Pendezwa Kibinafsi na Wengine —Kwa Kuwashukuru
1 Shukrani ya kweli inatia watu moyo, inawachochea kutenda mema, na inawaletea furaha. Wahubiri wengi wameona kwamba mara nyingi maneno machache tu ya shukrani yanayotoka moyoni, yanafanya watu wakubali kusikiliza mahubiri. Tunaweza namna gani kuwashukuru watu tunapotaka kuwahubiria habari njema?
2 Uwe Mtazamaji Mzuri: Baada ya Yesu kurudi mbinguni, yeye alitazama na kupendezwa na matendo mazuri ya makutaniko saba ya Asia Ndogo. (Ufu. 2:2, 3, 13, 19; 3:8) Vilevile, kupendezwa kweli na watu tunaokutana nao katika kazi yetu ya kuhubiri kutatuchochea kutafuta nafasi za kuwashukuru. Kwa mfano, tunaweza kumshukuru mtu aliye na uwanja wa nyumba ulio safi, mzazi anayependa watoto wake, au mtu anayeonyesha uso wa furaha na kusalimia watu wote, mifano yote hiyo inatutolea nafasi za kushukuru watu. Je, wewe unatazama watu na kutumia nafasi kama hizo ili kuwashukuru?
3 Uwe Msikilizaji Mzuri: Unapohubiria wengine, uwaombe watoe mawazo yao kwa kuwauliza maulizo yenye kufaa. Uwaonyeshe heshima kwa kusikiliza vizuri yale wanayosema. (Rom. 12:10) Labda kwa kufanya hivyo watasema jambo fulani linaloweza kukufanya umtolee mtu shukrani ya kutoka moyoni, na kisha hilo linaweza kukuwezesha kuendeleza mazungumzo juu ya habari mnazokubaliana.
4 Uwe Mwenye Kutambua Mambo: Tutafanya nini ikiwa msikilizaji anasema jambo fulani lisilopatana na kweli ya Biblia? Badala ya kumwambia kwamba yale anayosema si ya kweli, tutamshukuru na kuendelea kusema hivi: “Ninaona kwamba habari hii inakupendeza sana.” (Kol. 4:6) Hata ikiwa mtu ni mwenye ubishi, tunaweza kila mara kumshukuru kwa sababu anasema yale anayo moyoni kuhusu habari yetu. Kuongea hivyo kwa upole kunaweza kumtuliza mtu anayeonekana kuwa mwenye kupinga habari njema.—Met. 25:15.
5 Ili tuwe wenye kutia moyo, tunapaswa kuwashukuru watu kwa maneno yanayotoka moyoni. Maneno ya shukrani yanamheshimisha Yehova na yanaweza kuwavutia watu wakubali ujumbe wa Ufalme.