Msaada kwa Familia
1. Namna gani Sabato ya kila juma ilifaidi familia za Waisraeli?
1 Sabato ulikuwa mpango wenye upendo kutoka kwa Yehova ambao ulifaidi familia. Siku ya Sabato, Waisraeli waliacha kazi zao za kawaida na walipata wakati wa kufikiri sana juu ya wema wa Yehova na uhusiano wao pamoja naye. Wazazi walitumia wakati huo ili kukazia sheria ya Yehova katika mioyo ya watoto wao. (Kum. 6:6, 7) Kila juma, Sabato iliwatolea watu wa Yehova nafasi ya kufikiri sana kuhusu uhusiano wao pamoja na Yehova.
2. Sheria ya Sabato inatufundisha nini kumhusu Yehova?
2 Kwa kweli, Yehova haombi tena familia zishike Sabato. Hata hivyo, sheria hiyo inatufundisha jambo fulani kumhusu Mungu wetu. Sikuzote, anapenda kabisa watu wake wawe na hali njema ya kiroho. (Isa. 48:17, 18) Leo, Ibada ya Familia ya mangaribi ni njia moja inayoonyesha kwamba Yehova anapenda kabisa watu wake wawe na hali njema ya kiroho.
3. Ibada ya Familia ya mangaribi ina kusudi gani?
3 Ibada ya Familia ya Mangaribi Ina Kusudi Gani? Katika mwezi wa 1, 2009, kulianzishwa mpango wa kuhuzuria Funzo la Kitabu la Kutaniko, Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, na Mkutano wa Utumishi siku ileile. Moja ya sababu iliyofanya kuwe na badiliko hilo ni hii: kutolea familia nafasi ya kutia nguvu uhusiano wao pamoja na Yehova kwa kupanga mangaribi fulani kila juma kwa ajili ya ibada ya familia. Kila familia ilitiwa moyo ifanye funzo la familia siku ambayo walikuwa wakifanya funzo la kitabu, ikiwa iliwafaa, na kutumia wakati huo kwa ajili ya mazungumzo ya Biblia yasiyo ya haraka na funzo linalopatana na mahitaji ya familia.
4. Je, Ibada ya Familia ya mangaribi inahitaji kuchukua saa moja tu? Eleza.
4 Ili kuhuzuria Funzo la Kitabu la Kutaniko, tulihitaji wakati ili kuvaa, kujielekeza mahali ambapo mkutano huo utafanywa, na mambo mengine. Kwa wengi kati yetu, mambo hayo yaliwachukua wakati mwingi kupita saa moja ambayo mkutano huo ulichukua. Kwa kuwa programu ya mikutano yetu imebadilishwa, sasa mangaribi hiyo inatumiwa tu ili kumwabudu Yehova katika familia. Kwa hiyo, hatuwezi kusema kwamba Ibada ya Familia ya mangaribi itachukua tu saa moja. Tunapaswa kufikiria mahitaji ya familia na uwezo wa kila mmoja katika familia, na hivyo kupanga wakati kulingana na mahitaji hayo.
5. Je, wakati wote wa ibada watu wa familia wanapaswa kufanya mazungumzo wakiwa kikundi? Eleza.
5 Je, Wakati Wote wa Ibada Watu wa familia Watafanya Mazungumzo Wakiwa Kikundi? Waume na wake zao wanapozungumzia pamoja habari fulani za Maandiko, na familia zilizo na watoto wanapofanya hivyo, wanatiana moyo. (Rom. 1:12) Hilo linafanya watu wa familia wakaribiane. Kwa hiyo, mazungumzo yenye kutegemea Maandiko ndio sehemu ya maana zaidi ya Ibada ya Familia ya mangaribi. Lakini, kila mutu katika familia anaweza pia kutumia wakati huo ili kufanya funzo la pekee. Kwa mfano, kisha mazungumzo ya kikundi, kila mutu anaweza kuendelea kujifunza yeye mwenyewe, labda kutayarisha mikutano ao kusoma magazeti. Familia fulani zinazima televizyo muda wote wa mangaribi hiyo.
6. Mazungumzo yanaweza kuongozwa namna gani?
6 Mazungumzo Yanaweza Kuongozwa Namna Gani? Si lazima kila mara, kufanya mazungumzo kwa maulizo na majibu. Ili kufanya Ibada ya Familia ya mangaribi iwe yenye kuchangamsha na yenye kupendeza, familia nyingi zina programu iliyo kama ile ya mikutano tunayofanya katikati ya juma. Wanagawanya mazungumzo katika sehemu mbalimbali na wanashugulikia sehemu hizo kwa njia mbalimbali. Kwa mfano, wanaweza kusoma Biblia pamoja, kutayarisha sehemu fulani za mikutano, na kufanya vipindi vya mazoezi kwa ajili ya mahubiri. Ona mapendekezo fulani kwenye ukurasa wa 6.
7. Wazazi watajikaza ili kuwe hali gani?
7 Wazazi Watajikaza Ili Kuwe Hali Gani? Familia itafaidika zaidi na funzo ikiwa kuna hali ya upendo na utulivu. Nyakati fulani, munaweza kujifunzia inje, ikiwa hali ya hewa ni yenye kufaa. Munaweza kufanya mapumziko ikiwa inahitajiwa. Familia fulani zinapanga kufanya jambo fulani la kujifurahisha kisha ibada. Hata ikiwa wazazi wataepuka kukaripia watoto ao kuwapa malipizi wakati wa Ibada ya Familia ya mangaribi, wanaweza kutumia wakati fulani ili kuzungumzia mwelekeo ao tatizo fulani ambalo wametambua katika familia. Lakini, inaweza kuwa vizuri kuchagua wakati mwingine katika juma ili kuzungumzia na mtoto mambo fulani ya kipekee kwa siri na hivyo kuepuka kumpatisha haya mbele ya ndugu na dada zake. Ibada ya Familia ya mangaribi haipaswi kuwa kipindi chenye kuchosha ambacho hakifurahishe, lakini inapaswa kuonyesha kwamba tunamwabudu Mungu mwenye furaha.—1 Tim. 1:11.
8, 9. Baba wa familia wanaombwa kutayarisha nini?
8 Baba wa Familia Anaweza Kutayarisha Nini? Familia itafaidika zaidi ikiwa baba wa familia anatayarisha mbele ya wakati kila Ibada ya Familia ya mangaribi kwa kuchagua mambo ambayo watazungumzia na namna nzuri zaidi ya kuyazungumzia. (Met. 21:5) Itakuwa vizuri mume azungumze na muke wake ili kuchagua mambo hayo. (Met. 15:22) Nyakati fulani, baba wa familia wanaweza kuomba watoto watoe mapendekezo yao. Kwa kufanya hivyo, watajua vizuri mambo yanayowapendeza watoto ao kuwahangaisha.
9 Majuma mengine, baba wa familia hatatumia wakati mwingi ili kutayarisha. Labda familia itafurahia kufanya mambo fulani ya kawaida kila juma, na hivyo baba wa familia hatalazimika kutumia programu mpya kila wakati. Kisha kila funzo, linaweza kuwa jambo lenye kusaidia baba atayarishe funzo la juma lijalo kwa kuwa wakati huo anakukumbuka mahitaji ya kiroho ya familia yake. Baba fulani wa familia wanaandika programu fupi kwenye karatasi na kuibandika mahali ambapo watu wa familia wanaweza kuiona kwa urahisi. Kufanya hivyo kunawachochea na kuwafanya wangojee kwa hamu Ibada ya juma lijalo, na pia wanapata wakati wa kujitayarisha ikiwa inahitajiwa.
10. Wale wanaoishi peke yao wanaweza kufanya nini wakati wa Ibada ya Familia ya mangaribi?
10 Nitafanya Nini Ikiwa Niko Peke Yangu Katika Familia? Wale wanaoishi peke yao ao wale walio Mashahidi peke yao katika familia wanaweza kufanya funzo la pekee wakati wa Ibada ya Familia. Programu nzuri ya funzo la pekee inapaswa kutia ndani kusoma Biblia, kutayarisha mikutano, na kusoma Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Wahubiri fulani wanapanga kutafuta maelezo katika vichapo kuhusu habari fulani au jambo fulani ambalo hawaelewi vizuri. Wakati fulani, wanaweza kualika mhubiri mwingine ao familia fulani ishiriki katika funzo lao ili kufanya mazungumzo yenye kujenga yanayotegemea Maandiko.
11, 12. Ni faida gani fulani zinazotokana na kufanya Ibada ya Familia ya mangaribi kwa ukawaida?
11 Kufanya Ibada ya Familia ya Mangaribi kwa Ukawaida Kuna Faida Gani? Wale wanaoshiriki kwa moyo wote katika ibada ya kweli wanamkaribia Yehova zaidi. Pia, watu wa familia wanaomwabudu Yehova pamoja wanatia nguvu vifungo vya familia. Mume mmoja na muke wake waliandika hivi kuhusu baraka ambazo wamepata: “Tukiwa mume na muke mapainia wasio na watoto, tunangojea kwa hamu siku ya Ibada yetu ya Familia. Tunajisikia kwamba tunakaribiana na pia tunamkaribia Baba yetu wa mbinguni. Tunapoamka asubuhi siku ambayo tumepanga kujifunza, tunaambiana hivi: ‘Unakumbuka mangaribi tutafanya nini? Ibada ya Familia ya mangaribi!’”
12 Ibada ya Familia ya mangaribi inasaidia pia familia zilizo na mambo mengi ya kufanya. Mama mmoja anayelea watoto wawili peke yake na aliye painia wa kawaida aliandika hivi: “Hapo mbele, funzo letu la familia halikufaidi familia yetu. Lilikuwa la kushtukia na halikufanywa kwa ukawaida kwa kuwa nilikuwa mwenye kuchoka. Sikujua jinsi ya kupangia funzo la familia ili lisivurugwe na mambo mengine. Kwa hiyo, ninawaandikia ili kuwashukuru sana kwa ajili ya mpango wa Ibada ya Familia ya mangaribi. Sasa tunaifanya kwa ukawaida na tumepata faida nyingi.”
13. Familia yenu itafaidika na mpango huo kutokana na nini?
13 Kama mpango wa Sababo ulivyokuwa, mpango wa Ibada ya Familia ya mangaribi ni zawadi kutoka kwa Baba yetu wa mbinguni inayoweza kusaidia familia. (Yak. 1:17) Familia za Waisraeli zilifanya uhusiano wao pamoja na Mungu uwe mzuri zaidi kutokana na namna zilivyoshika Sabato. Leo pia, familia yetu itafanya uhusiano wake pamoja na Mungu uwe mzuri zaidi kutokana na namna tunavyotumia mangaribi iliyopangwa kwa ajili ya ibada ya familia. (2 Kor. 9:6; Gal. 6:7, 8; Kol. 3:23, 24) Kwa kufuata vizuri mpango huo, familia yenu inaweza kusema kama mtunga-zaburi: “Lakini mimi, kumkaribia Mungu ni kwema kwangu. Nimeweka kimbilio langu katika Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.”—Zab. 73:28.
[Wazo la fungu kwenye ukurasa 5]
Ibada ya Familia ya mangaribi haipaswi kuwa kipindi chenye kuchosha ambacho hakifurahishe, lakini inapaswa kuonyesha kwamba tunamwabudu Mungu mwenye furaha
[Sanduku katika ukurasa wa 6]
ICHUNGWE
Mapendekezo Fulani kwa Ajili ya Ibada ya Familia ya Mangaribi
Biblia:
• Musome pamoja sehemu ya usomaji wa Biblia wa kila juma. Katika Biblia, habari fulani zinaandikwa hivi kwamba mutu mmoja anaweza kusoma simulizi, na wengine wanaweza kusoma maneno ya watu fulani wanaozungumziwa katika Biblia.
• Munaweza kufanya kama mchezo sehemu fulani ya usomaji wa Biblia.
• Mutolee kila mutu wa familia mgawo wa kusoma sura fulani za Biblia mbele ya wakati na kumwomba aandike ulizo moja ao maulizo mawili kuhusu habari hiyo. Kisha mutafute pamoja majibu kwa maulizo ya kila mmoja.
• Kila juma, mutayarishe karatasi ndogo ambako munaandika andiko fulani la Biblia na mujaribu kuweka andiko hilo akilini na kulieleza. Mukusanye karatasi hizo, na kurudilia maandiko hayo kila juma ili kuona ni maandiko ngapi ambayo mumekwisha kuchunga akilini.
• Musikilize sehemu iliyorekodiwa ya usomaji wa Biblia mukifuata usomaji katika Biblia zenu.
Mikutano:
• Mutayarishe pamoja sehemu fulani za mikutano.
• Mwimbe nyimbo za Ufalme ambazo zitaimbwa kwenye mikutano ya juma lijalo.
• Ikiwa mutu fulani ana mgawo kwenye Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ao onyesho kwenye Mkutano wa Utumishi, azungumzie mawazo ambayo ametayarisha ili kutoa mgawo wake, ao afanye mazoezi ya mgawo wake mbele ya watu wengine wa familia.
Mahitaji ya Familia:
• Muzungumzie habari za kitabu Vijana Huuliza ao Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu.
• Mufanye mazoezi kuhusu jinsi ya kushugulikia tatizo fulani linaloweza kutokea kwenye masomo.
• Mufanye vipindi vya mazoezi ambamo wazazi na watoto wanabadilishana migawo. Watoto wanafanya utafiti kuhusu habari fulani na kisha wanafikiri pamoja na wazazi.
Mahubiri:
• Mufanye vipindi vya mazoezi ili kutayarisha jinsi ya kutolea watu ushahidi Siku ya Posho na Siku ya Yenga.
• Muzungumzie miradi fulani ambayo watu wa familia wanaweza kujiwekea ili kushiriki zaidi katika mahubiri katika kipindi cha Ukumbusho ao wakati wa mapumziko.
• Mutolee kila mutu wa familia dakika chache ili kutafuta habari katika vichapo kuhusu jinsi ya kujibu maulizo mbalimbali ambayo watu wanaweza kuuliza katika mahubiri, kisha mufanye vipindi vya mazoezi.
Mapendekezo Mengine:
• Musome pamoja habari fulani katika magazeti ya sasa.
• Mwombe kila mutu wa familia asome mbele ya wakati habari fulani inayompendeza zaidi ambayo aliona katika magazeti ya sasa, na kisha mumwombe azungumzie habari hiyo.
• Mara kwa mara, mwalike mhubiri fulani ao mume na muke wake washiriki katika Ibada yenu ya Familia na labda munaweza kuwauliza maulizo.
• Mutazame na kuzungumzia video moja kati ya video zetu.
• Muzungumzie pamoja habari “Vijana Huuliza” ao “Mazungumzo ya Familia” zilizo katika Amkeni!
• Muzungumzie pamoja habari “Wafundishe Watoto Wako” ao “Kwa Ajili ya Vijana” zilizo katika Mnara wa Mlinzi.
• Musome na kuzungumzia habari fulani ya Kitabu cha Mwaka cha sasa ao ya kitabu fulani kilichotolewa kwenye mkusanyiko wa wilaya uliopita.
• Kisha kuhuzuria mkusanyiko fulani, murudilie mambo makuu.
• Mutazame kiumbe fulani cha Yehova, na muzungumzie yale ambayo kiumbe hicho kinatufundisha kumhusu Yehova.
• Muchunguze pamoja kitu fulani, kama vile picha, ramani (carte) ao chati.