Jinsi Washiriki wa Familia Wanavyofanya Kazi Pamoja ili Kushiriki Kikamili—Katika Funzo la Biblia
1 Kweli huongeza maana halisi na kusudi juu ya maisha ya familia, lakini mafanikio katika kumtumikia Yehova hayajileti yenyewe. Kujenga familia yenye nguvu kiroho huchukua wakati na jitihada. Katika jitihada hiyo, washiriki wa familia wanahitaji sana kutumika pamoja kwa ukaribu. Makala hii ya kwanza ya mfululizo wenye sehemu tatu itakaza uangalifu juu ya jinsi familia zinavyoweza kushirikiana katika kusitawisha mazoea mazuri ya funzo.
2 Kwa Kusoma Biblia Kila Siku: Mezali 24:5 inasema kwamba “mtu wa maarifa anaongeza uwezo.” Ujuzi unaopatikana kwa kusoma Neno la Mungu kila siku humpa mtu nguvu ya ndani inayohitajiwa ili kukinza mashambulio ya Shetani yanayolenga hali yake ya kiroho. (Zab. 1:1, 2) Je! nyinyi husoma Biblia kila siku mkiwa familia? Programu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi huonyesha “Programu ya Ziada ya Usomaji wa Biblia” ya kila juma mwakani. Kuifuata kwaomba kuchukua kama dakika kumi tu kwenye wakati wa familia kila siku. Chagueni wakati wenye kufaa, kama vile wakati wa chakula cha asubuhi, baada ya mlo wa jioni, au kabla ya kulala, ili msome Biblia na kuchunguza andiko la siku kutoka Kuyachunguza Maandiko Kila Siku. Fanyeni jambo hilo liwe sehemu ya programu ya kila siku ya familia yenu.
3 Kwa Kujifunza Pamoja Kila Juma: Funzo la Biblia la familia lingepaswa kuwa ndilo jambo la maana zaidi katika juma. Kila mshiriki anapaswa kulitegemeza kwa kushiriki funzo kwa bidii. Kichwa cha familia atataka kufikiria mahitaji ya familia anapochagua habari ya funzo na siku, wakati, na urefu wa funzo. Wekeni funzo la familia pa nafasi ya kwanza katika programu ya juma. Msiruhusu mambo ya maana ndogo zaidi yalikatize.—Flp. 1:10, 11.
4 Baba mmoja ambaye mara nyingi alipigiwa simu nyumbani kuhusu mambo ya biashara alikata simu wakati wa funzo la familia. Ikiwa wanunuzi walikuja nyumbani, walikaribishwa wajiunge katika funzo au wangoje hadi mwisho wa funzo. Baba huyo alikuwa na nia thabiti kwamba kitu chochote kisizuie funzo la familia. Jambo hilo lilipenya moyo wa watoto wake. Biashara yake pia ilifanikiwa [Meaning: it prospered].
5 Ni jambo lenye kupendeza kama nini washiriki wa familia wanapofanya kazi pamoja katika utendaji wa kiroho. Uaminifu katika jitihada zetu za kushiriki kikamili katika funzo la Biblia la familia utaleta baraka ya Yehova.—Zab. 1:3.