Maagizo kwa Ajili ya Wale Walio na Migawo Kwenye Mkutano wa Utumishi
Kuanzia toleo hili la Huduma Yetu ya Ufalme, maneno ya programu ya Mkutano wa Utumishi yatarahisishwa. Maagizo na mambo ya kukumbuka yafuatayo yatatoa maelezo yaliyo wazi kuhusu yale yaliyosemwa katika habari “Jinsi ya Kujitayarisha kwa Ajili ya Mkutano wa Utumishi,” katika Huduma Yetu ya Ufalme ya Mwezi wa 5, 2009.
◼ Hotuba: Sehemu hii inahusu hotuba inayotegemea habari fulani inayotolewa. Itafanywa bila mazungumzo pamoja na wasikilizaji. Msemaji atakazia mawazo yatakayosaidia zaidi kutaniko.
◼ Maulizo na Majibu: Sehemu hii itatolewa kama Funzo la Mnara wa Mlinzi, itaanza na utangulizi mfupi sana na maneno ya kumalizia, na maulizo kuhusiana na kila fungu. Anayeongoza ataepuka kutoa maelezo mengi. Maandiko ya msingi yanaweza kusomwa ikiwa wakati unaruhusu. Wakati mwengine mafungu yanaweza kusomwa ikiwa tu maagizo yanaomba kufanya hivyo.
◼ Mazungumzo: Sehemu hii ni hotuba inayotia ndani mazungumzo pamoja na wasikilizaji kwa kiasi fulani. Si hotuba, na si sehemu ya maulizo na majibu.
◼ Maonyesho na Sehemu ya Kuuliza Maulizo: Maagizo yanaposema kwamba sehemu ina onyesho yanamaanisha kwamba ni ndugu anayeshugulikia sehemu hiyo ndiye aliye na daraka la kutia ndani onyesho; yeye mwenyewe hapaswi tena kufanya onyesho hilo. Wale atakaowachagua kufanya onyesho wanapaswa kuwa na uwezo wa kufanya hivyo na kuwa na mwenendo mzuri, na ikiwezekana ni vizuri wale watakaofanya onyesho wajue jambo hilo mbele ya wakati. Si vizuri kutumia wahubiri wapya na wasio na uzoefu ili kuonyesha kutaniko jinsi ya kuhubiri kwa mfano. Wanaweza kutumiwa kama wenye nyumba katika onyesho, lakini musiwatumie kama wahubiri katika onyesho ili tu kuwatolea nafasi ya kuonekana kwenye jukwaa (estrade). Wahubiri wanapofanya onyesho wanapaswa kuwatazama wasikilizaji. Wale wanaotumiwa katika sehemu ya kuuliza maulizo wanapaswa kuwa kwenye jukwaa wanapotoa maelezo yao pahali pa kufanya hivyo kwenye nafasi zao. Maonyesho na sehemu ya kuuliza maulizo yanapaswa kufanyiwa mazoezi. Ikionekana kwamba mkutano unataka kupitisha wakati, ndugu aliye na kipindi atafupisha sehemu yake, lakini asikose kufanya maonyesho na sehemu ya kuuliza maulizo. Ikiwa watumishi wa huduma wamepewa sehemu iliyo na onyesho ao sehemu ya kuuliza maulizo (interview) wataomba mratibu wa baraza la wazee ao mzee mwengine mawazo mbele ya kuchagua watu wa kutumia.
Ikiwa sehemu fulani ina maagizo ya pekee, maagizo hayo yanapaswa kufuatwa kwa uangalifu. Kwa kutoa sehemu ya Mkutano wa Utumishi kama inavyoelezwa hapo juu, ndugu watasaidia Mkutano wa Utumishi ‘utendeke kwa adabu na kwa mpango.’—1 Kor. 14:40.