahamu—wahamie maeneo mapya kuendeleza zaidi mapendezi ya Mungu. (Mathayo 24:14; 28:19, 20; Warumi 10:13-15) Wao wametambua kwamba “lile shamba ni ulimwengu” na kwamba mahali pengi pana uhitaji mkubwa wa msaada zaidi. (Mathayo 13:38, NW) Kama Isaya, wao wameyaitikia kwa sulubu maneno ya Yehova, “Ni nani ambaye mimi nitatuma, na ni nani ambaye ataenda kwa ajili yetu?” Kwa kuuona uhitaji, wao pia wamejibu, “Mimi nipo hapa! Tuma mimi.”—Isaya 6:8, NW.
Kwa Nini Wanatenda Hivyo?
Ni watu wa namna gani wanaofanya mhamo huo? Wao si wa kutoka umri au malezi yo yote ya kipekee, wala hawadai kwamba wana uwezo usio wa kikawaida. Wao ni watu tu ambao, kwanza, wana nia ya kuziona tamaa na starehe za kibinafsi kuwa zisizo za maana sana kwa sababu ya masilahi ya Ufalme wa Mungu. Iko kama vile ilivyokuwa kwa Abrahamu wakati alipohama kutoka kwenye lile jiji la Uri lenye ufanisi na starehe za kimwili ili akaishi katika mahema katika bara la ugenini.—Waebrania 11:8-10.
“Sikuzote sisi tungeweza kuuona uhitaji wa kufanya mengi iwezekanavyo katika utumishi wa Yehova,” wakasema mume na mke waliohama pamoja na wana wao matineja katika 1983. “Sisi tulihisi kama vile mtume Paulo alivyohisi wakati aliposema, ‘Wakati uliobaki umepunguzwa’; kwa hiyo sisi tukaamua ‘kupiga hatua kuingia Ailandi’ na kusaidia kazi huko.” (1 Wakorintho 7:29; linganisha Matendo 16:9, NW.) Kulingana na tafsiri moja isiyo halisi, maana ya maneno ya mtume Paulo kwenye 1 Wakorintho 7:29 ni: Jambo lililo la maana kukumbuka ni kwamba wakati wetu unaobaki ni mfupi sana, na ndivyo na fursa zetu za kufanya kazi ya Bwana. (The Living Bible) Wakristo wengi waaminifu wamehamia mahali kokote wanakohitajiwa ili kushika fursa hizi kabla hazijatoweka na kufanya utumizi ulio bora zaidi wa wakati wenye thamani unaobaki.
“Sisi tuliona kuwa fursa nzuri sana ‘kuwa sikuzote na utele wa kufanya katika kazi ya Bwana.’” (1 Wakorintho 15:58, NW) “Sisi tulitaka kutumikia Yehova mahali ambapo tungeweza kufanya mema yaliyo mengi zaidi.” “Sisi tulihisi kwamba tulikuwa katika msimamo wa kipesa wa kuweza kuhama na kwamba ikiwa tungeweza kujazia uhitaji fulani mahali fulani, lingekuwa kosa kwetu kutotenda hivyo.” Maelezo hayo yanasimulia hisia za wengi ambao wamechukua hatua za kutumikia mahali ambako wanahitajiwa zaidi. Wakristo hawa wamethamini kwa moyo onyo la upole linalopatwa kwenye Mithali 3:9, 27, NW: “Heshimu Yehova kwa vitu vyako vyenye kuthamanika na kwa matunda ya kwanza ya mazao yako yote. Usizuilie wema kutoka kwa wale ambao wanauwia, wakati inapotukia kuwa katika nguvu za mkono wako kutenda hivyo.” Wakiisha kuchunguza mastakimu zao kwa uangalifu, wao wameamua kwamba ‘imo katika nguvu za mikono yao kutenda’ wema wa kudumu kwa jirani zao katika sehemu nyinginezo za ulimwengu.—Ona pia Warumi 1:14, 15; Luka 10:27-37.
Huenda wewe ukawa katika msimamo wa kuweza kufanya mhamo huo. Ikiwa ndivyo, wewe utapendezwa kujua jinsi watu fulani ambao tayari wamehama wanajibu maswali yanayofuata.
Ni Mambo Gani Yanayopasa Kufikiriwa Kabla ya Kuhama?
Kabla ya kuhama, ushauriane pamoja na wazee katika kundi lako mwenyewe. Pata kujua wao wanafikiri nini juu ya mipango yako. (Mithali 24:6) Huenda kukawa na sababu ambazo mhamo huo haungeshaurika katika kisa chako, na wao watakusaidia wewe ukadirie hali yako ifaavyo. Mathalani, mtu anayehama anapaswa kuwa na imara ya kiroho ikiwa yeye anataka awe msaada mkubwa wala si dhima katika mahali pale papya.
Fanya kazi kupitia ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova katika nchi ambako unatumainia kuhamia—au kupitia ofisi ya tawi ya kwenu ikiwa unatumainia kuhama uende ndani ya nchi yako mwenyewe. Ikiwa inawezekana, fanya ziara kwenye eneo linalonuiwa ili upate kujua habari fulani juu ya bara hilo na watu wa huko kabla hujafanya uamuzi wa hatimaye.
Changanua makusudio yako kabla ya kuhama. Abrahamu alihama kwa sababu yeye alikuwa na tamaa yenye kina kirefu ya kutimiza mapenzi ya Mungu, si kwa sababu ya roho ya kutaka kujijasirisha katika matendo hodari ya sifa au msisimuko au kivutio fulani cha kibinafsi. Yapime kwa uangalifu mambo yote yanayohusika ndani. Je! huenda kukawa na tatizo la lugha? Je! wewe unaweza kujirekebisha upatane na utamaduni na tabia-hewa iliyo tofauti? Je! wewe una mahitaji yo yote ya kiafya yaliyo ya pekee? Je! washiriki wote wa jamaa wanajihusisha ndani ya mhamo huo kwa moyo mzima? Je! wewe umepanga kitengenezo mambo yako ya kipesa ili kwamba uweze kufanya mhamo huo kwa mafanikio? (Linganisha Luka 14:28.) Mambo haya na mambo mengineyo yanataka mfikirio wa uangalifu na wa sala.—Waefeso 6:18.
Ni Magumu Gani Ambayo Huenda Ikawa Lazima Kuyakabili?
Hata kabla ya kuhama, huenda wewe ukalazimika kukabili magumu. Si kila mmoja ambaye maoni yake juu ya mambo yatakuwa kama yako. Huenda ukasikia maelezo yenye kusemwa bila kufikiriwa vizuri au ya mwelekeo hasi. Ingawa hivyo, kumbuka hata mtume Petro aliitikia kwa mwelekeo hasi aliposikia jambo ambalo lingepata Yesu. Badala ya kumtia Yesu moyo awe na uthibitifu katika kutenda mapenzi ya Yehova, Petro alisema: “Uwe mwenye fadhili kwako mwenyewe, Bwana; wewe hutapatwa na tukio hilo hata kidogo.” Kama Yesu, na uazimie kukinza maongezi yoyote kama hayo ya mwelekeo hasi.—Mathayo 16:22, 23, NW.
Baada ya wewe kutulia katika eneo lile jipya, huenda hisia ya kuikosa maskani ya kwenu ikawa tatizo kubwa. Upendo kwa Yehova na kwa watu wanaohitaji kusikia zile habari njema za Ufalme wake utakusaidia wewe kukabili jambo hilo. Matatizo mengi yanaweza kupunguzwa ukifanya mahali pako papya pawe maskani yako kikweli. Epuka kufanya milinganisho ya mwelekeo hasi kuhusiana na maskani yako’ iliyotangulia, kwa kuwa kufanya hivyo kunaweza kusababisha kukosa uradhi na kuona uchungu moyoni. Unapokabili magumu, kumbuka Mwaliko wa Yehova kwenye Malaki 3:10: “Mnitahini mimi kabisa, tafadhali, .. kama mimi sitafungulia ninyi watu malango-mafuriko ya mbingu na kwa kweli nimwage kabisa baraka juu yenu ninyi mpaka kuwe hakuna ukosefu zaidi tena.”
Ni Baraka Gani Ambazo Zinaweza Kufurahiwa?
Kadiri ambavyo mhusiko wako katika kazi ya kutangaza zile habari njema unakua, ndivyo ubora wa huduma yako utakua. Wewe utasitawisha stadi zaidi ukiwa mwalimu wa Neno la Mungu. Hiyo italeta manufaa si kwako wewe tu, bali pia kwa wote watakaokusikiliza wewe. (1 Timotheo 4:15, 16) Ni pendeleo kama nini kuongoza mafunzo ya Biblia kwenye maskani za watu na kuwasaidia bila malipo wenye mioyo myeupe watoke katika mafundisho bandia ya Kibabuloni! Wewe unaweza kuwa na ile shangwe iliyosimuliwa na mtume Paulo wakati alipoandikia hivi baadhi ya watu aliokuwa amewasaidia wawe Wakristo: “Ni nini tumaini letu au shangwe au taji ya mchachawo—ala, hiyo kwa uhakika si ninyi?” (1 Wathesalonike 2:19, NW) Ndiyo, ni shangwe na baraka kuwa na ushiriki katika kusaidia watu mmoja mmoja na makundi kupata ufanisi kiroho.
Abrahamu aliitwa “rafiki ya Yehova” kwa sababu yeye alitii mwelekezo wa Mungu kwa utayari. (Yakobo 2:21-23; Isaya 41:8, NW) Wewe pia unaweza kuongeza kina cha uhusiano wako wa kibinafsi pamoja na Mungu. Wakati unapojitahidi katika utumishi wake, wewe utapata utunzaji na utegemezo wake wenye upendo. Utaelewa kwa ukamili zaidi lile ambalo mtunga zaburi alimaanisha aliposema: “Onjeni na mwone kwamba Yehova ni mwema, O ninyi watu.”—Zaburi 34:8, NW.
Tony, Margaret, na watoto wao walikabili matatizo wakati walipohama wakatumikie Yehova kwa ukamili zaidi. Lakini kwa msaada wa Yehova, wao waliyashughulikia kwa mafanikio. “Sisi hatukuruhusu magumu yatunyang’anye shangwe yetu,” wao wakasema. “Katika hali kama zile ambazo sisi tulikabili, tulijifunza kutegemea Yehova zaidi, na tuliona mkono wake katika kila jambo wakati tatizo moja baada ya jingine lilipoyeyukia mbali.” Maelfu ya watumishi wa ki-siku-hizi wa Yehova yameonyesha imani kama hiyo kwa kuhamia mahali kokote ambako kuna uhitaji mkubwa zaidi. Je! wewe unaweza kufanya hivyo hivyo?
[Picha katika ukurasa wa 23]
Mazungumzo ya kijamaa yanaweza kufanyiza mhamo wenye mafanikio zaidi