Siku ya Pekee ya Kuanzisha Mafunzo ya Biblia
1 Kuanzia mwezi wa 1, kila kutaniko litapanga Siku ya Posho moja ao Siku ya Yenga moja ya kila mwezi, labda juma la kwanza, ili kukazia mahubiri yao juu ya kuanzisha mafunzo ya Biblia. Siku hiyo itachaguliwa kulingana na hali yenye kufaa zaidi katika eneo lenu. Ikiwa watu hawakubali funzo la Biblia, wahubiri wanaweza hata kuwatolea kitabu Biblia Inafundisha ao magazeti ya sasa. Wazee na watumishi wa huduma wote watafanya mipango ili kushiriki kabisa katika kazi hiyo na kusaidia wahubiri waanzishe mafunzo ya Biblia.
2 Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko itaamua ni Siku ya Posho ao Siku ya Yenga gani itakayopangwa ili kuanzisha mafunzo ya Biblia. Mara kwa mara, halmashauri hiyo itawakumbusha wahubiri ili wajitayarishe na kujikaza sana kuanzisha mafunzo ya Biblia wanapohubiri nyumba kwa nyumba na wanaporudilia wale ambao walionyesha kupendezwa.
3 Jinsi ya Kujitayarisha: Tunaweza kupata mapendekezo kuhusu jinsi ya kuanzisha mafunzo ya Biblia katika nyongeza ya Huduma Yetu ya Ufalme ya mwezi wa 1, 2006, na kwenye ukurasa wa 10 wa kitabu Kutoa Sababu. Wengine wanaweza kupenda kutumia trakti, kama vile Je, Ungependa Kujua Kweli? Pia, Huduma Yetu ya Ufalme ya mwezi wa 8, 2007, kwenye ukurasa wa 3, inatoa mapendekezo kuhusu jinsi ya kuanzisha mafunzo ya Biblia tunaporudilia wale waliokubali magazeti. Wazee na watumishi wa huduma watapewa mgawo wa kuongoza mkutano kwa ajili ya utumishi wa shambani kwa dakika 10 ao zaidi, lakini usipite dakika 15; wakati wa mkutano huo watazungumzia ao kufanya onyesho la pendekezo moja ao mapendekezo mawili yenye kufaa kuhusu jinsi ya kuanzisha mafunzo ya Biblia.
4 Bila shaka, si kila mutu atakayekubali kujifunza Biblia ao kuendelea kujifunza kwa muda mrefu. Hatupaswi kuacha kwa sababu ya hilo, kwa kuwa Yehova ndiye anayevuta watu wenye mfano wa kondoo kwenye tengenezo lake. (Yoh. 6:44) Daraka letu si kupanda tu mbegu za kweli, lakini pia kulima na kumwagia maji mbegu ambazo zimetia mizizi, hilo linatia ndani kujifunza Biblia na watu wenye hali nzuri ya moyoni. Kwa kufanya hivyo, tunatimiza daraka la kuwa wafanyakazi pamoja na Mungu.—1 Kor. 3:9.