Kisanduku Cha Maulizo
◼ Je, funzo la Biblia katika familia linapaswa kuripotiwa kwa kutaniko?
Ikiwa mzazi Mkristo anaongoza funzo la Biblia katika familia na ikiwa watoto ambao hawajabatizwa wanahusika, kiasi cha juu zaidi ambacho mzazi huyo anaweza kuripoti ni saa moja kwa juma, ziara ya kurudia moja kwa juma, na funzo moja la Biblia kwa mwezi. Mambo ni hivyo hata ikiwa funzo linachukua zaidi ya saa moja, hata ikiwa linaongozwa zaidi ya mara moja kwa juma, au hata ikiwa mzazi anajifunza na kila mtoto kibinafsi.—Ona kitabu Huduma Yetu, uku. 104.
Ikiwa wote nyumbani ni Mashahidi waliobatizwa, wala wakati wala funzo lenyewe halitaripotiwa kuwa utumishi wa shambani (isipokuwa mtoto mmoja bado anajifunza kitabu cha pili baada ya ubatizo). Ni hivyo kwa kuwa ripoti ya utumishi wa shambani ya kutaniko inaonyesha kwanza kabisa yale yanayotimizwa katika kuhubiri habari njema na kufundisha kweli ya Biblia kwa wale wasio watumishi wa Yehova waliojiweka wakfu na kubatizwa. (Mt. 24:14; 28:19, 20) Hata hivyo, hilo halipunguzi kwa njia yoyote umaana wa kuongoza funzo hilo kwa ukawaida.
Ni daraka la wazazi Wakristo kujifunza na watoto wao. Wale wanaohitaji msaada ili kusitawisha au kuboresha funzo lao la familia wanaweza kuomba wazee wawasaidie. Ikiwa hali zinafanya iwe vizuri mhubiri mwingine ajifunze Biblia na mwana au binti asiyebatizwa katika familia ya Kikristo inayoshirikiana na kutaniko, mwangalizi msimamizi au mwangalizi wa utumishi anapaswa kuombwa shauri. Ikiwa funzo hilo linakubaliwa, yule anayeliongoza anaweza kuliripoti kama anavyofanya kuhusu funzo lingine lolote la Biblia.
Kuzoeza watoto katika njia za Yehova kunahusisha wakati mwingi na jitihada nyingi zaidi kuliko inavyoonekana kwenye ripoti ya utumishi wa shambani. (Kum. 6:6-9; Met. 22:6) Wazazi Wakristo wanapaswa kupongezwa kwa kutimiza daraka lao zito la kulea watoto wao “katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova.”—Efe. 6:4.