Je, Unaweza Kuhubiri Wakati wa Mangaribi?
1. Kulingana na kitabu kimoja, mutume Paulo alihubiri nyumba kwa nyumba wakati gani?
1 Kulingana na kitabu Daily Life in Bible Times, kwa kawaida mutume Paulo alihubiri nyumba kwa nyumba “kuanzia saa 10 ya mangaribi mupaka usiku sana.” Hatujue ikiwa ni hiyo iliyokuwa kabisa programu ya mutume Paulo, lakini tunajua kama Paulo alikusudia ‘kufanya mambo yote kwa ajili ya habari njema.’ (1 Kor. 9:19-23) Hilo linaweza kumaanisha kama mutume Paulo alipanga kuhubiri nyumba kwa nyumba wakati ambapo angewapata watu wengi zaidi.
2. Sababu gani mangaribi ni wakati unaofaa kwa ajili ya mahubiri?
2 Katika maeneo mengi, wahubiri wana desturi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba asubuhi katika juma. Katika eneo lenu, je, kuhubiri nyumba kwa nyumba asubuhi ndiyo wakati unaofaa zaidi? Painia mumoja anaeleza hivi kuhusu eneo lake: “Ni vigumu kuwapata watu nyumbani muchana. Lakini, watu wengi zaidi wanapatikana nyumbani mangaribi.” Mahubiri ya mangaribi yanaweza kututolea nafasi nzuri ya kuwapata watu, zaidi sana wanaume. Mara nyingi wakati huo wasikilizaji ni wenye kutulia zaidi na wako tayari kuzungumuza. Ikiwa ni jambo lenye kufaa, wazee watapanga mikutano kwa ajili ya mahubiri wakati wa mangaribi.
3. Namna gani tunaweza kutumia hekima tunapohubiri mangaribi?
3 Tumia Hekima: Tunapohubiri mangaribi, ni lazima kutumia hekima. Kwa mufano, ikiwa unatembelea mutu na unaona kama huo si wakati unaofaa, kama vile wakati wa kula, itakuwa vizuri kumuambia kama utarudia baadaye. Ikiwa giza limeingia, simama mahali ambapo musikilizaji atakuona vizuri, ujitambulishe kwake bila kukawia na umuambie kusudi lako. Tena, ni jambo la hekima kuhubiri mukiwa wawili-wawili ao vikundi-vikundi na kubaki katika njia yenye mwangaza wa kutosha, mahali ambapo hamutajitenga na watu. Musiwatembelee watu mangaribi sana kwa sababu hilo linaweza kuwasumbua wale wanaojitayarisha kulala. (2 Kor. 6:3) Ikiwa eneo fulani si salama giza linapoingia, muhubiri katika eneo hilo mangaribi mapema.—Met. 22:3.
4. Ni faida gani zinazotokana na kuhubiri wakati wa mangaribi?
4 Faida za Kuhubiri Mangaribi: Tunafurahia zaidi mahubiri wakati tunapata nafasi ya kuzungumuza na watu wengi. Kadiri tunavyowahubiria watu wengi zaidi, ndivyo tunavyopata nafasi nyingi zaidi za kuwasaidia wengine “waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Tim. 2:3, 4) Je, unaweza kubadili programu yako ili upate nafasi ya kuhubiri mangaribi?