Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • bt sura 5 kur. 36-43
  • “Lazima Tumtii Mungu Kuwa Mtawala”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Lazima Tumtii Mungu Kuwa Mtawala”
  • “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Malaika wa Yehova Akaifungua Milango” (Mdo. 5:12-21a)
  • “Lazima Tumtii Mungu Kuwa Mtawala Badala ya Wanadamu” (Mdo. 5:21b-33)
  • “Hamtaweza Kuwaangamiza” (Mdo. 5:34-42)
  • Wanaume Wanaostahili Washughulikie “Kazi Hii Muhimu” (Mdo. 6:1-6)
  • “Neno la Mungu Likazidi Kuenea” (Mdo. 6:7)
  • ‘Hatuwezi Kuacha Kusema Juu ya Yesu’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Wewe Humtii Nani—Mungu Au Wanadamu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Hakuna Chochote Ambacho Kingeweza Kuwazuia
    Masomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
  • Kunena Neno la Yehova Kwa Ujasiri
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
Pata Habari Zaidi
“Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
bt sura 5 kur. 36-43

SURA YA 5

“Lazima Tumtii Mungu Kuwa Mtawala”

Mitume wachukua msimamo unaowawekea kielelezo Wakristo wote wa kweli

Mdo. 5:12–6:7

1-3. (a) Kwa nini mitume wamepelekwa mbele ya Sanhedrini, na ni suala gani kuu linalohusika? (b) Kwa nini tupendezwe sana na msimamo wa mitume?

MAHAKAMA ya Sanhedrini imewaka hasira! Mitume wa Yesu wamefikishwa mbele ya mahakama hiyo. Kwa sababu gani? Yosefu Kayafa, kuhani mkuu aliyekuwa pia mkuu wa Sanhedrini, anawaambia hivi kwa ukali: “Tuliwakataza kabisa msifundishe kwa msingi wa jina hili.” Kwa sababu ya hasira hawezi hata kutamka jina la Yesu. Kayafa anaendelea kusema, “na bado tazama! mmejaza Yerusalemu fundisho lenu, nanyi mmeazimia kuileta damu ya mtu huyu juu yetu.” (Mdo. 5:28) Ujumbe wake uko wazi: Acheni kuhubiri!

2 Mitume hao watafanya nini? Yesu, aliye na mamlaka kamili kutoka kwa Mungu, ndiye aliyewapa kazi hiyo ya kuhubiri. (Mt. 28:18-20) Je, mitume hao wataogopa na kuacha kuhubiri? Au je, watasimama imara na kuendelea kuhubiri kwa ujasiri? Jambo kuu ni: Watamtii Mungu au mwanadamu? Bila kusita, mtume Petro anazungumza bila woga wowote kwa niaba ya mitume wengine.

3 Tukiwa Wakristo, tunaweza kujifunza mengi kutokana na jinsi mitume walivyotenda walipotishwa na Sanhedrini. Sisi pia tumepewa kazi ya kuhubiri. Tunapotimiza kazi hiyo tuliyopewa na Mungu, huenda pia tukakabili upinzani. (Mt. 10:22) Wapinzani wanaweza kujaribu kuzuia au kupinga kazi yetu. Tutafanya nini? Acheni tufikirie msimamo wa mitume na mambo yaliyotokea kabla ya kupelekwa kwao mbele ya Sanhedrini. Kufikiria mambo hayo kunaweza kutusaidia tunapokabili hali kama hizo.a

SANHEDRINI​—MAHAKAMA KUU YA WAYAHUDI

Roma iliwaruhusu Wayahudi waendeleze utamaduni wao na wajitawale ingawa Yudea ilikuwa mkoa wa Milki ya Roma. Kesi ndogo za uhalifu zilitatuliwa na mahakama ndogo, lakini kesi ambazo mahakama hizo hazingeweza kutatua zilipelekwa mbele ya Sanhedrini iliyokuwa Yerusalemu. Sanhedrini ilikuwa mahakama kuu ya Wayahudi. Pia, ilikuwa baraza lililosimamia mambo ya kitaifa. Iliamua mambo yaliyohusu sheria ya Kiyahudi, na mamlaka yake iliheshimiwa na Wayahudi wote.

Vikao vya Sanhedrini vilikuwa vikifanywa katika majengo ya hekalu au karibu na hekalu. Baraza hilo lilikuwa na washiriki 71—kuhani mkuu, alikuwa mkuu wa mahakama hiyo; washiriki wengine walikuwa makuhani, kutia ndani Masadukayo, watu kutoka katika jamii za wakuu, na waandishi wenye elimu. Uamuzi wa mahakama hiyo haungeweza kubatilishwa.

“Malaika wa Yehova Akaifungua Milango” (Mdo. 5:12-21a)

4, 5. Kwa nini Kayafa na Masadukayo ‘walijawa na wivu’?

4 Kumbuka kwamba Petro na Yohana walipokatazwa kuhubiri mara ya kwanza, walisema: “Hatuwezi kuacha kusema kuhusu mambo ambayo tumeyaona na kuyasikia.” (Mdo. 4:20) Walipoachiliwa, Petro na Yohana pamoja na wale mitume wengine waliendelea kuhubiri katika hekalu. Walifanya ishara kubwa, kama vile kuponya wagonjwa na kufukuza roho waovu. Hata inaonekana kwamba watu walioangukiwa na kivuli cha Petro waliponywa! Walifanya hivyo “kwenye Safu ya Nguzo za Sulemani” zilizokuwa upande wa mashariki wa hekalu, ambapo Wayahudi wengi walipenda kukusanyika. Wengi walioponywa kimwili walikubali pia kuponywa kiroho. Kwa sababu hiyo, “waliomwamini Bwana wakazidi kuongezeka, idadi kubwa ya wanaume na wanawake.”​—Mdo. 5:12-15.

5 Kayafa na Masadukayo, ‘wakajawa na wivu’ na kuagiza mitume wafungwe jela. (Mdo. 5:17, 18) Ni nini kilichowakasirisha Masadukayo? Mitume walikuwa wakifundisha kwamba Yesu amefufuliwa, nao Masadukayo hawakuamini ufufuo. Pia, mitume walifundisha kwamba ili mtu aokolewe anahitaji kumwamini Yesu, Masadukayo walihofu kwamba ikiwa watu wangekuwa wafuasi wa Yesu, Waroma wangewachukulia hatua kali. (Yoh. 11:48) Ndiyo sababu Masadukayo walikuwa wameazimia kabisa kuwanyamazisha mitume!

6. Ni nani hasa leo wanaochochea watumishi wa Yehova wateswe, na kwa nini hilo halitushangazi?

6 Leo pia, wapinzani wa kidini ndio hasa wanaochochea watu wawatese watumishi wa Yehova. Wapinzani hao hujaribu kutunyamazisha kwa kutumia serikali au vyombo vya habari. Wanafanya hivyo kwa sababu ujumbe wetu unafunua uwongo wa dini. Wanapokubali kweli za Biblia, watu wenye mioyo minyoofu huwekwa huru kutokana na imani na mazoea yasiyo ya kimaandiko. (Yoh. 8:32) Ndiyo sababu mara nyingi ujumbe wetu huwafanya viongozi wa kidini wawe na wivu na chuki.

7, 8. Amri ya malaika ilikuwa na matokeo gani kwa mitume, nasi tunapaswa kujiuliza swali gani?

7 Wakiwa jela kabla ya kupelekwa mahakamani, huenda mitume hao waliona kwamba watauawa kwa sababu ya imani yao. (Mt. 24:9) Lakini usiku huo, jambo lisilo la kawaida likatokea—“malaika wa Yehova akaifungua milango ya gereza.”b (Mdo. 5:19) Kisha malaika huyo akawaagiza: “Mkasimame hekaluni, na mwendelee kuwaambia” watu. (Mdo. 5:20) Bila shaka, amri hiyo iliwahakikishia mitume kwamba walikuwa wakifanya jambo linalofaa. Pia, huenda maneno hayo yaliwapa nguvu za kubaki imara hata hali ziweje. Wakiwa na imani yenye nguvu na ujasiri, mitume “wakaingia hekaluni wakati wa mapambazuko na kuanza kufundisha.”​—Mdo. 5:21.

8 Kila mmoja wetu anapaswa kujiuliza, ‘Nina imani na ujasiri unaohitajiwa kuendelea kuhubiri katika hali kama hizo?’ Kujua kwamba tunategemezwa na kuongozwa na malaika tunapofanya kazi hiyo muhimu ya “kutoa ushahidi kamili kuhusu Ufalme wa Mungu,” kunaweza kutupatia nguvu za kuendelea kuhubiri.​—Mdo. 28:23; Ufu. 14:6, 7.

“Lazima Tumtii Mungu Kuwa Mtawala Badala ya Wanadamu” (Mdo. 5:21b-33)

Kayafa akiwashutumu mitume kwa hasira mbele ya washiriki wengine wa Sanhedrini.

“Basi wakawaleta na kuwasimamisha mbele ya Sanhedrini.”—Matendo 5:27

9-11. Mitume walifanya nini mahakama ya Sanhedrini ilipowaamuru waache kuhubiri, na Wakristo wa kweli leo wanawezaje kuwaiga?

9 Kayafa na wale mahakimu wengine wa Sanhedrini wako tayari kuwachukulia hatua mitume hao. Kwa kuwa hawakujua yaliyokuwa yametokea usiku uliotangulia, wakawatuma maofisa wakawachukue wafungwa. Wazia jinsi maofisa hao walivyoshangaa walipogundua kwamba wafungwa hawapo, ijapokuwa jela ilikuwa imefungwa kabisa na “walinzi wakiwa wamesimama kwenye milango.” (Mdo. 5:23) Muda mfupi baadaye, kapteni wa hekalu ajulishwa kwamba mitume wamerudi hekaluni, na wanatoa ushahidi kumhusu Yesu Kristo—kazi ileile ambayo ilifanya wafungwe katika jela! Bila kupoteza wakati kapteni na maofisa wake wanaenda hekaluni kuwakamata na kuwaleta mbele ya Sanhedrini.

10 Kama ilivyotajwa mwanzoni mwa sura hii, viongozi hao wa kidini wenye hasira kali waliwaagiza mitume hao waache kabisa kuhubiri. Ikawaje? Petro akiwa msemaji wao, alijibu hivi kwa ujasiri: “Lazima tumtii Mungu kuwa mtawala badala ya wanadamu.” (Mdo. 5:29) Wakristo wote wa kweli wanaweza kuiga mfano huo mzuri uliowekwa na mitume. Hatuwezi kuwatii watawala wa kibinadamu wanapotukataza kufanya kile ambacho Mungu anataka tufanye au wanapotaka tufanye kile ambacho Mungu anatukataza. Hivyo, “mamlaka zilizo kubwa” zikipiga marufuku kazi yetu ya kuhubiri tuliyopewa na Mungu, hatutaacha. (Rom. 13:1) Badala yake, tutaendelea kwa busara kutoa ushahidi kamili kuhusu Ufalme wa Mungu.

11 Si ajabu kwamba jibu la ujasiri ambalo mitume walitoa liliwafanya mahakimu hao wawe na hasira. Waliazimia “kuwaangamiza” mitume hao. (Mdo. 5:33) Mashahidi hao wenye ujasiri waliamini kabisa kwamba sasa wangeuawa kwa sababu ya imani yao. Hata hivyo, hawakujua kwamba msaada ulikuwa njiani!

“Hamtaweza Kuwaangamiza” (Mdo. 5:34-42)

12, 13. (a) Gamalieli aliwapa wenzake shauri gani, nao walifanya nini? (b) Yehova anawezaje kuwasaidia watu wake leo, na tunaweza kuwa na uhakika gani iwapo ataruhusu ‘tuteseke kwa ajili ya uadilifu’?

12 Gamalieli, “mwalimu wa Sheria aliyeheshimiwa na watu wote,” akaanza kuzungumza.c Gamalieli aliheshimiwa sana na mahakimu wenzake ndiyo sababu angeweza kuamuru “[mitume] hao watolewe nje kwa muda mfupi.” (Mdo. 5:34) Gamalieli alitaja vikundi fulani ambavyo vilisambaratika baada ya viongozi wao kufa. Kisha akahimiza mahakama hiyo iwe na subira inaposhughulika na mitume hao, ambao Kiongozi wao, Yesu, alikuwa amekufa hivi karibuni. Gamalieli alikuwa mwenye kusadikisha kwelikweli. Aliwaambia hivi: “Msiingilie mambo ya watu hawa, bali waacheni. Kwa maana, ikiwa mpango huu au kazi hii ni ya wanadamu, itaangamizwa; lakini ikiwa imetoka kwa Mungu, hamtaweza kuwaangamiza. La sivyo, huenda ikawa mnapigana na Mungu mwenyewe.” (Mdo. 5:38, 39) Mahakimu hao walimsikiliza, hata hivyo, wakawapiga viboko mitume na kuwaagiza “waache kusema kwa msingi wa jina la Yesu.”​—Mdo. 5:40.

13 Leo, kama ilivyokuwa wakati huo, Yehova anaweza kuwatumia watu mashuhuri kama Gamalieli kuwasaidia watu Wake. (Met. 21:1) Anaweza kutumia roho yake kuwafanya watawala wenye nguvu, mahakimu, au wanasheria watende kulingana na mapenzi yake. (Neh. 2:4-8) Hata hivyo, huenda wakati mwingine akaruhusu ‘tuteseke kwa ajili ya uadilifu.’ (1 Pet. 3:14) Akiruhusu iwe hivyo, tunaweza kuwa na uhakika wa mambo mawili. Kwanza, anaweza kutupatia nguvu za kuvumilia. (1 Kor. 10:13) Pili, wapinzani ‘hawataweza kuiangamiza’ kazi ya Mungu.​—Isa. 54:17.

14, 15. (a) Mitume walifanya nini walipopigwa, na kwa nini? (b) Simulia jambo lililoonwa linaloonyesha kwamba watu wa Yehova huvumilia kwa shangwe.

14 Je, mitume hao walivunjika moyo au kukata tamaa baada ya kupigwa viboko? Hapana! ‘Walitoka mbele ya Sanhedrini, wakishangilia.’ (Mdo. 5:41) “Wakishangilia”​—kwa nini? Hawakuwa wakishangilia maumivu waliyokuwa nayo kwa sababu ya kupigwa. Walishangilia kwa kuwa walijua kwamba wameteswa kwa sababu ya kuwa waaminifu kwa Yehova na kwa kufuata hatua za Kielelezo chao, Yesu.​—Mt. 5:11, 12.

15 Kama walivyofanya ndugu zetu wa karne ya kwanza, sisi pia huvumilia kwa shangwe tunapoteseka kwa sababu ya habari njema. (1 Pet. 4:12-14) Si kwamba tunafurahia tunapotishwa, tunapoteswa, au kufungwa gerezani. Hata hivyo, tunaridhika kwa kujua kwamba tunadumisha uaminifu wetu kwa Yehova. Kwa mfano, fikiria kisa cha Henryk Dornik, aliyeteswa kwa miaka mingi katika nchi iliyokuwa ikitawaliwa kimabavu. Anakumbuka kwamba mnamo Agosti 1944, wenye mamlaka waliamua kumpeleka yeye pamoja na ndugu yake katika kambi ya mateso. Wapinzani hao walisema hivi: “Huwezi kuwalazimisha kufanya chochote. Hata ukiwaua wanashangilia.” Ndugu Dornik anaeleza: “Ingawa si kwamba nilitaka kufa, kuteseka kwa sababu ya ushikamanifu wangu kwa Yehova kuliniletea shangwe.”​—Yak. 1:2-4.

Wenzi wakitumia Biblia na machapisho yanayotegemea Biblia kumhubiria mwanamume mbele ya nyumba yake.

Kama walivyofanya mitume, leo pia tunahubiri “nyumba kwa nyumba”

16. Mitume walionyesha jinsi gani kwamba walikuwa wameazimia kutoa ushahidi kamili, nasi tunafuata mfano wao kwa kufanya nini?

16 Mitume hao walirudia kazi yao bila kukawia. Bila woga, waliendelea “kila siku hekaluni na nyumba kwa nyumba” kufanya kazi ya “kutangaza habari njema kumhusu Kristo.”d (Mdo. 5:42) Wahubiri hao wenye bidii walikuwa wameazimia kutoa ushahidi kamili. Ona kwamba waliwapelekea watu ujumbe nyumbani kwao, kama vile Yesu Kristo alivyokuwa amewaagiza. (Mt. 10:7, 11-14) Ndiyo sababu ilidaiwa kwamba wamejaza Yerusalemu mafundisho yao. Leo pia, kama walivyofanya mitume, Mashahidi wa Yehova huhubiri nyumba kwa nyumba. Tunapohubiri kila nyumba katika eneo letu, tunaonyesha waziwazi kwamba sisi pia tunatoa ushahidi kamili, tukimpa kila mtu nafasi ya kusikia habari njema. Je, Yehova amebariki huduma yetu ya nyumba kwa nyumba? Ndiyo! Mamilioni ya watu wameitikia ujumbe wa Ufalme wakati huu wa mwisho. Wengi walisikia habari njema kwa mara ya kwanza Shahidi alipowatembelea.

KUHUBIRI “NYUMBA KWA NYUMBA”

Ingawa Sanhedrini ilikuwa imepiga marufuku kazi ya kuhubiri, wanafunzi waliendelea kuhubiri na kufundisha “kila siku hekaluni na nyumba kwa nyumba.” (Mdo. 5:42) Maneno “nyumba kwa nyumba” yanamaanisha nini?

Maneno ya Kigiriki yanayotafsiriwa “nyumba kwa nyumba,” katʼ oiʹkon, kihalisi yanamaanisha “kulingana na nyumba.” Watafsiri kadhaa wanasema neno ka·taʹ linamaanisha kwamba wanafunzi walihubiri kutoka nyumba moja hadi nyingine. Neno hilo ka·taʹ linatumiwa katika maana hiyohiyo katika andiko la Luka 8:1, linalosema kwamba Yesu alikuwa akihubiri “kutoka jiji mpaka jiji na kijiji mpaka kijiji.”

Katika Matendo 20:20, neno hilo linatumiwa katika wingi, yaani, katʼ oiʹkous. Mtume Paulo aliwaambia waangalizi Wakristo: “Sikuepuka . . . kuwafundisha hadharani na nyumba kwa nyumba.” Tofauti na maoni ya watu fulani, inaonekana Paulo hakuwa akisema kwamba alifundisha nyumbani kwa wazee hao, kama vile mstari unaofuata unavyoonyesha: “Lakini nilitoa ushahidi kikamili kwa Wayahudi na Wagiriki kuhusu toba kwa Mungu na kuwa na imani katika Bwana wetu Yesu.” (Mdo. 20:21) Waabudu wenzake tayari walikuwa wametubu na kumwamini Yesu. Hivyo, alihubiri na kufundisha nyumba kwa nyumba, akiwatolea ushahidi wasio waamini.

Wanaume Wanaostahili Washughulikie “Kazi Hii Muhimu” (Mdo. 6:1-6)

17-19. Ni jambo gani lililoleta mgawanyiko, na mitume walitoa maagizo gani?

17 Jambo fulani lenye kuhatarisha amani ya kutaniko lilikuwa limeanza kutokea. Ni jambo gani hilo? Wanafunzi wengi waliobatizwa walikuwa wageni Yerusalemu nao walitaka kujifunza mengi kabla ya kurudi kwao. Wanafunzi waliokuwa wakiishi Yerusalemu walitoa michango kwa hiari ili kuwalisha wageni hao na kuwaandalia mahitaji mengine. (Mdo. 2:44-46; 4:34-37) Ndipo, tatizo fulani likatokea. Wajane waliozungumza Kigiriki “walikuwa wakipuuzwa katika ugawaji wa kila siku.” (Mdo. 6:1) Hata hivyo, mahitaji ya wajane Waebrania hayakukosa kuangaliwa. Hivyo, inaonekana kwamba tatizo lilikuwa ubaguzi. Ubaguzi ni mojawapo ya matatizo ambayo huleta mgawanyiko mkubwa.

18 Mitume, waliokuwa wakitenda kama baraza linaloongoza la kutaniko hilo lililokuwa likizidi kuongezeka, waliona kwamba haifai ‘waache neno la Mungu ili kugawa chakula.’ (Mdo. 6:2) Ili kutatua jambo hilo, waliwaagiza wanafunzi watafute wanaume saba “waliojaa roho na hekima,” ambao mitume wangeweza kuwaweka rasmi juu ya “kazi [hiyo] muhimu.” (Mdo. 6:3) Mbali na kugawa chakula, huenda kazi hiyo ilitia ndani kushughulikia pesa, kununua bidhaa, na kuweka rekodi kwa uangalifu. Hivyo, wanaume wanaostahili walihitajika. Wanaume wote waliochaguliwa walikuwa na majina ya Kigiriki, jambo ambalo huenda lingewafanya wajane waliolalamika wahisi kwamba watatendewa haki. Baada ya kusali na kutafakari mapendekezo yaliyotolewa, mitume waliwaweka rasmi wanaume hao saba washughulikie “kazi [hiyo] muhimu.”e

19 Kwa kuwa wanaume hao walipewa kazi ya kugawa chakula, je, hawakuwa na wajibu wa kuhubiri habari njema? Hapana! Stefano, mmoja wa wanaume waliochaguliwa, alikuwa mhubiri jasiri na mwenye bidii. (Mdo. 6:8-10) Filipo, ambaye pia alikuwa mmoja wao, aliitwa “mweneza-injili.” (Mdo. 21:8) Ni wazi kwamba wanaume hao saba waliendelea kutangaza Ufalme kwa bidii.

20. Watu wa Yehova leo huigaje kielelezo cha mitume?

20 Watumishi wa Yehova leo hufanya kazi waliyofanya mitume. Lazima wanaume wanaopendekezwa kutimiza majukumu mbalimbali kutanikoni waonyeshe kwamba roho takatifu inatenda kazi ndani yao. Chini ya mwelekezo wa Baraza Linaloongoza, wanaume wanaotimiza sifa za Kimaandiko huwekwa rasmi watumikie wakiwa wazee wa kutaniko au watumishi wa huduma.f (1 Tim. 3:1-9, 12, 13) Kwa kuwa wanatimiza sifa hizo, basi wamewekwa rasmi na roho takatifu. Wanaume hao wenye bidii hutimiza kazi mbalimbali muhimu. Kwa mfano, huenda wazee wa kutaniko wakapanga ndugu na dada waaminifu waliozeeka wapate msaada wanaohitaji. (Yak. 1:27) Wazee wengine wana kazi nyingi katika ujenzi wa Majumba ya Ufalme, kupanga makusanyiko, au kazi ya Halmashauri ya Uhusiano na Hospitali. Watumishi wa huduma hutimiza majukumu mengi ambayo hayahusiani moja kwa moja na kazi ya uchungaji au ufundishaji. Wanaume wote hao wenye sifa za kustahili wanapaswa kuwa na usawaziko waposhughulikia majukumu ya kutaniko, mapendeleo katika tengenezo, na wajibu waliopewa na Mungu wa kuhubiri habari njema za Ufalme.​—1 Kor. 9:16.

“Neno la Mungu Likazidi Kuenea” (Mdo. 6:7)

21, 22. Tunajuaje kwamba Yehova alilibariki kutaniko la karne ya kwanza?

21 Yehova alitegemeza kutaniko hilo jipya kukabiliana na mateso kutoka nje ya kutaniko na pia tatizo lenye kutokeza mgawanyiko lililozuka ndani ya kutaniko. Ni wazi kwamba Yehova alilibariki kutaniko. Tunasoma hivi: “Neno la Mungu likazidi kuenea, na idadi ya wanafunzi ikazidi kuongezeka sana huko Yerusalemu; na umati mkubwa wa makuhani wakawa waamini.” (Mdo. 6:7) Hiyo ni mojawapo ya ripoti nyingi zilizo katika kitabu cha Matendo, zinazoonyesha maendeleo ya kutaniko la Kikristo. (Mdo. 9:31; 12:24; 16:5; 19:20; 28:31) Je, si ni kweli kwamba sisi pia hutiwa moyo tunaposikia ripoti kuhusu maendeleo ya kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme katika maeneo mengine?

22 Katika karne ya kwanza, viongozi wa kidini wenye hasira hawakuchoka. Baada ya muda mfupi wafuasi wa Yesu wangeanza kuteswa. Kwa mfano, Stefano aliteswa vikali, kama sura inayofuata itakavyoonyesha.

GAMALIELI​—RABI ALIYEHESHIMIWA SANA

Gamalieli anayetajwa katika kitabu cha Matendo, kwa kawaida anaitwa Mzee Gamalieli, mjukuu wa Hilleli, mwanzilishi wa mojawapo ya shule za Mafarisayo, ambayo haikushikilia mambo kupita kiasi. Gamalieli alikuwa na cheo kikubwa katika Sanhedrini, naye aliheshimiwa sana kati ya marabi hivi kwamba ndiye wa kwanza kuitwa kwa jina la cheo, “Rabani.” Mishna inasema hivi: “Rabani Mzee Gamalieli alipokufa, Sheria ilipoteza utukufu, na huo ukawa mwisho wa watakatifu na watawa.” Inasemekana kwamba alileta mabadiliko mengi yaliyowanufaisha watu mbalimbali. “Uamuzi mmoja muhimu aliofanya,” kulingana na Encyclopaedia Judaica, “ni kumruhusu mwanamke aolewe tena iwapo kuna ushahidi wa angalau mtu mmoja aliyeshuhudia kifo cha mume wa mwanamke huyo.” Pia, inasemekana kwamba alitunga sheria za kuwalinda wake dhidi ya waume wasiowajali na wajane dhidi ya watoto wasiowajali. Na pia inadaiwa kwamba alisema Watu wa Mataifa waliokuwa maskini walipaswa kuwa na haki sawa za kuokota vyakula kama Wayahudi maskini.

a Ona sanduku lenye kichwa “Sanhedrini—Mahakama Kuu ya Wayahudi,.”

b Hii ndiyo mara ya kwanza kati ya mara 20 hivi ambapo malaika wanatajwa moja kwa moja katika kitabu cha Matendo. Mapema zaidi, andiko la Matendo 1:10 linazungumzia malaika kwa njia isiyo ya moja kwa moja likiwaita ‘wanaume wenye mavazi meupe.’

c Ona sanduku lenye kichwa “Gamalieli—Rabi Aliyeheshimiwa Sana,.”.

d Ona sanduku lenye kichwa “Kuhubiri ‘Nyumba kwa Nyumba,’.”

e Yawezekana kwamba wanaume hao walikuwa wametimiza sifa za kustahili kuwa wazee, kwa sababu “kazi [hiyo] muhimu” ilikuwa mgawo mzito. Hata hivyo, Maandiko hayataji wakati hususa ambapo akina ndugu walianza kuwekwa rasmi kutumikia wakiwa wazee au waangalizi katika kutaniko la Kikristo.

f Katika karne ya kwanza, wanaume wanaostahili waliruhusiwa kuwaweka rasmi wazee. (Mdo. 14:23; 1 Tim. 5:22; Tito 1:5) Leo, Baraza Linaloongoza huwaweka rasmi waangalizi wa mzunguko, na waangalizi hao wana jukumu la kuwaweka rasmi wazee wa kutaniko na watumishi wa huduma.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki