SOMO LA 43
Kutumia Habari Ambazo Umepewa
BIBLIA inalinganisha kutaniko la Kikristo na mwili wa binadamu. Kila kiungo ni muhimu, lakini ‘vyote havifanyi kazi ileile.’ Kwa hiyo, tufanye bidii tukipewa pendeleo lolote. Hiyo inamaanisha tuelewe hotuba yoyote ambayo tumepewa na kuishughulikia vizuri badala ya kuchukulia kijuu-juu tu habari fulani tukidhani hazipendezi kama habari nyinginezo. (Rom. 12:4-8) Jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara ina daraka la kuandaa chakula cha kiroho “kwa wakati ufaao.” (Mt. 24:45) Tukitumia vipawa vyetu kutoa hotuba kwa kufuata maagizo ambayo tumepokea, inaonyesha tunathamini mpango huo. Hiyo inachangia utaratibu mzuri wa kutaniko lote.
Mambo ya Kutaja Katika Hotuba. Kama umepewa habari ya kuzungumzia katika shule, hakikisha unazungumzia habari hiyo wala si mambo mengine. Mara nyingi, utapewa marejeo hususa. Ikiwa hujaagizwa habari hususa za kutumia, unaweza kukusanya habari vile unavyopenda. Lakini, unapotayarisha hotuba, hakikisha hotuba yote inategemea kichwa ulichopewa. Unapofikiria jambo la kutia ndani ya hotuba, wafikirie wasikilizaji pia.
Chunguza kwa makini marejeo ambayo umepewa na maandiko yaliyomo. Kisha fikiria jinsi ya kutumia habari hiyo kwa njia itakayofaidi wasikilizaji. Chagua mambo mawili au labda matatu katika marejeo yaliyochapishwa ambayo yatakuwa mambo makuu katika hotuba yako. Vilevile, katika zile habari ambazo umepewa chagua maandiko ambayo unapanga kusoma na kuzungumzia.
Unapaswa kutumia kiasi gani cha habari zilizo katika marejeo? Tumia tu habari ambayo unaweza kuzungumzia vizuri. Usikose kufundisha vizuri kwa kuzungumzia mambo mengi mno. Kama baadhi ya habari hizo hazichangii kusudi la hotuba yako, tilia maanani sehemu ambazo zitakusaidia kutimiza kusudi lako. Katika zile habari ambazo umepewa, tumia tu habari ambazo zitawaelimisha na kuwafaidi wasikilizaji. Kusudi la kutimiza shauri hili la usemi ni, kutumia habari ambazo umepewa na wala si wingi wa habari utakazozungumzia katika hotuba.
Hotuba si muhtasari tu wa habari ulizopewa. Panga kueleza mambo fulani, kuyafafanua, kutumia mifano, na labda kuonyesha jinsi watu wanavyoweza kuyatumia maishani. Tumia mambo ya ziada kufafanua mambo makuu katika habari ambazo umepewa badala ya kubadilisha habari hizo.
Baadaye ndugu ambao wamestahili kufundisha wanaweza kupewa migawo ya kufundisha katika Mkutano wa Utumishi. Wanafahamu kwamba wanapaswa kutumia vizuri habari ambazo wamepewa badala ya kuzibadilisha na mambo mengine. Vilevile ndugu wanaotoa hotuba za watu wote hupewa mihtasari ya kufuata. Ingawa mihtasari hiyo inamruhusu msemaji kubadilikana, inaonyesha wazi mambo makuu ya kuzungumzia, hoja zinazounga mkono mambo makuu, na maandiko yaliyo msingi wa hotuba. Kujifunza kufundisha ukitumia habari ambazo umepewa ni njia muhimu ya kujitayarishia mapendeleo mengine ya kufundisha.
Mazoezi hayo pia yanaweza kukusaidia kuongoza mafunzo ya Biblia ya nyumbani yenye maendeleo. Utajifunza kukazia akili habari unayozungumza badala ya kukengeuka na kuzungumzia mambo mengine ambayo huenda yakawa yanapendeza lakini hayachangii mazungumzo hayo. Kwa upande mwingine, ukielewa kusudi la somo hili hutashikilia mno habari mnayojifunza na kukosa kufafanua jambo ambalo huenda mwanafunzi anahitaji kujua.