Krismasi-Je! Hugharimu Zaidi ya Ufikirivyo?
“MAMA, baba—je! kweli kuna Baba Krismasi?” Hiyo ni pindi ambayo wazazi wengi huogopa. Macho yake yakiwa na mchanganyiko wa kukata tamaa na udhiko, Jimmy mwenye miaka saba asihi apate uhakikishio kwamba mtu huyo wa fantasia aliyeleta zawadi hizo zote nzuri ajabu yuko kikweli—na kwamba wazazi wake hawakumdanganya.
Jambo lililotukia ni kwamba, mvulana mdogo wa nyumba jirani ndiye mkosaji aliyefunua kweli isiyopendeza na kuwaweka wazazi hao katika kikao kisichopendeza. Labda kumbukumbu lako la utotoni latia ndani tukio kama hilo.
Sherehe za sikukuu za leo zatia mengi zaidi ya kuwa sherehe za kidini tu. Yaonekana kwamba Krismasi imekuja kukubaliwa katika mahali pengi pasipotazamiwa. Wabuddha-Wajapani, waabudu-asili Waafrika, Wayahudi-Waamerika, na Waislamu-Wasingapore vilevile wamemkubali yule mtu mnene, mwenye suti nyekundu na zawadi nyingi. Kiongozi mmoja wa kidini aliuliza hivi, “Je! Krismasi si sikukuu ya ulimwenguni pote isherehekewayo na wote?”1
Kulingana na maoni ya watu wengi, Krismasi imevua kibandiko chayo cha Magharibi cha “Kikristo” na kuwa pindi ya kusisimua ya furaha ya kisherehe kwa wote. Watoto wamo katika kiini cha sherehe hiyo. Watu fulani wangethubutu kusema kwamba maisha ya mtoto si kamili bila furaha ya kipekee ya sikukuu hiyo. Yaonekana kwamba itaendelea kuwapo. Mtalaa wa shule huitegemea. Televisheni huitukuza. Maduka makubwa na maduka ya bidhaa za aina-aina huitangaza kwa madoido mengi. Wazazi hutumia wakati na pesa nyingi kwa ajili ya Krismasi. Lakini zaidi ya yale matokeo ya kawaida ya kuwa na deni kubwa, je, kuna gharama kubwa zaidi ambayo familia yako huenda ikalipa?
Ngano ya Baba Krismasi —Kuvunja Hali ya Kutumainiwa?
“Mimi siamini kuna Mungu,” John mwenye miaka saba alimwambia mama yake. Makala ya World Herald yaeleza sababu: “Yaonekana kwamba mapema zaidi siku hiyo, John alikuwa amegundua kwamba Baba Krismasi hakuwa halisi. Labda Mungu hakuwa halisi vilevile, yeye akamwambia mama yake.” Akikumbuka hali yake ya mapema ya kukata tamaa, John mwenye miaka 25 alisema: “Wazazi wawaambiapo watoto kwamba Baba Krismasi ni halisi, nafikiri labda hilo ni kuvunja hali ya kutumainiwa.”2
Ni nini lapaswa kufanywa juu ya hali hiyo inayohitaji uangalifu? Wataalamu wa watoto hawakubaliani. Mmoja wao aliwatia moyo wazazi wawaambie watoto wao kweli kufikia umri wa miaka sita au saba, wakionya kwamba “huenda hasa ikadhuru akili zao ikiwa wazazi wasisitiza kuendeleza ngano hiyo.”5
Katika kitabu Why Kids Lie—How Parents Can Encourage Truthfulness, Dakt. Paul Ekman asema: “Hakuna shaka kwamba ninyi mkiwa wazazi mna uvutano mkubwa sana juu ya watoto wenu kwa habari ya mitazamo, itikadi, na matendo ya kijamii kama vile kusema uwongo au kudanganya.”6 Ekman aendelea kusema: “Huenda mahusiano yasiwe yaleyale uwongo ukiisha kuvunja tumaini. Ni vigumu kurekebisha hali ya kupoteza tumaini; nyakati nyingine hakurekebiki.”7 Kwa hiyo mbona uendeleze udanganyo kwa habari ya kutoa zawadi wakati wa sikukuu?
Mtafiti mmoja wa watoto alisisitiza hivi: “Nafikiri watoto hutaabishwa zaidi na wazazi wanaowaambia uwongo na kuwadanganya kuliko vile wataabishwavyo wanapogundua kwamba Baba Krismasi si halisi.”8 Dakt. Judith A. Boss, profesa wa falsafa, asema: “Nia ya watu wazima . . . ni kuwaarifu vibaya watoto juu ya jinsi Baba Krismasi alivyo. . . . Kwa kuwaambia watoto Baba Krismasi ni binadamu halisi, sisi hatuvuti uangalifu wa mawazo ya watoto. Twawaambia uwongo tu.”9
Ikiwa wewe ni mzazi, unakabiliwa na kazi kubwa sana—kulea watoto wenye kupenda, wenye furaha katika ulimwengu ambamo wajifunza kuanzia umri wa mapema kwamba watu si wa kutumainiwa. “Usiseme na watu usiowajua.” “Huwezi kuamini yote ambayo tangazo la televisheni lasema.” “Waambie mama hayuko nyumbani.” Mtoto hujifunzaje ni nani wa kutumaini? Kitabu How to Help Your Child Grow Up chasema: “Ni lazima watoto wadogo wajifunze mapema juu ya umaana na uzuri wa kufuatia haki, wa ujasiri, wa kushughulika na wengine kwa staha; na nyumbani ndimo hayo hupata mwanzo wayo.”12
Bila shaka, hakuna kitu kama familia kamilifu. Hata hivyo, mtungaji-vitabu Dolores Curran alinuia kutambua tabia ya familia zenye nguvu. Yeye aliomba wastadi 551 wa familia wa nyanja mbalimbali wachague sifa za maana zaidi. Magunduzi yake, yaliyo katika kitabu Traits of a Healthy Family, yazungumzia sifa kuu 15 zilizochaguliwa na wastadi hao. Sifa namba nne ilikuwa “hisia ya kutumaini.” “Katika familia bora,” yeye asema, “tumaini huonwa kuwa jambo la thamani kuwa nalo, lililositawishwa na kukuzwa kwa uangalifu huku watoto na wazazi pia wakiendelea pamoja kupitia hatua mbalimbali za maisha ya familia.”13
Wazazi ni wenye hekima kuuliza, ‘Je! kuendelezwa kwa ngano ya Baba Krismasi kwastahili gharama ya mtoto wangu kukosa kuwa na uhakika nami na kukosa kunitumaini?’ Huenda kusiwe na njia yoyote ya kupatana tena. Je! Krismasi ina gharama nyinginezo zisizo dhahiri?
Kutoa Kupita Kiasi?
“Anzia utotoni kumpa mtoto kila kitu akitakacho. Kwa njia hiyo atakua hali akiamini kwamba ulimwengu wamwia maisha,” lasema gazeti 12 Rules for Raising Delinquent Children.14 Kwa kweli kukazia vitu vya kimwili kupita kiasi kwaweza kudhuru.
Mwandikaji na mzazi Maureen Orth auliza, “Twaweza kukaziaje kanuni na tabia tuishipo katika ulimwengu huu wetu wenye kufuatia mali, ambamo uhitaji na pupa vyatukuzwa sana, bila hadhari mara nyingi?” Katika makala, “Zawadi ya Kutokutoa,” yeye aomboleza: “Kitoto kitendacho kama Maliki huamini kwamba zawadi ni kitu cha kupokea kila siku—kama vile kupokea barua.”15 Je! huo ndio ujumbe halisi wa Krismasi?
Vipi juu ya familia ambazo hazijimudu kifedha kuweza kununua zawadi nyingi zisemwazo kuwa za lazima kwa ajili ya Krismasi? Vijana hao huhisije wasikiapo kwamba Baba Krismasi huletea zawadi watoto wazuri peke yao? Vipi juu ya vijana katika nyumba zilizogawanyika ambao hujua kwa uchungu juu ya mgawanyiko katika familia zao wakati wa sikukuu?
“Mara nyingi sana jambo kuu la kikusanyiko cha sikukuu ni kufungua zawadi,” lasema The New York Times. “Mkazo huo huwapa watoto ujumbe kwamba kusudi la kikusanyiko cha familia ni kupata zawadi na hufanyiza njia ya wao kuvunjika moyo.”
Upendo ni kichocheo kingine chenye kuridhisha hata zaidi cha kufanya mema. Glenn Austin, mwandikaji wa Love and Power: Parent and Child, asema: “Katika familia yenye upatano ambamo mtoto hupenda na pia kumstahi mzazi, huenda mtoto huyo akatenda katika njia inayokubaliwa ili kumpendeza mzazi huyo.”17 Mashahidi wa Yehova hutia bidii ili kufanyiza hali hiyo ya upendo yenye uchangamfu nyumbani mwao. Zaidi ya hiyo, watoto wa Mashahidi wa Yehova hulelewa ili kupata kujua na kumpenda Mungu wanayemtumikia, Yehova. Hiyo ni kani yenye nguvu kama nini maishani mwao kwa ajili ya kufanya mema! Wao hawahitaji mtu fulani wa kingano ili kufanya matendo mema.
Mashahidi wa Yehova huwathamini watoto wao kuwa zawadi kutoka kwa Mungu. (Zaburi 127:3) Kwa hiyo, badala ya kungojea tarehe fulani ili kutoa zawadi, wazazi hao waweza kutoa zawadi muda wote wa mwaka. Nyakati hizo ni vigumu kujua ni nani anayesisimuliwa zaidi—kijana aliyeshtushwa au mzazi wake mwenye furaha. Mtoto hujua mahali ilipotoka zawadi. Isitoshe, wazazi Mashahidi watiwa moyo kutoa wakati wao uwe zawadi mara kwa mara. Kwani wakati msichana mdogo ajisikiapo kuwa hana furaha au mpweke, chumba kizima kilichojaa wanasesere chaweza kulinganaje na muda mfupi unaotumiwa huku msichana huyo akipakatwa na mamaye akisikiliza mama yake akimhadithia juu ya wakati alipokuwa mchanga? Je! mvulana mchanga atafundishwa jinsi ya kuwa mwanamume kwa kabati lililojaa vifaa vya besiboli au ni kwa mazungumzo marefu, yenye kupendeza pamoja na babaye huku wakienda matembezi pamoja?
Ukaribu huo uliositawishwa waweza kuokoa uhai. Watafiti wa watoto wamepata kwamba lile pengo hakika la kizazi lianzapo kwa kijana, yeye huvutwa kwa nguvu zaidi na marika. Utovu wa nidhamu wa ujanani na mtazamo unaodhoofika kuelekea watu wazima hufungamana pamoja. “Lakini wale wadumishao maoni yafaayo juu ya baba zao na watu wazima kwa ujumla hawakujiunga na marika wengineo katika utovu wa nidhamu.”18
Pindi kwa pindi Mashahidi wa Yehova wamechambuliwa kwa kutoshiriki furaha ya sikukuu pamoja na familia zao. Huenda ikaonekana kwamba watoto wa Mashahidi wa Yehova hunyimwa furaha hiyo ya pekee. Lakini wazazi na watoto hao wanyoofu wana sababu zifaazo za Kibiblia za kutoshiriki. (Tafadhali ona kurasa 11-14.) Na wachanga hao wanasitawisha uwezo wa kiadili wenye nguvu utakaohimili uzito wa mkazo wa marika unaovunjilia mbali uwezo wa vijana wengineo. Adili yachukuliwa mbali na mawimbi ya uovu yanayozidi kuongezeka. Ngono zisizo za adili, dawa za kulevya, ujeuri, kileo, madhehebu, watenda watoto vibaya—hatari nyingi sana zatisha vijana wasio na kinga.
Mzazi aweza kukingaje kijana asipatwe na hatari hizo za daima? Kuanzia utotoni watoto Mashahidi hupokea mazoezi yenye upatano ya kuegemea juu ya sheria za kiadili zenye nguvu za Biblia. Wazazi wenye kupenda huwasaidia kuelewa maoni ya Mungu si juu ya sikukuu tu bali pia juu ya mambo yote ya maisha. Utii kwa Mungu wao hutokana na upendo na staha kwake, hata ikimaanisha wao wawe tofauti. Wazia jinsi hilo lazima liwatayarishe kwa ajili ya hali ya kuwa vijana wenye mafanikio! Ikiwa mtoto mchanga aweza kuketi ndani ya darasa lililojaa marika wanaofanya yale yanayoonekana kuwa yenye kufurahisha na kuchukua msimamo kwa yale aaminiyo kuwa yenye kufaa, yeye ana uwezo mwingi kama nini wa kukinza kishawishi cha baadaye cha mambo zaidi yanayoonekana kuwa yenye kufurahisha—madawa ya kulevya, ngono kabla ya ndoa, na vishawishi vingine vyenye kudhuru! Watoto wa Mashahidi wa Yehova waweza kusitawisha uwezo wa kiadili ambao watoto wengine wengi huenda wakakosa.19
“Watoto walio wengi ambao nimechunguza hawana imani,” aonelea Dakt. Robert Coles, mtafiti wa Harvard. “Wamepoteza kila kitu isipokuwa kujishughulikia wenyewe, na hilo huendelezwa kila siku kwa namna wanavyolelewa.”
Tabibu mmoja wa watoto aeleza juu ya familia tofauti: “Wanataka watoto wanaowajali wengine na wanaojitoa kwa kiasi. . . . Wao huishi maisha sahili zaidi . . . , lakini wana jambo jingine. Kwa kukosa njia nyingineyo ya kulieleza, ningeliita uradhi.”22
Dolores Curran ataja kuthamini kutoa utumishi kwa wengine kuwa msingi wa kupata furaha. “Kwa familia fulani katika taifa letu [United States]—kwa kweli nyingi zazo, ningeweza kusema—ufanisi na kufuatia maisha mema ndilo kusudi la msingi.” Lakini “familia zinazodhani kwamba washiriki waweza na watakuwa wakiwajali wengine huja kuwa zile familia bora zinazothamini kutoa utumishi kwa wengine. . . . Watoto kutoka familia hizo wanapokua, wao huelekea kujali na kuwa watu wenye kuchukua madaraka kikweli kwa sababu ya maono yao ya familia.”23 Curran aona miongoni mwa wazazi wenye mafanikio “kurudia kwenye kanuni ya kutafuta furaha katika watu na katika kutoa badala ya kununua, kuchukua, na kutumia.”24
Ikisemwa kwa njia nyingine na mstadi mwenye kutokeza juu ya kutoa, “kuna furaha nyingi zaidi katika kutoa kuliko katika kupokea.” (Matendo 20:35, New World Translation) Familia za Mashahidi ni ithibati ionekanayo juu ya taarifa hiyo ya Kristo Yesu. Kama yeye maisha yao yategemea huduma ya Kikristo. Huenda watu fulani wakahisi kwamba vijana Mashahidi wanatumiwa vibaya na kulazimishwa kuandamana na wazazi wao mlango kwa mlango. Kinyume kabisa cha hilo, wao wanafundishwa kwa kielelezo cha kimzazi jinsi ya kupenda binadamu mwenzao kwa kutoa habari njema juu ya Ufalme wa Mungu kwa majirani wao bila kujizuia.—Mathayo 24:14.
‘Je! Hakutawazuia Watoto?’
Lakini je, malezi magumu ya kidini hayamzuii mtoto mchanga? Je! si afadhali kuacha maamuzi ya kidini yafanywe na kila mmoja afikiapo kuwa mtu mzima? Huenda hiyo ikawa sheria namba 3 kati ya (Sheria 12 za Kulea Watoto Watundu) 12 Rules for Raising Delinquent Children: “Usimpe kamwe mazoezi ya kiroho. Ngojea hadi afikiapo umri wa miaka 21 halafu umwache ‘ajiamulie.’”25
Hata hivyo, kulingana na Dakt. Coles, hisi ya msingi ya kiadili ya mtoto huanza kukua mapema kadiri ya umri wa miaka mitatu. “Katika mtoto kuna hisi ya kiadili inayokua. Mimi nafikiri ni ya kupewa na Mungu, kwamba kuna kutamani maadili.”26 Huu ndio wakati wa maana wa kukazia kanuni za adili za kweli. Mathalani, huo ni wakati wa kufundisha kwa njia ya kielelezo kanuni ya ukweli kinyume cha kudanganya. Biblia hukazia umaana wa kuzoeza wakati wa miaka ya uchanga: “Mlee mtoto katika njia impasayo, naye hataiacha, hata atakapokuwa mzee.”—Mithali 22:6.
Curran aonelea hivi: “Watoto leo hawawezi kutazamiwa kuwa wenye adili bila kusaidiwa. . . . Watu waliotoa maoni kwa uchunguzi wangu wadokeza kwamba kadiri familia ilivyo bora zaidi ndivyo hisi yao ya mema na mabaya inavyokuwa imesitawi zaidi.”27
Mfanyakazi mmoja wa jamii akiitikia uchunguzi wa Curran alionelea hivi: “Kuna kiini cha nguvu kisichoepukwa ambacho imani ya kidini hupa familia.” Kwa familia yenye kiini kimoja cha kidini, Curran asema, “imani katika Mungu huwa na sehemu ya kimsingi katika maisha ya familia ya kila siku. Kiini cha kidini huimarisha mfumo wa utegemeo wa familia. Wazazi huhisi daraka zito la kupitisha imani hiyo, lakini wao hufanya hivyo katika njia zifaazo zenye maana.”29
Saidia Watoto Wako Wampende Mungu
Onyesha watoto zawadi za Mungu zinazowaletea shangwe nyingi. Lala nyasini na uchunguze nao ua dogo lililobuniwa kwa uangalifu sana. Tazama mdudu-bibiarusi anayetokea katika msitu huu wa nyasi na kupanda kwenye ncha ya unyasi, na kuinua mabawa yake yenye vidoadoa vyekundu na vyeusi, na kuruka mbali hewani. Acha wahisi ajabu yenye kusisimua wakati kipepeo anapotua ghafula juu ya mkono ili kuinua na kushusha mabawa yake ya manjano yenye uangavu ili apumzike kidogo na kufyonza miale ya jua yenye joto. Geuka ulale chali ili uone mawingu meupe laini yakielea juu, na utazame yanapobadilika kutoka umbo la meli kuwa la farasi na la makao ya wafalme angani. Wakati huo wote waeleze watoto wako kwamba ni Mungu Muumba wetu anayetuletea zawadi hizo zenye kufurahisha.
Na zawadi nyinginezo nyingi, kama vile mwanapaka ambaye kuchezacheza kwake na jani hutuacha tukiangua kicheko au mtoto wa mbwa mwenye manyoya mengi “anayetushambulia,” kichwa kikitikiswa huku na huku, akinguruma kwa ukali huku akivuta mkono wa vazi letu, lakini mkia wenye urafiki ukitikiswa bila kuacha wakati huo wote. Au kucheza katika mawimbi meupe ya bahari, kupanda milima, au kutazama juu usiku kwa mshangao katika anga lililojaa nyota zinazomeremeta na kuangaza kule juu kabisa. Kujua kwamba zawadi hizo na nyinginezo zisizohesabika zatoka kwa Yule aliyetupa uhai wetu, kuweza kumshukuru kwa ajili ya zawadi hizo, kuhisi wenye shukrani kwa ajili ya kumjua yeye—yote hayo hutuletea shangwe na huonyesha upendo wenye kina na uthamini kwake.
Na hatimaye katika mazingira ya familia, kumbatio na busu nyingi kutoka kwa baba na mama, zinazosaidia watoto wahisi usalama wenye kuchangamsha na hali ya kushukuru kila siku. Wasaidie wawe na imani katika Yehova wakikataa udanganyo ulio mkubwa hata zaidi kuliko ule wa Baba Krismasi mwenye suti nyekundu, yaani, kwamba zawadi hizo zote nzuri kutoka kwa Mungu zilitukia tu, zilijitokeza kwa nasibu tu—uwongo unaofundishwa bila uthibitisho wa kisayansi, bila kuungwa mkono na njia ya kisayansi, na kudumishwa kwa mambo yaliyoshikiliwa sana yanayorudiwa-rudiwa ili kuyajaza katika akili za wachanga.a
Shiriki na watoto wako katika sala za kila mara kwa Mpaji mkuu zaidi ya wote—kwenye milo, mnaposoma Neno lake, na mwishoni mwa siku. Lea mtoto mwenye shukrani, na hisi hiyo ya uthamini itaboresha kila ono apatalo maishani. Yeye mwenyewe atakua na kuwa mtoaji mwenye furaha katika kumwiga Mungu wa kweli na wazazi apendao. Halafu furaha itakuja, si kwa siku za kalenda zilizotangulia kuwekwa, bali kwa pindi za hiari za shangwe nyingi katika kuishi. “Wenye furaha ni watu ambao Mungu wao ni Yehova!”—Zaburi 144:15, NW.
[Maelezo ya Chini]
a Ona kitabu Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation? kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Picha katika ukurasa wa 7]
Mojapo zawadi bora zaidi ya zote unazoweza kuwapa watoto wako ni wakati