Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g97 5/22 kur. 11-13
  • Miungu Mingi Sana, Hadi Nikapata Yule wa Kweli

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Miungu Mingi Sana, Hadi Nikapata Yule wa Kweli
  • Amkeni!—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Dhamiri Yangu Yaanza Kutenda
  • Mashahidi Watutembelea
  • Kutumikia Mahali Penye Uhitaji Mkubwa
  • Sababu kwa Nini Watu wa Namna Zote Wanakuwa Mashahidi wa Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Pigano Langu Gumu na Lililo Refu la Kutafuta Dini ya Kweli
    Amkeni!—1995
  • Niliacha Kupiga Watu Barabarani Nikawa Mhudumu Mkristo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Kumkaribia Mungu Kulinisaidia Niwezane na Hali
    Amkeni!—1993
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1997
g97 5/22 kur. 11-13

Miungu Mingi Sana, Hadi Nikapata Yule wa Kweli

NILIZALIWA katika Croydon, Uingereza, katika mwaka wa 1921, msichana mkubwa zaidi kati ya wasichana watatu na wavulana wawili. Nilipokuwa na umri wa miaka mitatu, baadhi yetu watoto tulipatwa na dondakoo. Nililazwa hospitalini. Ndugu yangu Johnnie alikufa, na kwa sababu hakuwa amebatizwa, Kanisa la Kiangalikana halikuruhusu ibada ya mazishi. Baba yangu alikasirishwa na jambo hilo na kumwomba kasisi asali wakati walipokuwa wakiteremsha jeneza la Johnnie ardhini. Yeye alikataa.

Mama yangu alisema kwamba jambo hilo lilimfanya baba aachane na dini kabisa. Alihofu sana kwamba jambo baya lingenipata au kupata dada zangu hivi kwamba bila baba kujua, yeye alitupeleka kanisani na kuhakikisha tumebatizwa. Baba yangu akawa mshiriki mtendaji wa kikundi cha Ukomunisti na kututia moyo tusome habari iliyohusiana na nadharia ya uyakinifu pembuzi, kutia ndani vitabu vilivyoandikwa na Huxley, Lenin, na Marx. Mungu hakutajwa kamwe nyumbani isipokuwa wakati baba alipokuwa akisema hakuna Mungu.

Katika 1931, nilipokuwa na umri wa miaka kumi hivi, nyakati fulani niliteremka barabarani kuwaona wazazi wa baba yangu. Mara nyingi babu alichambuliwa na watu wengine, lakini alikuwa na mng’ao katika macho yake mazuri ya buluu na sikuzote alikuwa mwenye furaha. Kwa kawaida yeye alinipa peremende na kitu fulani cha kusoma nilipokuwa nikirudi nyumbani. Nilikula peremende hiyo na kuitupa habari aliyonipa nisome. Wakati huo sikufahamu kwa nini wengine walikuwa wakisema kwa njia isiyofaa kumhusu.

Nilipokuwa katika umri wa utineja, nilijiunga na Young Communist League na baada ya muda nikawa katibu. Nilitoa hotuba kwenye ukumbi wa mji na kufanya kazi ya barabarani nikiwa na gazeti la habari Challenge, nikimpa yeyote ambaye angesikiliza. Wakati huo, kikundi cha Wafashisti kilichoitwa Blackshirts kilikuwa chenye utendaji na kilipinga kwa jeuri Ukomunisti. Nakumbuka nilipokuwa nimesimama kando ya barabara nikitoa Challenge, washiriki wa Blackshirts walikuwa wakinijia na kunizungumzia, wakiniita Sunshine, jina la utani walilokuwa wamenipa. Washiriki wakubwa zaidi wa kikundi cha Ukomunisti nilichokuwa nikishirikiana nacho walikuja kujua kwamba Wafashisti walikuwa wakipanga kunipiga kwa konzi zilizovishwa vyuma, kwa hiyo nikaanza kupewa mtu wa kunisindikiza.

Katika pindi moja, tuligundua kwamba Wafashisti walikuwa wamepanga kuandamana kupitia sehemu iliyoitwa East End of London (ambapo wakati huo palikaliwa na Wayahudi hasa). Tuliambiwa tuwakabili na tubebe mifuko iliyojaa gololi, ambazo tungezitupa chini ya makanyagio ya farasi wa polisi waliposhambulia ili kuachanisha vikundi vilivyokuwa vikipingana. Wengi walikamatwa siku hiyo, lakini kwa uzuri, sikuwa miongoni mwao, kwa kuwa niliamua kutoenda.

Dhamiri Yangu Yaanza Kutenda

Katika pindi nyingine, niliambiwa niseme jambo fulani hadharani ambalo nilijua halikuwa kweli. Nilikataa na nikaulizwa, “Kuna tofauti gani mradi tunawasilisha maoni yetu?” Ni wakati huu katika maisha yangu ambapo dhamiri yangu ilianza kunisumbua, nami nikaanza kujiuliza kuhusu mambo kadhaa.

Wakati mmoja katika miaka yangu ya mapema ya utineja, mama yangu alinitia moyo nihudhurie ibada ya kanisa, ili kuona tu kile kilichokuwa kikitukia kanisani. Nakumbuka nikiambiwa niende kwenye altare niungame dhambi zangu. Nilipokuwa hapo, niliona kwamba tarizi kwenye kitambaa cha altare ilikuwa na pete tatu zilizofunganishwa. Niliuliza ziliwakilisha nini nikaambiwa ziliwakilisha “Utatu Mtakatifu—Mungu Baba, Mungu Mwana, na Mungu Roho Mtakatifu.” Niliwaza, ‘Hili ni jambo la ajabu. Wanaamini katika miungu mitatu, lakini baba yangu husema hakuna hata mmoja!’ Nilipouliza maswali zaidi, nilielezwa kwamba yai lina sehemu tatu lakini kwa hakika ni yai moja tu. Wala hilo halikuniridhisha. Kisha nikaambiwa kwamba nilikuwa nikiuliza maswali mengi sana. Nilienda nyumbani na kumweleza mama yangu kwamba sikutaka tena kwenda kanisani, na sikuenda!

Kufikia wakati Vita ya Ulimwengu ya Pili ilipofyatuka, sikuwa tena mtendaji katika Young Communist League. Niliolewa na Mkanada ambaye alikuwa jeshini, na tukapata mwana. Makao yetu ya kwanza katika London yalilipuliwa kwa bomu. Kombora aina V-1 lilianguka mbele ya nyumba yetu wakati mimi na mwana wangu tulipokuwa nyumbani. Tulipoteza vitu vyetu vyote vya kimwili. Tulizikwa katika rundo la vifusi lakini kwa uzuri tuliponyoka tukiwa hai. Wakati huo mume wangu alikuwa Normandy, Ufaransa.

Katika wakati huo, nakumbuka nikizungumza na wanawake wawili vijana na kuwauliza, “Ikiwa kuna Mungu, kwa nini anaruhusu mateseko haya yote?” Walisema jambo fulani kuhusu Shetani kuwa mungu wa ulimwengu huu. “Ah,” nikawaza, “mungu mwingine ambaye sijui kitu kumhusu!” Kisha, mwanamume mmoja kijana akaja. Nilimuuliza maswali mengi, naye akasema alikuwa akitafuta kondoo, wala si mbuzi. Kwa kuwa sikujua vizuri kielezi cha Yesu, nilimuuliza ikiwa alikuwa mhudumu au mkulima. Miaka michache ilipita, na Vita ya Ulimwengu ya Pili ikaisha. Mume wangu akarudi nyumbani akiwa ameona asilimia 95 ya watu katika Saskatoon Light Infantry ambapo alikuwa akitumika wakiwa wameuawa. Tuliishi katika makao mengine katika Croydon.

Mashahidi Watutembelea

Jumapili moja, Mashahidi wa Yehova wawili walikuja na kupiga kengele ya mlango. Mume wangu alifungua mlango na kuzungumza nao kwa muda mrefu. Alikuwa amekasirikia dini zote kwa sababu ya unafiki aliouona wakati wa vita. Uhakika wa kwamba Mashahidi hao walikuwa wamechukua msimamo wa kutokuwamo ulimpendeza. Aliniambia kwamba alikuwa amewaalika kwa ajili ya mazungumzo ya Biblia. Nilihangaika sana nikamuuliza baba yangu nifanye nini. Alisema kwamba sikupaswa kujihusisha na kwamba ikiwa mume wangu angeendelea na dini hii yenye kichaa, ingekuwa vema nichukue hatua za talaka.

Niliamua kuketi katika mojawapo mazungumzo hayo ili nione yalihusu nini. Sote tuliketi kuzunguka meza, na Shahidi huyo akasema: “Siku moja hivi karibuni mtaweza kumzungushia mikono yenu simba kama vile mwezavyo kufanya na mbwa.” “Ah, wana kichaa,” nikafikiri. Sikuweza kukaza fikira kwa jambo jinginelo lote lililosemwa jioni hiyo. Baadaye, nilimwambia mume wangu kwamba sikutaka warudi tena. Tulitoa machozi mengi, na tukazungumzia kutalikiana.

Muda mfupi baada ya hilo, Shahidi mwingine akatutembelea. Tulipata kujua baadaye kwamba alikuwa mwangalizi wa mzunguko ambaye alikuwa akizuru kutaniko la mahali hapo na alikuwa amesikia habari zetu. Namkumbuka vizuri sana. Alikuwa na macho ya buluu na mtazamo wa fadhili na wa subira sana. Alinikumbusha babu yangu.” Nilitoa orodha ya maswali 32 niliyokuwa nimeyaandika. “Tutayazungumzia moja baada ya jingine,” akasema, na tukaendelea kufanya hivyo. Alinisaidia kujua kwamba ili kufahamu kikamili kinachosemwa na Biblia, nilihitaji kuisoma na kujifunza hiyo. Alidokeza kwamba mtu fulani atuzuru na kujifunza Biblia nasi kwa ukawaida. Nikakubali.

Nilianza kumfahamu Muumba wetu, Yehova Mungu hatua kwa hatua, na nikaguswa kiasi cha kutoa machozi. Nakumbuka nikienda kwenye chumba cha kulala na kumwomba Yehova anisamehe tafadhali na kunisaidia kufahamu Biblia na makusudi yake. Mume wangu, mwana wangu, nami tulibatizwa katika 1951. Baba yangu alihuzunishwa sana kusikia hilo na akasema kwamba ni afadhali anione nikiwa mfu kuliko nikiwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova.

Kutumikia Mahali Penye Uhitaji Mkubwa

Mume wangu aliamua kurudi Kanada, na katika 1952 tulihamia Vancouver, British Columbia. Baba yangu alikataa kutuaga, sikumwona tena wala kumsikia tena. Baada ya kuishi Vancouver kwa miaka kadhaa, kulikuwa na mwito wa kuenda mahali penye uhitaji mkubwa zaidi, hasa kwenye maeneo kama vile Quebec, ambapo Waziri Mkuu Duplessis alikuwa na mtazamo kama wa Hitler kuelekea Mashahidi wa Yehova.

Katika 1958 tulipakia vitu vyetu vyote vya kimwili katika gari letu na kuendesha hadi kwenye mkusanyiko wa kimataifa New York. Kutoka huko tuliendesha hadi Montreal, Quebec, na kupewa mgawo kwenye kutaniko la Kifaransa katika Ville de Jacques-Cartier. Tulijionea mengi tulipokuwa tukimtumikia Yehova katika Quebec. Wakati mmoja, gari letu lilipinduliwa, tulilengwa kwa mawe, na mwanamke mmoja akatufungulia mpira wa maji. Hapo ni mahali palipoitwa Magog.

Wakati mwingine, mwandamani wangu nami tulikuwa tukipita kanisa moja watu walipokuwa tu wakitoka. Mtu fulani akatutambua na kupaaza sauti: “Témoins de Jéhovah!” (“Mashahidi wa Yehova!”) Kufukuzwa kukaanza, kukiongozwa na kasisi, lakini tukashinda umati huo kwa mbio. Tulikamatwa mara nyingi. Hata hivyo, nilikuwa na furaha ya kusaidia watu wachache kujifunza kuhusu Yehova, wengi wao bado wanatumikia wakiwa watendaji.

Katika miaka ya mapema ya 1960, mwajiri wa mume wangu alimhamisha hadi Los Angeles, na tukatumikia katika kutaniko moja huko kwa zaidi ya miaka 30. Ilikuwa furaha kwetu kama nini kuzungumza juu ya kweli na watu waliohamia Los Angeles kutoka sehemu zote za dunia! Nilipata pendeleo la kujifunza na watu kutoka Lebanoni, Misri, China, Japani, Ufaransa, na Italia, kutaja wachache tu. Nakumbuka nilikutana na mwanamke mmoja kijana ambaye hakuweza kusema Kiingereza hata kidogo—kwa uzuri, mume wake aliweza. Kwa hiyo mume wangu nami tulijifunza nao pamoja. Hatimaye nikawa nikijifunza naye peke yake. Nilitumia kitabu Let God Be True katika Kiingereza, naye alikuwa akichunguza maandiko katika Biblia yake ya Kichina na kujibu maswali kwa Kichina. Kisha, ningesema jibu kwa Kiingereza, naye angerudia kwa Kiingereza. Hatimaye, akaja kusema Kiingereza kwa ufasaha, ingawa kwa lafudhi ya watu wa kutoka Uingereza. Nafurahi kusema kwamba yeye na mume wake sasa ni watumishi wa Yehova waliojiweka wakfu.

Hivi majuzi tulihamia Tucson, Arizona, na nimepata pendeleo la ziada la kuona washiriki wote wa familia yangu wakimtumikia Yehova kwa uaminifu, kutia ndani vitukuu wetu, ambao wanafundishwa kuhusu Muumba wetu Mtukufu, Yehova.

Kwa kutaja tu, nilifurahi kujua kutoka kwa akina ndugu katika Croydon kwamba babu yangu mwenye macho ya buluu yenye kung’aa alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova.—Kama ilivyosimuliwa na Cassie Bright.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki