Tumia Kijitabu “Utangulizi wa Neno la Mungu”—Kuanzisha Mazungumzo
1. Ni kifaa gani kipya tulichopokea kwa ajili ya utumishi wa shambani?
1 Biblia Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Kiingereza iliyorekebishwa ina sehemu kwenye kurasa za mwanzoni yenye kichwa “Utangulizi wa Neno la Mungu.” Habari hizo ziko katika kijitabu kilichotolewa kwenye kusanyiko la eneo lenye kichwa “Endeleeni Kuutafuta Kwanza Ufalme wa Mungu!” Tunawezaje kutumia kifaa hiki kipya tunapotayarisha utangulizi wetu kwa ajili ya utumishi wa shambani? Kwa sababu maandiko yamewekwa pamoja katika vichwa tofauti-tofauti vya mazungumzo ya Biblia, kama kilivyo kitabu Kutoa Sababu, kijitabu hicho kinaweza kutumiwa kuanzisha mazungumzo.
2. Tunawezaje kutumia kijitabu “Utangulizi wa Neno la Mungu” katika utumishi?
2 Unaweza kutumia swali la 8 na kusema hivi: “Tumewatembelea kwa muda mfupi kwa sababu watu wengi wanajiuliza hivi: ‘Je, Mungu ndiye chanzo cha mateso yanayotupata?’ [Katika maeneo fulani huenda ikafaa zaidi kumwonyesha swali hilo mwenye nyumba.] Wewe unaonaje? [Mruhusu ajibu.] Biblia ina jibu lenye kuridhisha kwa swali hilo.” Soma na uzungumzie andiko moja au zaidi yaliyonukuliwa moja kwa moja kutoka kwenye Biblia. Ikiwa mwenye nyumba anaonyesha upendezi, unaweza kumwonyesha swali la 20 katika kijitabu Utangulizi wa Neno la Mungu na kumwomba achague swali moja mtakalozungumzia katika ziara itakayofuata. Au unaweza kumpa chapisho lolote la funzo lenye habari zaidi kuhusu jambo mlilozungumzia.
3. Tunaweza kutumiaje kijitabu “Utangulizi wa Neno la Mungu” kuanzisha mazungumzo na watu ambao si wa dini ya Kikristo?
3 Swali la 4 na 13 hadi 17 yanaweza kufaa hasa tunapohubiri katika maeneo yaliyo na watu ambao si wa dini ya Kikristo. Kwa mfano, unaweza kutumia habari iliyo katika swali la 17 na kusema hivi: “Tumewatembelea kwa muda mfupi ili kuzungumza kuhusu familia. Je, si kweli kwamba familia zinakabili matatizo mengi sana leo? [Mruhusu ajibu.] Wenzi wa ndoa wengi wameona faida ya kutumia maneno haya yenye hekima: ‘Mke anapaswa kumheshimu sana mume wake.’ [Huhitaji kutaja kwamba jambo hilo linapatikana katika Waefeso 5:33. Ikiwa unazungumza na mwanamke unaweza kunukuu maneno ya Waefeso 5:28.] Je, unafikiri kutumia ushauri huu kunaweza kuwa na faida katika ndoa?”
4. Unaweza kufanya nini mwishoni mwa mazungumzo pamoja na mtu ambaye si wa dini ya Kikristo?
4 Unapomaliza mazungumzo, fanya mipango ya kurudi tena ili kuendeleza mazungumzo. Huenda unaweza kupanga kuzungumzia andiko lingine lililo chini ya swali hilo. Inapofaa, mjulishe mwenye nyumba kwamba maneno hayo yenye hekima mliyozungumzia yanatoka katika Biblia. Ikitegemea mazungumzo yenu na maoni yake kuhusu Biblia, unaweza kumpa chapisho linaloweza kumvutia.—Ona nyongeza ya Huduma Yetu ya Ufalme ya Desemba 2013.