Krismasi—Chanzo Chayo
NA MLETA-HABARI WA AMKENI! KATIKA ITALIA
SIKU tatu tu kabla ya Krismasi 1993, Papa John Paul 2 alikubali kwamba sherehe ya Krismasi haina msingi katika Biblia. Kuhusu tarehe Desemba 25, papa alikiri hivi: “Siku hiyo katika nyakati za kale za kipagani, siku ya kuzaliwa kwa ‘Jua Lisiloweza Kushindwa’ ilisheherekewa ili kupatana na mwanzo wa jua wa wakati wa baridi.” Basi Krismasi ilianzaje? Papa aliendelea hivi: “Lilionekana kuwa jambo la kiakili na la kawaida kwa Wakristo kubadilisha sherehe hiyo iwe sherehe ya Jua pekee na la kweli, Yesu Kristo.”
“Kwa maneno mengine,” akaandika mwandishi wa habari Nello Ajello katika La Repubblica, “mtu fulani alitangaza kwamba Yesu alizaliwa katika tarehe iliyowaziwa, iliyobuniwa na ya uwongo.” Ubuni huu ulitukia lini? Ripoti ya habari kutoka Vatican ilitaarifu hivi: “Sherehe ya Krismasi ilionekana kwa mara ya kwanza katika 354 [W.K.].”
Namna gani Epiphany ya Januari 6, ambayo huadhimisha kuja kwa Magi kumtembelea Yesu aliyezaliwa karibuni? “Uthibitisho mwingi hutufanya tuamini kwamba kuchaguliwa kwa Januari 6, kama kule kwa Desemba 25 kwa sikukuu ya Kiroma ya kusherehekea kuzaliwa kwa Yesu, pia kulichochewa na sherehe za kipagani,” ikaendelea hiyo ripoti ya habari. “Kwa hakika, katika Alexandria, kwenye usiku wa kati ya Januari 5 na 6, wapagani walizoea kusherehekea kuzaliwa kwa mungu Aeon (mungu wa wakati na umilele). . . . Ingeonekana kwamba Kanisa lilitaka kufanya sherehe hiyo iwe ya Kikristo.”
Yesu hakuruhusu kamwe wafuasi wake wachanganye ibada ya kweli na mapokeo ya kipagani. Badala ya hivyo, yeye aliwaambia wafunze “yote niliyowaagiza.” (Mathayo 28:19, 20, NW) Isitoshe, alipokabiliwa na viongozi wa kidini wa wakati wake, Yesu aliwauliza hivi: “Kwa nini mnavunja amri ya Mungu kwa sababu ya mapokeo yenu?” (Mathayo 15:3, New International Version) Swali lilo hilo laweza kuulizwa waitwao eti Wakristo ambao huendeleza mapokeo ya kipagani leo.