Programu ya Familia—Funzo la Familia
1 Zawadi kubwa kupita yote ambayo wewe mzazi Mkristo unaweza kutolea watoto wako ni upendo wako kwa Yehova. Kikao cha maana ambacho katika hicho jambo hilo linaweza kufanywa ni wakati ‘mnapoketi katika nyumba yenu’ kwa ajili ya programu ya kila juma ya funzo la Biblia la familia. (Kum. 6:5-7) Iwe una mwenzi mwenye kuamini, unaishi katika nyumba iliyogawanyika kidini, au wewe ni mzazi mwenye kulea watoto peke yako, unaweza kusaidia watoto wako wakukaribie wewe na wamkaribie Yehova kwa kuwa na funzo la familia la kawaida.
2 Jinsi ya Kuanza: Hatua ya kuanza ni kusitawisha kawaida ya kujifunza mkiwa familia. Ikiwa hamuna uhakika kuhusu wakati wa kufanya funzo, kwa nini msizungumzie jambo hilo mkiwa familia? (Met. 15:22) Ikiwa mna watoto wachanga, mnaweza kupendelea zaidi kuwa na vipindi vingi vya funzo vifupi vifupi katika juma. Amueni programu inayofaa zaidi watu wa nyumbani mwenu. Pangeni wakati kamili kwa ajili ya funzo kwenye programu ya familia yenu, na muazimie kushikamana na wakati huo.
3 Ni mambo gani mnayoweza kujifunza? Wengine wanatayarisha somo litakalochunguzwa kwenye Funzo la Kitabu la Kutaniko au Funzo la Mnara wa Mlinzi linalokuja. Wengine pia wanachunguza habari iliyotayarishwa hasa kwa ajili ya vijana. Baba ya mwana na binti walio wachanga alisema: “Jambo moja linalofanya watoto waone funzo letu kuwa jambo kuu katika juma ni kwamba sisi tunafanya mchezo wa kuigiza masimulizi ya Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia. Ufahamu na uelewevu tunaopata ni wa maana sana kuliko kusoma tu mafungu mengi.”
4 Jifunzeni Kila Juma: Funzo la familia linapaswa kufanywa kwa kawaida na kutazamiwa kwa shangwe na washiriki wote wa familia. Mabadiliko fulani kuhusu siku na wakati yanaweza kuruhusiwa ili kushughulikia hali zisizotazamiwa. Kunaweza pia kuwa pindi ambapo rekebisho fulani katika habari ya kujifunza linahitajiwa. Lakini rekebisho lolote linalohitajiwa halipaswi kusimamisha kwa muda mrefu funzo la familia kama lilivyopangwa katika programu. Katika familia moja, binti anaeleza: “Ikiwa wakati wa kufanya funzo letu lazima ubadilishwe, sikuzote Baba anaweka huo wakati mpya kwenye mlango wa friji (frigo), ili sisi sote tujue funzo litafanywa wakati gani.” Jitihada kama hizo ili kudumisha funzo la familia la kawaida zinastahili kupongezwa. Mnapoendelea kulea watoto wenu “katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova,” mnaonyesha upendo wenu kwao na kwa Baba yetu aliye mbinguni.—Efe. 6:4.