Pongezi Linaburudisha
1 “Je, sikuwa mtoto mzuri leo?” msichana yule mdogo akasema kwa kichefuchefu wakati wa kulala. Ulizo hilo lilimshtusha mama yake. Ijapokuwa aliona jinsi binti wake alivyokuwa akijitahidi sana kujiendesha siku hiyo, alikuwa amepuuza kusema hata neno moja la shukrani. Machozi ya msichana huyo mdogo yanapaswa kutukumbusha kwamba sisi sote—vijana na wazee—tunahitaji pongezi. Je, tunatia moyo wale tunaoshirikiana nao kwa kuonyesha kwamba tunathamini mema wanayofanya?—Met. 25:11.
2 Wakristo wenzetu wanatutolea sababu nyingi nzuri za kuwapongeza. Wazee, watumishi wa huduma, na mapainia wanafanya kazi ngumu ili kutimiza madaraka yao. (1 Tim. 4:10; 5:17) Wazazi wenye kuogopa Mungu wanafanya yote wawezayo ili kulea watoto wao katika njia za Yehova. (Efe. 6:4) Vijana Wakristo wanafanya pigano kali ili kupinga “roho ya ulimwengu.” (1 Kor. 2:12; Efe. 2:1-3) Wengine wanatumikia Yehova kwa uaminifu ijapokuwa uzee, matatizo ya kiafya, au majaribu mengine. (2 Kor. 12:7) Hao wote wanastahili pongezi. Je, tunawashukuru kwa jitihada zao zinazostahili kusifiwa?
3 Pongezi la Kibinafsi na la Waziwazi: Kwa kweli, sisi sote tunathamini kupongezwa kutoka jukwaani. Hata hivyo, pongezi linaburudisha hata zaidi linapoelekezwa kwetu binafsi. Kwa mfano, katika sura ya 16 ya barua yake kwa Waroma, Paulo alisema waziwazi maneno ya uthamini kuelekea Fibi, Priska na Akila, Trifaina na Trifosa, na Persisi, na wengine. (Rom. 16:1-4, 12) Bila shaka, maneno yake yaliburudisha waaminifu hao. Kusifu kwa namna hiyo kunahakikishia ndugu na dada zetu kwamba wanahitajiwa, na kunatuunganisha zaidi. Je, ulitoa pongezi la kibinafsi na la waziwazi hivi karibuni?—Efe. 4:29.
4 Pongezi la Kutoka Moyoni: Ili liburudishe kwa kweli, pongezi linapaswa kutoka moyoni. Watu wanaweza kutambua ikiwa tunasema kwa unyofu au ikiwa ‘tunabembeleza kwa ulimi’ tu. (Met. 28:23) Tunapojizoeza kutambua mema ya wengine, moyo wetu utachochewa kutoa pongezi. Acheni tuwe wakarimu kwa kutoa pongezi kwa unyofu, tukijua kwamba “neno linalosemwa wakati unaofaa ni jema kama nini!”—Met. 15:23.