Je, Mtoto Wako Aende Shule ya Bweni?
WAZIA kwamba unaishi katika mji mdogo katika nchi inayositawi. Una watoto kadhaa katika shule ya msingi, lakini wafikapo umri wa miaka 12, wataendelea na kuingia shule ya sekondari. Katika eneo lako, shule za sekondari zina watoto wengi sana, hazina vifaa vinavyohitajiwa, na hazina walimu wa kutosha au waliozoezwa vizuri. Nyakati nyingine migomo hufanya shule hizo zifungwe kwa majuma kadhaa na kwa miezi kadhaa nyakati fulani.
Mtu fulani akupa broshua yenye kupendeza inayofafanua shule ya bweni jijini. Waona picha za wanafunzi wenye furaha, waliovaa vizuri, wakijifunza madarasani, maabara, na maktaba yenye vifaa vya kutosha. Hao wanafunzi wanatumia kompyuta na kupumzika katika vyumba safi na vyenye kuvutia vya bweni. Wasoma katika broshua hiyo kwamba mojawapo ya makusudi ya shule hiyo ni kuwasaidia wanafunzi “kufikia kiwango cha juu zaidi cha kitaaluma wawezacho kukifikia.” Waendelea kusoma hivi: “Wanafunzi wote wanahitajiwa kutii kanuni za mwenendo sawa na zile zinazotarajiwa katika familia ambamo hisani, adabu, staha kwa wazazi na wazee, ushirikiano, ustahimilivu, fadhili, ufuatiaji wa haki, na uaminifu-maadili hukaziwa.”
Kijana anayetabasamu ananukuliwa kuwa akisema hivi: “Wazazi wangu walinipa pendeleo kubwa sana la kuhudhuria shule bora zaidi.” Msichana mmoja asema hivi: “Shule ni yenye kuvutia na kusisimua. Shule hii yafaa kwa ajili ya kujifunza.” Je, ungempeleka mwana au binti yako kwenye shule ya bweni kama hiyo?
Elimu na Hali ya Kiroho
Wazazi wote wenye kujali wanataka kuwapa watoto wao mwanzo mzuri maishani, na ili kufanya hivyo, elimu ya kikamili na iliyosawazika ni muhimu. Mara nyingi elimu ya kilimwengu hutokeza fursa za kazi ya kuajiriwa ya wakati ujao na husaidia vijana wakue na kuwa watu wazima wawezao kujitunza wenyewe na familia zao za wakati ujao.
‘Ikiwa shule ya bweni hutoa elimu nzuri pamoja na mwongozo fulani wa kimaadili, mbona tusijifaidi nayo?’ huenda ukauliza. Ili kujibu swali hilo, wazazi Wakristo wanapaswa kufikiria kwa sala jambo lenye umaana mkubwa—hali njema ya kiroho ya watoto wao. Yesu Kristo aliuliza hivi: “Kwa kweli, ina manufaa gani kwa mtu kupata faida ya kuwa na ulimwengu wote na kupoteza nafsi yake?” (Marko 8:36) Bila shaka, hakuna manufaa yoyote katika hilo. Kwa hiyo, kabla ya kuamua kuwapeleka watoto wao kwenye shule ya bweni, wazazi Wakristo wanapaswa kufikiria jinsi kufanya hivyo kwaweza kuathiri matazamio ya watoto wao ya kupata uhai udumuo milele.
Uvutano wa Wanafunzi Wengine
Huenda shule fulani za bweni zikawa na viwango vyenye kupendeza vya kitaaluma. Lakini vipi juu ya viwango vya kiadili vya wale wanaohudhuria au labda hata ya baadhi ya wale wanaoendesha shule hizo? Kuhusu aina ya watu ambao wangekuwapo kwa wingi katika “siku [hizi] za mwisho,” mtume Paulo aliandika hivi: “Katika siku za mwisho nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo zitakuwa hapa. Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wapenda-fedha, wenye kujitanguliza, wenye kiburi, wakufuru, wasiotii wazazi, wasio na shukrani, wasio waaminifu-washikamanifu, wasio na shauku ya kiasili, wasiotaka upatano wowote, wachongezi, wasio na hali ya kujidhibiti, wakali, wasio na upendo wa wema, wasaliti, wenye vichwa vigumu, wenye kututumuka kwa kiburi, wenye kuzipenda raha badala ya kuwa wapenda-Mungu, wakiwa na namna ya ujitoaji-kimungu lakini wakithibitika kuwa si kweli kwa nguvu ya hiyo; na geukia mbali kutoka kwa hawa.”—2 Timotheo 3:1-5.
Kushuka huko kwa maadili na hali ya kiroho kuko tufeni pote, kukiwatolea Mashahidi wa Yehova ushindani katika kuishi kulingana na kanuni za Biblia. Wanafunzi wanaorudi nyumbani kila siku huona kwamba hata ushirika wao mdogo pamoja na wanashule wenzao walio walimwengu waweza kutokeza uvutano usiofaa wenye nguvu juu ya hali yao ya kiroho. Kukinza uvutano huo kwaweza kuwa ushindani kwelikweli kwa watoto Mashahidi, hata wakiwa na utegemezo, shauri, na kitia-moyo cha kila siku kutoka kwa wazazi wao.
Hivyo, basi, hali ya watoto wanaoondoshwa nyumbani na kupelekwa kwenye shule za bweni ikoje? Wameachwa peke yao, wakiwa wametengwa mbali na utegemezo wa kiroho wa kawaida wa wazazi wenye upendo. Kwa kuwa wanaishi na wanadarasa wenzao muda wa saa 24 kwa siku, msongo wa kujipatanisha na umati huwa na uvutano mkubwa zaidi juu ya akili zao na mioyo yao michanga kuliko uelekeavyo kuwa nao juu ya wanafunzi wanaoishi nyumbani. Mwanafunzi mmoja alisema hivi: “Kiadili, mwanafunzi wa shule ya bweni anaishi katika hatari tangu asubuhi hadi usiku.”
Paulo aliandika hivi: “Msiongozwe vibaya. Mashirika mabaya huharibu mazoea yenye mafaa.” (1 Wakorintho 15:33) Wazazi Wakristo hawapasi kuongozwa vibaya wafikiri kwamba watoto wao hawatapata madhara yoyote ya kiroho ikiwa wanashirikiana wakati wote na wale wasiomtumikia Mungu. Baada ya kipindi fulani cha wakati, watoto wa kimungu wanaweza kufanywa sugu kuelekea kanuni za Kikristo na wanaweza kupoteza uthamini wote kuelekea mambo ya kiroho. Nyakati nyingine hilo haliwi dhahiri kwa wazazi mpaka baada ya watoto kuondoka katika shule ya bweni. Mara nyingi wakati huo huwa ni kuchelewa mno kurekebisha mambo.
Kisa cha Clement ni mfano halisi. Yeye aeleza hivi: “Kabla ya kwenda shule ya bweni, niliipenda kweli na nilikwenda katika huduma ya shambani pamoja na akina ndugu. Nilifurahia hasa kushiriki katika funzo letu la Biblia la familia na Funzo la Kitabu la Kutaniko. Hata hivyo, mara nilipoenda kwenye shule ya bweni nikiwa na umri wa miaka 14, niliiacha kweli kabisa. Miaka yote mitano niliyokuwa katika shule ya bweni, sikuhudhuria mikutano. Tokeo la ushirika mbaya ni kwamba, nilihusika katika kutumia dawa za kulevya, kuvuta sigareti, na kunywa sana.”
Uvutano wa Walimu
Katika shule yoyote kwaweza kuwa na walimu waliofisidika kiadili wanaotumia vibaya wadhifa wao wenye mamlaka. Baadhi yao ni wakatili na wenye kudhulumu, hali wengine huwatumia wanafunzi wao kwa faida ya kingono. Katika shule za bweni ni yamkini sana kwa matendo ya walimu hao kutoripotiwa.
Hata hivyo, walimu walio wengi hujaribu kwa moyo mweupe kuwazoeza watoto wawe washiriki wenye matokeo wa jamii, wawe sehemu ya ulimwengu unaowazunguka, wajipatanishe. Lakini humo mna tatizo lingine kwa watoto Mashahidi. Viwango vya ulimwengu havisadifiani sikuzote na kanuni za Kikristo. Huku walimu wakiwatia moyo wanafunzi wawe sehemu ya ulimwengu, Yesu alisema kwamba wafuasi wake wangekuwa “si sehemu ya ulimwengu.”—Yohana 17:16.
Vipi ikiwa matatizo yanazuka wakati watoto wanapofuata kanuni za Biblia? Ikiwa watoto hao wanaenda shule ya karibu nao wanaishi nyumbani, wanaweza kuzungumza mambo hayo pamoja na wazazi wao. Nao wazazi wanaweza kuwaongoza watoto wao na labda hata wazungumze na mwalimu. Tokeo ni kwamba, mara nyingi matatizo na kutoelewana yanasuluhishwa upesi.
Katika shule za bweni hali ni tofauti. Wanafunzi hao wako chini ya uongozi wenye kuendelea wa walimu wao. Watoto wakichukua msimamo kwa ajili ya kanuni za Kikristo, lazima wafanye hilo bila utegemezo wa kila siku wa wazazi wao. Nyakati nyingine, watoto wanafaulu kubaki wakiwa waaminifu kwa Mungu chini ya hali kama hizo. Hata hivyo, mara nyingi zaidi, hawafanyi hivyo. Yamkini mtoto atakubaliana na mapenzi ya mwalimu.
Miendo Yenye Mipaka
Tofauti na vyuo vikuu, ambamo kwa kawaida wanafunzi huwa na uhuru wa kuingia na kutoka wapendavyo, shule za bweni huwekea mipaka miendo ya watoto. Nyingi za shule hizo haziwaruhusu wanafunzi kuondoka kwenye uwanja wa shule ila Jumapili tu, na shule nyingine hata haziruhusu hilo. Mwanafunzi wa shule ya bweni mwenye umri wa miaka 11 aitwaye Eru asema hivi: “Wenye mamlaka wa shule hawaturuhusu kamwe kwenda kwenye mikutano yetu, sembuse katika utumishi wa shambani. Shuleni, kuna ibada kwa ajili ya Wakatoliki na Waislamu tu. Kila mwanafunzi lazima achague mojawapo ya dini hizo mbili au akabili upinzani mkali kutoka kwa walimu na pia wanafunzi. Pia wanafunzi wanalazimishwa kuimba wimbo wa taifa na nyimbo za kanisa.”
Wazazi wanapowaandikisha watoto wao katika shule kama hiyo, wanawatolea vijana wao ujumbe gani? Huo ujumbe waweza kuwa kwamba elimu ya kilimwengu ni yenye maana kuliko kukusanyika kwa ajili ya ibada na kushiriki katika kazi ya kufanya wanafunzi—hata ni yenye maana kuliko uaminifu-maadili kwa Mungu.—Mathayo 24:14; 28:19, 20; 2 Wakorintho 6:14-18; Waebrania 10:24, 25.
Katika shule za bweni fulani, wanafunzi Mashahidi wanafaulu kujifunza Biblia pamoja, lakini hata hilo mara nyingi huwa jambo gumu. Kijana anayeitwa Blessing, mwenye umri wa miaka 16, asema hivi juu ya shule ya bweni anakoenda: “Kila siku wenye kuitwa kwa kawaida Wakristo hukusanyika ili kusali. Sisi Mashahidi hujaribu kuwasihi ili tuweze kuwa na funzo letu, lakini wanafunzi wa vidato vya juu wanatuambia kwamba tengenezo letu halitambuliwi. Kisha wanajaribu kutulazimisha tusali nao. Tukikataa, wanatuadhibu. Kukata rufani kwa walimu hufanya mambo yawe mabaya zaidi. Wanatutukana na kuwaambia wanafunzi wa vidato vya juu watuadhibu.”
Kutokeza Tukiwa Tofauti
Wanafunzi wa shule ya bweni wajulikanapo waziwazi kuwa Mashahidi wa Yehova, hilo laweza kuwa na faida kwao. Wenye mamlaka wa shule waweza kuwaruhusu wasishiriki katika utendaji mbalimbali wa lazima wa dini zisizo za kweli, unaopingana na imani ya Mashahidi. Huenda wanafunzi wenzao wakaepuka kujaribu kuwahusisha katika utendaji na mazungumzo yasiyofaa. Huenda kukawa na fursa za kutoa ushahidi kwa wanafunzi wenzao na walimu. Zaidi ya hayo, wale wanaoishi kulingana na kanuni za Kikristo hawaelekei kushukiwa ukosaji mzito, na nyakati nyingine wanajishindia staha ya walimu na wanafunzi wenzao.
Hata hivyo, mambo hayawi hivyo sikuzote. Kijana kutokeza akiwa tofauti humfanya anyanyaswe na kudhihakiwa na wanafunzi na vilevile walimu. Yinka, mvulana mwenye umri wa miaka 15 aendaye shule ya bweni, asema hivi: “Shuleni, ukijulikana kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova unakuwa lengo. Kwa kuwa wanajua msimamo wetu wa kiroho na kiadili, wanaweka mitego ya kutunasa.”
Daraka la Wazazi
Hakuna mwalimu, shule, au chuo, awezaye kwa kufaa kujaribu kuchukua kazi ya kuwalea watoto wawe watumishi waliojiweka wakfu wa Yehova. Hiyo si kazi yao wala daraka lao. Neno la Mungu laelekeza kwamba wazazi wenyewe wanapaswa kushughulikia mahitaji ya kiroho ya watoto wao. Paulo aliandika hivi: “Nanyi, akina baba, msiwe mkiwasumbua watoto wenu, bali endeleeni kuwalea katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.” (Waefeso 6:4) Wazazi wanaweza kutumiaje shauri hilo la kimungu ikiwa watoto wao wako mbali katika shule ya bweni ambako kuzuru kwaweza kuwekewa mipaka hadi mara moja au mbili kwa mwezi?
Hali hutofautiana sana, lakini wazazi Wakristo hujitahidi kutenda kulingana na taarifa hii iliyopuliziwa: “Hakika ikiwa yeyote hawaandalii kitu wale walio wake mwenyewe, na hasa kwa ajili ya wale walio washiriki wa nyumbani mwake, ameikana imani naye ni mbaya zaidi kuliko mtu asiye na imani.”—1 Timotheo 5:8.
Je, Kuna Mambo Badala?
Wazazi waweza kufanya nini wakionekana kuwa na machaguo mawili tu—shule ya bweni au shule ya karibu isiyo na vifaa vya kutosha? Wazazi fulani ambao wamejikuta katika hali hiyo hupangia masomo ya nyumbani ili kuongezea elimu ya watoto kwenye shule ya karibu. Wazazi wengine huweka kando wakati wa kuwafundisha watoto wao wenyewe.
Nyakati nyingine wazazi huepuka matatizo kwa kupanga mapema vya kutosha kabla ya watoto wao kufikia umri wa kutosha kuingia shule ya sekondari. Ikiwa una watoto wachanga au unapanga kuwa na familia, waweza kuchunguza na kuona ikiwa kuna shule ya sekondari ifaayo katika eneo lako. Ikiwa hakuna, huenda ikawezekana kuhamia karibu zaidi na moja.
Kama wazazi wajuavyo vema, kukaza kikiki katika mtoto upendo kwa ajili ya Yehova, kwahitaji ustadi, subira, na wakati mwingi. Ikiwa hilo ni jambo gumu mtoto anapoishi nyumbani, jinsi litakavyokuwa gumu hata zaidi ikiwa mtoto huyo anakaa mbali! Kwa kuwa uhai udumuo milele wa mtoto unahusika, wazazi wanapaswa kuamua kwa uzito na kwa sala ikiwa kumpeleka kijana wao kwa shule ya bweni kwastahili hatari ya kufanya hivyo. Kungekuwa kutofikiri mbele kama nini kudhabihu masilahi ya kiroho ya mtoto kwa ajili ya manufaa ya elimu ya shule ya bweni! Kufanya hivyo kungekuwa sawa na kuingia haraka ndani ya nyumba inayochomeka ili kuokoa kipambo kidogo kizuri—kisha kuangamizwa katika miali ya moto.
Neno la Mungu husema hivi: “Mwenye busara huyaona mabaya na kujificha; bali wajinga huendelea mbele wakaumia.” (Mithali 22:3) Ni afadhali kuzuia hali mbaya kuliko kurekebisha moja baadaye. Lingekuwa jambo la hekima kufikiria hilo ukijiuliza, ‘Je, mtoto wangu aende shule ya bweni?’
[Sanduku katika ukurasa wa 28]
MASHAHIDI VIJANA WAELEZA JUU YA SHULE YA BWENI
“Kwenye shule ya bweni, watoto Mashahidi wametengwa mbali na ushirika wa kiroho. Ni mazingira yenye uhasama sana yenye msongo mwingi sana wa kufanya makosa.”—Rotimi, aliyeenda shule ya bweni akiwa na umri wa miaka kati ya 11 na 14.
“Kuhudhuria mikutano ya Kikristo kulikuwa kugumu hasa. Ningeweza kuhudhuria Jumapili tu, na ili kufanya hilo, nililazimika kutoroka huku wanafunzi walipokuwa wakipanga laini ili waingie kanisani. Sikuwa mwenye furaha kamwe, kwa kuwa nyumbani nilikuwa nimezoea kuhudhuria mikutano yote ya kutaniko, na nilienda kwenye huduma ya shambani siku za Jumamosi na Jumapili. Shule haikuwa jambo lenye kujenga. Nilikosa mengi sana.”—Esther, aliyechapwa viboko na walimu tena na tena kwa sababu alikataa kushiriki katika ibada za kanisa za shule.
“Kutolea wanafunzi wenzangu ushahidi hakukuwa rahisi katika shule ya bweni. Si rahisi kutokeza ukiwa tofauti. Nilitaka kufuata kikundi. Labda ningalikuwa na ujasiri zaidi ikiwa ningaliweza kwenda mikutanoni na kushiriki katika utumishi wa shambani. Lakini niliweza kufanya hivyo nilipokuwa likizoni tu, iliyokuwa mara tatu tu kwa mwaka. Ukiwa na taa isiyojazwa upya mafuta, nuru husinzia. Ndivyo ilivyokuwa shuleni.”—Lara, aliyeenda shule ya bweni akiwa na umri wa kuanzia miaka 11 hadi 16.
“Kwa kuwa sasa siko katika shule ya bweni tena, ninafurahi kwamba naweza kuhudhuria mikutano yote, kushiriki katika huduma ya shambani, na kufurahia andiko la kila siku pamoja na wengine wa familia. Ingawa kukaa shuleni kulikuwa na faida fulani, hakuna lolote lililo muhimu zaidi ya uhusiano wangu na Yehova.”—Naomi, aliyemsadikisha baba yake amwondoe katika shule ya bweni.