Kukusanya Watu wa Lugha Zote
1 Neno la Mungu ni lenye kutimizwa sasa! Watu “wa lugha zote za mataifa” wanakubali ibada ya kweli. (Zek. 8:23) Mashahidi wa Yehova wanasaidiaje watu wa ‘makabila zote, na vikundi vya watu, na lugha’ wawe na msimamo safi mbele ya Yehova, wakiwa na tazamio la kuokoka “dhiki kubwa”?—Ufu. 7:9, 14.
2 Tengenezo la Mungu Linajibu: Baraza Linaloongoza limechukua mipango ili vichapo vya kibiblia vipatikane katika lugha yapata 380 kusudi watu duniani pote waweze kuelewa waziwazi maana ya habari njema. Kutayarisha na kuchapisha vichapo katika lugha nyingi kama hizo ni kazi kubwa. Inahusisha kukusanya timu za watafsiri wenye kustahili na kuwaandalia msaada wanaohitaji ili kutafsiri vichapo vyetu katika lugha hizo zote, na pia kuchapisha na kusafirisha vichapo hivyo. Hata hivyo, fungu kubwa linatimizwa na wahubiri wa Ufalme wakiwa watu mmojammoja ambao wanapelekea watu ujumbe wa Biblia wenye kuokoa uhai.
3 Kukubali Ugumu: Vikundi vikubwa vya watu wenye kusema lugha za kigeni vinapatikana sasa mahali pengi. Ili kuwafikishia watu hao habari njema, watumishi wa Mungu wengi zaidi na zaidi wanajitahidi kujifunza Kichina, Kirusi, Kihispania, au lugha nyingine inayosemwa kwa ukawaida katika eneo lao. Wengine wanajifunza Lugha ya Ishara ya Kiamerika. Katika Congo zote mbili, kuna makutaniko 2,489 hivi na vikundi 63 vinavyohubiri na kutumia vichapo katika lugha 17 zaidi ya Kifaransa. Watu fulani ambao walikuwa hawajasikia kamwe kuhusu Yehova au ambao hawakujua lolote kuhusu Biblia wanakubali kweli ya Neno la Mungu.—Rom. 15:21.
4 Je, tunaweza kujitahidi kikamili zaidi kutangaza habari njema kwa watu walio katika eneo letu lakini ambao ni wa nchi nyingine? (Kol. 1:25) Makutaniko mengi yanapanga kazi ya kuhubiria vikundi vya watu wa kigeni wanaokaa katika maeneo yayo. Kwanza, wahubiri hujifunza vya kutosha kuhusu lugha hiyo ili kufanya utoaji mfupi kama huu: “Jambo. Hii ni habari njema kwa ajili yako. [Kisha toa trakti au broshua ambayo inapatikana katika lugha hiyo.] Kwa heri.” Yehova ni mwenye kubariki kwelikweli maneno hayo machache ya mwanzoni!
5 Ujumbe wa Ufalme unavutia watu wa hali zote na lugha zote. Acheni tuchukue nafasi ya kuushiriki nao.