Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • wp21 Na. 3 kur. 12-14
  • Je, Kuna Mwongozo Unaotegemeka wa Kuwa na Maisha Bora ya Wakati Ujao?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Kuna Mwongozo Unaotegemeka wa Kuwa na Maisha Bora ya Wakati Ujao?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu wote)—2021
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MWONGOZO KUTOKA KATIKA CHANZO KIKUU
  • Biblia Inasema Nini?
    Amkeni!—2017
  • Mafundisho ya Kweli Yanayompendeza Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Mema na Mabaya: Biblia​—⁠Mwongozo Unaotegemeka
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu wote)—2024
  • Waweza Kupata Wapi Mwongozo Wenye Kutumainika?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu wote)—2021
wp21 Na. 3 kur. 12-14
Mwanamume akisoma Biblia.

Je, Kuna Mwongozo Unaotegemeka wa Kuwa na Maisha Bora ya Wakati Ujao?

Kama tulivyozungumzia kwenye makala zilizopita, watu wamejaribu kutafuta maisha bora ya wakati ujao kupitia mambo kama vile majaliwa, elimu, utajiri, na kuwa watu wema. Hata hivyo, kutumia njia hizo ni sawa na kutumia ramani isiyo sahihi ukitumaini utafika mahali unapotaka kwenda. Je, hilo linamaanisha hakuna mwongozo unaotegemeka wa wakati ujao? Hapana!

MWONGOZO KUTOKA KATIKA CHANZO KIKUU

Mara nyingi tunapotaka kufanya uamuzi tunaomba ushauri kutoka kwa mtu mwenye umri mkubwa na mwenye hekima zaidi kuliko sisi. Vilevile, tunaweza kupata mwongozo unaofaa wa wakati ujao kutoka kwa Mtu aliyeishi kwa muda mrefu zaidi na mwenye hekima nyingi zaidi kuliko sisi. Tunapata ushauri Wake kutoka katika maandishi matakatifu yaliyoanza kuandikwa karibu miaka 3,500 hivi iliyopita. Maandishi hayo matakatifu ni Biblia.

Kwa nini uitumaini Biblia? Kwa sababu Mtungaji wake ameishi muda mrefu zaidi na ana hekima nyingi kuliko mtu yeyote ulimwenguni. Anaitwa “Mzee wa Siku” ambaye ni wa “tangu milele hadi milele.” (Danieli 7:9; Zaburi 90:2) Yeye ni “Muumba wa mbingu, Mungu wa kweli, Yule aliyeiumba dunia.” (Isaya 45:18) Anajitambulisha kwa jina lake la kibinafsi, Yehova.—Zaburi 83:18.

Kwa sababu Biblia ni kitabu kutoka kwa Muumba wa wanadamu wote, hakisemi kwamba utamaduni fulani au watu fulani ni bora kuliko wengine. Ushauri wake haupitwi na wakati na unawanufaisha watu wote ulimwenguni. Biblia inapatikana katika lugha nyingi na imesambazwa kwa wingi kuliko kitabu kingine chochote.a Inamaanisha watu ulimwenguni pote wanaweza kusoma, kuelewa, na kuongozwa na ushauri wa Biblia. Mambo hayo yanathibitishwa na ukweli huu tunaosoma kwenye Biblia:

“Mungu hana ubaguzi, lakini katika kila taifa mtu anayemwogopa na kutenda uadilifu anakubaliwa naye.”​—MATENDO 10:34, 35.

Kama mzazi mwenye upendo anavyowaongoza watoto wake, Yehova Mungu ni Baba mwenye upendo anayetusaidia kupitia Neno lake, Biblia. (2 Timotheo 3:16) Tunaweza kulitumaini Neno lake; isitoshe, yeye ndiye aliyetuumba na anajua njia tunayopaswa kuifuata maishani ili tufanikiwe.

MWONGOZO UNAOTEGEMEKA

Picha: 1. Mwanamume akiwa kwenye garimoshi, anasoma Biblia kwenye simu yake. 2. Mwanamume amefungua Biblia kwenye simu yake ya mkononi.

Tunaweza kutumaini kwamba Biblia ndio mwongozo unaotegemeka wa kuwa na maisha bora ya wakati ujao, kwa sababu miaka 2,000 hivi iliyopita, ilitabiri kwa usahihi tabia ambazo watu wanaonyesha leo na matukio yanayotukia katika siku zetu.

MATUKIO

“Taifa litapigana na taifa, na ufalme kupigana na ufalme. Kutakuwa na matetemeko makubwa ya ardhi, na magonjwa na upungufu wa chakula katika sehemu mbalimbali.”​—LUKA 21:10, 11.

TABIA

“Katika siku za mwisho kutakuwa na nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo. Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, wenye kujidai, wenye majivuno, wakufuru, wasiotii wazazi, wasio na shukrani, wasio washikamanifu, wasio na upendo wa asili, wasiotaka makubaliano yoyote, wachongezi, wasiojizuia, wakali, wasiopenda wema, wasaliti, wenye vichwa vigumu, waliojaa kiburi, wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu.”​—2 TIMOTHEO 3:1-4.

Inawezekanaje kwamba Biblia ilitabiri kwa usahihi kabisa mambo yanayotukia leo? Bila shaka utakubaliana na Leung, kutoka Hong Kong, anayesema: “Unabii wa Biblia uliandikwa zamani sana. Haiwezekani kwa mwanadamu yeyote kutabiri kwa usahihi mambo hayo. Lazima Biblia iliongozwa na Mungu ambaye ni Mkuu zaidi kuliko sisi.”

Kwenye Biblia kuna unabii mwingi ambao tayari umetimizwa.b Hilo linathibitisha kwamba, kwa kweli, Biblia ni Neno la Mungu. Yehova anasema: “Mimi ni Mungu, na hakuna aliye kama mimi. Tangu mwanzo ninatabiri matokeo.” (Isaya 46:9, 10) Hivyo una sababu nzuri ya kutumaini kile ambacho Biblia inasema kuhusu wakati ujao.

MWONGOZO UTAKAOKUNUFAISHA SASA NA MILELE

Wazazi wamewashika mkono watoto wao wawili huku wakitembea mashambani kwa furaha.

Unapofuata mwongozo wa Maandiko Matakatifu, unajinufaisha mwenyewe. Fikiria mifano ifuatayo.

MAONI YENYE USAWAZIKO KUHUSU PESA NA KAZI

“Ni afadhali konzi moja ya pumziko kuliko konzi mbili za kazi ngumu na kukimbiza upepo.”​—MHUBIRI 4:6.

MAISHA YA FAMILIA

“Kila mtu kati yenu anapaswa kumpenda mke wake kama anavyojipenda mwenyewe; kwa upande mwingine, mke anapaswa kumheshimu sana mume wake.”​—WAEFESO 5:33.

KUWA NA UHUSIANO MZURI NA WENGINE

“Acha hasira na uache ghadhabu; usikasirike na kuanza kutenda uovu.”​—ZABURI 37:8.

Kutumia kanuni za Biblia kunakunufaisha sasa na pia kunakufungulia njia ya kuwa na maisha bora ya wakati ujao. Kwenye Biblia, tunasoma kuhusu ahadi za Mungu za kuwa na maisha bora ya wakati ujao, ambazo zinatia ndani

AMANI NA USALAMA

“Nao watafurahia kwelikweli wingi wa amani.”​—ZABURI 37:11.

KILA MTU ATAKUWA NA CHAKULA NA MAKAZI

“Watajenga nyumba na kuishi ndani yake, nao watapanda mashamba ya mizabibu na kula matunda yake.”​—ISAYA 65:21.

HAKUTAKUWA NA MAGONJWA WALA KIFO

“Kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.”​—UFUNUO 21:4.

Unapaswa kufanya nini ili upate maisha hayo? Chunguza makala inayofuata.

a Kwa maelezo zaidi kuhusu kutafsiriwa na kusambazwa kwa Biblia, tembelea tovuti ya www.jw.org/sw na utazame chini ya MAFUNDISHO YA BIBLIA > HISTORIA NA BIBLIA.

b Kwa maelezo zaidi, ona sura ya 9 ya kitabu Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Pia, kinapatikana mtandaoni kupitia www.jw.org/sw. Tazama chini ya MAKTABA > VITABU NA BROSHUA.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki