Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • kr sura 17 kur. 182-191
  • Kuwazoeza Wahudumu wa Ufalme

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuwazoeza Wahudumu wa Ufalme
  • Ufalme wa Mungu Unatawala!
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Kama Vile Baba Alivyonifundisha, Ndivyo Ninavyosema”
  • Kuwazoeza Wahudumu Kuwa Waeneza-Injili
  • Kuwazoeza Akina Ndugu Kushughulikia Majukumu ya Pekee
  • Shule za Kitheokrasi Zinathibitisha Upendo wa Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
  • Mashahidi wa Yehova Wanazoezwa Jinsi Gani ili Kutimiza Huduma Yao?
    Maswali Yanayoulizwa Mara Nyingi Kuhusu Mashahidi wa Yehova
  • Je, Unajifunza Yote Uwezayo Kutoka kwa Yehova?
    Huduma Yetu ya Ufalme—2011
  • Mapainia Huzoezwa Katika Shule Gani?
    Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
Pata Habari Zaidi
Ufalme wa Mungu Unatawala!
kr sura 17 kur. 182-191

SURA YA 17

Kuwazoeza Wahudumu wa Ufalme

WAZO KUU KATIKA SURA HII

Jinsi ambavyo shule za kitheokrasi zinawatayarisha wahudumu wa Ufalme kutimiza migawo yao

1-3. Yesu aliipanuaje kazi ya kuhubiri, na hilo linatokeza maswali gani?

KWA miaka miwili, Yesu alihubiri kotekote Galilaya. (Soma Mathayo 9:35-38.) Alitembelea majiji na vijiji vingi, akifundisha katika masinagogi na kuhubiri habari njema ya Ufalme. Mahali popote alipohubiri, umati ulimiminika kwake. “Mavuno ni mengi” Yesu akasema, na wafanyakazi zaidi walihitajika.

2 Yesu alipanga kuipanua kazi ya kuhubiri. Jinsi gani? Kwa kuwatuma mitume wake 12 “kuhubiri ufalme wa Mungu.” (Luka 9:1, 2) Huenda mitume hao walijiuliza jinsi ambavyo wangeifanya kazi hiyo. Kabla ya kuwatuma, kwa upendo Yesu aliwapa kitu ambacho Baba yake wa mbinguni alikuwa amempa—mazoezi.

3 Maswali mengi sasa yanakuja akilini: Yesu alipata mazoezi gani kutoka kwa Baba yake? Yesu aliwapa mitume wake mazoezi gani? Namna gani leo—je, Mfalme wa Kimasihi amewazoeza wafuasi wake kutimiza huduma yao? Ikiwa ndivyo, amefanya hivyo jinsi gani?

“Kama Vile Baba Alivyonifundisha, Ndivyo Ninavyosema”

4. Yesu alifundishwa na Baba yake lini na wapi?

4 Yesu alikubali waziwazi kwamba alifundishwa na Baba yake. Wakati wa huduma yake, Yesu alisema: “Kama vile Baba alivyonifundisha, ndivyo ninavyosema mambo haya.” (Yoh. 8:28) Yesu alifundishwa lini na wapi? Kwa wazi, mazoezi yake yalianza mara tu Yesu—akiwa Mwana mzaliwa wa kwanza wa Mungu—alipoumbwa. (Kol. 1:15) Akiwa kando ya Baba yake mbinguni, Mwana alimsikiliza na kumtazama “Mfundishaji Mkuu” kwa miaka mingi sana. (Isa. 30:20) Matokeo yakawa kwamba Mwana alipata elimu isiyo na kifani kuhusu sifa, kazi, na makusudi ya Baba yake.

5. Baba alimpa Mwana maagizo gani kuhusu huduma ambayo angefanya duniani?

5 Wakati ulipofika, Yehova alimfundisha Mwana wake kuhusu huduma ambayo angefanya duniani. Ona unabii ambao ulieleza uhusiano kati ya Mfundishaji Mkuu na Mwana wake mzaliwa wa kwanza. (Soma Isaya 50:4, 5.) Unabii huo unasema kwamba Yehova alimwamsha Mwana wake “asubuhi baada ya asubuhi.” Maneno hayo yanatoa wazo la mwalimu anayemwamsha mwanafunzi wake asubuhi na mapema ili amfundishe. Kitabu kimoja cha marejeo ya Biblia kinasema hivi: “Ni kana kwamba Yehova . . . anampeleka shuleni kama mwanafunzi na kumfundisha mambo atakayohubiri na jinsi atakavyohubiri.” Katika “shule” hiyo iliyokuwa mbinguni, Yehova alimfundisha Mwana wake “jambo la kutangaza na la kusema.” (Yoh. 12:49) Baba alimpa pia Mwana wake maagizo ya jinsi ya kufundisha.a Alipokuwa duniani, Yesu alitumia vizuri mazoezi hayo katika huduma yake na pia aliyatumia kuwazoeza wafuasi wake kutimiza huduma yao.

6, 7. (a) Yesu aliwapa mitume wake mazoezi gani, na mazoezi hayo yaliwatayarisha kwa ajili ya kazi gani? (b) Yesu amehakikisha kwamba wafuasi wake leo wamepata mazoezi gani?

6 Kama ilivyotajwa mwanzoni mwa sura hii, Yesu aliwapa mitume wake mazoezi gani? Katika Mathayo sura ya 10, aliwapa maagizo hususa kwa ajili ya huduma ya shambani, kutia ndani mambo yafuatayo: eneo ambalo wangehubiri (mstari wa 5, 6), ujumbe ambao wangehubiri (mstari wa 7), uhitaji wa kumtumaini Yehova (mstari wa 9, 10), jinsi ya kuwafikia wenye nyumba (mstari wa 11-13), jinsi ya kutenda watu wanapokataa ujumbe (mstari wa 14, 15), na jinsi ya kukabiliana na mateso (mstari wa 16-23).b Mazoezi ambayo Yesu aliwapa mitume wake yaliwatayarisha ili waongoze kazi ya kuhubiri habari njema katika karne ya kwanza W.K.

7 Namna gani leo? Yesu, Mfalme wa Ufalme wa Mungu, amewapa wafuasi wake mgawo muhimu zaidi, yaani, kuhubiri “hii habari njema ya ufalme . . . katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote.” (Mt. 24:14) Je, Mfalme ametuzoeza jinsi ya kufanya kazi hiyo muhimu sana? Ndiyo! Akiwa mbinguni, Mfalme amehakikisha kwamba wafuasi wake wamezoezwa jinsi ya kuhubiri nje ya kutaniko na jinsi ya kutimiza majukumu ya pekee ndani ya kutaniko.

Kuwazoeza Wahudumu Kuwa Waeneza-Injili

8, 9. (a) Kusudi kuu la Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ni nini? (b) Shule ya Huduma ya Kitheokrasi imekusaidiaje kuwa na matokeo zaidi katika huduma yako?

8 Tangu zamani, tengenezo la Yehova limetumia makusanyiko na mikutano ya kutaniko kama vile Mkutano wa Utumishi, ili kuwazoeza watu wa Mungu kwa ajili ya huduma. Hata hivyo, kuanzia miaka ya 1940, ndugu waliokuwa wakiongoza katika makao makuu walianza kuandaa mazoezi kupitia shule mbalimbali.

9 Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Kama tulivyoona katika sura iliyotangulia, shule hiyo ilianza mwaka wa 1943. Je, kusudi la shule hiyo ni kuwazoeza tu wanafunzi ili waweze kutoa hotuba nzuri katika mikutano ya kutaniko? Hapana. Tangu zamani, kusudi kuu la shule hiyo limekuwa kuwazoeza watu wa Mungu kutumia zawadi yao ya kusema ili kumsifu Yehova katika huduma. (Zab. 150:6) Shule hiyo huwasaidia ndugu na dada wote ambao wamejiandikisha wawe wahudumu wa Ufalme wenye matokeo mazuri.

10, 11. Ni nani sasa wanaoweza kuandikishwa katika Shule ya Gileadi, na shule hiyo ina kusudi gani?

10 Shule ya Gileadi. Shule ya Gileadi ilianza Jumatatu, Februari 1, 1943. Mwanzoni, shule hiyo ilikusudiwa iwazoeze mapainia na watumishi wengine wa wakati wote kwa ajili ya utumishi wa umishonari mahali popote ulimwenguni. Lakini kuanzia Oktoba 2011, wanaoandikishwa katika shule hiyo ni wale ambao tayari wako katika utumishi wa pekee wa wakati wote, kama vile mapainia wa pekee, waangalizi wanaosafiri na wake zao, Wanabetheli, na wamishonari walio shambani ambao hawajahudhuria shule hiyo.

11 Kusudi la masomo ya Shule ya Gileadi ni nini? Ndugu mmoja ambaye amefundisha shule hiyo kwa miaka mingi anajibu: “Ni kuimarisha imani ya wanafunzi kupitia kujifunza kwa kina Neno la Mungu na kuwasaidia wasitawishe sifa za kiroho ambazo zitawasaidia kukabiliana na magumu katika migawo yao. Pia, kusudi kuu la masomo hayo ni kuwachochea wanafunzi washiriki zaidi katika kazi ya kueneza injili.”—Efe. 4:11.

12, 13. Shule ya Gileadi imekuwa na matokeo gani katika kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote? Toa mfano.

12 Shule ya Gileadi imekuwa na matokeo gani katika kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote? Tangu mwaka wa 1943, zaidi ya ndugu na dada 8,500 wamezoezwa katika shule hiyo,c na wamishonari waliozoezwa katika Shule ya Gileadi wametumikia katika nchi zaidi ya 170 ulimwenguni. Wamishonari hao hutumia vizuri mazoezi waliyopata, na hivyo wanaweka mfano mzuri kwa kuwa na bidii katika huduma na wanawazoeza wengine kufanya vivyo hivyo. Katika visa vingi, wamishonari waliongoza kazi ya kuhubiri katika maeneo yaliyokuwa na wahubiri wachache wa Ufalme.

13 Fikiria kilichotokea nchini Japani kazi ya kuhubiri hadharani ilipokoma wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu. Kufikia Agosti 1949, kulikuwa na wahubiri wasiozidi kumi nchini Japani. Hata hivyo, kufikia mwishoni mwa mwaka huo, wamishonari 13 waliozoezwa Gileadi walikuwa wakihubiri kwa bidii nchini humo. Wamishonari wengine wengi walitumwa baadaye. Mwanzoni, wamishonari walihubiri tu katika majiji makubwa, lakini baadaye walihamia majiji mengine. Wamishonari hao waliwatia moyo wanafunzi wao na wengine wawe mapainia. Bidii hiyo ya wamishonari ilikuwa na matokeo mazuri sana. Sasa, kuna watangazaji wa Ufalme zaidi ya 216,000 nchini Japani, na karibu asilimia 40 wanatumikia wakiwa mapainia!d

14. Shule za kitheokrasi ni uthibitisho wenye nguvu wa nini? (Ona pia sanduku “Shule Zinazowazoeza Wahudumu wa Ufalme,” ukurasa wa 188.)

14 Shule nyingine za kitheokrasi. Shule ya Utumishi wa Painia, Shule ya Biblia ya Wenzi wa Ndoa Wakristo, na Shule ya Biblia ya Ndugu Waseja zimewasaidia wanafunzi kukua kiroho na kuongoza kwa bidii katika kazi ya kueneza injili.e Shule hizo zote za kitheokrasi ni uthibitisho wenye nguvu kwamba Mfalme wetu amewapa wafuasi wake vifaa kamili ili watimize huduma yao.—2 Tim. 4:5.

Kuwazoeza Akina Ndugu Kushughulikia Majukumu ya Pekee

15. Wanaume walio na majukumu kutanikoni wanataka kumwiga Yesu katika njia gani?

15 Kumbuka unabii wa Isaya ulisema kwamba Yesu alifundishwa na Mungu. Katika “shule” hiyo iliyokuwa mbinguni, Mwana alijifunza “jinsi ya kumjibu neno yeye aliyechoka.” (Isa. 50:4) Yesu alitumia mafunzo hayo; alipokuwa duniani aliwaburudisha wale ‘waliotaabika na kulemewa na mizigo.’ (Mt. 11:28-30) Wakimwiga Yesu, wanaume walio na majukumu kutanikoni wanataka kuwaburudisha ndugu na dada zao. Ili kutimiza hilo, shule kadhaa zimeanzishwa ili kuwasaidia ndugu wanaostahili waweze kuwatumikia waamini wenzao kwa njia nzuri zaidi.

16, 17. Shule ya Huduma ya Ufalme ina kusudi gani? (Ona pia maelezo ya chini.)

16 Shule ya Huduma ya Ufalme. Darasa la kwanza la shule hiyo lilianza Machi 9, 1959, huko South Lansing, New York. Waangalizi wanaosafiri na pia watumishi wa kutaniko walialikwa wahudhurie masomo hayo ya mwezi mmoja. Baadaye, masomo hayo yaliyokuwa katika Kiingereza, yalitafsiriwa katika lugha nyingine, na hatua kwa hatua shule hiyo ilianza kuwazoeza akina ndugu ulimwenguni pote.f

Ndugu Lloyd Barry akifundisha Shule ya Huduma ya Ufalme nchini Japani, 1970

Ndugu Lloyd Barry akifundisha Shule ya Huduma ya Ufalme nchini Japani, 1970

17 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova cha 1962, kilisema hivi kuhusu kusudi la Shule ya Huduma ya Ufalme: “Katika ulimwengu huu wenye shughuli nyingi, mwangalizi katika kutaniko la mashahidi wa Yehova anapaswa kuwa mtu anayeweza kupanga maisha yake vizuri ili aweze kuwapa wote kutanikoni uangalifu unaofaa na kuwa baraka kwao. Wakati huohuo hapaswi kuipuuza familia yake kwa sababu ya kutaniko, bali anapaswa kuwa na utimamu wa akili. Watumishi wa kutaniko ulimwenguni pote wamepewa fursa nzuri ya kukutanika pamoja katika Shule ya Huduma ya Ufalme ili wapate mazoezi ambayo yatawasaidia kufanya yale ambayo Biblia inasema mwangalizi anapaswa kutimiza!”—1 Tim. 3:1-7; Tito 1:5-9.

18. Watu wote wa Mungu wananufaikaje na Shule ya Huduma ya Ufalme?

18 Watu wote wa Mungu wamenufaika na Shule ya Huduma ya Ufalme. Kwa njia gani? Wazee na watumishi wa huduma wanapofuata yale waliyojifunza katika shule hiyo, wanamwiga Yesu na kuwaburudisha waamini wenzao. Bila shaka, sisi huthamini sana mzee au mtumishi wa huduma anayejali anapotuambia neno lenye fadhili, anapotusikiliza, au anapotutembelea ili kututia moyo! (1 The. 5:11) Kwa kweli, wanaume hao ni baraka kwa makutaniko yao!

19. Halmashauri ya Ufundishaji inasimamia shule gani nyingine, na ni nini kusudi la shule hizo?

19 Shule nyingine za kitheokrasi. Halmashauri ya Ufundishaji ya Baraza Linaloongoza inasimamia shule nyingine ambazo huwazoeza ndugu wenye majukumu katika tengenezo. Kusudi la shule hizo ni kuwasaidia ndugu wenye majukumu—wazee wa kutaniko, waangalizi wanaosafiri, na washiriki wa Halmashauri za Tawi—kutimiza majukumu yao mengi kwa njia yenye matokeo zaidi. Masomo hayo yanayotegemea Biblia huwatia moyo akina ndugu wadumishe hali yao ya kiroho na kufuata kanuni za Kimaandiko wanaposhughulika na kondoo wenye thamani ambao Yehova amewakabidhi wawatunze.—1 Pet. 5:1-3.

Darasa la kwanza la Shule ya Mazoezi ya Kihuduma nchini Malawi

Darasa la kwanza la Shule ya Mazoezi ya Kihuduma nchini Malawi

20. Kwa nini Yesu angeweza kusema kwamba sisi sote‘tunafundishwa na Yehova,’ nawe umeazimia kufanya nini?

20 Ni wazi kwamba Mfalme wa Kimasihi amehakikisha kwamba wafuasi wake wanazoezwa vizuri. Mazoezi hayo yote yalianzia kwa Yehova ambaye alimzoeza Mwana wake, kisha Mwana wake amewazoeza wafuasi wake. Kwa sababu hiyo, Yesu angeweza kusema kwamba sisi sote ‘tunafundishwa na Yehova.’ (Yoh. 6:45; Isa. 54:13) Acheni tuazimie kutumia kikamili mazoezi ambayo Mfalme wetu ametuandalia—iwe ni katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, mikutano mingine ya kutaniko, au shule nyingine zilizozungumziwa katika sura hii. Na tukumbuke kwamba kusudi kuu la mazoezi hayo yote ni kutusaidia tuwe imara kiroho ili tutimize kwa ukamili huduma yetu.

a Tunajuaje kwamba Baba alimfundisha Mwana jinsi ya kufundisha? Fikiria hili: Mifano mingi ambayo Yesu alitumia alipokuwa akifundisha ilitimiza unabii uliotolewa karne nyingi kabla ya kuzaliwa kwake. (Zab. 78:2; Mt. 13:34, 35) Ni wazi kwamba Yehova, Mtungaji wa unabii huo, aliamua tangu zamani kwamba Mwana wake angetumia mifano kufundisha.—2 Tim. 3:16, 17.

b Miezi kadhaa baadaye, Yesu ‘aliwachagua wengine 70 na kuwatuma wawili-wawili’ wakahubiri. Pia aliwapa mazoezi.—Luka 10:1-16.

c Baadhi ya wanafunzi wamehudhuria Shule ya Gileadi zaidi ya mara moja.

d Kwa habari zaidi kuhusu jinsi ambavyo wamishonari waliozoezwa Gileadi wamekuwa na matokeo mazuri katika kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote, ona sura ya 23 ya kitabu Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu.

e Shule ya Biblia ya Wenzi wa Ndoa Wakristo na Shule ya Biblia ya Ndugu Waseja zimeunganishwa na kuwa shule moja inayoitwa Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme.

f Sasa wazee wote hunufaika na Shule ya Huduma ya Ufalme ambayo huwa na vipindi vyenye urefu mbalimbali na hufanywa kila baada ya miaka michache. Tangu mwaka wa 1984, watumishi wa huduma pia wamezoezwa katika shule hiyo.

Ufalme Ni Halisi Kwako Kadiri Gani?

  • Yesu alipata mazoezi gani kutoka kwa Baba yake?

  • Mfalme amewazoeza jinsi gani wafuasi wake kuwa waeneza-injili?

  • Ndugu wanaostahili wamezoezwa jinsi gani kutimiza majukumu yao?

  • Unaweza kuonyeshaje kwamba unathamini mazoezi ambayo Mfalme ameandaa?

SHULE ZINAZOWAZOEZA WAHUDUMU WA UFALME

SHULE YA HUDUMA YA KITHEOKRASI

Kusudi: Kuwazoeza wahubiri watoe ushahidi na kufundisha habari njema kwa njia yenye matokeo.

Muda: Shule hii ni ya kuendelea.

Mahali: Jumba la Ufalme.

Kujiandikisha: Wote wanaoshirikiana kwa ukawaida na kutaniko, wanaokubali mafundisho ya Biblia, na kuishi kupatana na kanuni za Kikristo wanaweza kujiandikisha. Ikiwa unataka kujiunga na shule hii, zungumza na mwangalizi wa Shule ya Huduma ya Kitheokrasi.

Faida: Sharon, aliye na ugonjwa wa kupooza unaoitwa amyotrophic lateral sclerosis (ALS), anasema: “Shule ya Huduma ya Kitheokrasi imenifundisha kufanya utafiti na kutoa habari kwa njia inayoeleweka. Nimejifunza pia kuwasikiliza wengine na kukazia fikira mahitaji yao ya kiroho, na si yangu tu.”

Arnie, ambaye amekuwa mwangalizi anayesafiri kwa muda mrefu, anasema: “Nilizaliwa nikiwa na tatizo la kigugumizi na ilikuwa vigumu kwangu kuwatazama wengine usoni. Shule hii imenisaidia kujiamini. Kwa msaada wa Yehova kupitia mazoezi hayo, nimejifunza mbinu zinazonisaidia kukaza fikira na kupumua vizuri. Ninashukuru sana kwa kuwa na uwezo wa kumsifu Mungu katika kutaniko na katika huduma yangu.”

Mhubiri mchanga akisoma Biblia katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi

SHULE KWA AJILI YA WAZEE WA KUTANIKOg

Kusudi: Kuwasaidia wazee waboreshe hali yao ya kiroho na kushughulikia majukumu yao kutanikoni.

Muda: Siku tano.

Mahali: Ofisi ya tawi huamua; kwa kawaida katika Jumba la Ufalme au Jumba la Kusanyiko.

Kujiandikisha: Ofisi ya tawi huwaalika wazee.

Faida: Ona baadhi ya maelezo ya akina ndugu wa darasa la 92 la shule hiyo huko Patterson, New York, Marekani:

“Nimefaidika sana na shule hiyo, imenisaidia kujichunguza mwenyewe na kuona jinsi ninavyoweza kuwatunza kondoo wa Yehova.”

“Nitayatumia mazoezi hayo maishani mwangu.”

SHULE YA UTUMISHI WA PAINIA

Kusudi: Kuwasaidia mapainia ‘kutimiza kwa ukamili’ huduma yao.—2 Tim. 4:5.

Muda: Siku sita.

Mahali: Ofisi ya tawi huamua; kwa kawaida katika Jumba la Ufalme.

Kujiandikisha: Wale ambao wamekuwa mapainia wa kawaida kwa angalau mwaka moja hivi hawahitaji kujiandikisha, wanapata mwaliko kutoka kwa mwangalizi wa mzunguko. Baadhi ya mapainia wa zamani ambao hawajahudhuria shule hii katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, wanaweza kualikwa wahudhurie tena.

Faida: “Shule hii imenisaidia kukabiliana na magumu ninayopata katika huduma na maishani mwangu,” anasema Lily. “Njia yangu ya kujifunza, kufundisha, na kuitumia Biblia imekuwa bora zaidi. Niko tayari zaidi kuwasaidia wengine, kuwaunga mkono wazee, na kuchangia ukuzi wa kutaniko.”

Brenda, ambaye amehudhuria shule hii mara mbili, anasema: “Shule hii ilinizoeza kuzama kabisa katika mambo ya kiroho, kuimarisha dhamiri yangu, na kukazia fikira kuwasaidia wengine. Kwa kweli, Yehova ni mkarimu!”

SHULE YA WANABETHELI WAPYA

Kusudi: Shule hii imekusudiwa iwasaidie Wanabetheli wapya wafanikiwe katika utumishi wao wa Betheli.

Muda: Dakika 45 kila juma kwa majuma 16.

Mahali: Betheli.

Kujiandikisha: Washiriki wa kudumu wa familia ya Betheli na wajitoleaji wa muda ambao wametumikia Betheli kwa muda mrefu (kwa mwaka mmoja au zaidi) wanaandikishwa moja kwa moja.

Faida: Demetrius, aliyehudhuria shule hiyo katika miaka ya 1980, anasema: “Shule hiyo iliboresha mazoea yangu ya kujifunza na ilinisaidia kuwa tayari kutumikia Betheli kwa muda mrefu. Walimu, masomo, na mashauri yenye kufaa yalinisaidia kusadiki kwamba Yehova ananihangaikia kwa upendo na anatamani kuona nikifanikiwa katika utumishi wangu wa Betheli.”

SHULE YA WAENEZA-INJILI WA UFALMEh

Kusudi: Wale ambao wako katika utumishi wa wakati wote (wenzi wa ndoa, ndugu waseja, na dada waseja) mazoezi ya pekee ili waweze kutumiwa kikamili na Yehova na tengenezo lake. Wahitimu wengi watapewa mgawo wa kutumikia katika maeneo yenye uhitaji mkubwa zaidi katika nchi yao. Wahitimu walio na umri usiozidi miaka 50 wanaweza kutumikia wakiwa mapainia wa pekee wa muda ili kuanzisha na kupanua kazi ya kuhubiri habari njema katika maeneo ya mbali.

Muda: Miezi miwili.

Mahali: Ofisi ya tawi huamua; kwa kawaida katika Jumba la Ufalme au Jumba la Kusanyiko.

Dada akiwa katika ya utumishi

Ndugu na dada wanafaidika na mazoezi ya kitheokrasi

Kujiandikisha: Watumishi wa wakati wote ambao wana umri wa miaka 23 hadi 65, ambao wana afya nzuri, na hali zao zinawaruhusu watumikie popote penye uhitaji mkubwa zaidi, na wenye mtazamo huu: “Mimi hapa! Nitume mimi,” wanaweza kujiandikisha. (Isa. 6:8) Wote wanaohudhuria shule hiyo, iwe ni ndugu au dada waseja na pia wenzi wa ndoa, wanapaswa wawe wamekuwa katika utumishi wa wakati wote kwa angalau miaka miwili mfululizo. Wenzi wa ndoa wanapaswa kuwa wamefunga ndoa kwa angalau miaka miwili. Ni lazima akina ndugu wawe wametumikia wakiwa wazee au watumishi wa huduma kwa angalau miaka miwili mfululizo. Iwapo shule hiyo inafanywa katika maeneo yaliyo chini ya tawi lenu, mkutano utafanywa katika kusanyiko la kanda ili kuwapa habari wale ambao wangependa kuhudhuria shule hiyo.

Faida: Wengi wametaja faida za kuhudhuria Shule ya Biblia ya Ndugu Waseja na Shule ya Biblia ya Wenzi wa Ndoa Wakristo. Katika mwaka wa 2013, Baraza Linaloongoza lilikubali shule hizo mbili ziunganishwe na kuwa shule moja inayoitwa Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme. Sasa mapainia wengi waaminifu, kutia ndani dada waseja watafaidika na masomo hayo.

SHULE YA GILEADI

Kusudi: Wahitimu wanaweza kupewa mgawo wa kuwa waangalizi wanaosafiri, wamishonari shambani, au Wanabetheli. Wanapotumia mazoezi yao vizuri, wahitimu wanasaidia kuimarisha na kuitegemeza kazi ya kuhubiri na kupanga mambo katika ofisi za tawi.

Muda: Miezi mitano.

Mahali: Kituo cha Elimu cha Watchtower huko Patterson, New York, Marekani.

Wanafunzi katika darasa la Shule ya Gileadi wakimsikiliza mwalimu

Darasa la Gilead​—Patterson, New York

Kujiandikisha: Wenzi wa ndoa, ndugu waseja, na dada waseja, ambao tayari wanatumika katika utumishi wa pekee wa wakati wote. Wamishonari walio shambani ambao hawajahudhuria shule hiyo, mapainia wa pekee, Wanabetheli, au waangalizi wanaosafiri na wake zao, wanaweza kuombwa na Halmashauri ya Tawi wajaze fomu. Wanapaswa kujua kuongea na kuandika Kiingereza.

Faida: Lade na Monique, wenzi wa ndoa kutoka Marekani ambao wamekuwa katika mgawo wao kwa miaka mingi, wanasema hivi:

“Shule ya Gileadi ilitutayarisha kwenda mahali popote ulimwenguni, tukiwa tayari kabisa kufanya kazi na ndugu zetu wapendwa,” anasema Lade.

Monique anaongeza hivi: “Ninapotumia yale niliyojifunza kutoka katika Neno la Mungu, ninapata shangwe nyingi katika mgawo wangu. Ninaona shangwe hiyo kuwa uthibitisho zaidi wa upendo wa Yehova.”

SHULE YA HUDUMA YA UFALME

Kusudi: Kuwazoeza waangalizi wanaosafiri, wazee, na watumishi wa huduma kushughulikia majukumu yao ya uangalizi na ya kitengenezo. (Mdo. 20:28) Hali zilizopo, mielekeo, na mahitaji ya makutaniko huzungumziwa. Shule hii hufanywa baada ya miaka michache ikitegemea uamuzi wa Baraza Linaloongoza.

Muda: Katika miaka ya hivi karibuni, shule hii imefanywa kwa vipindi vyenye urefu mbalimbali.

Mahali: Kwa kawaida, katika Jumba la Ufalme au Jumba la Kusanyiko.

Kujiandikisha: Mwangalizi wa mzunguko huwajulisha wazee na watumishi wa huduma. Ofisi ya tawi huwaalika waangalizi wanaosafiri.

Faida: “Ingawa shule hii inazungumzia mambo mengi kwa muda mfupi, inawachochea wazee kudumisha shangwe yao na kuendelea kuwa kama wanaume katika utumishi wa Yehova. Wazee wa zamani na wapya wanajifunza kufanya uchungaji kwa njia yenye matokeo ili kuunganishwa vyema katika njia ileile ya kufikiri.”—Quinn.

“Mazoezi haya yalikuwa yenye usawaziko—yalitusaidia kusitawisha uthamini wetu kuelekea mambo ya kiroho, yalituonya kuhusu hatari, na kutuandalia mapendekezo yanayofaa kuhusu kulitunza kundi.”—Michael.

SHULE YA WAANGALIZI WANAOSAFIRI NA WAKE ZAOi

Kusudi: Kuwasaidia waangalizi wanaosafiri wayatumikie makutaniko kwa njia bora zaidi ‘wanapofanya kazi kwa bidii katika kusema na kufundisha,’ na kuwachunga wale walio chini ya uangalizi wao.—1 Tim. 5:17; 1 Pet. 5:2, 3.

Muda: Miezi miwili.

Mahali: Ofisi ya tawi huamua.

Kujiandikisha: Ofisi ya tawi huwaalika waangalizi wanaosafiri na wake zao.

Faida: “Tulithamini zaidi ukichwa wa Yesu juu ya tengenezo. Tuliona uhitaji wa kuwatia moyo ndugu na dada tunaowatumikia na kuimarisha umoja katika kila kutaniko. Shule hiyo ilitusaidia kuelewa kuwa ingawa mwangalizi anayesafiri hutoa mashauri na kuwarekebisha ndugu pindi fulani, lengo lake kuu ni kuwasaidia waone kwamba Yehova anawapenda.”—Joel na Connie, darasa la 1, mwaka wa 1999.

SHULE YA WASHIRIKI WA HALMASHAURI YA TAWI NA WAKE ZAO

Kusudi: Kuwasaidia wale wanaotumikia kwenye Halmashauri za Tawi ili waweze kusimamia makao ya Betheli, kushughulikia masuala ya utumishi yanayohusu makutaniko, na kusimamia mizunguko katika eneo lao.—Luka 12:48b.

Muda: Miezi miwili.

Mahali: Kituo cha Elimu cha Watchtower huko Patterson, New York, Marekani.

Kujiandikisha: Halmashauri ya Utumishi ya Baraza Linaloongoza huwaalika washiriki wa Halmashauri za Tawi au Halmashauri za Nchi pamoja na wake zao.

Faida: Lowell na Cara walihudhuria darasa la 25. Sasa wanatumikia Nigeria.

“Nilikumbushwa kwamba hata niwe na shughuli nyingi kadiri gani au iwe nimepewa kazi gani, siri ya kumpendeza Yehova ni kuwa na hali nzuri ya kiroho,” anasema Lowell.

Cara anakumbuka jambo moja alilojifunza katika shule hiyo: “Ikiwa siwezi kueleza jambo kwa njia rahisi, ninahitaji kujifunza jambo hilo kwa undani kabla ya kujaribu kuwafundisha wengine.”

g Shule hii haifanywi katika kila nchi.

h Shule hii haifanywi katika kila nchi.

i Shule hii haifanywi katika kila nchi.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki