Aprili—Wakati wa ‘Kufanya Kazi kwa Bidii na Kujikakamua Wenyewe’
1 Majuma ya kabla na baada ya Ukumbusho ni wakati ambao watu wa Yehova hutafakari. Ni wakati wa kutafakari yale ambayo yalitimizwa na kifo cha Kristo na kutafakari tumaini letu kutoka kwa Mungu linalowezekana kwa damu ya Yesu iliyomwagwa. Unapofikiria tarehe ya Aprili 19 mwaka jana, unakumbuka nini? Je, waweza kukumbuka nyuso ulizoona jioni hiyo, na hali bora ya kiroho iliyokuwapo kwenye Ukumbusho huo? Je wakumbuka ile hotuba iliyozungumzia mambo yenye kina kutoka kwa Biblia na sala za kutoka moyoni? Labda uliazimia kushukuru zaidi kwa sababu ya upendo ulioonyeshwa na Yehova na Yesu. Kutafakari huko kumekuwa na matokeo gani kwako sasa?
2 Ni wazi kwamba watu wa Yehova hawaridhiki tu na kusema asante. (Kol. 3:15, 17) Katika mwezi wa Aprili mwaka jana, tulifanya mengi ili kuonyesha uthamini wetu kwa maandalizi ya Yehova ya wokovu kwa kushiriki katika huduma yaKikristo. Idadi ya mapainia-wasaidizi katika Afrika Mashariki ilikuwa maelfu kadhaa na ilipita kilele kilichotangulia kwa asilimia 48. Jitihada yao pamoja na ya watangazaji wengine wote wa Ufalme, ilitokeza vilele vipya katika saa, magazeti, na ziara za kurudia. Shangwe yetu iliongezeka kwa kuona maelfu ya mafunzo mapya ya Biblia yakianzishwa na kilele kipya cha hudhurio la Ukumbusho!
3 Kwa kweli, tumaini letu hakika hutuchochea tutende. Ni kama vile mtume Paulo alivyoandika: “Kwa maana kwa madhumuni haya tunafanya kazi kwa bidii na kujikakamua wenyewe, kwa sababu tumeweka tumaini letu juu ya Mungu aliye hai, ambaye ni Mwokozi wa namna zote za watu, hasa wa walio waaminifu.”—1 Tim. 4:10.
4 Utaonyeshaje imani yako kwa maandalizi ya Yehova ya uhai katika majira haya ya Ukumbusho? Mwezi wa Aprili mwaka jana, idadi yetu ya watangazaji wa Ufalme katika Afrika Mashariki ilifikia kilele ambacho ndicho cha pili kati ya vilele vyote ambavyo tumewahi kuwa navyo. Je, twaweza kupita kilele hicho mwezi wa Aprili mwaka huu? Tunaweza kufanya hivyo. Lakini kila mhubiri aliyebatizwa na asiyebatizwa atahitaji kushiriki. Wapya wengi huenda pia wakastahili kushiriki. Hivyo, unapojiandaa kufanya kazi kwa bidii na kujikakamua katika mwezi wa Aprili, fikiria njia ambazo unaweza kuchochea wengine, kutia ndani wapya na wasio na uzoefu waandamane nawe.
5 Kusaidia Wengine Warudie Utendaji Wao: Ikiwa wajua watu fulani ambao hawajahubiri kwa mwezi mmoja au miwili, labda unaweza kuwatia moyo na kuwaalika waandamane nawe katika utumishi wa shambani. Ikiwa kuna wasiotenda kutanikoni, wazee watajitahidi sana kuwatembelea na kuwatia moyo waanze tena kuhubiri katika mwezi wa Aprili.
6 Ni lazima sisi sote twendelee kuomba roho ya Yehova ituimarishe katika utumishi wake. (Luka 11:13) Tufanyeje ili tupokee roho hiyo? Soma Neno la Mungu lililopuliziwa. (2 Tim. 3:16, 17) Lazima pia “[tusikilize] lile ambalo roho huyaambia makutaniko” kwa kuhudhuria mikutano yote mitano ya kila juma. (Ufu. 3:6) Sasa ndio wakati ufaao wa kusaidia wasio wa kawaida na wasiotenda kuboresha mazoea yao ya kujifunza na kuhudhuria mikutano kwa ukawaida. (Zab. 50:23) Tutafanya hivyo bila kusahau hali yetu wenyewe ya kiroho. Lakini kuna jambo jingine linalohitajiwa.
7 Mtume Petro alieleza kwamba Mungu huwapa roho yake takatifu “wale wanaomtii yeye akiwa mtawala.” (Mdo. 5:32) Utii huo wahusisha kutii amri ya ‘kuwahubiri watu na kutoa ushahidi kamili.’ (Mdo. 1:8; 10:42) Basi, ijapokuwa ni kweli kwamba twahitaji roho ya Mungu ili itutie nguvu tuhubiri, pia ni kweli kwamba tunapoanza kuonyesha tamaa yetu ya kumpendeza Yehova, yeye huandaa msaada zaidi. Tusipuuze kamwe umuhimu wa kuchukua hatua hizo za kwanza za kutii!
8 Kusaidia Wachanga: Wazazi, je, watoto wenu wanaonyesha hamu ya kuongea na wengine kuhusu kweli? Je, wamekuwa wakiandamana nanyi kwenye utumishi wa shambani? Je, wao ni vielelezo bora katika mwenendo wao? Ikiwa ndivyo, kwa nini ukawie? Mwendee mmojawapo wa ndugu wa Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko, uone kama mtoto wako anastahili kuwa mhubiri mwezi wa Aprili. (Ona kitabu Huduma Yetu, ukurasa wa 99-100.) Msisahau kwamba watoto wenu wanaweza kuchangia kwa njia kubwa sifa kwa Yehova majira haya ya Ukumbusho.—Mt. 21:15, 16.
9 Mama mmoja Mkristo huko Georgia, Marekani, sikuzote alimtia moyo binti yake mchanga aongee na wengine juu ya Yehova. Mwaka jana msichana huyo alipokuwa katika huduma pamoja na mama yake, alimwachia mwanamume mmoja broshua Anataka na akamweleza kifupi yaliyomo. Mwanamume huyo alimwuliza: “Una miaka mingapi?” Akasema: “Saba.” Mwanamume huyo alishangazwa na jinsi alivyoeleza habari waziwazi. Kumbe alikuwa ameshirikiana na Mashahidi tangu utotoni lakini hakuchukua hatua yoyote. Funzo la Biblia lilianzishwa pamoja na mwanamume huyo, mke wake, na binti yake.
10 Vijana wengi tayari ni wahubiri, na sisi hufurahia kuhubiri pamoja nao shambani. Vijana hao wanaweza kuwachochea marika zao. Isitoshe, mwezi wa Aprili waweza kuwa wakati wa washiriki wa familia kuimarisha uhusiano wao na kujenga hali yao ya kiroho wanapokuwa kwenye utumishi mtakatifu pamoja. Vichwa vya familia wapaswa kuongoza katika jambo hilo.—Mit. 24:27.
11 Kusaidia Wapya: Vipi wapya ambao tunajifunza Biblia pamoja nao? Je, wanaweza kuchangia utendaji wa pekee katika Aprili? Labda walionyesha hamu ya kusema na wengine kuhusu mambo ambayo wamejifunza mlipokuwa mkisoma sura ya 2, fungu la 22, au sura ya 11, fungu la 14, katika kitabu Ujuzi. Iwapo mwaelekea kumaliza kitabu hicho, zungumzia jambo hilo waziwazi mnaposoma sura ya 18, fungu la 8, linalosema: “Labda una hamu ya kuwaambia watu wako wa ukoo, rafiki zako, na wengine juu ya yale unayojifunza. Kwa kweli, huenda ukawa umekuwa ukifanya hivyo tayari, sawa na vile Yesu alivyoshiriki habari njema na wengine katika hali zisizo rasmi. (Luka 10:38, 39; Yn. 4:6-15) Sasa huenda ukataka kufanya zaidi.” Je, watu unaojifunza nao wana hamu iyo hiyo?
12 Je, mwanafunzi wako anaamini Neno la Mungu? Je, anafuata kanuni za Biblia katika maisha yake? Je, amerekebisha maisha yake kupatana na kanuni za kimungu? Amekuwa akihudhuria mikutano ya kutaniko? Je, ana tamaa ya kumtumikia Yehova Mungu? Basi, kwa nini usimtie moyo aseme na wazee ili waone kama ataweza kustahili kuwa mhubiri asiyebatizwa na kushiriki katika utumishi pamoja nawe katika Aprili? (Ona kitabu Huduma Yetu, ukurasa wa 97-99.) Kwa njia hiyo ataweza kujionea kibinafsi jinsi tengenezo la Yehova liwezavyo kumtegemeza anapojitahidi kumtumikia Yehova.
13 Ni kweli kwamba baadhi ya wanafunzi hufanya maendeleo haraka kuliko wengine. Kwa hivyo, kupatana na mwongozo katika Huduma Yetu ya Ufalme ya Juni 2000, ukurasa wa 4, fungu la 5-6, wahubiri wengi wameendeleza funzo wakitumia kitabu cha pili na watu ambao wanahitaji msaada wa ziada ili wafanye maendeleo. Bado tunatumaini kwamba hatimaye watu hao wanyofu watakuwa wanafunzi halisi wa Kristo iwe itawachukua ‘muda mfupi au muda mrefu.’ (Mdo. 26:29) Hata hivyo, ikiwa mwanafunzi huyo amekuwa akijifunza kwa “muda mrefu,” je, ataweza kuonyesha kina cha uthamini wake kwa fidia ya Kristo wakati wa majira haya ya Ukumbusho?
14 Jinsi ya Kuwasaidia Washiriki: Tunajifunza jinsi ya kuwasaidia wengine kustahili kuwa wahubiri kwa kuchunguza namna Yesu alivyowazoeza wengine. Hakuwaleta mitume mbele ya umati wa watu na kuwaagiza waseme nao. Alianza kwa kukazia umuhimu wa kuhubiri, akawatia moyo kusali, kisha akawaandalia mambo matatu ya msingi: mwenzi wa kuambatana nao, eneo la kuhubiri, na ujumbe. (Mt. 9:35-38; 10:5-7; Mk. 6:7; Luka 9:2, 6) Waweza kufanya vivyo hivyo. Iwe unamsaidia mtoto wako, mwanafunzi mpya, au mtu ambaye hajaripoti utumishi kwa muda fulani inafaa kuzingatia mambo yafuatayo.
15 Kazia Umuhimu: Onyesha mtu huyo umuhimu wa kazi ya kuhubiri. Uwe mchangamfu unapomweleza jambo hilo. Simulia mambo yaliyoonwa kuonyesha yale ambayo kutaniko linatimiza katika huduma. Onyesha roho inayoelezwa na Yesu katika Mathayo 9:36-38. Mtie moyo mtu anayetaka kuwa mhubiri au mhubiri asiyetenda asali kuhusu kushiriki kwake utumishini na pia kufanikiwa kwa kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote.
16 Mtie Moyo Mtu Huyo Kufikiri Juu ya Fursa za Kutoa Ushuhuda: Mjulishe kwamba anaweza kujiunga na kikundi cha funzo la kitabu kwa ajili ya utumishi wa nyumba kwa nyumba. Mtie moyo awahubirie watu wa ukoo na marafiki au wafanyakazi au wanashule wenzake wakati wa mapumziko. Tunaposafiri tunaweza kuanzisha mazungumzo kwa kuwajulia hali abiria wenzetu. Mara nyingi kuanzisha mazungumzo hutokeza fursa za kutoa ushuhuda. Kwa kweli, kuna fursa nyingi za kushiriki na wengine tumaini letu “siku kwa siku.”—Zab. 96:2, 3.
17 Hata hivyo, usikawie kwenda nyumba kwa nyumba pamoja na mhubiri mpya. Ikiwa umeweka mradi wa kuongeza utumishi wako mwezi wa Aprili, muulize ndugu anayetunza maeneo kama kuna eneo la karibu. Iwapo liko, basi itakuwa rahisi kupata fursa ya kulihubiri kikamili. Kwa mfano, unapoondoka kwenye eneo ukielekea mikutanoni au mahali penginepo, huenda ukaona kwamba kuna mtu katika nyumba ambayo wenyewe hawakuwapo ulipohubiri sehemu hiyo au ambayo mtu alionyesha kupendezwa. Iwezekanapo, fanya ziara fupi wakati unaofaa. Hilo litakufanya uhisi umetimiza jambo fulani katika utumishi na utakuwa mwenye shangwe.
18 Tayarisha Habari Yenye Kuvutia: Mtu aweza kuwa na tamaa ya kushiriki habari za Ufalme lakini asiwe na ujasiri wa kusema, hasa ikiwa ni mpya au amekuwa asiyetenda kwa muda mrefu. Tutakuwa tumetumia wakati wetu ifaavyo tunapowasaidia wapya au wasiotenda kujitayarisha. Mikutano ya Utumishi na mikutano kwa ajili ya utumishi wa shambani inaweza kuandaa madokezo, lakini bado kuna uhitaji wa mtu kujitayarisha.
19 Unawezaje kutayarisha wapya kwa ajili ya utumishi? Anza na utumishi wa kutoa magazeti, na fanya utoaji huo uwe mfupi na sahili! Waombe wafikirie matukio yaliyozungumziwa katika vyombo vya habari ambayo yanahangaisha watu katika eneo, kisha tafuta habari inayozungumzia matukio hayo katika mojawapo ya magazeti ya karibuni. Fanyieni utoaji huo mazoezi pamoja na kuutumia bila kukawia.
20 Sitawisha Msingi wa Ukuzi wa Wakati Ujao: Watu zaidi ya milioni 14.8 walihudhuria Ukumbusho mwaka jana. Wahubiri walioripoti walizidi kidogo watu milioni sita. Hiyo inamaanisha kwamba watu milioni 8.8 hivi wenye kupendezwa walifika kwenye mkutano huo wa pekee na kusikiliza mojawapo ya mafundisho muhimu ya Biblia yakifafanuliwa. Walifahamiana na wengine wetu na huenda walivutiwa sana. Wengi wa watu hao hutusifu sana, hutoa michango yao kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote, na hututetea mbele ya wengine. Kundi hilo kubwa linaonyesha uwezekano wa ongezeko wakati ujao. Twaweza kufanya nini ili kuwasaidia wafanye maendeleo?
21 Idadi kubwa ya wapya hufika kwenye Ukumbusho kwa sababu walialikwa na mmoja wetu. Kwa kawaida, wanajua angalau mtu mmoja miongoni mwa watu wanaohudhuria. Ikiwa mtu amefika kwa sababu tulimwalika, tuna daraka la kufanya astarehe na kumsaidia afaidike kabisa na programu hiyo. Kwa sababu kutakuwa na watu wengi, msaidie kupata kiti. Mpe Biblia na shiriki pamoja naye kitabu cha wimbo. Jibu maswali yoyote atakayouliza. Kumshughulikia hivyo kwa uchangamfu kwaweza kuchochea upendezi wake. Bila shaka, kila mmoja wetu ana daraka hilo—umwonapo mgeni, msalimu kwa uchangamfu na useme naye kifupi ili kufahamiana naye.
22 Kuhudhuria Ukumbusho kwaweza kugusa moyo wa mtu sana. Kufika kwake kwenye mkutano huo kwaonyesha kwamba hajapata anachotafuta mahali penginepo na kwamba tuna habari ambayo anahisi anapaswa kuchunguza kwa uangalifu zaidi. Maelezo juu ya uandalizi ajabu wa fidia huenda yakawa mambo mapya kwa mtu asiyefahamu upendo wa Yehova usio na kifani. Huenda akatambua upesi kwamba sisi ni tofauti—wanyofu, wenye urafiki, wenye upendo, na wenye kustahi wengine. Majumba yetu ni tofauti na makanisa yaliyo na sanamu na desturi nyingi zisizo za maana. Kwa hakika, wapya wataweza kuona kwamba wahudhuriaji wanatoka katika tabaka zote na kwamba hakuna sadaka zinazokusanywa. Jambo hilo huenda likachochea sana tamaa yao ya kutaka kuja tena.
23 Baada ya Ukumbusho, inafaa kupanga kuwatembelea wapya waliohudhuria ili kutoa msaada zaidi. Ikiwa ulimwalika mtu yeyote mpya, una wajibu huo. Wajulishe kuhusu mikutano mingine kwenye Jumba la Ufalme kabla hawajaondoka. Taja kichwa cha hotuba ya watu wote ya juma linalofuata. Wajulishe kuhusu saa na mahali pa Funzo la Kitabu la Kutaniko lililo karibu na makazi yao. Baadaye, wapelekee kitabu Muumba, na uwajulishe kwamba sehemu itakayozungumziwa juma la Aprili 30 ni “Unaweza Kujifunza Nini Juu ya Muumba Katika Kitabu?” Eleza mtu huyo kwa nini kutaniko zima linapanga kuhudhuria hivi karibuni kusanyiko la wilaya lililoratibiwa.
24 Panga ziara ya kirafiki nyumbani mwao. Hakikisha wanapata nakala zao wenyewe za broshua Anataka na kitabu Ujuzi, ili wapate kufahamu mafundisho ya msingi ya Biblia. Ikiwa bado hawajaanza kujifunza, wajulishe mpango wa funzo la Biblia. Dokeza wasome broshua Mashahidi wa Yehova—Wao Ni Nani? Wanaamini Nini? inayoeleza wazi namna tengenezo letu linavyofanya kazi. Waonyeshe vidio zetu, kama vile Our Whole Association of Brothers. Wajulishe kwa wengine kutanikoni. Katika miezi inayofuata, endelea kuwatembelea wapya hao, waalike kwenye mikutano mwangalizi wa mzunguko anapozuru, au kwenye kusanyiko la mzunguko au la siku ya pekee. Wape fursa ya kuonyesha kwamba wana “mwelekeo ufaao kwa ajili ya uhai udumuo milele”!—Mdo. 13:48.
25 Lile Wazee Wawezalo Kufanya: Kufanikiwa kwa mradi huu wa kupanua utumishi katika Aprili kwategemea hasa wazee. Ikiwa wewe ni kiongozi wa funzo la kitabu, orodhesha mambo uwezayo kufanya ili kusaidia kila mmoja katika funzo lako ashiriki katika utendaji huu maalum. Je, kuna wachanga, wapya, wasio wa kawaida shambani au wasiotenda katika funzo lako la kitabu? Chunguza uone kama wazazi, mapainia au wahubiri wamechukua hatua za kuwasaidia. Andaa msaada wowote wa kibinafsi uwezao kutoa. Dada mmoja aliyekuwa asiye wa kawaida kwenye utumishi kwa miaka miwili, alihubiri saa 50 katika Aprili mwaka jana. Alichochewa na nini? Alisema alichochewa na ziara za uchungaji zilizofanywa na wazee.
26 Wazee na watumishi wa huduma wanapaswa kuhakikisha kwamba kuna eneo, magazeti, na vichapo vya kutosha mwezi huo. Je, mikutano ya ziada kwa ajili ya utumishi wa shambani yaweza kupangwa? Ikiwa ndivyo, julisheni kutaniko mipango hiyo maalum. Zaidi ya mambo yote, katika sala zenu za hadharani na za kibinafsi ombeni Yehova abariki mwezi huu wenye shughuli nyingi ya Ufalme.—Rom. 15:30, 31; 2 The. 3:1.
27 Katika kutaniko moja huko North Carolina, wazee walitia wengine moyo sana waongeze utumishi wao katika Aprili mwaka jana. Kwenye mikutano ya kila juma walisihi wahubiri wafikirie kwa sala uwezekano wa kuwa mapainia-wasaidizi. Wazee na watumishi wa huduma walitumia kila fursa kuchochea wengine kwa uchangamfu kufanya Aprili kuwa mwezi wa utendaji mwingi kupita mwezi mwingine wowote. Tokeo likawa kwamba, asilimia 58 ya wahubiri, kutia ndani wazee na watumishi wote wa huduma walikuwa mapainia-wasaidizi mwezi huo!
28 Shangwe ya Kushiriki Kikamili: Tunapata baraka zipi kwa ‘kufanya kazi kwa bidii na kujikakamua wenyewe’ katika huduma? (1 Tim. 4:10) Kuhusu utumishi wenye bidii katika kutaniko lao mwezi wa Aprili mwaka uliopita, wazee hao wa North Carolina waliandika hivi: “Mara nyingi, ndugu na dada husema kwamba upendo na urafiki umeongezeka zaidi miongoni mwao tangu waongeze huduma yao ya shambani.”
29 Ndugu mmoja mlemavu alitaka kushiriki katika utendaji maalum mwezi wa Aprili mwaka jana. Alipanga mambo yake kwa uangalifu na kwa msaada wa mama yake na ndugu na dada kutanikoni, aliweza kuwa painia msaidizi mwenye matokeo. Alihisije? Alisema hivi: “Kwa mara ya kwanza katika maisha yangu, nilihisi kama mtu asiye mlemavu.”
30 Kwa wazi, Yehova hubariki sana wote wenye kuthamini pendeleo lao la kusema juu ya ufalme wake. (Zab. 145:11, 12) Ukumbusho wa kifo cha Bwana wetu hutukumbusha kwamba baraka za ujitoaji kimungu zitaongezeka hata zaidi wakati ujao. Mtume Paulo alitarajia kwa hamu nyingi thawabu ya uhai udumuo milele. Hata hivyo, alijua kwamba hawezi kuketi kitako na kutarajia thawabu hiyo. Aliandika hivi: “Kwa madhumuni haya kwa kweli ninafanya kazi kwa bidii, nikijikakamua mwenyewe kwa kupatana na utendaji wake na unaofanya kazi ndani yangu kwa nguvu.” (Kol. 1:29) Yehova, kupitia Yesu, alimtia nguvu Paulo atimize utumishi wenye kuokoa uhai. Leo, Anaweza kututia nguvu pia. Je, itakuwa hivyo kwako mwezi wa Aprili?
[Sanduku katika ukurasa wa 3]
Utatia Nani Moyo Awe Mhubiri Mwezi wa Aprili?
Mtoto wako?
Mwanafunzi wa Biblia?
Mtu asiyetenda?