Wasaidie Wale Ambao kwa Sasa Hawako Tayari Kujifunza Kitabu Biblia Inafundisha
1. Je, kitabu Biblia Inafundisha kitawavutia watu wote mwanzoni? Eleza.
1 Ili mtu amwabudu Yehova ni lazima ajifunze yale ambayo Biblia inafundisha. Hata hivyo, kuna watu ambao si wa dini ya Kikristo na hawaamini kuwa Biblia ni Neno la Mungu. Wengine hawamwamini Mungu kabisa na hawaiheshimu Biblia. Ni machapisho gani ambayo yamewasaidia wale ambao mwanzoni hawakuwa tayari kujifunza kitabu Biblia Inafundisha? Yafuatayo ni mapendekezo yanayotegemea maelezo ya wahubiri kutoka katika nchi 20 hivi tofauti.
2. Ikiwa mtu fulani anasema hamwamini Mungu, tufanyeje na kwa nini?
2 Wale Ambao Hawaamini Mungu: Ikiwa mtu fulani anasema kwamba hamwamini Mungu, itafaa kujua sababu. Je, ni kwa sababu anaamini mageuzi? Je, amekosa imani kwa sababu ya ukosefu wa haki ulimwenguni au unafiki wa dini? Je, ametoka katika eneo ambalo watu hawaamini Mungu? Labda hapingi kishupavu kuwepo kwa Mungu, lakini hajawahi kuona uhitaji wa kumwamini Mungu. Wahubiri wengi wametambua kwamba kuuliza, “Je, umekuwa na maoni hayo nyakati zote?” kunamchochea mtu ajieleze. Msikilize bila kumkatisha. Tunapoelewa kwa nini mtu huyo hamwamini Mungu, tutajua jinsi ya kujibu na chapisho tunaloweza kumwachia.—Met. 18:13.
3. Tunawezaje kumheshimu mtu na mambo anayoamini?
3 Unapomjibu, uwe makini ili usimfanye mtu huyo ahisi kwamba unapinga maoni yake. Ona dokezo hili kutoka Marekani: “Ni muhimu sana kuheshimu uhuru wa mtu wa kuamua anachoamini. Badala ya kubishana, ni bora kuuliza maswali yatakayowachochea watu wafikiri na kufikia mkataa.” Baada ya kusikiliza maelezo ya mwenye nyumba, kwa kawaida mwangalizi mmoja anayesafiri hujibu kwa kuuliza hivi: “Je, umewahi kufikiria uwezekano wa jambo hili?”
4. Tunaweza kuwasaidiaje Wabudha?
4 Kwa Wabudha wengi wazo la kuwepo kwa Mungu ni geni. Wahubiri fulani nchini Uingereza wanapenda kutumia broshua Lasting Peace and Happiness—How to Find Them wanapowahubiria watu kama hao. Baada ya kuzungumzia sehemu ya utangulizi, wanazungumzia sehemu “Je, Kweli Kuna Muumba Aliye Juu Zaidi?” na sehemu “Kitabu cha Mwongozo Kilichokusudiwa Kuwabariki Watu Wote.” Baada ya hapo, wanaweza kumwonyesha mwenye nyumba kitabu Biblia Inafundisha na kumwambia, “Hata kama humwamini Mungu, kujifunza Biblia kuna manufaa kwa sababu ina mwongozo unaotegemeka.” Painia mmoja nchini Marekani anayehubiri eneo ambalo watu huzungumza Kichina anasema: “Watu wengi katika eneo letu wanapenda kusoma. Kwa hiyo wanasoma chapisho lote kabla hatujawarudia. Lakini huenda wasielewe umuhimu wa kujifunza Biblia. Kwa hiyo ninapenda kuwaachia broshua Habari Njema katika ziara ya kwanza kwa sababu imeandikwa kwa njia inayochochea mazungumzo.” Mwangalizi wa mzunguko anayetumika katika mzunguko wa lugha ya Kichina nchini Marekani anasema ni rahisi kutumia kitabu Biblia Inafundisha katika ziara ya kwanza. Hata hivyo, ingekuwa vizuri zaidi kuanzisha funzo kwenye sura ya 2, inayozungumzia Biblia yenyewe, badala ya sura ya 1, inayozungumzia kuhusu Mungu.
5. Kwa nini subira ni muhimu?
5 Inachukua muda ili mtu ajenge imani katika Mungu, hivyo ni muhimu kuwa na subira. Tunapoanza kuzungumza na mwenye nyumba huenda asikubali mara moja kwamba kuna Muumba. Hata hivyo, labda baada ya muda fulani kupita huenda ataona kwamba kuna Muumba, au anaweza kusema kwamba anaelewa ni kwa nini wengine wanaamini kuwepo kwa Mungu.
6. Kwa nini huenda watu fulani wasipendezwe na Biblia?
6 Wale Ambao Hawaipendi au Hawaitumaini Biblia: Mara nyingi, mtu anayekubali kwamba kuna uwezekano wa kuwepo kwa Mungu, huenda asipendezwe na yale ambayo Biblia hufundisha kwa sababu haamini kuwa Biblia ni Neno la Mungu. Labda anaishi eneo ambalo si la Kikristo na anahusianisha Biblia na dini zinazodai kuwa za Kikristo. Au huenda anaishi kwenye eneo linalodai kuwa la Kikristo na hivyo asione umuhimu wa Biblia katika maisha yake. Tunaweza kuwasaidiaje watu hao waipende Biblia hatua kwa hatua na hatimaye wakubali kujifunza kitabu Biblia Inafundisha?
7. Kwa kawaida ni njia gani nzuri ya kuwachochea watu waipende Biblia?
7 Ofisi ya tawi ya Ugiriki iliandika hivi: “Njia bora ya kuwasaidia watu wasiopendezwa na Biblia ni kuifungua na kuisoma. Wahubiri wengi wamegundua kwamba ujumbe wa Biblia unaathiri moyo wa mtu kwa kiwango kikubwa zaidi kuliko chochote kile tunachoweza kusema. (Ebr. 4:12) Kuona jina la Mungu katika Biblia kumewasaidia wengi wasitawishe tamaa ya kuichunguza Biblia.” Ofisi ya tawi nchini India iliandika hivi: “Ukweli kuhusu uhai na kifo na ahadi ya Biblia ya ulimwengu usio na ubaguzi wa matabaka, huwavutia sana watu wengi wa dini ya Kihindu.” Kuzungumzia matatizo yanayowakabili wakaaji mara nyingi huwapa wahubiri fursa za kuwaonyesha mambo ambayo Biblia husema yatatimizwa na Ufalme wa Mungu.
8. Tunaweza kuwaambia nini watu ambao kwa sababu ya dini zinazodai kuwa za Kikristo wana maoni yasiyofaa kuhusu Biblia?
8 Ikiwa kwa sababu ya dini zinazodai kuwa za Kikristo, mtu fulani ana maoni yasiyofaa kuhusu Biblia, unaweza kumweleza kwamba dini hizo hazifuati mafundisho ya Biblia. Ofisi ya tawi nchini India iliandika hivi: “Nyakati nyingine, tunahitaji kuwasaidia watu waone kwamba makanisa si wamiliki wa Biblia.” Ofisi hiyo ilisema kwamba mara nyingi Wahindu huvutiwa hasa na sehemu ya 4 ya broshua Ni Nini Lililo Kusudi la Uhai? Wewe Waweza Kulipataje?, inayoeleza jinsi makanisa yamejaribu kulitia Neno la Mungu unajisi na kuliharibu. Painia mmoja nchini Brazili huwaambia watu hivi: “Kwa nini usichunguze zaidi yaliyomo katika Biblia? Watu wengi wanafanya hivyo wakiwa na maoni yaliyosawazika, bila kulazimika kujihusisha na dini yoyote. Huenda ukastaajabishwa na mambo utakayojifunza.”
9. Kwa nini tusikate tamaa ikiwa mwanzoni watu hawapendezwi na yale ambayo Biblia inafundisha?
9 Yehova huuchunguza moyo wa kila mtu. (1 Sam. 16:7; Met. 21:2) Anawavuta wale wenye moyo mnyoofu kwenye ibada ya kweli. (Yoh. 6:44) Wengi wao hawakuwahi kufundishwa kuhusu Mungu au walikuwa na ujuzi mdogo tu wa Biblia. Huduma yetu inawapa fursa ya ‘kuokolewa na kupata ujuzi sahihi wa kweli.’ (1 Tim. 2:4) Kwa hiyo, ikiwa mwanzoni wengine hawapendezwi na yale ambayo Biblia hufundisha, usikate tamaa! Tumia machapisho yanayopatikana katika lugha yenu ili kuwachochea wapendezwe. Hatimaye, unaweza kumwelekeza kwenye kitabu chetu cha msingi cha kuongoza mafunzo ya Biblia, yaani kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?
[Sanduku katika ukurasa wa 4]
Ikiwa mwenye nyumba anasema hamwamini Mungu, unaweza kusema hivi:
• Ili kujua sababu muulize, “Je, sikuzote umekuwa na maoni hayo?”.
• Ikiwa ni Mbudha, tumia broshua Lasting Peace and Happiness—How to Find Them, ukurasa wa 9-12.
• Ikiwa anaamini mageuzi unaweza kutumia vifaa vifuatavyo:
Mfululizo wenye kichwa “Je, Ni Kazi ya Ubuni?” kwenye gazeti la Amkeni!
Video Maajabu ya Uumbaji Yanafunua Utukufu wa Mungu
Broshua zifuatazo: Jinsi ya Kupata Maisha Yenye Kuridhisha, sehemu ya 4; Uhai—Ulitokana na Muumba?; na Maswali Matano Muhimu Kuhusu Chanzo cha Uhai
• Ikiwa hamwamini Mungu kwa sababu ya ukosefu wa haki na kuteseka, machapisho haya yanaweza kumsaidia:
Kitabu Je, Kuna Muumba Anayekujali?, sura ya 10
Broshua zifuatazo: Je! Kweli Mungu Anatujali?, sehemu ya 6, na Ni Nini Lililo Kusudi la Uhai?, sehemu ya 6
•Mara tu mwenye nyumba anapokubali kwamba kuna Mungu mwelekeze kwenye kitabu Biblia Inafundisha. Huenda ikawa vizuri kuanza na sura ya 2 au somo lingine linalofaa hali zake.
[Sanduku katika ukurasa wa 5]
Ikiwa mwenye nyumba haamini Biblia unaweza:
• Kuzungumzia sura ya 17 na ya 18 ya kitabu Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation?
• Ukipata Wahindu, tumia broshua Why Should We Worship God in Love and Truth?
• Ukipata Wayahudi, tumia broshua Je! Ulimwengu Usio na Vita Utakuwako Wakati Wowote?, ukurasa wa 3-11.
• Zungumzia faida za kufuata kanuni za Biblia. Yafuatayo ni machapisho unayoweza kutumia kumwonyesha mtu faida ya kufuata kanuni za Biblia:
Mfululizo wenye kichwa “Msaada kwa Ajili ya Familia” kwenye gazeti la Amkeni!
Video The Bible—Its Power in Your Life
Broshua Habari Njema Kutoka kwa Mungu!, somo la 9 na 11; Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote, ukurasa wa 22-26; na Jinsi ya Kupata Maisha Yenye Kuridhisha, sehemu ya 2
Ukipata Wabudha, tumia broshua The Pathway to Peace and Happiness, ukurasa wa 3-7.
Ukipata Waislamu, tumia broshua Imani ya Kweli—Siri ya Kuwa na Maisha Yenye Furaha, sehemu ya 3.
Ikiwa unahubiri katika maeneo ambayo watu hawapendi Biblia, huenda ikafaa zaidi kutotaja chanzo cha maneno yenye hekima mnayozungumzia hadi tu baada ya kufanya ziara kadhaa.
• Eleza jinsi unabii wa Biblia umetimia. Unaweza kutumia vifaa vifuatavyo:
Video The Bible—Accurate History, Reliable Prophecy
Broshua Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote, ukurasa wa 27-29
• Mwelekeze kwenye kitabu Biblia Inafundisha mara tu anapouliza yale ambayo Biblia hufundisha.
[Sanduku katika ukurasa wa 6]
Ikiwa mwenye nyumba anasema: “Siamini kuwapo kwa Mungu” unaweza kusema:
• “Je, naweza kukueleza kwa ufupi jambo lililonisadikisha mimi niamini kwamba kuna Muumba?” Halafu unaweza kumwonyesha kitabu Kutoa Sababu ukurasa wa 390-392, au ufanye mpango wa kumletea kitabu ulichofurahia kusoma.
• “Lakini ikiwa kuna Mungu, ungependa awe na sifa gani?” Wenye nyumba wengi wangesema kwamba wangependa kuwa na uhusiano wa karibu na Mungu mwenye upendo, haki, rehema, na asiye na ubaguzi. Mwonyeshe kutoka kwenye Biblia kwamba Mungu ana sifa hizo. (Unaweza hata kutumia sura ya 1 ya kitabu Biblia Inafundisha, kuanzia fungu la 6.)
Ikiwa mwenye nyumba anasema: “Siamini Biblia” unaweza kusema:
• “Watu wengi wana maoni kama hayo. Wengine wanafikiri kwamba Biblia haipatani na sayansi au kwamba viwango vya Biblia haviwezi kutusaidia. Niambie, je, umewahi kusoma Biblia? [Mruhusu ajibu. Kisha mwonyeshe sehemu ya utangulizi katika ukurasa wa 3 wa broshua Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote, na kisha umwachie broshua hiyo.] Wengi hawaithamini Biblia kwa sababu dini hazifuati yale ambayo Biblia hufundisha. Wakati ujao ningependa tuzungumzie mfano ulio kwenye ukurasa wa 4 na 5.”
• “Watu wengi wana maoni kama yako. Je, ninaweza kukuonyesha jambo fulani linalonivutia kuhusu Biblia? [Soma Ayubu 26:7; au Isaya 40:22, maandiko yanayoonyesha kwamba Biblia ni sahihi kisayansi.] Biblia pia ina maneno yenye hekima yanayoweza kusaidia familia. Wakati ujao ningependa kukuonyesha mfano mmoja.”
• “Asante kwa habari hiyo. Ikiwa Mungu ameandika kitabu kwa ajili ya wanadamu, unafikiri kingekuwa na ujumbe gani?” Kisha mwonyeshe jambo fulani kutoka kwenye Biblia ambalo linaunga mkono maelezo yake.