Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • “Mahali Ambapo Kijito Hicho Kinapita, Kila Kitu Kitaishi”
    Hatimaye Ibada Safi ya Yehova Yarudishwa!
    • Ezekieli akitembea ndani ya mto unaotiririka huku mwanamume anayeonekana kama shaba akimtazama kutoka kwenye ukingo wa mto.

      SURA YA 19

      “Mahali Ambapo Kijito Hicho Kinapita, Kila Kitu Kitaishi”

      EZEKIELI 47:9

      WAZO KUU: Jinsi maono ya mto unaotiririka kutoka hekaluni yalivyotimizwa nyakati za kale, yanavyotimiza sasa, na wakati ujao

      1, 2. Kulingana na Ezekieli 47:1-12, Ezekieli anaona na kujifunza nini? (Tazama picha mwanzoni mwa sura hii.)

      EZEKIELI anaona jambo lingine lenye kushangaza katika maono ya hekalu: Kijito kinachotiririka kutoka katika jengo takatifu! Mwazie akichunguza mkondo wa maji hayo yaliyo safi kabisa. (Soma Ezekieli 47:1-12.) Yanatiririka kutoka patakatifu; kisha yanatoka kwenye majengo ya hekalu karibu na lango la mashariki. Malaika anamwongoza Ezekieli kwenda nje ya hekalu, wanapima huku wakienda. Malaika anamwagiza Ezekieli tena na tena apite katika maji, na nabii huyo anatambua kwamba kina cha maji kinaongezeka haraka, na baada ya muda mfupi yanakuwa mengi sana hivi kwamba anaweza tu kuvuka kwa kuogelea!

      2 Ezekieli anatambua kwamba mto huo unaingia kwenye Bahari ya Chumvi na kila mahali ambapo maji ya mto yanafika yanaponya maji yenye chumvi yasiyo na uhai, na kufanya yawe na samaki wengi. Kwenye kingo za mto, anaona miti mingi ya kila aina ikikua. Kila mwezi, inazaa matunda yenye lishe na kuchipua majani yanayoponya. Ezekieli anapoona mambo hayo yote, moyo wake unakuwa na amani na tumaini. Lakini sehemu hii ya maono ya hekalu ilimaanisha nini kwa Ezekieli na kwa wahamishwa wenzake? Na inamaanisha nini kwetu leo?

      Mto Alioona Ezekieli Ulimaanisha Nini kwa Wahamishwa?

      3. Kwa nini Wayahudi wa nyakati za kale walijua kwamba mto ambao Ezekieli aliona haukuwa halisi?

      3 Kwa kweli, Wayahudi wa kale walijua kwamba mto huo haukuwa halisi. Badala yake, inaelekea kwamba simulizi hilo la Maandiko liliwakumbusha unabii mwingine wa kurudishwa, ambao nabii Yoeli aliandika labda zaidi ya karne mbili mapema. (Soma Yoeli 3:18.) Wahamishwa Wayahudi waliposoma unabii wa Yoeli, hawakutazamia kwamba milima ‘ingedondosha divai tamu’ kihalisi au vilima ‘vingetiririka maziwa’; wala hawakutazamia kwamba kijito kingetiririka “kutoka katika nyumba ya Yehova.” Vivyo hivyo, huenda Wayahudi wenzake walielewa kwamba ujumbe wa maono ya nabii Ezekieli haukuhusu mto halisi.a Basi, Yehova alikuwa akitoa ujumbe gani? Maandiko yanatusaidia kuelewa baadhi ya mambo katika maono hayo. Hata hivyo, kwa ujumla tutachunguza katika simulizi hili la kinabii mambo matatu yaliyo wazi yanayotupatia uhakika.

      Mto unaotiririka

      SANDUKU LA KUFUNDISHIA LA 19A: Mito ya Baraka Kutoka kwa Yehova

      4. (a) Mto ambao Ezekieli aliona ulifanya Wayahudi watazamie baraka gani kutoka kwa Yehova? (b) Katika Biblia maneno “mto” na “maji” yanatuhakikishiaje kwamba Yehova atawabariki watu wake? (Tazama sanduku “Mito ya Baraka Kutoka kwa Yehova.”)

      4 Mto wa baraka. Katika Biblia, mara nyingi mito na maji hutumiwa kuonyesha kutiririka kwa baraka za Yehova zinazoleta uhai. Ezekieli aliona mto kama huo ukitiririka kutoka hekaluni, basi maono hayo yangewafanya watu wa Mungu watazamie kupata baraka za kiroho za Yehova zinazoleta uhai ikiwa tu wangeshikamana na ibada safi. Ni baraka gani? Wangepokea tena maagizo ya kiroho kutoka kwa makuhani. Dhabihu zingetolewa hekaluni, na hivyo wangekuwa tena na uhakika kwamba dhambi zao zingefunikwa. (Eze. 44:15, 23; 45:17) Hivyo, wangekuwa safi tena, kana kwamba wameoshwa kwa maji safi yanayotoka hekaluni.

      5. Maono ya mto yanaonyeshaje kwamba kutakuwa na baraka za kuwatosha watu wote?

      5 Je, sikuzote kungekuwa na baraka za kuwatosha watu wote? Maono hayo yanatoa uhakikisho kwa kuonyesha maji yanayoongezeka kimuujiza—maji kidogo yanayotiririka ambayo baada ya kilomita mbili hivi yanakuwa mengi sana! (Eze. 47:3-5) Huenda idadi ya Wayahudi waliorudishwa ingeongezeka; lakini baraka za Yehova zingeongezeka ili kutosheleza uhitaji huo. Mto huo uliwakilisha maandalizi mengi sana!

      6. (a) Maono hayo ya kinabii yalitoa ahadi gani yenye kufariji? (b) Maono hayo pia yalitoa onyo gani? (Tazama maelezo ya chini.)

      6 Maji yanayoleta uhai. Katika maono ya Ezekieli, mto uliingia kwenye Bahari ya Chumvi, na kuponya sehemu kubwa ya bahari hiyo. Ona kwamba maji hayo yalitokeza samaki wengi wa aina mbalimbali kama samaki walio katika Bahari Kuu, yaani, Bahari ya Mediterania. Pia, kulikuwa na biashara kubwa ya uvuvi kwenye ufuo wa Bahari ya Chumvi katika miji miwili ambayo haikuwa imekaribiana sana. Malaika alisema: “Mahali ambapo kijito hicho kinapita, kila kitu kitaishi.” Je, hilo linamaanisha kwamba maji yanayotoka katika nyumba ya Yehova yalifika kila mahali katika Bahari ya Chumvi? Hapana. Malaika alieleza kwamba kulikuwa na sehemu zenye matope ambazo hazikufikiwa na maji yanayoleta uhai. Sehemu hizo ‘zingebaki zikiwa sehemu za chumvi.’b (Eze. 47:8-11) Basi maono hayo ya kinabii yalitoa ahadi yenye kufariji kwamba ibada safi ingewafanya watu wawe hai, na wasitawi. Lakini pia onyo hili lililotolewa: Si watu wote ambao wangekubali baraka za Yehova; wala si wote wangeponywa.

      7. Miti iliyo kwenye kingo za mto katika maono iliwapa Wayahudi waliohamishwa uhakikisho gani?

      7 Miti kwa ajili ya chakula na kuponya. Namna gani miti iliyokuwa kwenye kingo za mto? Inafanya maono hayo yapendeze zaidi, sivyo? Pia, inaongeza maana ya maono hayo. Kwa hakika, Ezekieli na Wayahudi wenzake walifurahia kufikiria kuhusu matunda matamu ya miti hiyo, ambayo ingezaa kila mwezi! Unabii huo wenye kuvutia uliwahakikishia kwamba Yehova angewalisha kiroho. Uliwahakikishia jambo gani lingine? Ona kwamba majani ya miti hiyo ‘yangetumiwa kuponya.’ (Eze. 47:12) Yehova alijua kwamba kuliko jambo lingine lolote, wahamishwa waliorudishwa wangehitaji kuponywa kiroho, na aliahidi kufanya hivyo. Unabii mwingine wa kurudishwa ulionyesha jinsi alivyofanya hivyo, kama tulivyoona kwenye Sura ya 9 ya kitabu hiki.

      8. Ni nini kinachoonyesha kwamba unabii wa Ezekieli ungetimizwa kwa njia kubwa zaidi?

      8 Hata hivyo, kama tulivyozungumzia kwenye Sura ya 9, wahamishwa waliorudi waliona utimizo mdogo tu wa unabii huo. Watu ndio waliofanya unabii huo utimizwe kwa njia ndogo. Yehova angewezaje kuwabariki kikamili huku wakirudia njia zao mbaya, wakikosa kutii, na kupuuza ibada safi mara kwa mara? Watu waaminifu waliumia na kuvunjwa moyo na mwenendo wa Wayahudi wenzao. Hata hivyo, waabudu washikamanifu wa Yehova walijua kwamba ahadi zake hazikosi kamwe kutimia; zinatimia sikuzote. (Soma Yoshua 23:14.) Hivyo, siku moja unabii wa Ezekieli ungetimizwa kwa njia kubwa zaidi. Ungetimizwa lini?

      Jinsi Mto Huo Unavyotiririka Leo!

      9. Maono ya hekalu aliloona Ezekieli yanatimizwa lini kwa njia kubwa zaidi?

      9 Kama tulivyoona kwenye Sura ya 14 ya kitabu hiki, maono ya hekalu aliloona Ezekieli yanatimizwa kwa njia kubwa zaidi katika “siku za mwisho,” ambapo ibada safi imeinuliwa kuliko wakati mwingine wowote. (Isa. 2:2) Maono hayo ya Ezekieli yanatimizwaje leo?

      10, 11. (a) Leo, tunapata baraka gani zinazotiririka kama mto? (b) Baraka zinazotiririka kutoka kwa Yehova zimeongezekaje ili kutimiza uhitaji unaoongezeka katika siku za mwisho?

      10 Mto wa baraka. Maji yanayotiririka kutoka kwenye nyumba ya Yehova yanatukumbusha baraka gani leo? Kwa kweli, yanatukumbusha mambo mengi ambayo Yehova anatuandalia ili kutunufaisha kiroho. Jambo muhimu zaidi ni dhabihu ya fidia ya Kristo inayosafisha, ambayo hutuwezesha kupata msamaha wa dhambi. Kweli safi za Neno la Mungu zinalinganishwa pia na maji yanayoleta uhai, ambayo husafisha. (Efe. 5:25-27) Baraka hizo zimetiririkaje leo?

      11 Mwaka wa 1919 idadi ya watumishi wa Yehova ilikuwa elfu kadhaa, na walishangilia kupata chakula cha kiroho walichohitaji. Miaka iliyofuata, idadi yao ilizidi kuongezeka. Leo, idadi ya watu wa Mungu ni zaidi ya milioni nane. Je, maji safi ya kweli yamezidi kuongezeka? Ndiyo! Tumepata ufafanuzi mwingi sana wa kweli za kiroho. Katika karne iliyopita mabilioni ya Biblia, vitabu, magazeti, broshua, na trakti zimetiririka kwa watu wa Mungu. Kama mto ambao Ezekieli aliona, kweli safi zimezidi kutiririka kwa kasi ili kutimiza uhitaji unaoongezeka wa kutosheleza kiu ya kiroho ya watu ulimwenguni kote. Machapisho yanayotegemea Biblia yamechapishwa kwa muda mrefu. Na sasa kupitia tovuti ya jw.org, habari hizo zinapatikana kielektroniki katika lugha zaidi ya 900! Maji hayo ya kweli yana matokeo gani kwa watu wenye mioyo minyoofu?

      12. (a) Tumeona jinsi gani ujumbe wa kweli ukiwaletea watu uhai na afya ya kiroho? (b) Maono hayo yanatupatia onyo gani leo? (Pia, tazama maelezo ya chini.)

      12 Maji yanayoleta uhai. Ezekieli aliambiwa: “Mahali ambapo kijito hicho kinapita, kila kitu kitaishi.” Fikiria jinsi ambavyo ujumbe wa kweli umetiririka kwa wote ambao wamekuja katika nchi yetu ya kiroho iliyorudishwa. Kweli za Biblia zimegusa mioyo ya mamilioni ya watu na kuwafanya wawe hai na wenye afya kiroho. Lakini maono hayo pia yanatoa onyo muhimu kwamba si watu wote wanaoendelea kufuata kweli hizo. Kama sehemu zenye majimaji na matope katika Bahari ya Chumvi kwenye maono ya Ezekieli, mioyo fulani inakuwa migumu, haikubali kweli na inakataa kuifuata.c Tusiwe hivyo kamwe!​—Soma Kumbukumbu la Torati 10:16-18.

      13. Leo, tunaweza kupata masomo gani kutokana na miti aliyoona Ezekieli?

      13 Miti kwa ajili ya chakula na kuponya. Je, leo tunapata masomo yanayotutia moyo kutokana na ile miti iliyo kwenye kingo za mto? Bila shaka! Kumbuka kwamba miti hiyo inazaa matunda matamu kila mwezi, na majani yake yanaponya. (Eze. 47:12) Inatukumbusha kwamba tunamtumikia Mungu anayetulisha kwa ukarimu na kutuponya kwa njia muhimu zaidi, yaani, kiroho. Ulimwengu wa leo ni mgonjwa na una njaa kiroho. Kinyume chake, fikiria mambo ambayo Yehova anaandaa. Baada ya kusoma makala katika machapisho yetu, kuimba wimbo wa mwisho kusanyikoni, au kutazama video au programu ya JW Broadcasting, je, umewahi kuhisi umebarikiwa kwa kupata chakula hicho cha kiroho? Kwa kweli tunalishwa vizuri. (Isa. 65:13, 14) Je, chakula chetu cha kiroho kinatusaidia kuwa na afya kiroho? Ushauri wenye manufaa tunaopata unaotegemea kabisa Neno la Mungu, hutusaidia kuepuka dhambi kama vile uasherati, pupa, na kukosa imani. Pia, Yehova amefanya mpango wa kuwasaidia Wakristo washinde ugonjwa wa kiroho unaoletwa na dhambi nzito. (Soma Yakobo 5:14.) Kwa kweli tumebarikiwa, kama inavyoonyeshwa na miti katika maono ya Ezekieli.

      14, 15. (a) Tunapata somo gani kutokana na sehemu zenye matope ambazo hazikuponywa katika maono ya Ezekieli? (b) Leo tunafaidikaje kutokana na maono ya Ezekieli kuhusu mto?

      14 Wakati huohuo, tunajifunza somo kutokana na maeneo hayo yenye matope yasiyoweza kuponywa. Hatungependa kamwe kuzuia baraka za Yehova kutiririka kwenye maisha yetu. Lingekuwa jambo hatari kukataa kuponywa, kama ilivyo kwa wengi katika ulimwengu huu mgonjwa. (Mt. 13:15) Kinyume chake, tunafurahia na kufaidika kutokana na mto wa baraka. Tunapokunywa kwa bidii maji safi ya kweli za Neno la Mungu, tunapowahubiria wengine kweli hizo, tunapopokea mwongozo wenye upendo, faraja, na msaada kutoka kwa wazee waliozoezwa na mtumwa mwaminifu, tunaweza kukumbuka mto wa maono ya Ezekieli. Mto huo unaendeleza uhai na kuponya popote unapoenda!

      15 Namna gani kuhusu utimizo wa wakati ujao wa maono ya mto huo? Kama tutakavyoona, mto huo utatiririka kwa kiwango kikubwa zaidi katika Paradiso inayokuja.

      Maono Hayo Yatamaanisha Nini Katika Paradiso?

      16, 17. (a) Maji ya uzima yataongezekaje hata zaidi katika Paradiso? (b) Tutafaidikaje kutokana na mto huo wa baraka katika Paradiso?

      16 Je, unajiwazia katika Paradiso, ukiwa umezungukwa na marafiki na familia, ukifurahia maisha kikamili? Kuchunguza maono ya Ezekieli kuhusu mto kunaweza kukusaidia uone jambo hilo waziwazi. Jinsi gani? Fikiria tena mambo matatu yaliyo wazi na yenye upendo katika maono hayo.

      17 Mto wa baraka. Katika Paradiso, mto huo wa mfano utapanuka hata zaidi kwa kuwa utaleta baraka za kiroho na pia za kimwili. Wakati wa Utawala wa Miaka Elfu Moja wa Yesu, Ufalme wa Mungu utawasaidia watu waaminifu wafaidike na fidia kwa njia kubwa zaidi. Hatua kwa hatua, watakuwa wakamilifu! Hakutakuwa tena na magonjwa, madaktari, wauguzi, hospitali, wala bima ya afya! Maji hayo ya uzima yatatiririka kwa mamilioni watakaooka Har–Magedoni, yaani, “umati mkubwa” watakaotoka kwenye “dhiki kuu.” (Ufu. 7:9, 14) Hata hivyo, ingawa mwanzo huo wa kutiririka kwa mto wa baraka utakuwa wenye kustaajabisha, ni mdogo kwa kulinganishwa na mambo yatakayotokea baadaye. Kama inavyoonyeshwa na maono ya Ezekieli, mto huo utapanuka ili kutimiza uhitaji mkubwa zaidi.

      Watu wenye nguvu za ujana, wenye afya nzuri na furaha wakifanya kazi kwenye Paradiso. Mto unatiririka nyuma yao.

      Katika Paradiso, mto wa baraka utafanya kila mtu awe kijana na mwenye afya (Tazama fungu la 17)

      18. “Mto wa maji ya uzima” utafurikaje wakati wa Utawala wa Miaka Elfu Moja?

      18 Maji yanayoleta uhai. Wakati wa ile Miaka Elfu Moja, “mto wa maji ya uzima” utafurika. (Ufu. 22:1) Mamilioni, au hata mabilioni, watafufuliwa na kupewa nafasi ya kuishi milele katika Paradiso! Baraka za Yehova kupitia Ufalme zitatia ndani kuwafufua watu wengi sana waliokufa, yaani, wanadamu ambao kwa muda mrefu wamelala mavumbini. (Isa. 26:19) Hata hivyo, je, watu hao wote waliofufuliwa wataendelea kuwa hai milele?

      19. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba maji ya kweli mpya kutoka kwa Mungu yataandaliwa katika Paradiso? (b) Ni kwa njia gani baadhi ya watu watabaki ‘wakiwa chumvi’ wakati ujao?

      19 Lazima kila mmoja aamue. Wakati huo, vitabu vipya vya kukunjwa vitafunguliwa. Basi maji yenye kuburudisha kutoka kwa Yehova yatatia ndani kweli mpya zitakazofunuliwa, yaani, mwongozo mpya wa kiroho. Je, si jambo lenye kupendeza kufikiria tumaini hilo? Hata hivyo, baadhi ya watu watakataa mwongozo huo na kuamua kutomtii Yehova. Huenda baadhi ya watu wataasi wakati wa ile Miaka Elfu Moja, lakini hawataruhusiwa kuvuruga Paradiso. (Isa. 65:20) Tunaweza kukumbuka maono ya Ezekieli kuhusu maeneo yenye matope ambayo hayakuponywa, ‘yaliyobaki yakiwa sehemu za chumvi.’ Wale watakaokataa kwa ukaidi kunywa maji yenye thamani yanayoleta uhai watakuwa wapumbavu kwelikweli! Baada ya ile Miaka Elfu Moja, kundi la waasi litajiunga na Shetani. Wote watakaokataa utawala wa Yehova wa uadilifu watapatwa na jambo lilelile: kifo cha milele.—Ufu. 20:7-12.

      20. Ni mpango gani utakaotunufaisha wakati wa Utawala wa Miaka Elfu Moja unaotukumbusha miti aliyoona Ezekieli?

      20 Miti kwa ajili ya chakula na kuponya. Yehova hangependa yeyote kati yetu akose uzima wa milele. Ili kutusaidia kunufaika na nafasi ya kipekee anayotupatia, atahakikisha tena kwamba kuna mpango kama wa miti ambayo Ezekieli aliona. Hata hivyo, katika Paradiso Yehova atatubariki kimwili na pia kiroho. Huko mbinguni, Yesu Kristo pamoja na watawala wenzake 144,000 watatawala wakiwa wafalme kwa Miaka Elfu Moja. Wakiwa makuhani, wale 144,000 watatumia thamani ya dhabihu ya fidia ya Kristo, kuwasaidia wanadamu waaminifu kuwa wakamilifu. (Ufu. 20:6) Mpango huo wa uponyaji wa kimwili na kiroho unatukumbusha miti aliyoona Ezekieli kwenye kingo za mto, ambayo ilizaa matunda yenye lishe na iliyokuwa na majani yanayoponya. Maono ya Ezekieli yanapatana na unabii mwingine wenye kupendeza ulioandikwa na mtume Yohana. (Soma Ufunuo 22:1, 2.) Majani ya miti ambayo Yohana aliona “yalikuwa ya kuponya mataifa.” Mamilioni ya wanadamu watafaidika kutokana na utumishi wa kikuhani wa wale 144,000.

      Ezekieli aliona kijito cha maji kikiongezeka na kuwa mto mkubwa.

      SANDUKU LA KUFUNDISHIA LA 19B: Kijito Kinakuwa Mto Mkubwa!

      21. Unafaidikaje kwa kutafakari kuhusu mto alioona Ezekieli, na sasa tutachunguza nini? (Tazama sanduku “Kijito Kinakuwa Mto Mkubwa!”)

      21 Unapotafakari mto alioona Ezekieli, je moyo wako unajawa na amani na tumaini? Tunatazamia kipindi kizuri sana wakati ujao! Fikiria jambo hilo—maelfu ya miaka iliyopita Yehova alitoa unabii mwingi ili kutusaidia kuwazia jinsi Paradiso itakavyokuwa, na kutualika kwa subira tuone utimizo mkubwa, uhalisi wa mambo yaliyotabiriwa. Je, utakuwapo? Huenda ukajiuliza kama kweli utapata nafasi katika Paradiso. Acheni sasa tuchunguze jinsi masimulizi ya mwisho ya unabii wa Ezekieli yanavyotupatia uhakikisho.

      a Isitoshe, Wayahudi wahamishwa ambao walikumbuka mandhari ya kijiografia ya nchi yao inaelekea walijua kwamba mto huo haukuwa halisi kwa sababu ulitiririka kutoka hekaluni kwenye mlima mrefu sana, ambao kihalisi haukuwepo katika eneo lililotajwa. Pia, maono hayo yalidokeza kwamba mto huo ulitiririka moja kwa moja hadi kwenye Bahari ya Chumvi, jambo ambalo halingewezekana kulingana na mandhari ya kijiografia ya eneo hilo.

      b Baadhi ya wasomi wanaelewa kwamba maneno haya yanatoa wazo zuri, wanasema kwamba kuvuna chumvi ili kuitumia kuhifadhi vitu ni biashara ya muda mrefu yenye faida katika eneo la Bahari ya Chumvi. Hata hivyo, ona kwamba simulizi hilo lilisema waziwazi kwamba sehemu hizo zenye matope “hazitaponywa.” Zinabaki bila uhai, bila kuponywa, kwa sababu maji yanayoleta uhai kutoka katika nyumba ya Yehova hayafiki huko. Basi inaonekana kwamba katika simulizi hili chumvi ya maeneo hayo yenye matope inatajwa kwa njia isiyo nzuri.—Zab. 107:33, 34; Yer. 17:6.

      c Kuhusiana na hilo, kumbuka mfano wa Yesu wa wavu wa kukokotwa. Samaki wengi wananaswa na wavu, lakini si wote walio “wazuri.” Samaki wasiofaa wanatupwa. Basi Yesu alionya kwamba huenda baadaye idadi kubwa ya watu wanaoingia katika tengenezo la Yehova wakakosa kuwa waaminifu.—Mt. 13:47-50; 2 Tim. 2:20, 21.

      SEHEMU YAKO KATIKA IBADA SAFI

      1. Maono ya Ezekieli kuhusu mto yalitimizwaje nyakati za kale?

      2. Leo, tunaona maono hayo yakitimizwaje?

      3. Mto alioona Ezekieli utatiririkaje kwa njia kubwa zaidi wakati wa Utawala wa Miaka Elfu Moja wa Kristo?

  • ‘Mtaigawa Nchi Iwe Urithi’
    Hatimaye Ibada Safi ya Yehova Yarudishwa!
    • Mto ukitiririka kuelekea baharini ukiwa umezungukwa na nchi ambayo ingegawanywa.

      SURA YA 20

      ‘Mtaigawa Nchi Iwe Urithi’

      EZEKIELI 45:1

      WAZO KUU: Maana ya kuigawa nchi

      1, 2. (a) Ezekieli anapokea maagizo gani kutoka kwa Yehova? (b) Tutachunguza maswali gani?

      EZEKIELI ametoka tu kuona maono ambayo yamemkumbusha miaka 900 hivi iliyopita katika siku za Musa na Yoshua. Wakati huo, Yehova alimweleza Musa kuhusu mipaka ya Nchi ya Ahadi na baadaye akamwambia Yoshua jinsi ambavyo nchi hiyo ingegawanywa kati ya makabila ya Israeli. (Hes. 34:1-15; Yos. 13:7; 22:4, 9) Lakini sasa, katika mwaka wa 593 K.W.K., Yehova anamwagiza Ezekieli na wahamishwa wenzake waigawe tena Nchi ya Ahadi kati ya makabila ya Israeli!—Eze. 45:1; 47:14; 48:29.

      2 Maono hayo yalikuwa na ujumbe gani kwa Ezekieli na wahamishwa wenzake? Kwa nini maono hayo yanawatia moyo watu wa Mungu leo? Je, yatatimizwa kwa njia kubwa zaidi wakati ujao?

      Maono Yanayotoa Uhakikisho kwa Njia Nne

      3, 4. (a) Ni mambo gani manne katika maono ya mwisho ya Ezekieli yaliyowapa wahamishwa uhakikisho? (b) Tutachunguza uhakikisho gani katika sura hii?

      3 Maono aliyoona Ezekieli yanazungumziwa katika sura tisa za kitabu chake. (Eze. 40:1–48:35) Yaliwatia moyo wahamishwa kwa kutaja mambo manne yaliyowapa uhakika kuhusu taifa la Israeli lililorudishwa. Ni mambo gani hayo yaliyowapa uhakika? Kwanza, ibada safi ingerudishwa katika hekalu la Mungu. Pili, makuhani na wachungaji waadilifu wangeongoza taifa hilo lililorudishwa. Tatu, wote ambao wangerudi Israeli wangepata urithi wa nchi. Na nne, Yehova angekuwa pamoja nao, na kukaa katikati yao tena.

      4 Sura ya 13 na 14 ya kitabu hiki zilizungumzia jinsi ambavyo mambo mawili ya kwanza yangetimizwa, yaani, kurudishwa kwa ibada safi na kuongozwa na wachungaji waadilifu. Katika sura hii, tutakazia uhakikisho wa tatu, ahadi ya kurithi nchi. Katika sura inayofuata tutachunguza ahadi kuhusu kuwapo kwa Yehova.—Eze. 47:13-21; 48:1-7, 23-29.

      ‘Mmegawiwa Nchi Hii Iwe Urithi Wenu’

      5, 6. (a) Katika maono ya Ezekieli ni nchi gani waliyopaswa kuigawa? (Tazama picha mwanzoni mwa sura hii.) (b) Maono kuhusu kugawa nchi yalikuwa na kusudi gani?

      5 Soma Ezekieli 47:14. Katika maono, Yehova alimwonyesha Ezekieli sehemu ya nchi ambayo baadaye ingekuwa kama “bustani ya Edeni.” (Eze. 36:35) Kisha Yehova akasema: “Hili ndilo eneo ambalo mtayagawia yale makabila 12 ya Israeli kuwa urithi wao wa ardhi.” (Eze. 47:13) “Eneo” ambalo wangegawiwa lilikuwa nchi ya Israeli iliyorudishwa ambako wahamishwa wangerudishwa. Baadaye, kama ilivyoandikwa kwenye Ezekieli 47:15-21, Yehova alifafanua kwa undani mipaka hususa ya nchi yote.

      6 Maono hayo ya kuigawa nchi yalikuwa na kusudi gani? Ufafanuzi wa vipimo hususa vya mipaka ulimhakikishia Ezekieli na wahamishwa wenzake kwamba kwa hakika nchi yao waliyoipenda ingerudishwa. Wazia jinsi ambavyo uhakikisho huo kutoka kwa Yehova, wenye habari nyingi na maelezo yaliyo wazi, ulivyowatia moyo wahamishwa hao! Je, kweli watu hao wa Mungu waligawiwa urithi katika nchi waliyopewa? Ndiyo.

      Mto ukitiririka kuelekea baharini ukiwa umezungukwa na nchi ambayo ingegawanywa.

      7. (a) Ni matukio gani yaliyoanza mwaka wa 537 K.W.K., na yanatukumbusha nini? (b) Tutachunguza swali gani kwanza?

      7 Mwaka wa 537 K.W.K., miaka 56 hivi baada ya Ezekieli kupata maono, maelfu ya wahamishwa walianza kurudi katika nchi ya Israeli na kuimiliki. Matukio hayo makubwa ya zamani yanatukumbusha jambo kama hilo ambalo wakati wetu limekuwa likitokea kati ya watu wa Mungu. Kwa njia fulani, wao pia walipokea urithi wa nchi. Jinsi gani? Yehova aliwaruhusu watu wake waingie katika nchi ya kiroho na kuimiliki. Kwa hiyo, kurudishwa kwa Nchi ya Ahadi zamani kunatufundisha mengi kuhusu kurudishwa kwa nchi ya kiroho ya watu wa Mungu leo. Lakini kabla ya kuchunguza mambo hayo, acheni kwanza tujibu swali hili, “Kwa nini tunaweza kusema kwamba kwa kweli leo kuna nchi ya kiroho?”

      8. (a) Yehova alichagua taifa gani baada ya kuwakataa Waisraeli wa asili? (b) Nchi, au paradiso ya kiroho ni nini? (c) Ilianzishwa lini, na ni nani wanaoishi humo?

      8 Katika maono ambayo Ezekieli aliona awali, Yehova alionyesha kwamba unabii kuhusu kurudishwa kwa Israeli ungetimizwa kwa njia kubwa zaidi baada ya ‘mtumishi wake Daudi,’ yaani, Yesu Kristo, kuanza kutawala akiwa Mfalme. (Eze. 37:24) Jambo hilo lilitokea mwaka wa 1914 W.K. Kufikia wakati huo, muda mrefu ulikuwa umepita tangu Waisraeli wa asili walipoacha kuwa watu wa Mungu na nafasi yao kuchukuliwa na taifa la Israeli wa kiroho, lililofanyizwa na Wakristo waliotiwa mafuta. (Soma Mathayo 21:43; 1 Petro 2:9.) Hata hivyo, Yehova hakulikataa tu taifa la asili la Israeli na kuanzisha taifa la kiroho bali pia aliikataa nchi halisi ya Israeli na kuanzisha nchi, au paradiso ya kiroho. (Isa. 66:8) Kama tulivyoona katika Sura ya 17 ya kitabu hiki, nchi ya kiroho ni mazingira salama ya kiroho, au mahali pa utendaji, ambapo watiwa mafuta waliobaki wamekuwa wakimwabudu Yehova tangu mwaka wa 1919. (Tazama sanduku la 9B, “Kwa Nini 1919?”) Muda ulipozidi kupita, wale walio na tumaini la kuishi duniani, yaani, “kondoo wengine,” walianza pia kuingia katika nchi hiyo ya kiroho. (Yoh. 10:16) Ingawa paradiso ya kiroho inazidi kukua na kupanuka leo, baraka zake zitaonekana kikamili baada ya Har–Magedoni.

      Kuigawa Nchi kwa Usawa na Kikamili

      9. Yehova alitoa maagizo gani yenye kina kuhusu kuigawa nchi?

      9 Soma Ezekieli 48:1, 28. Baada ya kuweka mipaka ya nje ya nchi hiyo, Yehova alieleza kwa undani jinsi ya kuigawa nchi hiyo. Aliagiza maeneo ya urithi ya makabila 12 yapimwe kwa usawa na ukamili kuanzia kaskazini hadi kusini, akianza na kabila la Dani upande wa kaskazini wa nchi na kumalizia na kabila la Gadi kwenye mpaka wa kusini. Kila eneo la urithi la makabila yote 12 lilikuwa na mipaka iliyonyooka kutoka mpaka wa mashariki wa nchi hadi Bahari Kuu, yaani, Bahari ya Mediterania, upande wa magharibi.—Eze. 47:20.

      10. Inaelekea sehemu hii ya maono iliwapa wahamishwa uhakikisho gani?

      10 Inaelekea sehemu hii ya maono iliwapa wahamishwa uhakikisho gani? Ufafanuzi wenye kina ambao Ezekieli alitoa kuhusu kuigawa nchi uliwasadikishia wahamishwa kwamba nchi hiyo ingegawanywa kwa mpangilio mzuri. Isitoshe, kuigawa nchi kihususa kati ya makabila yote 12 kulikazia kwamba kwa hakika kila mhamishwa aliyerudi angepata urithi katika nchi iliyorudishwa. Hakuna mtu aliyerudi ambaye angekosa ardhi au makazi.

      Mwanamume anayeonekana kama shaba akimwonyesha Ezekieli urithi wa nchi.

      SANDUKU LA KUFUNDISHIA LA 20A: Kuigawa Nchi

      11. Tunapata masomo gani kutokana na maono kuhusu kuigawa nchi? (Tazama sanduku “Kuigawa Nchi.”)

      11 Leo tunapata masomo gani yenye kuimarisha kutokana na maono hayo? Nchi ya Ahadi iliyorudishwa haikuwa tu na eneo kwa ajili ya makuhani, Walawi, na wakuu, bali pia kulikuwa na maeneo kwa ajili ya watu wengine wote wa makabila 12. (Eze. 45:4, 5, 7, 8) Vivyo hivyo, leo paradiso ya kiroho ina nafasi kwa ajili ya watiwa mafuta waliobaki, washiriki wa “umati mkubwa” wanaoongoza, na pia washiriki wengine wote wa umati mkubwa.a (Ufu. 7:9) Hata iwe tunatimiza jukumu dogo kadiri gani katika tengenezo, tuna hakika kwamba tuna mahali na mgawo wenye thamani katika nchi ya kiroho. Huo ni uhakikisho wenye kutia moyo!

      Mkusanyiko wa picha: Watu wa Mungu leo. 1. Dada akimsaidia mama yake aliyezeeka kutumia dawa. 2. Mmishonari akimsaidia mhubiri mchanga katika huduma. Wanahubiri kwenye ufukwe. 3. Mama akiwafundisha Biblia wanawe wawili. 4. Gerrit Lösch akiongoza familia ya Betheli katika ibada ya asubuhi. 5. Dada mwenye umri mkubwa akisali. Mbele yake kuna orodha ya akina ndugu waliofungwa gerezani. 6. Ndugu akisafisha vyoo katika Jumba la Ufalme. 7. Ndugu akiwahudumia wengine kwenye maegesho ya magari kwenye Jumba la Kusanyiko. 8. Akina ndugu wakiwa studio kwenye ofisi ya tafsiri.

      Hata iwe tunatimiza jukumu gani katika tengenezo la Mungu, Yehova anathamini jitihada zetu (Tazama fungu la 11)

      Tofauti Mbili Kubwa—Zina Maana Gani Kwetu?

      12, 13. Yehova alitoa maagizo gani hususa kuhusu kuyagawia makabila urithi katika nchi?

      12 Huenda Ezekieli alishangazwa na baadhi ya maagizo ambayo Yehova alimpatia kwa sababu yalitofautiana na maagizo ambayo Mungu alimpa Musa. Fikiria tofauti mbili. Moja inahusu nchi, na nyingine wakaaji wake.

      13 Kwanza, nchi. Musa aliagizwa ayagawie makabila makubwa eneo kubwa kuliko makabila madogo. (Hes. 26:52-54) Hata hivyo, katika maono ya Ezekieli, Yehova alitoa maagizo hususa ya kuyagawia urithi makabila yote “kwa usawa [“kila mtu kama ndugu yake,” maelezo ya chini].” (Eze. 47:14) Basi umbali kutoka mpaka wa kaskazini hadi mpaka wa kusini katika urithi wa kila kabila ulipaswa kulingana katika maeneo yote 12. Waisraeli wote—bila kuzingatia kabila lao—wangepata kwa usawa mazao mengi ambayo yangetokezwa na Nchi ya Ahadi yenye maji mengi.

      14. Maagizo ya Yehova kuhusu wakaaji wageni yalitofautianaje na maagizo katika Sheria ya Musa?

      14 Pili, wakaaji. Sheria ya Musa iliwalinda wageni na kuwaruhusu washiriki katika ibada ya Yehova, lakini hawangepata urithi katika nchi. (Law. 19:33, 34) Hata hivyo, jambo ambalo Yehova alimwambia Ezekieli ni tofauti na jambo alilokuwa amesema kwenye Sheria. Yehova alimwagiza hivi: “Mnapaswa kumpa mkaaji mgeni urithi katika eneo la kabila analoishi ndani yake.” Kupitia amri hiyo, Yehova alifutilia mbali tofauti kubwa kati ya “Waisraeli wenyeji” na wakaaji wageni katika nchi. (Eze. 47:22, 23) Katika nchi iliyorudishwa ambayo Ezekieli aliona katika maono, aliona kwamba wakaaji wake walikuwa na usawa na umoja wa ibada.—Law. 25:23.

      15. Ni jambo gani lisilobadilika kumhusu Yehova ambalo lilithibitishwa na maagizo yake kuhusu nchi na wakaaji wake?

      15 Maagizo hayo muhimu ambayo Ezekieli alipokea kuhusu nchi na wakaaji wake yaliwafariji wahamishwa. Walijua kwamba Yehova angewagawia maeneo yaliyo sawa, iwe walikuwa Waisraeli kwa kuzaliwa au wageni waliomwabudu Yehova. (Ezra 8:20; Neh. 3:26; 7:6, 25; Isa. 56:3, 8) Maagizo hayo pia yalitoa uhakikisho wenye kutia moyo na usiobadilika kwamba Yehova anawaona watumishi wake wote kuwa wenye thamani. (Soma Hagai 2:7.) Leo, iwe tuna tumaini la kwenda mbinguni au kuishi duniani, tunaamini jambo hilo.

      16, 17. (a) Tunafaidikaje kwa kuchunguza habari kuhusu nchi na wakaaji wake? (b) Tutachunguza nini katika sura inayofuata?

      16 Tunafaidikaje kwa kuchunguza habari hizo kuhusu nchi na wakaaji wake? Tunakumbushwa kwamba leo usawa na umoja unapaswa kuonekana waziwazi katika undugu wetu wa ulimwenguni pote. Yehova hana ubaguzi. Tunapaswa kujiuliza: ‘Je, ninamwiga Yehova kwa kuepuka ubaguzi? Je, ninamtendea kila mmoja kati ya waabudu wenzangu kwa heshima inayotoka moyoni, bila kuangalia jamii aliyotoka na hali zake maishani?’ (Rom. 12:10) Tunashangilia kwamba Yehova ametupatia sisi sote nafasi sawa katika paradiso ya kiroho, ambapo tunamtolea Baba yetu wa mbinguni utumishi mtakatifu kwa nafsi yote na kufurahia baraka kutoka kwake.—Gal. 3:26-29; Ufu. 7:9.

      Akina dada wa jamii na umri mbalimbali wakiwa katika ibada ya familia nyumbani mwa dada mlemavu.

      Je, tunamwiga Yehova kwa kuwaheshimu wengine kutoka moyoni na kuepuka ubaguzi? (Tazama fungu la 15 na 16)

      17 Acheni sasa tuchunguze uhakikisho wa nne katika sehemu ya kumalizia ya maono ya mwisho ya Ezekieli—ahadi kwamba Yehova atakuwa pamoja na wahamishwa. Tunajifunza masomo gani kutokana na ahadi hiyo? Tutapata jibu katika sura inayofuata.

      a Ili upate habari kuhusu mahali pa pekee na mgawo ambao Yehova ameweka kwa ajili ya makuhani na mkuu katika paradiso ya kiroho, tazama Sura ya 14 ya kitabu hiki.

      SEHEMU YAKO KATIKA IBADA SAFI

      1. Kwa nini unaamini kwamba kuna paradiso ya kiroho leo?

      2. Kwa nini unaweza kuwa na uhakika kwamba una mahali na mgawo wenye thamani katika paradiso ya kiroho?

      3. Maono ya kinabii kuhusu kuigawa nchi yanakufundisha nini kumhusu Yehova?

  • “Jina la Jiji Hilo . . . Litakuwa, Yehova Yupo Hapo”
    Hatimaye Ibada Safi ya Yehova Yarudishwa!
    • Picha iliyopigiwa angani ya jiji linaloitwa ‘Yehova Yupo Hapo.’

      SURA YA 21

      “Jina la Jiji Hilo . . . Litakuwa, Yehova Yupo Hapo”

      EZEKIELI 48:35

      WAZO KUU: Maana ya jiji na mchango

      1, 2. (a) Ni eneo gani la pekee lililopaswa kuwekwa kando? (Tazama picha kwenye jalada.) (b) Maono hayo yanawapa wahamishwa uhakikisho gani?

      KATIKA maono yake ya mwisho, Ezekieli anaona sehemu ya nchi ambayo inapaswa kuwekwa kando kwa ajili ya kusudi la pekee. Sehemu iliyotengwa, haitolewi kuwa urithi wa kabila fulani la Israeli, bali kama mchango kwa Yehova. Pia, Ezekieli anaona jiji la pekee lenye jina la kushangaza. Sehemu hiyo ya maono inawapa wahamishwa uhakikisho huu muhimu zaidi: Yehova atakuwa pamoja nao watakaporudi katika nchi yao wanayoipenda.

      2 Ezekieli anatupatia ufafanuzi wa kina kuhusu mchango huo. Acheni tuchunguze simulizi hili, ambalo lina maana kubwa kwetu waabudu wa kweli wa Yehova.

      Picha ilipigiwa angani ya eneo la nchi linaloitwa ‘mchango mzima’ na jiji linaloitwa ‘Yehova Yupo Hapo.’ Maono ya hekalu ambalo Ezekieli aliona liking’aa kwa utukufu wa Yehova juu ya mlima mrefu na mto ukitiririka kutoka katika hekalu hilo.

      “Mchango Mtakatifu Pamoja na . . . Jiji”

      Ramani ya nchi ambayo Yehova aliiweka kando na kuiita ‘mchango’ na mraba unaoonyesha sehemu ya nchi hiyo iliyoitwa ‘mchango mzima.’

      SANDUKU LA KUFUNDISHIA LA 21A: “Mchango Mtakaoweka Kando”

      3. Eneo ambalo Yehova aliweka kando lilikuwa na sehemu gani tano, na sehemu hizo zilitimiza kusudi gani? (Tazama sanduku “Mchango Mtakaoweka Kando.”)

      3 Eneo hilo la pekee lilikuwa na urefu wa mikono 25,000 (kilomita 13) kuanzia kaskazini hadi kusini, na mikono 25,000 kuanzia mashariki hadi magharibi. Eneo hilo la mraba liliitwa “mchango mzima.” Liligawanywa katika sehemu tatu. Sehemu ya juu ilikuwa ya Walawi, sehemu ya katikati ilitengwa kwa ajili ya hekalu na makuhani. Sehemu hizo mbili zilifanyiza “mchango mtakatifu.” Sehemu ya chini iliyokuwa ndogo, au ‘sehemu iliyobaki,’ ilikuwa kwa ajili ya “matumizi ya kawaida.” Ilikuwa kwa ajili ya jiji.—Eze. 48:15, 20.

      4. Tunajifunza somo gani kutokana na simulizi kuhusu mchango kwa Yehova?

      4 Tunajifunza somo gani katika simulizi hili kuhusu mchango kwa Yehova? Kwa kutenga kwanza eneo kwa ajili ya mchango wa pekee na kisha maeneo ya makabila, Yehova alionyesha kwamba kituo hicho cha mambo ya kiroho kilipaswa kuwa muhimu zaidi. (Eze. 45:1) Bila shaka, wahamishwa walijifunza mengi kutokana na mpangilio huo wa kugawa nchi. Walipaswa kutanguliza ibada ya Yehova maishani. Vivyo hivyo, leo tunaona mambo ya kiroho, kama vile kujifunza Neno la Mungu, kuhudhuria mikutano ya Kikristo, na kuhubiri, kuwa mambo muhimu zaidi. Tunaiga mfano wa Yehova wa kutanguliza mambo muhimu kwa kufanya ibada yake iwe jambo kuu katika maisha yetu ya kila siku.

      “Jiji Litakuwa Katikati Yake”

      5, 6. (a) Jiji lilikuwa la nani? (b) Jiji hilo halikuwa nini, na kwa nini?

      5 Soma Ezekieli 48:15. “Jiji” na maeneo yaliyolizunguka yalikuwa na maana gani? (Eze. 48:16-18) Yehova alikuwa amemwambia hivi Ezekieli katika maono: “Jiji . . . [litakuwa la] watu wote wa nyumba ya Israeli.” (Eze. 45:6, 7) Basi, jiji na maeneo yaliyolizunguka hayakuwa sehemu ya “mchango mtakatifu” ambao ulipaswa ‘kuwekwa kando kwa ajili ya Yehova.’ (Eze. 48:9) Tukiwa na hilo akilini, acheni tuchunguze jambo tunalojifunza leo kutokana na mpangilio wa jiji hilo.

      6 Ili kujifunza masomo kutokana na jiji hilo, kwanza tunahitaji kujua, jiji hilo halikuwa nini? Halikuwa jiji la Yerusalemu pamoja na hekalu lake lililojengwa upya. Kwa nini? Kwa sababu jiji ambalo Ezekieli aliona katika maono halingekuwa na hekalu ndani yake. Pia, jiji hilo halikuwa jiji lingine katika nchi ya Israeli iliyorudishwa. Kwa nini? Kwa maana wahamishwa waliorudi pamoja na wazao wao hawakujenga jiji lenye mambo yaliyotajwa katika maono. Isitoshe, jiji hilo halikuwa jiji la kimbingu. Kwa nini? Kwa kuwa lilijengwa kwenye eneo lililotengwa kwa ajili ya “matumizi ya kawaida [au, matumizi yasiyo matakatifu]” tofauti na majengo yaliyojengwa kwenye eneo lililotengwa hasa kwa ajili ya ibada takatifu.—Eze. 42:20.

      7. Jiji ambalo Ezekieli aliona ni nini, na inaelekea linawakilisha nini? (Tazama picha mwanzoni mwa sura hii.)

      7 Basi, jiji ambalo Ezekieli aliona ni nini? Kumbuka kwamba aliona jiji hilo katika maono yaleyale aliyoona nchi. (Eze. 40:2; 45:1, 6) Neno la Mungu linaonyesha kwamba nchi hiyo ni nchi ya kiroho, basi jiji hilo linamaanisha jiji la kiroho. Kwa ujumla, neno “jiji” linamaanisha nini? Neno hilo linatoa wazo la watu wanaoishi pamoja katika kikundi na kufanyiza mfumo wenye utaratibu na mpangilio. Basi, inaonekana jiji lenye mpangilio mzuri ambalo Ezekieli aliona—lililokuwa mraba kamili—linawakilisha kituo cha usimamizi chenye mpangilio mzuri.

      Picha iliyopigiwa angani ya jiji linaloitwa ‘Yehova Yupo Hapo.’

      8. Kituo hicho cha usimamizi kinaongoza milki, au eneo gani, na kwa nini?

      8 Kituo hicho cha usimamizi kinaongoza milki, au eneo gani? Maono ya Ezekieli yanafunua kwamba jiji hilo linafanya kazi katika nchi ya kiroho. Basi, leo kituo hicho cha usimamizi kinaongoza katika utendaji wa watu wa Mungu. Wazo la kwamba jiji hilo liko katika eneo la matumizi ya kawaida, au lisilo takatifu linamaanisha nini? Hilo linatukumbusha kwamba jiji hilo si usimamizi wa kimbingu, bali ulio duniani, ambao umekuwa ukitenda kwa faida ya watu wote walio katika paradiso ya kiroho.

      9. (a) Leo, ni nani wanaofanyiza usimamizi huo duniani? (b) Yesu atafanya nini wakati wa Utawala wa Miaka Elfu Moja?

      9 Ni nani wanaofanyiza usimamizi huo ulio duniani? Katika maono ya Ezekieli, serikali ya jiji iliongozwa na “kiongozi.” (Eze. 45:7) Alikuwa mwangalizi kati ya watu, lakini hakuwa kuhani wala Mlawi. Kiongozi huyo anatukumbusha wazee wa kutaniko leo ambao si watiwa mafuta. Wachungaji hao wa kiroho wenye kujali kutoka kati ya “kondoo wengine” ni watumishi wanyenyekevu walio duniani wa serikali ya Kristo iliyo mbinguni. (Yoh. 10:16) Wakati wa Utawala wa Miaka Elfu Moja unaokuja, Yesu atawachagua na kuwaweka rasmi “katika dunia yote” wazee wanaostahili, au “wakuu.” (Zb. 45:16) Chini ya mwongozo wa Ufalme wa mbinguni, watawatunza watu wa Mungu wakati wa Utawala wa Miaka Elfu Moja.

      “Yehova Yupo Hapo”

      10. Jina la jiji hilo ni nini, na hilo linatoa uhakikisho gani?

      10 Soma Ezekieli 48:35. Jina la jiji hilo ni “Yehova Yupo Hapo.” Jina hilo linatoa uhakikisho kwamba kuwapo kwa Yehova kunaonekana katika jiji hilo. Yehova alipomwonyesha Ezekieli jiji hilo lililo katikati, ni kana kwamba aliwaambia wahamishwa hivi: ‘Nitakuwa pamoja nanyi tena!’ Kwa kweli uhakikisho huo uliwatia moyo!

      11. Tunapata masomo gani kutokana na maono ya Ezekieli kuhusu jiji na jina lake lenye maana kubwa?

      11 Tunapata masomo gani kutokana na sehemu hii ya unabii wa Ezekieli? Tukiwa watumishi wa Mungu, jina la jiji hilo la usimamizi linatuhakikishia kwamba Yehova ataendelea kukaa pamoja na watumishi wake waaminifu duniani sasa na milele. Jina hilo lenye maana linakazia ukweli huu muhimu: Kusudi la jiji hilo si kumpa mwanadamu yeyote mamlaka, bali kutekeleza njia za Yehova zenye upendo na usawaziko. Kwa mfano, Yehova hajawapa wasimamizi mamlaka ya kuigawa nchi, wakiongozwa na maoni ya kibinadamu. Badala yake, Yehova anatazamia wasimamizi hao waheshimu urithi, au mapendeleo ambayo yeye mwenyewe amewapa watumishi wake, kutia ndani watu “wa hali ya chini.”—Met. 19:17; Eze. 46:18; 48:29.

      12. (a) Ni jambo gani muhimu lililo katika jiji hilo, nalo linamaanisha nini? (b) Waangalizi Wakristo wanapata kikumbusho gani muhimu kutokana na jambo hilo?

      12 Ni jambo gani lingine la pekee lililo katika jiji linaloitwa “Yehova Yupo Hapo”? Ingawa majiji ya kale yalikuwa na kuta kwa ajili ya ulinzi na malango machache iwezekanavyo, jiji hili lina malango 12! (Eze. 48:30-34) Idadi hiyo kubwa ya malango (matatu kila upande wa jiji hilo la mraba) inaonyesha kwamba watumishi wote wa Mungu wanaweza kuwafikia wasimamizi wa jiji hilo wakati wowote. Isitoshe, malango 12 ya jiji yanakazia kwamba jiji hilo liko wazi kwa kila mtu, “watu wote wa nyumba ya Israeli.” (Eze. 45:6) Jiji hilo lililo wazi ni kikumbusho muhimu kwa waangalizi Wakristo. Yehova anataka wawe wenye urafiki na wanaoweza kufikiwa wakati wowote na watu wote wanaoishi katika paradiso ya kiroho.

      Mzee wa kutaniko akizungumza na watoto kwenye Jumba la Ufalme na kutazama picha walizochora.

      Waangalizi Wakristo ni wenye urafiki na wanapatikana wakati wowote (Tazama fungu la 12)

      Watu wa Mungu ‘Wanaingia Ili Kuabudu’ na ‘Kulitumikia Jiji’

      13. Yehova alisema nini kuhusu kazi mbalimbali ambazo watu wangefanya?

      13 Acheni turudi wakati wa Ezekieli ili tujue mambo zaidi anayoandika katika maono hayo marefu ya kuigawa nchi. Yehova anasema kwamba watu wanashiriki kufanya kazi mbalimbali. Makuhani—“wahudumu wa mahali patakatifu”—wangetoa dhabihu na kumkaribia Yehova ili kumhudumia. Nao Walawi—“wahudumu wa hekaluni”—wangeshughulikia “utumishi wa hekaluni na mambo yote yanayopaswa kufanywa humo.” (Eze. 44:14-16; 45:4, 5) Isitoshe, wafanyakazi wangekuwa na shughuli nyingi karibu na jiji. Wafanyakazi hao ni nani?

      14. Wafanyakazi walio karibu na jiji wanatukumbusha nini?

      14 Wafanyakazi walio karibu na jiji wanatoka “katika makabila yote ya Israeli.” Wanaunga mkono kazi. Jukumu lao ni kukuza mazao ambayo “yatakuwa chakula cha wale wanaolitumikia jiji.” (Eze. 48:18, 19) Je, mpango huo unatukumbusha nafasi muhimu tuliyo nayo leo? Ndiyo. Leo, wakaaji wote katika paradiso ya kiroho wana nafasi ya kuunga mkono utumishi wa ndugu za Kristo watiwa mafuta na utumishi wa wale walio kati ya “umati mkubwa” ambao Yehova amewaweka rasmi waongoze. (Ufu. 7:9, 10) Njia kuu tunayounga mkono kazi hiyo ni kwa kutii kwa hiari mwongozo wa mtumwa mwaminifu.

      15, 16. (a) Tunapata habari gani nyingine katika maono ya Ezekieli? (b) Tuna nafasi gani ya kufanya kazi kama hiyo?

      15 Maono ya Ezekieli yana jambo lingine linalotufundisha somo kuhusu huduma yetu. Ni jambo gani? Yehova anasema kwamba watu wa makabila 12 yasiyo ya Walawi wangefanya kazi mbalimbali katika maeneo mawili: katika ua wa hekalu na kwenye viwanja vya malisho vya jiji. Wanafanya kazi gani katika maeneo hayo? Katika ua wa hekalu, makabila yote ‘yanaingia ili kuabudu’ kwa kumtolea Yehova dhabihu. (Eze. 46:9, 24) Kwenye eneo la jiji, watu kutoka makabila yote wanakuja kuunga mkono kwa kulima eneo hilo. Tunajifunza nini kutokana na mfano wa wafanyakazi hao?

      16 Leo, washiriki wa umati mkubwa wana nafasi ya kufanya kazi kama zile zilizofanywa katika maono ya Ezekieli. Wanamwabudu Yehova “katika hekalu lake” kwa kumtolea dhabihu za sifa. (Ufu. 7:9-15) Wanafanya hivyo kwa kuhubiri na pia kutoa maelezo na kuimba katika mikutano ya Kikristo. Wanaona kumwabudu Yehova kuwa jukumu lao muhimu zaidi. (1 Nya. 16:29) Isitoshe, wengi kati ya watu wa Mungu wanaunga mkono tengenezo la Mungu kwa njia mbalimbali. Kwa mfano, wanasaidia kujenga na kudumisha Majumba ya Ufalme na ofisi za tawi, na kusaidia katika miradi mingine mingi inayofanywa na tengenezo la Yehova. Wengine wanaunga mkono miradi hiyo kwa kutoa michango ya kifedha. Kwa njia ya mfano, wanalima “kwa utukufu wa Mungu.” (1 Kor. 10:31) Wanafanya kazi yao kwa bidii na shangwe kwa sababu wanajua kwamba Yehova “hupendezwa na dhabihu kama hizo.” (Ebr. 13:16) Je, unatumia nafasi hizo kikamili?

      Watu wakiwa wamebeba nafaka na wakitunza ng’ombe na kondoo karibu na malango ya jiji linaloitwa ‘Yehova Yupo Hapo.’

      Tunajifunza masomo gani kutokana na maelezo ya Ezekieli kuhusu kazi mbalimbali zilizofanywa katika malango ya jiji? (Tazama fungu la 14-16)

      “Tunangojea Mbingu Mpya na Dunia Mpya”

      17. (a) Tutaona utimizo gani mkubwa wa maono ya Ezekieli wakati ujao? (b) Wakati wa Utawala wa Miaka Elfu Moja, ni nani watakaofaidika na jiji la usimamizi?

      17 Je, wakati ujao tutaona utimizo mkubwa zaidi wa maono ya Ezekieli kuhusu mchango? Ndiyo! Fikiria jambo hili: Ezekieli aliona kwamba eneo lililoitwa “mchango mtakatifu” lilikuwa katikati ya nchi. (Eze. 48:10) Vivyo hivyo, baada ya Har–Magedoni, hata iwe tutaishi wapi duniani, Yehova atakaa pamoja nasi. (Ufu. 21:3) Wakati wa Utawala wa Miaka Elfu Moja, jiji la usimamizi—yaani, wale walio duniani ambao watachaguliwa ili kushughulikia masilahi ya watu wa Mungu—wataongoza mambo ulimwenguni pote kwa kutoa mwongozo wenye upendo kwa wote watakaofanyiza “dunia mpya,” yaani, jamii mpya ya wanadamu.—2 Pet. 3:13.

      18. (a) Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba jiji la usimamizi litakuwa na upatano na utawala wa Mungu? (b) Tunapata uhakikisho gani thabiti kutokana na jina la jiji hilo?

      18 Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba jiji la usimamizi litaendelea kutenda kwa upatano na utawala wa Mungu? Kwa sababu Neno la Mungu linaonyesha kwamba jiji la kidunia lenye malango 12 linapatana na jiji la mbinguni lenye malango 12, Yerusalemu Jipya, linalofanyizwa na watawala wenzi wa Kristo 144,000. (Ufu. 21:2, 12, 21-27) Jambo hilo linaonyesha kwamba usimamizi huo ulio duniani utafuata maamuzi yote yanayofanywa na Ufalme wa Mungu na kuyatekeleza kwa makini. Jina la jiji “Yehova Yupo Hapo” linatuhakikishia sote kwamba ibada safi itadumu na kusitawi milele katika Paradiso. Kwa kweli tunatazamia wakati ujao utakaokuwa mzuri sana!

      SEHEMU YAKO KATIKA IBADA SAFI

      1. Tunapata somo gani kuhusu mambo tunayopaswa kutanguliza kutokana na maono ya mchango kwa Yehova?

      2. Unawezaje kuunga mkono kazi za mtumwa mwaminifu?

      3. Ni mambo gani unayoona kuwa muhimu zaidi kwako?

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki