‘Tung’ae Tukiwa Wamulikaji’
1 Katika giza la kiroho na la kiadili la mfumo wa mambo wa sasa, waabudu milioni sita hivi wa Mungu wa kweli, Yehova, ‘wanang’aa wakiwa wamulikaji’ katika nchi 234 ulimwenguni pote. (Flp. 2:15) Hilo linafanya tuonekane wazi. Tunaonyeshaje nuru ya kweli yenye thamani inayotoka kwa Yehova?—2 Kor. 3:18.
2 Matendo Yetu: Watu wanaona mwenendo wetu upesi. (1 Pet. 2:12) Mwanamke mmoja alitambua kwamba Shahidi aliyetumika naye alikuwa mwenye fadhili na mwenye kusaidia na hakutumia lugha chafu au kuchekea mizaha isiyo safi. Wengine walipojaribu kuchokoza Shahidi huyo kwa kutumia maneno machafu mahali alipokuwa, alibaki mwenye kutulia huku akiwa imara kwa lililo sawa. Jambo hilo lilikuwa na uvutano gani juu ya mwanamke huyo? Anakumbuka: “Niliguswa sana na mwenendo wake hivi kwamba nikaanza kuuliza maulizo kuhusu Biblia. Nikaanza kujifunza Neno la Mungu na nikabatizwa baadaye.” Anaongeza: “Mwenendo wake ndio ulionisadikisha nichunguze imani za Mashahidi wa Yehova.”
3 Mtazamo wetu kuelekea mamlaka, maoni yetu kuhusu mazoea ya kilimwengu, na usemi wetu safi hufanya Mashahidi wa Yehova waonekane kuwa watu wanaoishi kulingana na viwango vya juu vya Biblia. Kazi bora kama hizo zinaweza kuletea Yehova utukufu na kuvuta wengine kwenye ibada yake.
4 Maneno Yetu: Bila shaka, huenda wale wanaoona mwenendo wetu mzuri wasijue kwa nini tuko tofauti isipokuwa tunazungumza nao kuhusu imani zetu. Je, wale unaotumika nao au unaoenda shuleni nao wanajua kwamba wewe ni Shahidi wa Yehova? Je, unatafuta nafasi za kugeuza mazungumzo ya kawaida kuwa ushahidi? Je, azimio lako ni ‘kuacha nuru yako ing’ae mbele ya watu’ kila wakati nafasi inayofaa inapojitokeza?—Mt. 5:14-16.
5 Kutimiza utume wetu tukiwa wachukuaji-nuru kunaomba roho ya kujinyima. Mtazamo wa kujitoa kwa nafsi yote utatuchochea tuache mambo yasiyo ya maana sana ili kufanya mengi zaidi iwezekanavyo katika ile kazi inayookoa uhai ya kuhubiri na kufanya wanafunzi.—2 Kor. 12:15.
6 Kupitia matendo na maneno yetu, na tuendelee kung’aa kama wamulikaji. Tukifanya hivyo, wengine wanaweza kuchochewa wajiunge nasi katika kumpa Yehova utukufu.