-
Kutoka 3:2-10Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
-
-
2 Kisha malaika wa Yehova akamtokea katika mwali wa moto katikati ya kichaka cha miiba.+ Musa alipoendelea kutazama, aliona kwamba kichaka hicho cha miiba kilikuwa kikiwaka moto, lakini hakikuteketea. 3 Basi Musa akasema: “Nitaenda kuchunguza jambo hili la ajabu, nione kwa nini kichaka kile cha miiba hakiteketei.” 4 Yehova alipoona akienda kukitazama, Mungu akamwita kutoka katika kichaka cha miiba: “Musa! Musa!” naye akajibu: “Mimi hapa.” 5 Akamwambia: “Usikaribie zaidi. Vua viatu vyako, kwa sababu mahali unaposimama ni ardhi takatifu.”
6 Akaendelea kusema: “Mimi ni Mungu wa baba yako, Mungu wa Abrahamu,+ Mungu wa Isaka,+ na Mungu wa Yakobo.”+ Ndipo Musa akauficha uso wake, kwa sababu aliogopa kumtazama Mungu wa kweli. 7 Kisha Yehova akasema: “Hakika nimeyaona mateso ya watu wangu walio Misri, nami nimesikia kilio chao kwa sababu ya wale wanaowalazimisha kufanya kazi; ninajua vema maumivu yao.+ 8 Nitashuka huko ili niwaokoe kutoka mikononi mwa Wamisri+ na kuwapandisha kutoka katika nchi hiyo na kuwapeleka katika nchi nzuri na kubwa, nchi inayotiririka maziwa na asali,+ eneo la Wakanaani, Wahiti, Waamori, Waperizi, Wahivi, na Wayebusi.+ 9 Sasa tazama! Kilio cha Waisraeli kimenifikia, nami nimeona pia jinsi Wamisri wanavyowakandamiza kwa ukatili.+ 10 Sasa njoo, nitakutuma kwa Farao, nawe utawatoa watu wangu Waisraeli kutoka Misri.”+
-