Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g93 11/22 kur. 15-17
  • Naweza Kushughulikaje na Wazazi Wenye Hisia Zinazobadilika-Badilika?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Naweza Kushughulikaje na Wazazi Wenye Hisia Zinazobadilika-Badilika?
  • Amkeni!—1993
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ishara Zenye Kuonya
  • ‘Je! Kuna Jambo Baya?’
  • Tenda kwa Busara!
  • Kwa Nini Wazazi Wangu Huwa na Hali ya Moyo Ibadilikayo Upesi?
    Amkeni!—1993
  • Nifanye Nini Wazazi Wangu Wanapogombana?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
  • Nifanye Nini Wazazi Wangu Wakipigana?
    Amkeni!—1990
  • Ninawezaje Kuwafahamu Wazazi Wangu Vizuri Zaidi?
    Amkeni!—2009
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1993
g93 11/22 kur. 15-17

Vijana Huuliza...

Naweza Kushughulikaje na Wazazi Wenye Hisia Zinazobadilika-Badilika?

“TATIZO langu,” asema Claudia, “ni kwamba mama yangu huwa mwenye wasiwasi na kasirani-kasirani.a Siku moja aliniuliza mazoezi yangu ya piano yalikuwaje. Nilisema kwamba yalikuwa sawa tu na nikaingia ili nijizoeze piano. Mama aliingia ndani, akasema kwa hasira kwamba nilikuwa mfidhuli, halafu akaondoka kwa kasirani. Nilikasirika na nikapiga piano kwa mkono na kukimbia kwenye chumba changu. Halafu mama akaja na kunikemea kwa sababu ya kupiga piano kwa mkono.”

Wazazi waweza kuwa wenye hisia nyepesi kwelikweli wanapokuwa wenye hali mbaya ya moyo. Nyakati nyingine huenda ukahisi kwamba ni lazima uwe mwenye tahadhari sana unapokuwa karibu nao, ukingojea kwa wasiwasi wakati ule mwingine ambapo utachambuliwa, upigiwe kelele, au hata kulaumiwa. Hata hivyo, ile makala “Kwa Nini Wazazi Wangu Huwa na Hali ya Moyo Ibadilikayo Upesi?” katika toleo la Amkeni! lililotangulia, ilionyesha kwamba ni jambo la kawaida kabisa kwa wazazi kuwa na hisia zinazobadilika-badilika mara kwa mara. Mara nyingi visababishi ni mikazo, uchovu, afya mbaya, na misongo ya maisha.b Kujua hivyo kwaweza kukusaidia kuwahurumia wazazi wako. (Linganisha Mithali 19:11.) Lakini hilo halibadili uhakika wa kwamba nyakati nyingine huenda wakawa wagumu kushughulika nao. Waweza kufanya nini ili kuboresha mambo?

Ishara Zenye Kuonya

Mithali 24:3 husema: “Nyumba hujengwa kwa hekima, na kwa ufahamu huthibitika.” Kupatana na kanuni hiyo, jambo moja unaloweza kufanya ni kujaribu kutambua ni wakati gani wazazi wamo katika hali mbaya ya moyo. Mtunga-zaburi alisema hivi juu ya hali yake mwenyewe ya mshuko wa moyo: “Mchana kutwa nimekwenda nikihuzunika.” (Zaburi 38:6) Mtu aliye macho kwa hakika angeweza kuona kwamba jambo fulani lilimsumbua! Kwa njia iyo hiyo, mara nyingi mzazi atatoa ishara zilizo wazi kwamba yuko katika hali mbaya ya moyo.

Hivyo waandikaji wachanga wa kitabu The Kids’ Book About Parents walikusanya orodha ya ishara za kawaida zenye kuonya ambazo vijana waweza kuwa macho kuona. Miongoni mwa mambo yaliyoonyeshwa ni wazazi ‘kula sana, kukosa kuzungumza, kwenda kulala mapema, kutowasalimu wanapokuja nyumbani kutoka kazini, kutolea kila mtu ukali, kupuuza maswali yako,’ na ‘kuzubaa huku wakitazama televisheni.’ Katika familia nyinginezo, wazazi nyakati nyingine hujulikana kuwa watakuwa na hisia nyepesi—kama wakati ambapo yabidi madeni yalipwe. Hata iweje, kwa kuwa macho, huenda ukaweza kutambua ishara za kuonya za wazazi wako mwenyewe.

‘Je! Kuna Jambo Baya?’

Basi, ufanye nini uhisipo kwamba mzazi wako ana hisia nzito? Je! umtoroke? Labda sivyo. Mithali 15:20 husema: “Mwana mwenye hekima humfurahisha babaye.” Hiyo haimaanishi kwamba ni lazima ujitwike matatizo ya watu wazima ya wazazi wako. Kwa vyovyote, kila mzazi lazima ‘abebe mzigo wake mwenyewe.’ (Wagalatia 6:5) Lakini angalau unaweza kuonyesha kupendezwa nao. Kwa kielelezo, unaweza kuuliza hivi kwa busara: ‘Je! kuna jambo baya?’ (Linganisha Nehemia 2:1, 2.) Huenda kusiwe mengi ya kufanya ili kubadili hali, lakini wao waweza kuthamini kupendezwa kwako kwa upendo kwa ajili ya hali njema yao.

Hivi ndivyo kijana aitwaye Kama apendekezavyo juu ya kushughulikia mambo wakati mzazi mwenye hisia zinazobadilika-badilika anapofika nyumbani: “Baada ya wewe kumsalimu, ingia chumbani mwako kwa muda, hadi watulie. Halafu utoke na kuuliza kuna nini kibaya na siku yao ilikuwaje . . . Ona kama wanakutaka ufanye lolote.” Nyakati nyingine, kuonyesha tu mzazi uangalifu au shauku nyororo ihitajiwayo kwaweza kuondoa hali mbaya ya moyo.

Katika kitabu chake My Parents Are Driving Me Crazy, Dakt. Joyce Vedral asema jinsi msichana mmoja tineja aitwaye Deena alivyoitikia hali ya moyo ya mamake yenye hasira. Deena asema: “Nilipotoka [chumbani mwangu] na kuona mkunjo wa uso wake, nilimkamata na kumkumbatia kwa uchangamfu kabla ya yeye kufanya lolote kunikomesha. Halafu nikampa busu kubwa na kusema, ‘Nakupenda, mama.’ Wapaswa kuona jinsi hisia yake ilivyobadilika—mara hiyo.” Dakt. Vedral amalizia hivi: “Utatuzi unaofaa kabisa kwa mzazi mwenye hali mbaya ya moyo ni shauku nyororo. . . . Shauku nyororo yaweza kutokeza hisia yenye furaha kwelikweli.” Biblia husema hivi: “Upendo hujenga.”—1 Wakorintho 8:1.

Hata hivyo, nyakati nyingine wazazi wako huonekana kuwa wamekasirika juu yako binafsi. Ikiwa huna uhakika sababu ni nini, jaribu kuzungumza na wazazi wako ili waweze kutoa malalamiko yao yoyote. (Linganisha Mithali 20:5.) Kwa kielelezo, msichana mchanga aitwaye Ruth, aliona kwamba yeye na babake walikuwa “wakizidi kukosana” na kwamba babake alikuwa mwenye kuchambua maksi zake kupita kiasi. Baada ya mazungumzo ya familia juu ya makala ya “Vijana Huuliza . . . ” Ruth aliuliza ni nini kilichokuwa kikimsumbua babake. “Tuligundua kwamba baba alikuwa akijaribu kupata mafanikio kupitia watoto wake, kwa kuwa alikuwa amelazimika kuacha shule. Yeye alitutaka tuwe na maksi bora kabisa.” Ruth alipopata maksi chache ya zile zilizotazamiwa, babake angekasirika. Matokeo ya mzungumzo yao? “Yalinisaidia nione mambo jinsi yeye alivyoyaona,” yeye asema. Bila shaka, babake pia ilimbidi afanye marekebisho fulani katika kufikiri kwake. Ruth aripoti hivi: “Mambo yaanza kuboreka.”

Kwa kuwa na mazungumzo kama hayo, huenda ukang’amua kwamba wazazi wako wana sababu zifaazo za kukasirika juu yako. Huenda likawa jambo dogo kama vile wewe kusahau kufanya mgawo fulani wa kazi nyumbani. Mithali 10:5 yakumbusha hivi: “Akusanyaye wakati wa hari ni mwana mwenye hekima; bali asinziaye wakati wa mavuno ni mwana mwenye kuaibisha.” Labda bidii zaidi upande wako yaweza kufanya mengi katika kuboresha hisia za wazazi wako.

Tenda kwa Busara!

Hata hivyo, nyakati nyingine mzazi hana mwelekeo wa kuzungumza kwa uhuru, na jitihada zote za kumtia moyo azungumze zakabiliwa na kasirani au ukinzani. Sasa iweje? Biblia hutuambia jinsi Daudi, akiwa kijana, alivyokabili hali kama hiyo isiyo nzuri. Akiwa kijana, Daudi alifanya kazi katika ua wa Mfalme Sauli akiwa mwanamuziki. Hata hivyo, Sauli alikuwa na hisia zisizotabirika na kasirani kuu. Kwani, katika pindi moja Sauli alijaribu kumpigilia Daudi ukutani kwa mkuki! Hata hivyo, ona kwamba Biblia husema hivi kwenye 1 Samweli 18:14 juu ya tabia ya Daudi: “Naye Daudi akatenda kwa busara ka-tika njia zake zote; naye BWANA [Yehova, NW] alikuwa pamoja naye.”

Ni wazazi wachache walio na kasirani kama ya Mfalme Sauli. Lakini, huenda ukahitaji kuwa mwenye busara unaposhughulika nao. Mathalani, Sam mchanga asema: “Baba yangu si Mkristo, naye huwa na kasirani wee! Anapokasirikia mtu, yeye huanza kupiga kelele kwelikweli. Yakubidi uwe mwangalifu kwelikweli juu ya yale usemayo na kutenda. Ni lazima ujaribu usimkasirishe.” Biblia husema hivi juu ya hilo: “Mwenye busara huyaona mabaya na kujificha.”—Mithali 22:3.

Si kwamba uwaepuke wazazi wako. Jaribu kuwa mchangamfu na mwenye urafiki kadiri uwezavyo. Ukimsumbua mzazi mwenye kununa kwa maswali yasiyo ya maana au kwa matatizo madogo yanayoweza kuzungumziwa wakati mwingine, huenda ikawa wamchokoza mzazi wako. (Linganisha Mithali 15:23; 25:11.) Kwa kweli, wanapokuwa wenye mkazo na wachovu, huenda hata wakahisi kama yule mwanamume mwadilifu Ayubu alipouliza hivi: “Je! mtanichukiza nafsi yangu hata lini”? (Ayubu 19:2) Basi wewe ni mwenye hekima kuepuka mazoea yoyote yenye kusumbua ambayo wajua hukasirisha wazazi wako—kama vile kutafuna peremende (ya gamu) huku ukitoa sauti zisizopendeza, au kupinda vidole vyako kwa njia inayotokeza kelele. Vivyo hivyo, hakungekuwa kuwafikiria wengine kupiga muziki wako kwa sauti kubwa au kufungua televisheni kwa sauti ya juu kabisa.

Njia nyingine ya kutenda kwa busara ni kuchukua hatua ya kwanza. Je! sikuzote mama huwa na hali mbaya ya moyo anapokuja nyumbani kutoka kazini? Ufikapo nyumbani kwanza, mbona usiandike meza, utoe takataka nje, au uoshe vyombo? Msalimu mama yako kwa shauku nyororo. Mambo hayo yaweza kumfanya atamani wakati wa kuja nyumbani. Msichana mmoja tineja aitwaye Julie huchukua hatua hiyo ya kwanza. Yeye asema: “Mama yangu huendesha basi la shule, na mara nyingi yeye huja nyumbani akiwa amekasirika. Kwa hiyo yanibidi nisimkaribie. Mimi humwepuka hadi anapotulia. Halafu nitamtunzia watoto au nimfanyie usafi au jambo fulani.”

Hata ujaribu jinsi gani kuliepuka, kwa hakika hitilafiano fulani hutukia wazazi wanapokuwa wepesi kukasirika au kukasirishwa. Hilo likitukia, kutumia kanuni za Biblia kwaweza kukusaidia kuepuka kufanya hali isiyofaa iwe mbaya zaidi. Kwa kielelezo, Mithali 15:1, yasema: “Jawabu la upole hugeuza hasira; bali neno liumizalo huchochea ghadhabu.” Mwongozo zaidi umetolewa kwenye Mithali 17:27, isemayo: “Azuiaye maneno yake ni mwenye maarifa; na mwenye roho ya utulivu ana busara.” Kumbuka pia kwamba ingawa wazazi wako wana hisia zao mbaya, yaelekea kwamba kuna nyakati pia ambapo wao hupendeza, ni wacheshi, na ni wenye furaha kuwa nawe. Thamini nyakati hizo, na uzitumie kuwa fursa ya kusitawisha uhusiano mwema na wazazi wako. Itafanya zile nyakati ngumu zisiwe ngumu sana.

[Maelezo ya Chini]

a Majina fulani yamebadilishwa.

b Makala hii yashughulika na mabadiliko-badiliko ya hisia yaliyo ya kawaida ambayo watu walio wengi hupatwa nayo. Wazazi wanaopatwa na usumbufu wa kihisiamoyo kwa sababu ya mshuko mkuu wa moyo, kileo au uzoefu wa madawa, au maradhi mengine makubwa ya kimwili na kihisiamoyo huenda wakahitaji msaada wa kitiba.

[Picha katika ukurasa wa 17]

Wazazi wafanyao kazi huthamini watoto wao wanapowasaidia na kazi za nyumbaniy

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki