2 Timotheo
2 Kwa hiyo, wewe mtoto wangu, fuliza kujipatia nguvu katika fadhili isiyostahiliwa kwa kuhusiana na Kristo Yesu, 2 na mambo uliyoyasikia kutoka kwangu kwa uthibitisho wa mashahidi wengi, mambo haya uyakabidhi watu waaminifu, ambao, nao, watakuwa na sifa za ustahili wa kutosha kufundisha wengine. 3 Ukiwa askari-jeshi mwema wa Kristo Yesu chukua sehemu yako katika kupatwa na uovu. 4 Hakuna mtu anayetumikia akiwa askari ajihusishaye mwenyewe katika shughuli za kibiashara za maisha, ili aweze kupata kibali cha yule aliyemwandika kuwa askari-jeshi. 5 Zaidi ya hayo, ikiwa yeyote ashindana hata katika michezo, havikwi taji isipokuwa awe ameshindana kulingana na kanuni. 6 Mkulima mwenye kufanya kazi kwa bidii lazima awe wa kwanza kushiriki sehemu ya matunda. 7 Fikiria daima yale ninayosema; kwa kweli Bwana atakupa wewe ufahamu katika mambo yote.
8 Kumbuka kwamba Yesu Kristo alifufuliwa kutoka kwa wafu na alikuwa wa mbegu ya Daudi, kulingana na habari njema nihubiriyo; 9 ambayo kwa kuhusiana nayo ninavumilia uovu kufikia hatua ya vifungo vya gereza kama mtenda-maovu. Hata hivyo, neno la Mungu halifungwi. 10 Kwa ajili ya hilo ninaendelea kuvumilia mambo yote kwa sababu ya wachaguliwa, ili wao pia waweze kupata wokovu ulio katika muungano na Kristo Yesu pamoja na utukufu udumuo milele. 11 Usemi huu ni wa uaminifu: Hakika ikiwa tulikufa pamoja, tutaishi pamoja pia; 12 tukiendelea kuvumilia, tutatawala pamoja pia tukiwa wafalme; tukikana, yeye pia atatukana sisi; 13 tukiwa wasio waaminifu, yeye adumu mwaminifu, kwa maana hawezi kujikana mwenyewe.
14 Fuliza kuwakumbusha mambo haya, ukiwaagiza mbele ya Mungu akiwa shahidi, wasipigane kuhusiana na maneno, ambalo ni jambo lisilofaa hata kidogo kwa sababu hupindua wale wanaosikiliza. 15 Fanya yote uwezayo kabisa ili ujionyeshe mwenyewe kuwa mwenye kukubaliwa na Mungu, mtenda-kazi asiye na lolote la kuaibikia, ukilitumia sawasawa neno la ile kweli. 16 Lakini epuka kabisa semi tupu ambazo huhalifu lililo takatifu; kwa maana wataendelea kwenye ukosefu wa kumwogopa Mungu ulio mwingi zaidi na zaidi, 17 na neno lao litasambaa kama kioza cha kidonda. Himenayo na Fileto ni kati ya hao. 18 Watu hawahawa wamekengeuka kutoka kwenye kweli, wakisema kwamba ufufuo tayari umetukia; nao wanapindua imani ya wengine. 19 Hata hivyo, msingi thabiti wa Mungu wakaa umesimama, ukiwa na muhuri huu: “Yehova ajua wale walio wake,” na: “Acha kila mtu anayeliita jina la Yehova akatae kabisa ukosefu wa uadilifu.”
20 Basi katika nyumba kubwa mna vyombo si vya dhahabu na fedha tu bali pia vya mbao na vya udongo, na baadhi yavyo ni kwa kusudi lenye kuheshimika lakini vingine ni kwa kusudi lenye kukosa heshima. 21 Kwa hiyo, ikiwa yeyote ajiepusha kabisa na hawa wa mwisho, atakuwa chombo kwa kusudi lenye kuheshimika, kilichotakaswa, chenye mafaa kwa mmiliki wacho, kilichotayarishwa kwa kila kazi njema. 22 Kwa hiyo, kimbia tamaa zenye kutukia ujanani, lakini fuatia uadilifu, imani, upendo, amani, pamoja na wale wamwitiao Bwana kutokana na moyo safi.
23 Zaidi, kataa maswali-maswali ya upumbavu na yasiyo na ujuzi, ukijua hayo hutokeza mapigano. 24 Lakini mtumwa wa Bwana hahitaji kupigana, bali ahitaji kuwa mwanana kuelekea wote, mwenye sifa za ustahili kufundisha, akifuliza kujizuia mwenyewe chini ya uovu, 25 akiagiza kwa upole wale wasio na mwelekeo ufaao; kwa kuwa huenda Mungu akawapa toba inayoongoza kwenye ujuzi sahihi juu ya kweli, 26 nao wapate kurudiwa na fahamu zao nzuri kutoka katika mtego wa Ibilisi, kwa kuwa wameshikwa naye wakiwa hai kwa ajili ya mapenzi ya huyo.