Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ya 2015 Itatusaidia Kuboresha Ufundishaji Wetu
1 Mtunga zaburi Daudi aliandika hivi: “Maneno ya kinywa changu na kutafakari kwa moyo wangu na yawe yenye kupendeza mbele zako, Ee Yehova Mwamba wangu na Mkombozi wangu.” (Zab. 19:14) Sisi pia, tunapenda maneno yetu yampendeze Yehova, kwa sababu tunathamini pendeleo letu la kuzungumza kuhusu kweli kutanikoni na katika huduma. Njia moja ambayo Yehova anatumia kutuzoeza kwa ajili ya huduma, ni kupitia Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Mazoezi hayo hufanywa kila juma katika makutaniko zaidi ya 111,000 ulimwenguni pote. Mazoezi hayo yamewasaidia ndugu na dada kutoka malezi tofauti-tofauti ulimwenguni pote, wastahili kuwa wahudumu wa habari njema wenye uwezo wa kufundisha kwa ushawishi, busara, na ujasiri.—Mdo. 19:8; Kol. 4:6.
2 Ratiba ya shule ya mwaka wa 2015 inatia ndani habari zilizo katika “Vichwa vya Mazungumzo ya Biblia” [td] vinapopatikana kwenye Tafsiri ya Ulimwengu Mpya, na kijitabu Utangulizi wa Neno la Mungu [igw]. Kwa kuongezea, kuna badiliko katika muda utakaotumiwa kwenye mambo makuu ya usomaji wa Biblia na Hotuba Na. 1. Mafungu yanayofuata yanazungumzia mabadiliko hayo pamoja na maagizo ya jinsi migawo ya shule inavyopaswa kutolewa.
3 Mambo Makuu ya Usomaji wa Biblia: Ndugu aliyepewa mgawo huo anapaswa kutumia dakika mbili za kwanza kukazia jambo moja la Kimaandiko lenye kupendeza kutoka katika usomaji wa Biblia wa juma hilo na kuonyesha jinsi tunavyoweza kulitumia. Tukijitayarisha vizuri tutaweza kueleza jambo ambalo litanufaisha kutaniko ndani ya wakati uliowekwa. Baada ya hapo, wasikilizaji watakuwa na dakika sita za kutoa maelezo yasiyozidi sekunde 30 kuhusu mambo yenye kupendeza waliyopata katika usomaji wa Biblia wa juma hilo. Ili tutoe maelezo yenye kujenga yasiyozidi sekunde 30, tunapaswa kujitayarisha vizuri na kujidhibiti, na kwa kufanya hivyo tunapata mazoezi mazuri. Pia, jambo hilo linawapa nafasi wengine waeleze mambo ambayo wamejifunza walipokuwa wakifanya utafiti.
4 Hotuba Na. 1: Muda kwa ajili ya usomaji wa Biblia umepunguzwa na kuwa dakika tatu. Wanaopata mgawo wa usomaji wanapaswa kufanya mazoezi ya kusoma kwa sauti mara nyingi ili wawasilishe mawazo kwa njia inayoeleweka kwa kuzingatia matamshi mazuri na kwa ufasaha. Kwa kuwa kusoma ni sehemu muhimu sana ya ibada yetu, watumishi wote wa Yehova wanapaswa kujitahidi kusoma vizuri. Inapendeza kama nini kuona watoto wengi miongoni mwetu wakisoma vizuri, na tunawapongeza sana wazazi kwa kujitahidi kwa upendo kuwasaidia watoto wao wawe wasomaji wazuri.
5 Hotuba Na. 2: Hii ni hotuba ya akina dada na inapaswa kutolewa kwa dakika tano. Aliyepewa mgawo huo anapaswa kuzungumzia kichwa alichopewa. Ikiwa habari inategemea kijitabu Utangulizi wa Neno la Mungu, anapaswa kuitoa kwa njia inayoonyesha kihalisi jinsi inavyoweza kutumiwa katika utumishi wa shambani kwenye eneo la kutaniko. Ikiwa habari inategemea Vichwa vya Mazungumzo ya Biblia, mwanafunzi anapaswa kuzungumzia kichwa alichopewa, kuchagua maandiko yanayofaa kutumiwa, na kuzungumzia mambo tunayojifunza kutokana na habari hiyo. Maandiko ya ziada yanayohusiana na habari yanaweza kutumiwa. Mwangalizi wa shule atampa mwanafunzi msaidizi mmoja.
6 Hotuba Na. 3: Hii ni hotuba ya dakika tano na inaweza kutolewa na ndugu au dada. Dada akipewa hotuba hii, anapaswa kuitoa kama Hotuba Na. 2. Ndugu akipewa mgawo huu, habari inayotegemea Vichwa vya Mazungumzo ya Biblia inapaswa kutolewa kama hotuba kwa njia itakayowafaidi wasikilizaji. Mwanafunzi anapaswa kuzungumzia kichwa alichopewa, kuchagua maandiko yanayofaa kutumiwa, na kuonyesha mambo tunayojifunza.
7 Jambo Jipya Katika Hotuba Na. 3 kwa Akina Ndugu: Ikiwa hotuba inategemea habari iliyo katika kijitabu Utangulizi wa Neno la Mungu, inapaswa kutolewa kama onyesho la funzo la familia au utumishi wa shambani. Kwa kawaida, mwangalizi wa shule atachagua msaidizi na kikao. Msaidizi anapaswa kuwa mshiriki wa familia ya ndugu aliyepewa mgawo au ndugu mwingine kutanikoni. Maandiko ya ziada yanayokazia kanuni za Biblia zinazohusiana na habari yanaweza kutumiwa. Wakati mwingine mzee wa kutaniko anaweza kupewa mgawo huo. Wazee wanaweza kujichagulia msaidizi na kikao. Bila shaka, kutaniko litatiwa moyo sana kuona wazee wakionyesha ufundi wa kufundisha wakiwa na mshiriki wa familia au ndugu mwingine.
Fanya maendeleo kwa kukubali na kutumia mashauri
8 Mashauri: Mwangalizi wa shule atatumia dakika mbili baada ya kila hotuba ya mwanafunzi kutoa pongezi pamoja na mashauri yenye kujenga yanayotegemea kitabu Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Mwangalizi wa shule hatatangaza somo ambalo mwanafunzi anafanyia kazi anapomkaribisha jukwaani. Baada ya kila hotuba, mwangalizi wa shule anapaswa kutoa pongezi inayofaa, kutangaza somo ambalo mwanafunzi anafanyia kazi, na kueleza kihususa kwa nini mwanafunzi amefanya vizuri katika kutumia somo hilo, au kueleza kwa fadhili kwa nini ingefaa ikiwa mwanafunzi angekazia uangalifu zaidi somo lake.
9 Fomu ya mashauri ya kila mwanafunzi inapatikana kwenye ukurasa wa 79 hadi 81 katika kitabu Shule ya Huduma. Baada ya mwanafunzi kutimiza mgawo wake, mwangalizi wa shule ataweka alama kwenye kitabu cha mwanafunzi na kumwuliza faraghani ikiwa alifanya mazoezi ya somo lake. Pongezi na mashauri ya ziada yenye kujenga yanaweza kutolewa faraghani baada ya mkutano au wakati mwingine. Msaada wa kibinafsi ambao kila mwanafunzi anapokea katika shule ni nafasi ya kufanya maendeleo ya kiroho.—1 Tim. 4:15.
10 Mwangalizi wa shule au msaidizi wake anapaswa kuwa makini na kutoa ishara kwa busara, kama vile kupiga kengele, ili kumjulisha mwanafunzi kwamba muda wake umeisha. Mwanafunzi anapaswa kutambua jambo hilo kwa kumalizia sentensi yake na kuondoka jukwaani.—Ona kitabu Shule ya Huduma, uku. 282, fu. 4.
11 Wote ambao wametimiza matakwa wanatiwa moyo kujiandikisha katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. (Ona kitabu Shule ya Huduma, uku. 282, fu. 6.) Elimu inayotolewa katika shule hiyo imewasaidia watumishi wa Yehova kuhubiri na kufundisha habari njema ya Ufalme kwa usadikisho, heshima, na upendo. Bila shaka, Yehova anafurahia kupokea sifa kutoka kwa wote wanaofaidika na elimu ya kitheokrasi!—Zab. 148:12, 13; Isa. 50:4.