1 Wakorintho
Ya Kwanza kwa Wakorintho
1 Paulo, aliyeitwa kuwa mtume wa Yesu Kristo kupitia mapenzi ya Mungu, na Sosthenesi ndugu yetu 2 kwa kutaniko la Mungu lililo Korintho, kwenu nyinyi ambao mmetakaswa katika muungano pamoja na Kristo Yesu, mlioitwa kuwa watakatifu, pamoja na wote ambao kila mahali wanaita jina la Bwana wetu, Yesu Kristo, Bwana wao na wetu:
3 Na mwe na fadhili isiyostahiliwa na amani kutoka kwa Mungu Baba yetu na Bwana Yesu Kristo.
4 Sikuzote mimi namshukuru Mungu kwa ajili yenu kwa kufikiria fadhili isiyostahiliwa ya Mungu mliyopewa katika Kristo Yesu; 5 kwamba katika kila jambo mmetajirishwa katika yeye, katika uwezo kamili wa kusema na katika ujuzi kamili, 6 kama vile ushahidi juu ya Kristo umefanywa kuwa imara miongoni mwenu, 7 ili kwamba msipungukiwe hata kidogo katika zawadi yoyote, huku mkiungoja kwa hamu ufunuo wa Bwana wetu Yesu Kristo. 8 Pia, yeye atawafanya nyinyi imara hadi mwisho, ili msilaumike katika siku ya Bwana wetu Yesu Kristo. 9 Mungu ni mwaminifu, aliyewaita kuingia katika ushirika pamoja na Mwana wake Yesu Kristo Bwana wetu.
10 Sasa nawahimiza nyinyi kwa bidii, akina ndugu, kupitia jina la Bwana wetu Yesu Kristo kwamba nyote mseme kwa upatano, na kwamba kusiwe na migawanyiko miongoni mwenu, bali kwamba mpate kuunganishwa kwa kufaa katika akili ileile na katika mstari uleule wa fikira. 11 Kwa maana, ndugu zangu, wale wa nyumba ya Kloe walinifunulia juu yenu kwamba mitengano imo miongoni mwenu. 12 Nimaanishalo ni hili, kwamba kila mmoja wenu husema: “Mimi ni wa Paulo,” “Lakini mimi ni wa Apolo,” “Lakini mimi ni wa Kefa,” “Lakini mimi ni wa Kristo.” 13 Kristo awa amegawanyika. Paulo hakutundikwa mtini kwa ajili yenu nyinyi, je, ndivyo? Au je, mlibatizwa katika jina la Paulo? 14 Mimi nashukuru sikubatiza hata mmoja wenu ila Krispo na Gayo, 15 ili yeyote asipate kusema kwamba nyinyi mlibatizwa katika jina langu. 16 Ndiyo, nilibatiza pia watu wa nyumbani mwa Stefanasi. Kwa habari ya wale wengine, sijui kama nilibatiza yeyote mwingine. 17 Kwa maana Kristo alinituma, si kwenda nikibatiza, bali kwenda nikitangaza habari njema, si kwa hekima ya usemi, ili mti wa mateso wa Kristo usifanywe kuwa usiofaa.
18 Kwa maana usemi juu ya mti wa mateso ni upumbavu kwa wale wanaoangamia, lakini kwetu sisi tunaookolewa ni nguvu ya Mungu. 19 Kwa maana imeandikwa: “Hakika nitafanya hekima ya watu wenye hekima iangamie, na akili ya watu wenye akili hakika nitaisukuma kando.” 20 Yuko wapi mtu mwenye hekima? Wapi mwandishi? Wapi mshindania-maneno wa mfumo huu wa mambo? Je, Mungu hakuifanya hekima ya ulimwengu iwe pumbavu? 21 Maana, kwa kuwa katika hekima ya Mungu, ulimwengu kupitia hekima yao haukupata kumjua Mungu, Mungu aliona vema kupitia upumbavu wa linalohubiriwa aokoe wale wanaoamini.
22 Kwa maana Wayahudi waomba ishara nyingi na pia Wagiriki watafuta hekima; 23 lakini sisi twahubiri Kristo aliyetundikwa mtini, kwa Wayahudi ni sababu ya kukwaza lakini kwa mataifa upumbavu; 24 hata hivyo, kwa wale ambao ndio wenye kuitwa, Wayahudi na pia Wagiriki, Kristo ni nguvu ya Mungu na hekima ya Mungu. 25 Kwa sababu kitu kipumbavu cha Mungu ni chenye hekima zaidi kuliko wanadamu, na kitu dhaifu cha Mungu ni chenye nguvu zaidi kuliko wanadamu.
26 Kwa maana mwatazama wito wake kwenu, akina ndugu, kwamba si wengi wenye hekima katika njia ya kimwili walioitwa, si wengi wenye nguvu, si wengi wa uzawa wa kikabaila; 27 bali Mungu alivichagua vitu vipumbavu vya ulimwengu, ili apate kuaibisha watu wenye hekima; na Mungu alivichagua vitu dhaifu vya ulimwengu, ili apate kuaibisha vitu vyenye nguvu; 28 na Mungu alivichagua vitu vinyonge vya ulimwengu na vitu vyenye kudharauliwa, vitu ambavyo havipo, ili apate kuvifanya viwe si kitu vitu ambavyo vipo, 29 ili mwili wowote usipate kujisifu machoni pa Mungu. 30 Lakini ni kwa sababu yake kwamba nyinyi mumo katika muungano pamoja na Kristo Yesu, ambaye amekuwa kwetu hekima kutoka kwa Mungu, pia uadilifu na utakaso na kuachiliwa kupitia fidia; 31 ili ipate kuwa kama vile imeandikwa: “Yeye ajisifuye, acheni ajisifu katika Yehova.”