Wakati Ujao wa Dini kwa Kutegemea Wakati Wayo Uliopita
Sehemu ya 18: Karne ya 15 na kuendelea—Wakati “Wakristo” na “Wasio Wakristo” Walipokutana
“Dini imo katika moyo, si katika magoti”—D. W. Jerrold, mwanatamthilia Mwingereza wa karne ya 19
UTENDAJI wa kimisionari, ambao ni alama yenye kupambanua Ukristo wa mapema, ulipatana na amri ya Yesu ‘kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote’ na kuwa mashahidi wake “kwenye sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia.”—Mathayo 28:19, 20; Matendo 1:8, NW.
Katika karne ya 15, Jumuiya ya Wakristo ilianza programu ya duniani pote ya kuongoa “wasio Wakristo.” Jamii hizi za watu “wasio Wakristo” zilikuwa zimekuwa zikizoea dini ya aina gani kufikia wakati huo? Na je! kuongolewa ili kufuata “Ukristo” baada ya hapo kuligusa moyo wao au kulisababisha wanyenyekee kidesturi tu kwa kupiga magoti?
Katika Afrika kuna vikundi vya kikabila vinavyokadiriwa kuwa 700 kusini ya Sahara. Kwa asili, kila kimoja kilikuwa na dini yacho chenyewe ya kikabila, ingawa mifanano yavyo huonyesha vina asili moja. Katika Australia, makontinenti ya Amerika, na visiwa vya Pasifiki, kuna dini nyingi sana za kienyeji.
Walio wengi huamini katika mungu mmoja aliye mkubwa wa wote na, hata hivyo, kwa kuruhusu maoni ya kuwako miungu mingi, bado wao huachia nafasi miungu ya cheo kidogo zaidi—miungu ya jamaa, ya mbari, au ya kishirika. Uchunguzi mmoja uliofanywa juu ya orodha za dini ya Kiazteki huorodhesha majina ya miungu tofauti-tofauti 60 na yenye kuhusiana.
Katika Afrika na makontinenti ya Amerika, watu wenye dini zilizo “za kikale” zaidi huamini katika umbo fulani lililo na nguvu zipitazo zile za kiasili ambalo hujulikana kuwa Mfanya-Viini-Macho. Nyakati fulani yeye huelezwa kuwa muumba wa kosmosi (ulimwengu wote mzima), nyakati fulani kuwa mpangaji upya wa uumbaji, na sikuzote huonwa kuwa mdanganyifu mwenye ujanja na uchu, ingawa kwa lazima si mwenye nia ya kuumiza. Wahindi Wanavaho wa Amerika ya Kaskazini husema kwamba ndiye aliyeagiza kifo; kabila la Oglala Lakota hufundisha kwamba yeye ni malaika aliyeanguka aliyesababisha wanadamu wa kwanza waondoshwe katika paradiso kwa kuwaahidi maisha mazuri zaidi mahali penginepo. The Encyclopedia of Religion husema kwamba mara nyingi huyo Mfanya-Viini-Macho hutokea katika “hadithi za uumbaji,” akitimiza sehemu yake “upande ulio tofauti na mungu-muumba wa kiroho.”
Dini fulani za wenyeji hufundisha utatu, hiyo ikikumbusha hali zilizokuwako Babuloni na Misri. Kitabu The Eskimos husema kwamba Roho wa Hewa, Roho wa Bahari, na Roho wa Mwezi hufanyiza utatu ambao “ulidhibiti kabisa karibu kila jambo katika mazingira ya Kieskimo.”
Wanadamu—“Hawaharibiki Kiroho”
Ronald M. Berndt wa Chuo Kikuu cha Australia Magharibi atupasha habari kwamba Waaborijini Waustralia huamini kwamba mrudio-rudio wa maisha “huendelea baada ya kifo, kutoka kuwa ya kimwili hadi kuwa ya kiroho kabisa, baada ya muda wa kutosha yakirudia hali ya kimwili.” Hiyo yamaanisha kwamba “wanadamu hawaharibiki kiroho.”
Makabila fulani ya Kiafrika huamini kwamba baada ya kifo watu wa kawaida huwa mizuka, hali watu mashuhuri huwa roho za mababu waliokufa, wapasao kuheshimiwa na kuombwa kirasmi wakiwa viongozi wasioonekana wa jumuiya. Kulingana na Manus wa Melanesia, mzuka wa mwanamume au ule wa mtu wa ukoo wa karibu huendelea kusimamia jamaa yake.
Wahindi fulani Waamerika waliamini kwamba hesabu ya nafsi ni ndogo, ikitokeza uhitaji wa kwamba ‘wapewe tena umbo kwanza wakiwa katika binadamu halafu wawe roho ama mnyama.’ The Encyclopedia of Religion hueleza hivi: “Kifo cha mwanadamu kiliweka huru nafsi ili iwe mnyama au roho, na roho au mnyama awe mwanadamu, hiyo ikiunganisha wanadamu, wanyama, na roho katika kawaida ya utegemeano.”
Hivyo, wapeleleza-nchi wa mapema walishangaa kupata kwamba wazazi Waeskimo walikuwa wazembe kuwatia nidhamu watoto wao, hata wakiwaita mitajo ya cheo kama vile “mama” au “babu.” Mtungaji Ernest S. Burch, Jr., aeleza kwamba hii ni kwa sababu mtoto huyo alikuwa ameitwa jina la mtu wa ukoo mwenye kuonyeshwa na mtajo uliotumiwa, na kwa asili baba Mweskimo “aliogopa wazo la kumwadhibu nyanya yake, hata ikiwa sasa alikuwa amehama akaingia katika mwili wa mwana wake.”
“Maisha ya baadaye” yalionyeshwa na makabila fulani ya Wahindi wa Amerika Kaskazini kuwa uwanja wa mawindo ulio na furaha, ambapo wanadamu na wanyama pia walienda baada ya kufa. Waliungana upya na wapendwa wa ukoo wao lakini pia wakakabiliwa na waliokuwa adui zao hapo kwanza. Wahindi fulani walichuna ngozi ya kichwa cha adui zao pamoja na nywele baada ya kuwaua, yaonekana wakiamini kwamba hiyo ilizuia adui zao wasiingie katika ulimwengu wa roho.
Je! imani iliyoenea miongoni mwa dini za kienyeji juu ya namna fulani ya uhai baada ya kifo huthibitisha Jumuiya ya Wakristo kuwa sahihi katika kufundisha kwamba wanadamu wana nafsi isiyokufa? Hata kidogo. Katika Edeni ambamo dini ya kweli ilianzia, Mungu hakusema lolote juu ya uhai baada ya kifo; alitolea tazamio la uhai wa milele kwa utofautisho na kifo. Wazo la kwamba kifo ni lango la kwenda kwenye uhai bora lilitokezwa na Shetani na baadaye likafundishwa katika Babuloni.
Mahitaji ya Kibinadamu au Mapendezi ya Kimungu?
Mkazo katika dini za kienyeji huelekea kuwa juu ya usalama wa kibinafsi au halinjema ya kijumuiya. Hivyo, kuhusu dini ya Waaborijini Waustralia wa mapema, Ronald Berndt aandika hivi: “Ilionyesha mahangaikio mbalimbali ya watu katika maisha ya kila siku. Ilikaza fikira juu ya mahusiano ya kijamii, juu ya hatari za kuwako kwa kibinadamu, na juu ya mambo yenye mafaa ya kuokokea.”
Zilizoundwa kushughulikia mahitaji hayo hasa ya kibinadamu ni namna za ibada kama kuabudu vitu, imani na utumizi wa hirizi-hirizi, na ushamani, ulio katika jamii mbalimbali katika miungano mbalimbali na kadiri zenye kutofautiana.
Kuabudu vitu (animism) husema kwamba vitu vya kimwili kama mimea na mawe na hata nguvu za kiasili kama ngurumo za radi na matetemeko ya dunia vina uhai wenye fahamu na roho yenye kukaa ndani yavyo. Huenda pia vikatia ndani wazo la kwamba kuna roho zilizoacha miili (mizimu) ambazo huathiri walio hai kwa madhara ya muda tu au ya daima.
Imani na Utumizi wa Hirizi-hirizi (fetishism) hutokana na neno la Kireno ambalo nyakati fulani hutumiwa kueleza juu ya vitu vyenye kufikiriwa kuwa na nguvu zipitazo zile za kiasili ambavyo hutoa ulinzi au msaada wavyo vyenyewe. Kwa hiyo wapeleleza-nchi Wareno walitumia mtajo huo kuonyesha hirizi na makago ambayo walipata Waafrika wa Magharibi wakitumia katika dini yao. Imani na utumizi wa hirizi-hirizi yahusiana sana na ibada ya sanamu, nayo ni ya namna nyingi. Kwa kielelezo, Wahindi Waamerika fulani waliyahesabu manyoya kuwa na nguvu zipitazo zile za kiasili, wakiyaona kuwa vyombo vyenye matokeo katika “kurusha” sala au jumbe kuelekea mbinguni.
Ushamani, kutokana na neno la Kitunguso-Kimanchuria lenye kumaanisha “yeye ajuaye,” hutegemea shamani hasa, mtu ambaye hudhaniwa kuwa aweza kufanya maponyo na kuwasiliana na makao ya roho. Huyo mganga, mchawi, mlozi—neno lolote lile utakalo kutumia—hudai kuhifadhi afya au kurudisha nguvu za uzazi. Kama ilivyo katika makabila fulani ya msituni ya Amerika Kusini, huenda matibabu yakataka utoboe matundu katika midomo yako, katika ukuta wa pua, au katika ndewe za masikio, kwamba uupake rangi mwili wako, au kwamba uvae mapambo fulani. Au huenda ukaambiwa utumie vinywaji vya kuchochea utendaji wa mwili na kufisha mwili ganzi, kama vile tumbako na majani ya koka.
Dini za wenyeji haziwezi kupitisha maarifa sahihi ya Muumba kwa sababu hizo ni dhaifu katika mafundisho. Na kwa kukweza mahitaji ya kibinadamu juu ya mapendezi ya kimungu, hizo humnyang’anya yeye haki impasayo. Kwa hiyo Jumuiya ya Wakristo ilipokuwa ikianza umisionari wayo wa ki-siku-hizi, swali lilikuwa: Je! “Wakristo” wataweza kuvuta mioyo ya “wasio Wakristo” imkaribie Mungu zaidi?
Katika karne ya 15, Hispania na Ureno zikawa programu ya mpanuko wa kupeleleza-nchi na kufanyiza ukoloni. Serikali hizo kuu za Kikatoliki zilipokuwa zikigundua mabara mapya, kanisa lilianza jitihada ya kuwaongoa wenyeji, likiwapa masharti ya kukubali serikali yao mpya “ya Kikristo.” Amri za kipapa ziliipa Ureno haki za kimisionari katika Afrika na Esia. Halafu, baada ya kuvumbuliwa kwa Amerika, mpaka wa kuwazia tu ulichorwa na Papa Aleksanda 6 katikati ya Atlantiki, ukiipa Hispania haki za kwenda magharibi na Ureno kwenda mashariki.
Kwa sasa, Waprotestanti walikuwa wenye shughuli mno kuweka cheo chao kikiwa salama dhidi ya Ukatoliki hata wakawa hawawezi kuelekeza fikira juu ya kuongoa wengine, wala warekebishi wa Kiprotestanti hawakuwa wamewahimiza wafanye hivyo. Lutheri na Melankthoni yaonekana waliamini kwamba mwisho wa ulimwengu ulikuwa karibu sana hivi kwamba ilikuwa kuchelewa mno kuwafikia “wasio Wakristo.”
Hata hivyo, katika karne ya 17 harakati moja ya Kiprotestanti yenye kuitwa “Pietism” (Uchaji) ilianza kusitawi. Ikiwa ni chipuko la ule Mrekebisho, ilikazia kuwa na ujuzi wa kibinafsi kuhusu dini kuliko kufuata desturi rasmi tu na ikakazia kusoma Biblia na kujikabidhi kwenye dini. “Njozi [yayo] juu ya jamii ya kibinadamu yenye kuhitaji gospeli ya Kristo,” kama vile mwandikaji mmoja alivyoieleza, ilisaidia hatimaye kuhimiza Uprotestanti uanze safari katika “meli” ya utendaji wa kimisionari mwishoni mwa karne ya 18.
Kuanzia karibu sehemu moja kwa tano ya idadi ya wakaaji wa ulimwengu katika 1500, kiasi cha wenye kudai kuwa Wakristo kikawa kimeongezeka kuwa karibu robo moja kufikia 1800 na kuwa karibu moja kwa tatu kufikia 1900. Sasa theluthi moja ya ulimwengu ilikuwa “ya Kikristo”!
Je! Kweli Walifanya Wanafunzi Wakristo?
Dalili za ukweli wenye kupatikana katika dini za wenyeji husawazishwa na masalio mengi ya ubandia wa Kibabuloni, lakini mambo yako hivyo hivyo kuhusu Ukristo wenye kuasi imani. Kwa hiyo urithi huu wa dini kwa ujumla ulifanya iwe rahisi sana “wasio Wakristo” kuwa “Wakristo.” Kitabu The Mythology of All Races husema hivi: “Hakuna jimbo katika Amerika huonekana kuwa lilitumika kuhifadhi mifano mingi sana au ya kadiri kubwa ajabu kuhusu desturi na mifano ya Kikristo kama vile Mayan ilivyofanya.” Kuuheshimu mno msalaba na mifanano mingine katika desturi “kuliendeleza badiliko la dini bila upinzani mwingi.”
Waafrika—ambao kwa miaka kama 450 walitoroshwa kwa ukawaida na “Wakristo” na kuletwa kwenye Ulimwengu Mpya ili watumikie wakiwa watumwa—waliweza pia kubadili dini “bila upinzani mwingi.” Kwa kuwa “Wakristo” waliheshimu mno “watakatifu” wafu wa Ulaya, ni kitu gani kingefanya “Wakristo wafuata-mila” wasiabudu roho za mababu wafu wa Kiafrika? Hivyo, The Encyclopedia of Religion husema hivi: “Vuduu [uchawi] . . . , ambayo ni dini ya muunganisho uliopigwa viraka kutokana na dini za Afrika Magharibi, ulozi, dini ya Kikristo, na utamaduni . . . , imekuwa ndiyo dini halisi ya wengi wa watu wa Haiti, kutia na wale walio Wakatoliki wa jina.”
Concise Dictionary of the Christian World Mission hukiri kwamba uongofu wa Amerika ya Kilatini na Ufilipino ulikuwa wa kijuu-juu sana, ikiongezea kwamba “Ukristo wa majimbo haya leo umetatanishwa na ushirikina na ukosefu wa maarifa.” Kwa Waazteki, Wamaya, na Wainka, “‘uongofu’ ulimaanisha tu ongezeo la mungu mwingine wa ziada ndani ya hekalu lao la ujumla wa miungu.”
Kuhusu jamii za Waakani wa Ghana na Côte d’Ivoire, Michelle Gilbert wa Peabody Museum of Natural History asema hivi: “Dini ya kimapokeo huendelea kwa sababu watu walio wengi huhisi kwamba huo ndio mfumo wa imani ulio na matokeo mazuri zaidi, mmoja ambao huendelea kuupa ulimwengu maana.”
M. F. C. Bourdillon, Chuo Kikuu za Zimbabwe, hunena juu ya “mhamo-hamo wa dini” miongoni mwa washiriki wa dini ya Shona, akieleza hivi: “Namna zile mbalimbali za Ukristo pamoja na vidhehebu vyote mbalimbali vya kimapokeo huandaa mchanganyiko wa maombi ya kidini ambayo mtu aweza kuchagua kutokana nayo, ikitegemea mahitaji yake ya wakati ule.”
Lakini ikiwa “Wakristo wafuata-mila” hutambulika kwa tabia ya kufuata mambo kijuu-juu tu, kukosa maarifa, kuwa na ushirikina, na kuabudu miungu mingi, ikiwa wao huziona dini za kimapokeo kuwa zenye matokeo mazuri kuliko Ukristo, ikiwa wao huiona dini kuwa kitu cha kufuatwa wakati imfaapo mtu au kumletea faida, ikiwaruhusu wahame kutoka moja hadi nyingine kwa kadiri hali ziamuavyo, je! wewe ungesema kwamba Jumuiya ya Wakristo imefanya wanafunzi wa kweli Wakristo?
Ikiwa Si Wanafunzi, Wao Ni Nini?
Ni kweli kwamba wamisionari wa Jumuiya ya Wakristo wamejenga mamia ya shule za kuelimisha wasiojua kusoma. Wamejenga hospitali za kuponya wagonjwa. Na kwa kadiri fulani, wameendeleza staha kwa Biblia na kanuni zayo.
Lakini je! “wasio Wakristo” wamelishwa chakula kigumu cha Neno la Mungu au ni makombo tu ya Ukristo wa uasi-imani? Je! imani na mazoea ya “wasio Wakristo” yametupiliwa mbali au yamefungwa tu katika nguo za “Kikristo”? Kwa ufupi, je! wamisionari wa Jumuiya ya Wakristo wamevuta mioyo ya watu imwelekee Mungu au wamelazimisha tu magoti ya “wasio Wakristo” yapigwe mbele ya madhabahu za “Kikristo”?
Mtu aliyeongolewa kufuata Ukristo wa uasi-imani huongeza dhambi mpya za Ukristo wa kinafiki kwenye dhambi zake za zamani za kukosa maarifa, kwa njia hiyo akirudufisha mzigo wa hatia. Hivyo, maneno ya Yesu yafaa kwa Jumuiya ya Wakristo: “Nyinyi hupekua sana bahari na bara ili kufanya mwongofu mmoja, halafu mwamfanya awe tayari maradufu kwa ajili ya uharibifu kama mlivyo nyinyi wenyewe.”—Mathayo 23:15, Phillips.
Kwa wazi Jumuiya ya Wakristo imeshindwa kutimiza takwa la kufanya wanafunzi Wakristo. Je! imefanya vizuri zaidi katika kutimiza takwa la kukabiliana na badiliko la ulimwengu? Katika toleo letu linalokuja, makala “Jumuiya ya Wakristo Yamenyana na Badiliko la Ulimwengu” itajibu swali hilo.
[Picha katika ukurasa wa 22]
Wamisionari hawa halisi Wakristo katika Jamhuri ya Dominika huufikia moyo, si magoti tu