Kusanyiko Lipya La Pekee La Siku Moja
1 “Wanaofundishwa na Yehova.” Hicho ndicho kitakuwa kichwa cha makusanyiko ya pekee ya siku moja yanayoanza mnamo Septemba. (Yn. 6:45) Mafundisho ya Yehova yanatusaidia kwelikweli kuishi maisha yenye kuridhisha. Yanakuza ndani yetu shukrani kubwa kwa ajili ya urithi wetu wa kiroho. Bidii tunayofanya ili kwamba wengine wasikie habari njema inatufanya tuwe washiriki wenye manufaa wa jamii. Kusanyiko hilo la pekee la siku moja litaonyesha wazi baraka wanazopata wale wanaofundishwa na Yehova.
2 Faida za mafundisho ya kimungu zitalinganishwa na hatari za ujuzi kutoka ulimwengu. Tutatambua waziwazi zaidi kwamba Yehova anatutolea mafundisho ya juu, mafundisho kutoka Neno lake, Biblia. Mkazo utawekwa juu ya sehemu tatu za ibada yetu katika hizo sisi ni wenye furaha kufundishwa na Mungu. Zaidi ya hilo, vijana watatiwa moyo kuiga mifano bora ya kibiblia, kama vile Daudi na Timotheo, na kujenga maisha yao kutokana na utendaji mbalimbali wa kiroho. Imani yetu itatiwa nguvu wakati tutakaposikia mifano ya uaminifu ya Mashahidi wazee-wazee. Wale ambao walijiweka wakfu kwa Mungu hivi karibuni na ambao wanatimiza matakwa yanayoombwa wataweza kubatizwa. Ikiwa hiyo ndiyo tamaa yao, wangepaswa kumjulisha mwangalizi-msimamizi mapema kabla ya kusanyiko.
3 Hotuba kuu ya kusanyiko la pekee la siku moja ni yenye kichwa: “Wanaofundishwa na Yehova Ili Kufanya Mapenzi Yake.” Itaonyesha kwa nini tunapaswa sote kuendelea kujifunza, wote kuwa imara katika imani na kuendelea kufanya maendeleo. Tutahimizwa kumwiga Yehova kwa kufundisha wengine kweli iongozayo kwenye uhai udumuo milele. Mambo yaliyoonwa yenye kujenga imani yetu yataonyesha jinsi vichapo vya Sosaiti vilivyosaidia watu wengi kupokea mafundisho ya Yehova. Mkazo utatiwa juu ya matokeo yenye manufaa ya programu ya ulimwenguni pote ya mafundisho ya Yehova.
4 Tuchukue mipango kamili ili kuhudhuria kusanyiko hilo. Tuwatie moyo wale wote wanaoonyesha kupendezwa kuwako. Tufurahie mapema mambo mazuri ambayo Mwelimishaji Mkuu atatufundisha.—Is. 30:20.