Nyumba ya Ibada Yachomwa Moto
KATIKA alasiri ya Jumapili, Oktoba 4, 1992, mtu mwenye kichaa aliingia katika Jumba la Ufalme dogo katika orofa ya pili katika Wŏnju, Korea, ambalo lilikuwa limesongamana kwa waabudu zaidi ya 90. Alipiga kelele mara kadhaa: “Mtoeni nje mke wangu.” Alipomsikia, mke wake aliondoka kwa haraka kupitia mlango wa dharura wa nyuma.
Mtu huyo akamwaga petroli kwenye zulia mbele ya mlango mkuu wa kutokea. Kisha, kujapokuwa sihi za wale waliokuwamo, akaiwasha moto. Petroli hiyo ikalipuka kihalisi, ikirusha miali ya moto na moshi mweusi darini, kuelekea upande wa jukwaa, na kisha ukarudi kupitia jumba zima. Kwa sekunde chache, wengi wa wasikilizaji walifunikwa kwa moshi. Miali ya moto na moshi ukawa unatokea kupitia kila dirisha.
Wengi walitoroka kupitia mlango wa nyuma au madirishani na kuingia katika ukingo mwembamba. Kutoka hapo walienda kwenye paa ya jengo lililoshikana na hilo na kisha wakashuka chini. Wengine waliruka tu kutoka orofa ya pili. Baada ya kuepa, mchomaji nyumba huyo akapiga mateke watu waliojeruhiwa waliokuwa wameruka kutoka juu.
Mwangalizi asafiriye, aliyekuwa akitoa hotuba ya pekee ya watu wote, akapaaza sauti: “Haraka, okoeni watoto.” Waokokaji wanaamini kwamba yeye na mke wake wangeokoka ikiwa hawangejaribu kusaidia wengine. Walikuwa miongoni mwa wale 15 waliokufa; kwa ujumla, wengine 26 walijeruhiwa. Mtu mwingine aliyekufa baadaye katika hospitali, alihatarisha uhai wake akisaidia wazee-wazee kutoka nje.
Wale waliokufa walikuwa katika sehemu ya mbele ya jumba. Mwangalizi huyo asafiriye pamoja na mke wake waliwezwa na moshi mzito na wakasongwa pumzi. Waliokufa walitoka katika familia tisa; watatu walikuwa watoto, wenye miaka 3, 4, na 14. Ilikuwa karibu kuwa muujiza kwamba wengi zaidi hawakufa wala kujeruhiwa, ukifikiria kwamba jumba lilijaa sana na kwamba miali ya moto ilifunga njia kuu ya kutorokea.
Upesi malori saba ya kuzima moto na wazima moto 30 wakafika hapo, lakini uharaka wa miali ya moto tayari ulikuwa umeua watu. Moto ulizimwa kwa muda usiopita saa nzima. Hata hivyo, kwa sababu ya ukubwa wa moto, ilikuwa vigumu sana kuwatambua waliokufa, kukichukua zaidi ya muda wa saa mbili.
Baadaye polisi wa Wonju walimkamata yule mtu aliyesababisha moto na kumshtaki kwa uuaji wa kimakusudi na uchomaji nyumba. Alipokuwa katika rumande, alijaribu kujiua lakini hakufanikiwa.
Alivumilia Matendo ya Kikatili
Wakati mke wa mchomaji-nyumba huyo alipopendezwa na mafundisho ya Biblia, ilikuja kuwa tabia ya mume huyo kumtisha. Katikati ya Septemba, karibu majuma mawili kabla ya mwangalizi asafiriye kuzuru Kundi la Wonju la Mashahidi wa Yehova, mchomaji-nyumba huyo alimpiga mke wake mpaka akazimia. Kisha baada ya kupata fahamu, akammwagilia mafuta ya rangi na kumwasha moto. Lakini mara tu moto ulipoanza, akapata fahamu zake na kuuzima haraka.
Karibu na adhuhuri ya Jumapili hiyo yenye msiba, mtu huyo aliamuru kwamba mke wake asiende kwenye Jumba la Ufalme. Hata ingawa mtu huyo alikuwa na ghadhabu nyingi sana, mke huyo hakutishika. Alihisi kwamba ni lazima atii Mungu kwa habari ya ibada badala ya mtu yeyote, kutia na mume wake. (Matendo 5:29; Waebrania 10:24, 25) Kwa hiyo akahudhuria mkutano.
Baada ya kuchomwa kwa Jumba la Ufalme, wakili wa mume huyo akajaribu kumsonga mwanamke huyo atie sahihi taarifa iliyosema kwamba mume wake alitenda kitendo hicho kio-vu kwa sababu yeye [mwanamke] alikataa kuacha dini yenye ushupavu na kwa sababu alikuwa ameshindwa kuwa mke mwema kwake. Hata hivyo, alikataa kutia sahihi taarifa hiyo. Alikataa kuridhiana juu ya kweli kwa kutoonyesha kwamba kwa njia fulani msiba huo mbaya ulitukia kwa sababu ya kujifunza kwake Biblia.
Mwisho-juma baada ya msiba huo, katika kusanyiko la Mashahidi wa Yehova, mwanamke huyo akafanya kupatana na uamuzi wake wa kubatizwa katika kuonyesha wakfu wake wa kumtumikia Yehova Mungu, Mwenye Enzi Kuu wa ulimwengu wote mzima.—Zaburi 83:18.
Msaada Kutoka Mbali na Karibu
Mara tu habari ya msiba huo ilipopokewa katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova katika Seoul, karibu kilometa 100 kutoka Wonju, msaada ulipelekwa kwa waliojeruhiwa na kwa familia zao, pamoja na kwa washiriki wa familia ya waliokufa. Si pesa tu zilizoandaliwa, bali pia wazee Wakristo kutoka ofisi ya tawi walitumwa kuchunguza ni msaada gani mwingine ungehitajiwa.
Mipango ilifanywa ya kundi kuhamia Jumba la Ufalme jingine katika Wonju, na maandalizi mengine yalitolewa kwa wenye uhitaji. Upesi utegemezo ulikuwa ukifika kutoka kwa washiriki wenzi wa Kikristo kutoka kotekote Korea. Kwa hakika, watu wengi walikuja kutoka majiji mengine na kutoa msaada muda mfupi baada ya msiba huo. Mfano mmoja ulikuwa ni upaji wa dola 1,200 kutoka kwa kundi lenye Mashahidi 75, na kundi jingine lenye watu 87 lilitoa upaji wa dola 2,200.
Wazee Wakristo katika kundi ambalo msiba huo ulitokea walifanya kadiri wawezavyo kusaidia wengine, lakini walikuwa miongoni mwa wale waliopata hasara kubwa zaidi. Watoto wawili wa mwangalizi msimamizi walikuwa miongoni mwa wale waliokufa, mzee mwingine Mkristo alipoteza mwana wake, na uso wa mzee mwingine tena ulichomeka vibaya sana. Yajapokuwa yale yote Wakristo hao walipoteza, wao na kundi zima lilibaki limetulia na kubaki imara katika imani.
Siku chache baada ya msiba huo, mwakilishi kutoka ofisi ya tawi katika Seoul alishughulikia mazishi hizo za watu wengi. Mashahidi wengi kutoka nchini kote walihudhuria, hivyo wakionyesha upendo wao na hangaiko lao kwa rafiki zao. Maelezo ya masikitiko yalipokewa hata kutoka kwenye ofisi nyingi za tawi za Mashahidi wa Yehova katika sehemu nyingi za dunia
Mkuu wa Sehemu ya Upelelezi katika idara ya polisi ya huko alihudhuria mazishi na alivutiwa sana na mwenendo wa Mashahidi. Aliona jinsi walivyonyamaza na kutulia na jinsi walivyowatendea kwa fadhili wengine waliopata hasara kwa moto huo. Mkurugenzi wa Shirika la Jamii na Viwanda alikuwa pia katika mazishi. Baadaye, alipoambiwa juu ya upaji wenye upendo uliokuwa umepokewa kutoka nchini kote, alisema kwamba bila imani jambo hilo halingewezekana. Makamu wa meya wa Wonju pia alionyesha kupendezwa kwa kweli. Alisema kwamba yeye binafsi alivutiwa sana na utulivu, upendo wa mmoja na mwenzake, na uwezo wa Mashahidi kupanga mambo.
Msiba huo ni dhihirisho tu la ziada kwamba tunaishi ‘katika siku za mwisho zenye hatari.’ (2 Timotheo 3:1) Inatazamiwa kwamba mambo kama hayo ya kuogofya yatatendeka. Lakini Mashahidi wa Yehova katika Wonju hawajavunjika moyo. Wameazimia kuendelea na ibada yao ya Mungu wa pekee wa kweli, Yehova, na kuendelea kufanya mapenzi yake.—Imeripotiwa na mleta habari za Amkeni! katika Korea.
[Picha katika ukurasa wa 26]
Upande wa kulia: Hilo Jumba la Ufalme, na (chini) jukwaa lililochomeka ambapo wengi walikufa
Chini: Suh, Sun-ok, aliyepoteza watoto wawili katika moto, akifarijiwa na Shahidi mwenzi, na Shim, Hyo-shin, mzee Mkristo ambaye watoto wake wawili walijeruhiwa