“Watangazaji Wenye Bidii wa Ufalme”—Mkusanyiko wa Wilaya wa Mashahidi wa Yehova Mnamo 2002
1 “Nilifurahi wakati waliponiambia: twende kwa nyumba ya BWANA.” (Zab. 122:1) Katika kuchunguza maneno ya mtunga-zaburi, ona (1) jinsi alivyohisi wakati alipoalikwa kujiunga katika kuabudu Yehova, (2) washiriki wazuri aliokuwa nao, ambao pia walipendezwa sana na ibada ya kweli, na (3) mipango ambayo lazima iwe ilihitajiwa ili kutoa mwaliko, kukusanyika pamoja, na kusafiri kwenda kwenye nyumba ya Mungu.
2 Je, maneno ya mtunga-zaburi hayarudilii hisia zetu wenyewe wakati tunaposikia kwamba mipango inachukuliwa kwa ajili ya mkusanyiko wetu ujao? Tunajaa matumaini tunapokumbuka furaha tulizopata kwenye mikusanyiko iliyopita na tazamio la kuwa tena kwenye mkusanyiko wa pekee pamoja na wenzetu wanaompenda Yehova. Mipango imechukuliwa kwa ajili ya Mkusanyiko wa Wilaya wa siku tatu “Watangazaji Wenye Bidii wa Ufalme” katika eneo lote la tawi la Congo mnamo 2002. Sasa ndio wakati wa kuchukua mipango ili tuhudhurie na kupokea faida kamili zaidi kutokana na karamu ya kiroho inayotungojea.
3 “Msimamizi-nyumba mwaminifu, mwenye busara,” ameanza kutayarisha chakula cha kiroho chenye kufika pa wakati wenye kufaa, ambacho kitatolewa kwenye mkusanyiko. (Luka 12:42) Kila kutaniko limetumwa kwenye mkusanyiko fulani hasa ili kuepuka msongamano. Kwa kuongezea, ndugu wengi wameanza kupanga zile idara mbalimbali za mkusanyiko ili “mambo yote yatukie kwa adabu na kwa mpango.” (1 Kor. 14:40) Kwa kuwa mambo mengi sana yamekwisha kutayarishwa kwa ajili ya faida yetu na hali yetu yenye kufaa, tunaweza kufanya nini kibinafsi ili kujitayarisha kwa ajili ya mkusanyiko?
4 Panga Mambo Sasa ili Kuhudhuria Zile Siku Tatu Zote: Je, unahitaji kuomba mapumziko kwa bwana wako wa kazi ili uhudhurie mkusanyiko wote ambao kwenye huo mmetumwa? Yehova anaelewa kwamba mabwana wengine wa kazi ni “wagumu kupendeza.” (1 Pet. 2:18) Lakini mikusanyiko yetu ni ya maana sana, nasi tunataka kufanya jitihada yenye bidii ili kuhudhuria programu nzima. Karibia Yehova katika sala kuhusu mambo kama hayo, ukitafuta mwongozo wake ili upate tokeo zuri.—Neh. 2:4.
5 Upangishaji: Kwa kawaida, upangishaji unafanywa kwa watu binafsi. Tunapaswa kuonyesha shukrani kwa ndugu na dada wanaokubali kutupangisha. Zaidi ya hayo, halingekuwa jambo lenye kufaa kwa wale wanaoonyeshwa ukaribishaji kama huo kuutumia vibaya kwa kuomba wapangishwe muda mrefu kabla au baada ya mkusanyiko. Upangishaji unatolewa tu muda wa mkusanyiko. Wale wanaofaidika na aina hiyo ya upangishaji wanapaswa kuheshimu mali ya wale wanaowapangisha, kutoharibu kitu chochote, kutokwenda mahali wasipoalikwa, na kuangalia kwamba watoto wao wafanye hivyohivyo. Ikiwa wapangishaji fulani wanakabiliana na tatizo lolote upande huo, wanapaswa mara moja kujulisha idara ya upangishaji, ambayo itafurahi kuwatolea msaada. Kazi nzuri na matokeo mazuri ya idara ya upangishaji vinategemea ushirikiano wa kila mmoja. (Ebr. 13:17) Tumepata ripoti kwamba wengine huacha kwa kutaka kwao wenyewe mahali walipopangishwa ili kwenda mahali pengine kunakopatikana labda rafiki au mtu mwingine wanayejuana naye. Hilo linafanya kazi ya akina ndugu wa idara ya upangishaji kuwa ngumu. Tunaomba wote washirikiane na idara hiyo.
6 Hakuna shaka kwamba Yehova anatoa utegemezo wake kwa kile kinachofanywa kwa ajili ya mikusanyiko ya kila mwaka. Kwa kuwa ndugu wengi wanaosafiri ili kwenda kwenye mkusanyiko wa wilaya wanahitaji mahali pa kupangishwa, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatosheleza ifaavyo mahitaji yao. Kwa kuwa mambo hayo yanahusiana na ibada ya kweli, tunapaswa kufuata kwa furaha maagizo yanayotolewa. Acheni tuonyeshe kwamba sisi ni waaminifu katika lililo dogo zaidi; hivyo tutaweza kupokea baraka tele zinazongojea wale wanaopendwa na Yehova.—Luka 16:10.
7 Tazama Pote Katika Kutaniko: Ikiwa tunajua kwamba ndugu au dada fulani ana uhitaji wa kimwili ambao unaweza kufanya iwe vigumu kwake kuhudhuria mkusanyiko, je, tunaweza ‘kupanuka’ katika upendo wetu na kutoa msaada fulani? (2 Kor. 6:12, 13; Kum. 15:7) Hiyo ndiyo roho ambayo Paulo alichochea kwenye 2 Wakorintho 8:14. Kwa nini usialike watu kama hao wasafiri nawe kwenda kwenye mkusanyiko? Ikiwa wao ni mapainia, yaelekea wana mambo mengi yaliyoonwa ya kushiriki nawe mnaposafiri. Ikiwa wao ni washiriki wa kutaniko wenye umri mkubwa, huenda wakawa na historia nzuri ajabu ya kitheokrasi ambayo haujapata kamwe kusikia. Je, kushirikiana na ndugu na dada kama hao hakutakuwa na uvutano mzuri juu yako na familia yako? Roho yako ya ukarimu itathaminiwa nao, nayo itathawabishwa na Yehova.—Mez. 28:27; Mt. 10:42.
8 Ingawa wale walio na mahitaji ya pekee hushughulikiwa kwanza na washiriki wa familia zao walio Wakristo, wazee na wengine katika kutaniko wanaojua mahitaji kama hayo wanaweza kwa upendo kusaidia katika kuchukua mipango. (1 Tim. 5:4) Wakati barua za Ombi la Chumba kwa Ajili ya Mahitaji ya Pekee zinapotolewa kwa Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko, halmashauri inapaswa kuchunguza sifa za kila mtu anayetoa ombi kabla ya kutuma maombi hayo kwenye Idara ya Upangishaji.
9 Itikia kwa Utayari Kuwa Mfanyakazi wa Kujitolea: Wakati wa mkusanyiko, mamia ya wafanyakazi wa kujitolea husaidia kuendesha vizuri zile idara mbalimbali. Wakaribishaji wanaotumikia mahali wanapokaa wasikilizaji na mahali pa kuegeshea magari hutoa mwelekezo kuhusiana na viti, nao huchunga magari yetu na makinga yetu wakati wa mchana. Idara ya Usafi inalo pendeleo la kulinda sifa tuliyo nayo ya kuwa safi, ikiacha mahali petu pa ibada pa muda pakiwa safi kuliko jinsi tulivyopakuta. Je, tunaweza kusaidia idara hizo na zingine zinazoweza kutumia utegemezo wetu? Je, utakuwa mfanyakazi wa kujitolea ili kutumikia “bega kwa bega” pamoja na ndugu zako?—Zef. 3:9, NW.
10 Je, Watu Wanaona Kweli Yale Tunayofanya? Wakati wa mkusanyiko wa wilaya mwaka uliopita, mwanamume mmoja ambaye alikuwa ameacha kujifunza na Mashahidi wa Yehova kwa zaidi ya miaka 20 iliyopita alikuwa akifanya kazi katika hoteli moja. Alieleza Mashahidi fulani kwamba alikuwa sasa akifikiria kurudilia funzo lake la Biblia na kwenda tena kwenye mikutano. Kwa nini? Kwa sababu ya jinsi alivyotendewa kwa upendo siku ambazo Mashahidi walipitisha katika hoteli hiyo.
11 Mchuuzi mmoja kwenye hoteli alisema kuhusu ndugu zetu: “Kikundi chenu ndicho kikundi bora zaidi kinachokaa katika hoteli zetu. Watu wenu ni wavumilivu na wenye adabu sana.” Hilo linapaswa kumfanya Baba yetu wa mbinguni ajisikie mwenye sifa kama nini anapotuona tukifuata shauri la Yesu: “Acheni nuru yenu ing’ae mbele ya watu, ili wapate kuona kazi zenu bora na kumpa utukufu Baba yenu aliye katika mbingu”!—Mt. 5:16.
12 Acheni tuonyeshe mtazamo wa Mfalme Daudi, aliyetarajia kwa furaha kwenda kwenye nyumba ya Yehova ya ibada. Mikusanyiko yetu ya wilaya ni chanzo cha maana sana cha chakula cha kiroho na ni nafasi isiyolinganika ya kupata ushirika wenye upendo. Kwa hiyo, tunawaalika kwa shauku mwanze kuchukua mipango ili kuhudhuria vipindi vyote vya zile siku tatu zote za Mkusanyiko wa Wilaya wa mwaka huu “Watangazaji Wenye Bidii wa Ufalme”!
[Kisanduku kwenye ukurasa wa 3]
Saa za Programu
Siku ya Tano na Siku ya Posho
3:30 - 11:00
Siku ya Yenga
3:30 - 10:00
[Kisanduku kwenye ukurasa wa 4]
Mipango Fulani ya Kuchukua kwa Ajili ya Kuhudhuria Mikusanyiko “Watangazaji Wenye Bidii wa Ufalme”
1. Ikiwa unapaswa kutembea mwendo mrefu ili kuhudhuria mkusanyiko, anza kuweka akibani fedha ili kulipia safari yako na ya familia yako, na pia chakula chenu.
2. Fikiria pia kutegemeza matayarisho ya mkusanyiko kupitia zawadi zako za kujitakia. ‘Usitokee mbele ya Yehova na mikono mitupu,’ lakini ‘mheshimu Yehova kwa vitu vyako vya thamani.’—Kum. 16:16; Mez. 3:9.
3. Tunatukuza pia jina la Yehova kwa kuwa na mwenendo mzuri na mavazi safi na yenye kufaa wakati wa mikusanyiko.—1 Kor. 10:31.
4. Azimieni kushirikiana na akina ndugu wanaoshughulika na utaratibu. Usichunge nafasi bure, ila tu kwa ajili ya washiriki wa familia yako au wale unaosafiri nao.
5 Wakati wa mapumziko, angalia kwamba ule chakula chepesi kusudi uweze kufaidika kikamili na vipindi vya kisha mchana-kati. Chakula kizito huleta usingizi.—Luka 8:18.
6. Usafi humheshimisha Yehova. Baada ya kila kipindi cha mkusanyiko, kila mmoja atataka kutimiza fungu lake ili kuacha mahali pa mkusanyiko pakiwa safi kwa kuokota karatasi na mambo mengine yenye kufanana na hayo kusudi hayo yatupwe katika mapipa ya kutupia takataka yaliyotayarishwa kwa kusudi hilo.—1 Pet. 1:15, 16.