Kisanduku Cha Maulizo
◼ Ni nani anayepaswa kujaza sehemu hiyo?
Kwenye ukurasa wa mwisho wa vichapo vyetu, kunapatikana mara nyingi sehemu ambayo mutu anaweza kujaza ili kuomba vichapo ao kuomba Mashahidi wa Yehova wamutembelee. Pia, mutu anaweza kutumia kituo chetu cha Internet www.watchtower.org ili kuomba funzo la Biblia. Watu wengi wanajifunza kweli kwa kutumia njia hizo. Lakini, matatizo yametokea wahubiri wanapojazia watu wa jamaa zao ao watu wengine sehemu hiyo ili kuwasaidia wapate musaada wa kiroho, bila watu hao kujua.
Watu fulani wameonyesha kutokufurahi kwa kuwa ofisi ya tawi imewatumia vichapo ambavyo hawakuomba, wamefikiri kwamba tengenezo letu linawasumbua na kwamba limeandika majina zao ili kuwatumia vichapo kwa ukawaida bila wao kujua. Wahubiri ambao wameombwa kutembelea mutu fulani ambaye hakuomba yeye mwenyewe atembelewe wamejikuta katika hali ngumu mutu huyo alipokasirika. Kwa hiyo, ni watu wenye kupendezwa wao wenyewe ndio wanaopaswa kujaza sehemu zilizo kwenye ukurasa wa mwisho wa vichapo fulani ao kwenye Internet ili kuomba vichapo ao funzo, si wahubiri wanaopaswa kufikiri kwamba watu wa jamaa ao marafiki wao wanahitaji mambo hayo. Kwa kawaida ofisi ya tawi haishugulikie ombi kama hilo inapotambua kwamba ni muhubiri fulani aliyelijaza kwa ajili ya mutu mwingine.
Basi, unaweza kufanya nini ili kumusaidia mutu wa jamaa ao mutu unayefahamiana naye apate musaada wa kiroho? Ikiwa unapenda apate kichapo fulani, unaweza kumutumia zawadi ya kichapo hicho. Ikiwa mutu anapendezwa na anataka kutembelewa na Mashahidi wa Yehova lakini haujui namna ya kujulisha wazee wa kutaniko katika eneo ambamo anaishi, unapaswa kujaza fomu Tafadhali Fuatia Upendezi (S-43) na kuitolea mwandishi wa kutaniko lenu. Mwandishi wa kutaniko lenu ataichunguza na kuituma kwenye ofisi ya tawi. Lakini, ikiwa mutu mwenye kupendezwa ni mwenye kufungwa katika gereza, katika jengo la wale wanaotumia vibaya vileo ao dawa zinazolewesha, ao anapatikana katika hospitali, haupaswi kujulisha ofisi ya tawi kwa njia yoyote. Unaweza kumutia moyo mutu huyo azungumuze na ndugu wanaotembelea watu walio katika jengo hilo ao aandikie ofisi ya tawi yeye mwenyewe.