Samehe Kutoka Katika Moyo Wako
“Kwa njia kama hiyo Baba yangu wa kimbingu atashughulika nanyi pia ikiwa hamsamehi kila mmoja ndugu yake kutoka katika mioyo yenu.”—MATHAYO 18:35.
1, 2. (a) Mtenda-dhambi aliyejulikana sana alionyeshaje kwamba alimthamini Yesu? (b) Yesu alikazia nini katika jibu lake?
YAELEKEA mwanamke huyo alikuwa malaya, na hungetarajia kumkuta katika nyumba ya mtu wa kidini. Ikiwa watu wengine walishtuka kumwona huko, matendo yake hata yalishtusha zaidi. Alimfikia mtu mwenye maadili bora zaidi na kuonyesha kwamba alithamini kazi za mtu huyo kwa kumwosha miguu kwa machozi yake na kuipangusa kwa nywele zake.
2 Mtu huyo, ambaye ni Yesu, hakuchukizwa na mwanamke huyo, “aliyejulikana katika jiji kuwa mtenda-dhambi.” Lakini Simoni Farisayo, mwenye nyumba hiyo, alihangaika kwamba mwanamke huyo ni mtenda-dhambi. Yesu akajibu kwa kusimulia juu ya watu wawili waliokuwa wadeni kwa mkopeshaji fulani. Mmoja wao alikuwa na deni kubwa sana—mshahara wa miaka miwili hivi wa kibarua. Yule mwingine alikuwa na deni linalotoshana na sehemu moja kwa kumi ya deni la yule wa kwanza—mshahara wa muda unaopungua miezi mitatu. Wote waliposhindwa kulipa madeni hayo, yule mkopeshaji “aliwasamehe kwa hiari wote wawili.” Bila shaka, yule aliyesamehewa mengi zaidi alikuwa na sababu kubwa zaidi ya kuonyesha upendo. Baada ya Yesu kuhusisha masimulizi hayo na tendo la fadhili la mwanamke huyo, aliongezea kutaja kanuni hii: “Yeye ambaye asamehewa kidogo, hupenda kidogo.” Kisha akamwambia huyo mwanamke: “Dhambi zako zimesamehewa.”—Luka 7:36-48.
3. Twahitaji kufikiria nini juu yetu sisi wenyewe?
3 Jiulize, ‘Kama ningalikuwa mwanamke huyo au kama ningalikuwa katika hali kama yake halafu nionyeshwe rehema, je, mimi ningalikuwa mgumu sana wa kuwasamehe wengine?’ Huenda ukajibu, ‘La, hasha!’ Hata hivyo, je, kweli unaamini kwamba una mwelekeo wa kusamehe? Je, una tabia ya kusamehe? Je, mara nyingi umesamehe kwa utayari, na je, wengine hukuona kuwa mtu mwenye kusamehe? Ebu tuone ni kwa nini kila mmoja wetu anapaswa kujichunguza kwa unyofu kuhusu kusamehe.
Twahitaji Kusamehewa —Nasi Husamehewa
4. Twapaswa kukiri nini juu yetu sisi wenyewe?
4 Unajua vizuri sana kwamba wewe hujakamilika. Hata wewe mwenyewe ukiulizwa utakubali, labda ukikumbuka maneno yanayopatikana kwenye 1 Yohana 1:8: “Ikiwa twatoa taarifa: ‘Sisi hatuna dhambi yoyote,’ tunajiongoza wenyewe vibaya na kweli haimo katika sisi.” (Waroma 3:23; 5:12) Huenda wengine walikuwa na dhambi nzito zenye kuchukiza. Lakini hata kama unajua wewe hujafanya dhambi nzito kama hizo, bila shaka kuna nyakati nyingi na njia nyingi ambazo umekosa kufikia viwango vya Mungu—ukatenda dhambi. Sivyo?
5. Twapaswa kumshukuru Mungu kwa ajili ya nini?
5 Kwa hiyo, hali yako inaweza kulingana na ufafanuzi wa mtume Paulo: “Ingawa nyinyi mlikuwa wafu katika makosa yenu na katika hali ya kutotahiriwa ya mwili wenu, Mungu aliwafanya nyinyi kuwa hai pamoja naye [Yesu]. Yeye alitusamehe kwa fadhili makosa yetu yote.” (Wakolosai 2:13; Waefeso 2:1-3) Ona maneno haya “alitusamehe kwa fadhili makosa yetu yote.” Hayo yanatia ndani mambo mengi sana. Kila mmoja wetu ana sababu nzuri za kusihi kama alivyosihi Daudi: “Ee BWANA, kwa ajili ya jina lako, unisamehe uovu wangu, maana ni mwingi.”—Zaburi 25:11, italiki ni zetu.
6. Twaweza kuwa na hakika gani kuhusu Yehova na msamaha?
6 Wewe—au yeyote kati yetu—wawezaje kusamehewa? Jambo kuu ni kwamba Yehova Mungu ana mwelekeo wa kusamehe. Hiyo ni sifa ya utu wake. (Kutoka 34:6, 7; Zaburi 86:5) Inaeleweka kwamba Mungu hututazamia tumwendee katika sala na kumwomba radhi, tukimwomba atusamehe. (2 Mambo ya Nyakati 6:21; Zaburi 103:3, 10, 14) Naye amepanga kuwe na msingi halali wa kuonyesha msamaha—dhabihu ya fidia ya Yesu.—Waroma 3:24; 1 Petro 1:18, 19; 1 Yohana 4:9, 14.
7. Inatakikana umwige Yehova katika njia gani?
7 Utayari wa Mungu wa kusamehe unatoa kielelezo cha jinsi wewe unavyopaswa kuwatendea wanadamu wengine. Paulo alikazia jambo hilo alipoandika: “Iweni wenye fadhili nyinyi kwa nyinyi, wenye huruma kwa njia nyororo, mkisameheana kwa hiari mtu na mwenzake kama vile Mungu pia kupitia Kristo alivyowasamehe nyinyi kwa hiari.” (Waefeso 4:32) Hakuna shaka kwamba jambo analokazia Paulo lahusu kujifunza kwetu kutokana na kielelezo cha Mungu, kwa sababu mstari ufuatao waendelea kusema: “Kwa hiyo, iweni waigaji wa Mungu, mkiwa watoto wapendwa.” (Waefeso 5:1) Je, waona uhusiano uliopo kati ya mambo hayo? Yehova Mungu alikusamehe, basi—Paulo asababu kwa kutilia mkazo—unahitaji kumwiga Mungu na kuwa ‘mwenye huruma kwa njia nyororo, ukisamehe wengine kwa hiari.’ Lakini jiulize, ‘Je, ninafanya hivyo? Ikiwa si kawaida yangu kusamehe, je, nafanyia kazi jambo hilo, nikijitahidi kwelikweli kumwiga Mungu katika kusamehe?’
Twahitaji Kujitahidi Kuwa Wenye Kusamehe
8. Twapaswa kutambua nini kuhusu watu walio katika kutaniko letu?
8 Ingekuwa vizuri kufikiri kwamba katika kutaniko la Kikristo, kuna pindi chache ambazo ni lazima tufuate mwendo wa kimungu wa kusamehe. Lakini sivyo hali ilivyo. Ni kweli kwamba ndugu na dada zetu Wakristo wanajaribu kufuata kielelezo cha Yesu cha kuonyesha upendo. (Yohana 13:35; 15:12, 13; Wagalatia 6:2) Wao wamejitahidi kwa muda mrefu, na wangali wanajitahidi, kuacha njia za kufikiri, kusema, na kutenda ambazo zimejaa katika ulimwengu huu mwovu. Kwa kweli wao wanataka kudhihirisha utu mpya. (Wakolosai 3:9, 10) Lakini, hatuwezi kupuuza uhakika wa kwamba kutaniko la duniani pote, na kila kutaniko, lina watu wasiokamilika. Kwa hakika, kwa ujumla wao ni bora kuliko walivyokuwa pindi moja, lakini bado hawajakamilika.
9, 10. Kwa nini hatupaswi kushangaa matatizo yakitokea kati ya akina ndugu?
9 Katika Biblia, Mungu atuambia wazi kwamba tunaweza kutarajia hali ya kutokamilika katika kutaniko miongoni mwa ndugu na dada zetu. Kwa mfano, fikiria maneno ya Paulo yaliyorekodiwa kwenye Wakolosai 3:13: “Endeleeni kuchukuliana mtu na mwenzake na kusameheana kwa hiari mtu na mwenzake ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika dhidi ya mwingine. Kama vile Yehova alivyowasamehe nyinyi kwa hiari, fanyeni hivyo nyinyi pia.”
10 Jambo muhimu ni kwamba hapo Biblia inatukumbusha juu ya uhusiano uliopo baina ya msamaha wa Mungu na wajibu na uhitaji wetu wa kuwasamehe wengine. Kwa nini ni vigumu kusamehe? Kwa sababu Paulo alikiri kwamba mtu anaweza kuwa na “sababu ya kulalamika dhidi ya mwingine.” Alitambua kwamba sababu kama hizo zingekuwapo. Ni lazima zilikuwapo katika karne ya kwanza, hata miongoni mwa Wakristo “watakatifu,” waliokuwa na ‘tumaini ambalo limewekwa akiba kwa ajili yao katika mbingu.’ (Wakolosai 1:2, 5) Basi, je, tuseme kwamba hali ingekuwa tofauti leo ambapo Wakristo wengi wa kweli hawana ushuhuda wa roho kwamba wao ni “wachaguliwa wa Mungu, watakatifu na wapendwa”? (Wakolosai 3:12) Kwa hiyo, hatupaswi kukata kauli ya kwamba kuna kasoro fulani mbaya sana ikiwa katika kutaniko letu kuna sababu za kulalamika—kuumizwa kwa sababu ya makosa ya kweli au yale yanayoonwa kuwa makosa.
11. Mwanafunzi Yakobo alitutahadharisha juu ya nini?
11 Maneno ya Yakobo ndugu-nusu ya Yesu pia yaonyesha kwamba ni lazima tutarajie kwamba angalau mara kwa mara tutapata hali ambazo tutahitaji kuwasamehe ndugu zetu. “Ni nani aliye mwenye hekima na mwenye kuelewa miongoni mwenu? Acheni aonyeshe kutokana na mwenendo wake bora kazi zake kwa upole ulio wa hekima. Lakini ikiwa nyinyi mna wivu wenye uchungu na ugomvi katika mioyo yenu, msiwe mkijigamba na kusema uwongo dhidi ya kweli.” (Yakobo 3:13, 14) “Wivu wenye uchungu na ugomvi” katika mioyo ya Wakristo wa kweli? Ndiyo, maneno ya Yakobo yaonyesha wazi kwamba mambo hayo yalikuwa yametokea katika kutaniko la karne ya kwanza nayo yatatokea leo.
12. Kulitokea tatizo gani katika kutaniko la kale la Filipi?
12 Mfano halisi ulihusu Wakristo wawili watiwa-mafuta ambao walikuwa na sifa nzuri ya kufanya kazi kwa bidii pamoja na Paulo. Huenda unakumbuka kusoma juu ya Euodia na Sintike, washiriki wa kutaniko la Filipi. Japo andiko la Wafilipi 4:2, 3 halifafanui kisa chao kindani, linaonyesha kwamba kulikuwa na tatizo kati yao. Je, tatizo hilo lilianza kwa maneno yasiyo yenye fadhili yaliyosemwa bila kufikiri, jambo lililoonwa kuwa madharau dhidi ya mtu wa ukoo, au uthibitisho fulani wa wivu wenye ushindani? Liwe lilikuwa nini, tatizo hilo lilipata kuwa baya sana hivi kwamba Paulo alilisikia akiwa mbali sana kule Roma. Huenda dada hao wawili wa kiroho walinyamaziana, na kufanya waepukane mikutanoni au kuambia rafiki zao maneno mabaya juu ya yule mwingine.
13. Yaelekea Euodia na Sintike walitatuaje tatizo lao, tukipata somo gani?
13 Je, umewahi kusikia jambo kama hilo, likifanana na jambo lililotokea katika kutaniko lenu au lililokuhusisha? Huenda tatizo kama hilo lipo sasa kwa kiasi fulani. Tunaweza kufanya nini? Katika kile kisa cha zamani, Paulo aliwahimiza dada hao wawili waliojiweka wakfu “wawe wenye akili ileile katika Bwana.” Huenda walikubali kuzungumzia jambo hilo, kusuluhisha tatizo hilo, kuonyesha utayari wa kusameheana, kisha kwa kweli kuiga mtazamo wa Yehova wa kusamehe. Hakuna sababu ya kufikiria vingine ila kwamba Euodia na Sintike walifaulu, nasi pia twaweza kufaulu. Mtazamo kama huo wa kusamehe waweza kutumika leo kwa mafanikio.
Fanya Amani—Samehe
14. Kwa nini mara nyingi inawezekana na ni bora kuziachilia tofauti za kibinafsi?
14 Ni nini kinachohitajika kwa kweli ili usamehe kunapokuwa na tatizo kati yako na Mkristo mwingine? Kwa wazi, hakuna hata njia moja rahisi, lakini Biblia hutoa vielelezo vizuri na mashauri halisi. Pendekezo kuu—ingawa si rahisi kukubaliwa na kutumiwa—ni kusahau tu jambo hilo, kuliachilia tu. Mara nyingi tatizo linapozuka, kama ilivyokuwa kati ya Euodia na Sintike, kila mtu huhisi kwamba yule mwingine ndiye mwenye makosa au ndiye wa kulaumiwa zaidi. Basi katika hali kama hiyo, huenda ukafikiri kwamba yule Mkristo mwingine ndiye mwenye makosa au ndiye wa kulaumiwa zaidi. Lakini, je, huwezi kuliachilia tu jambo hilo kwa kusamehe? Tambua kwamba ikiwa yule Mkristo mwingine ndiye amechangia zaidi hali hiyo au ndiye pekee mwenye makosa, japo haielekei kuwa hivyo, wewe uko katika hali nzuri kabisa ya kuliachilia jambo hilo kwa kusamehe na kulimaliza.
15, 16. (a) Mika alimfafanuaje Yehova? (b) Inamaanisha nini kwamba Mungu ‘anaachilia kosa’?
15 Tusisahau kwamba Mungu ndiye kielelezo chetu katika kusamehe. (Waefeso 4:32–5:1) Kuhusu kielelezo cha Mungu cha kuachilia kosa, nabii Mika aliandika: “Ni nani aliye Mungu kama wewe, mwenye kusamehe uovu, na kuliachilia kosa la watu wa urithi wake waliosalia? hashiki hasira yake milele, kwa maana yeye hufurahia rehema.”—Mika 7:18.
16 Kwa kumfafanua Yehova kuwa mwenye ‘kuachilia kosa,’ Biblia haisemi kwamba yeye hawezi kuyasahau makosa, kwa njia fulani akisahau makosa mengine. Fikiria visa vya Samsoni na Daudi, wote wawili walifanya makosa mazito. Mungu aliweza kuzikumbuka dhambi hizo muda mrefu baadaye; na hata sisi twajua baadhi ya dhambi zao kwa sababu Yehova alifanya ziandikwe katika Biblia. Na bado, Mungu wetu mwenye kusamehe aliwaonyesha rehema, akiwataja kuwa vielelezo vya imani tunaopaswa kuiga.—Waebrania 11:32; 12:1.
17. (a) Ni hali gani iwezayo kutusaidia kuachilia makosa ya wengine? (b) Tukijaribu kufanya hivyo, tutakuwa tukimwigaje Yehova? (Ona kielezi-chini.)
17 Naam, Yehova aliweza ‘kuyaachilia’a makosa, kama ambavyo Daudi alimwomba tena na tena ayaachilie. (2 Samweli 12:13; 24:10) Je, tunaweza kumwiga Mungu katika jambo hilo, kwa kuwa tayari kuachilia mambo yenye kuudhi na makosa ambayo watumishi wenzetu wanafanya wakiwa wanadamu wasiokamilika? Ebu wazia ukiwa katika ndege inayoondoka kwenye uwanja. Unapotazama nje, karibu na njia ya ndege unaona mtu unayemfahamu akitoa nje ulimi wake kwa njia ya kitoto yenye kuudhi. Unajua kwamba alikuwa amekasirika na huenda ni wewe anayekufanyia dhihaka hiyo. Au huenda hata si wewe anayekufikiria. Hata hivyo, ndege hiyo izungukapo ikipaa juu, unapita juu sana ya mwanamke yule, ambaye sasa anaonekana kama doa tu. Baada ya muda wa saa moja uko umbali wa mamia ya kilometa, na tayari umesahau kabisa dhihaka yake. Vivyo hivyo, mara nyingi tutasaidiwa kusamehe tukijaribu kuiga Yehova na kuliachilia kosa hilo kwa hekima. (Mithali 19:11) Je, kosa hilo halitaonekana kuwa jambo dogo sana miaka kumi ijayo au miaka mia mbili katika Milenia? Mbona usiliachilie tu?
18. Tukiona kama hatuwezi kuachilia kosa, tunaweza kutumia shauri gani?
18 Katika visa vichache, huenda umesali juu ya jambo hilo na kujaribu kusamehe, lakini unaona kwamba huwezi kusamehe? Ufanyeje sasa? Yesu alihimiza kwamba umwendee yule aliyekukosea na kujaribu kusuluhisha tofauti zenu kwa faragha ili mfanye amani. “Basi, ikiwa wewe unaleta zawadi yako kwenye madhabahu na huko wakumbuka kwamba ndugu yako ana jambo fulani dhidi yako, acha zawadi yako hapo mbele ya madhabahu, na uende zako; kwanza fanya amani yako na ndugu yako, na ndipo, ukiisha kurudi, toa zawadi yako.”—Mathayo 5:23, 24.
19. Twapaswa kuwa na mtazamo gani na twapaswa kuepuka mtazamo gani tunapofuatia amani na ndugu yetu?
19 Jambo la maana ni kwamba Yesu hakusema umwendee ndugu yako ukamsadikishe kwamba wewe huna kosa na kwamba ni yeye aliyekosea. Labda alikosea. Lakini yaelekea sana kwamba kila mmoja wenu alikosea kwa njia fulani. Hata hivyo, lengo si kumlazimisha yule mwingine akubali kosa, au anyenyekee. Ikiwa hilo ndilo lengo lako la mazungumzo, haielekei utafaulu. Wala si lazima lengo liwe kupitia kila kijambo kidogo cha kosa lililofanywa au linalowaziwa tu. Wakati mazungumzo matulivu katika roho ya upendo wa Kikristo yafunuapo kwamba kwa kusikitisha ni kutoelewana ndiko kumesababisha tatizo, nyote wawili mwaweza kujaribu kusuluhisha tatizo hilo. Hata kama hamkubaliani kabisa kwenye mazungumzo hayo, je, ni lazima mkubaliane nyakati zote? Je, haingekuwa afadhali ikiwa angalau mwakubaliana kwamba nyote wawili mnataka kumtumikia kwa unyofu Mungu mwenye kusamehe? Ukabilipo hali hiyo, huenda ikawa rahisi kwa kila mmoja kusema kutoka moyoni, “Pole kwamba kwa sababu ya kutokamilika tumekuwa na tofauti hii. Tafadhali tuiachilie.”
20. Twaweza kujifunza nini kutokana na kielelezo cha mitume?
20 Kumbuka kwamba mitume walikuwa na tofauti zao, kama wakati ambapo wengine wao walitaka utukufu zaidi. (Marko 10:35-39; Luka 9:46; 22:24-26) Jambo hilo lilisababisha uvutano, labda wengine wakaumizwa, au hata kuudhika sana. Lakini wao waliachilia tofauti hizo na kuendelea kufanya kazi pamoja. Baadaye mmoja wao aliandika: “Yeye ambaye angependa uhai na kuona siku zilizo njema, acheni azuie ulimi wake kutokana na lililo baya na midomo yake isiseme udanganyo, lakini acheni ageuke mbali kutoka lililo baya na kufanya lililo jema; acheni atafute sana amani na kuifuatia.”—1 Petro 3:10, 11.
21. Yesu alitoa shauri gani muhimu juu ya kusamehe?
21 Mwanzoni tulishughulikia sehemu moja ya mazungumzo yetu: Mungu alitusamehe dhambi nyingi tulizofanya wakati uliopita, basi tunapaswa kumwiga na kuwasamehe ndugu zetu. (Zaburi 103:12; Isaya 43:25) Lakini kuna sehemu nyingine ya mazungumzo hayo. Baada ya kuandaa ile sala ya kigezo, Yesu alisema: “Ikiwa mwasamehe watu makosa yao, Baba yenu wa kimbingu atawasamehe nyinyi pia.” Zaidi ya mwaka mmoja baadaye, alirudia kutaja wazo kuu la jambo hilo, akiwafundisha wanafunzi wake wasali hivi: “Utusamehe dhambi zetu, kwa maana sisi wenyewe pia husamehe kila mtu aliye na deni letu.” (Mathayo 6:12, 14; Luka 11:4) Kisha, siku chache tu kabla ya kifo chake, Yesu aliongezea kusema: “Msimamapo mkisali, sameheni chochote kile mlicho nacho dhidi ya yeyote; ili Baba yenu aliye katika mbingu apate kuwasamehe makosa yenu nyinyi pia.”—Marko 11:25.
22, 23. Utayari wetu wa kusamehe waweza kuathirije wakati wetu ujao?
22 Naam, kuendelea kupokea msamaha wa Mungu kwategemea sana utayari wetu wa kuwasamehe wengine. Tatizo la kibinafsi likizuka kati ya Wakristo, jiulize, ‘Je, si ni muhimu zaidi kupata msamaha wa Mungu kuliko kuthibitisha kwamba ndugu au dada alikosea kidogo tu, au kukazia kutokamilika fulani kwa wanadamu?’ Unajua jibu.
23 Lakini, namna gani ikiwa jambo hilo ni zito kuliko kosa au tatizo dogo tu la kibinafsi? Na shauri la Yesu linalopatikana kwenye Mathayo 18:15-18 latumika wakati gani? Ebu tuchunguze mambo hayo.
[Maelezo ya Chini]
a Msomi mmoja asema kwamba neno la kitamathali la Kiebrania lililotumiwa katika Mika 7:18 “limetokana na tabia ya msafiri ambaye anapita bila kuona kitu ambacho hataki kukifikiria. Halimaanishi kwamba Mungu haoni dhambi, wala kwamba anaiona kuwa jambo dogo au lisilo muhimu, bali kwamba haioni katika visa fulani hususa ili atoe adhabu; kwamba hatoi adhabu, bali asamehe.”—Waamuzi 3:26; 1 Samweli 16:8.
Je, Wakumbuka?
◻ Yehova anatuwekeaje kiolezo cha kufuata cha msamaha?
◻ Ni lazima tukumbuke nini juu ya wale walio katika kutaniko?
◻ Katika hali nyingi, twapaswa kuwa na uwezo wa kufanya nini juu ya makosa au mambo yenye kuudhi?
◻ Ikihitajika, twaweza kufanya nini ili kufanya amani na ndugu yetu?
[Picha katika ukurasa wa 15]
Kukizuka tofauti kati yako na Mkristo mwingine, jaribu kuliachilia; tatizo hilo litazidi kuwa dogo muda uzidipo kupita