Tumia Vizuri Zaidi Wakati Wako Katika Kazi ya Kuhubiri
1 Kwa kweli, kuna mambo mengi ya kutimiza katika kazi yetu ya kuhubiri, na wakati uliobaki umepungua. (Yoh. 4:35; 1 Kor. 7:29) Kwa kupanga mambo vizuri na mbele ya wakati, tunaweza kutumia vizuri zaidi wakati ambao tumejipangia kwa ajili ya mahubiri.
2 Uwe Umejitayarisha: Mbele ya kwenda kwenye mkutano kwa ajili ya mahubiri, hakikisha kwamba una vitabu unavyohitaji na kwamba umetayarisha vizuri utoaji wako. Mkutano unapokwisha kwa sala, ujielekeze mara moja katika kazi ya kuhubiri. Hilo litakuwezesha, wewe na wale wanaotumika pamoja nawe, kufanya mengi zaidi iwezekanavyo katika wakati uliopangwa kwa ajili ya mahubiri.
3 Ikiwa umepewa mgawo wa kuongoza mkutano kwa ajili ya mahubiri, anza pa wakati. Fanya mkutano uwe mfupi; unaweza kuchukua dakika 10 ao zaidi, lakini usipite dakika 15. Mbele ya kuruhusu watu waende, hakikisha kwamba kila mhubiri anajua eneo ambamo atatumikia na ni nani atahubiri naye.
4 Unapohubiri: Munapomaliza mkutano kwa ajili ya mahubiri, musikawiekawie bila sababu, lakini mujielekeze mara moja kwenye eneo. Ikiwa unaona kwamba utarudi nyumbani mbele ya wakati, labda unaweza kutayarisha namna yako ya kurudi wewe mwenyewe ili wahubiri wengine katika kikundi wasilazimishwe kuondoka mbele ya wakati. Unapohubiri na kikundi, uwafikirie wengine ambao labda ni wenye kungojea umalize mazungumzo. Hilo linaweza kukuomba kutumia hekima ili kuachana na mtu mwenye ubishi ao kufanya mpango wa kurudilia yule anayependezwa.—Mt. 10:11.
5 Unaporudilia watu, unaweza kuona kwanza wale walio katika eneo moja mbele ya kwenda kwenye eneo lingine, ili kuepuka kufanya safari zisizo za lazima. Inawezekana kuzungumza kwa njia ya telefone na watu fulani kati ya wale ambao unapanga kurudilia ili kuhakikisha kwamba utawakuta nyumbani. (Met. 21:5) Ikiwa unaona kwamba utazungumza na mtu kwa muda mrefu, munaweza kufanya mipango na wengine katika kikundi ili wahubiri karibu karibu ao warudilie watu wengine.
6 Tunaishi wakati wa mavuno makubwa ya kiroho. (Mt. 9:37, 38) Hivi karibuni kazi itafikia mwisho. Kwa hiyo, nia yetu inapaswa kuwa kutumia vizuri wakati wetu katika kazi ya kuhubiri.