Habari Nyingi Kupita Kiasi
KARNE ya 20 imepatwa na habari nyingi isiyo na kifani. Iwe ni kwa chapa, redio au televisheni, Internet, au kwa njia nyingine yoyote, ulimwengu umejaa habari kabisa. David Shenk, aandika hivi katika kitabu chake Data Smog—Surviving the Information Glut: “Habari nyingi kupita kiasi imetokea kuwa tisho halisi. . . . Sasa twakabili tazamio la kujazwa habari kupita kiasi.”
Chukua kielelezo kimoja cha gazeti la habari lenye kujulikana sana. Inasemekana kwamba toleo la kawaida la siku moja ya juma la gazeti The New York Times lina habari nyingi kuliko habari ambazo mtu wa kawaida angaliweza kupata katika muda wote wa maisha yake huko nyuma katika karne ya 17 katika Uingereza. Lakini kuongezea gazeti la habari la kila siku, magazeti na vitabu vya namna zote kuhusu habari nyingi tofauti-tofauti huongezea habari nyingi zinazotokezwa. Kila mwaka makumi ya maelfu ya vitabu huchapishwa. Na kwa vile habari za kisayansi huongezeka maradufu kila baada ya miaka sita, haishangazi kuwa ulimwenguni pote, majarida ya kiufundi peke yake ni zaidi ya 100,000. Na Internet ina maktaba nyingi sana za habari kwa watumiaji wa kompyuta.
Namna gani magazeti? Majarida ya kibiashara, magazeti ya wanawake, magazeti ya matineja, magazeti ya michezo na vitumbuizo—kwa kweli, magazeti kuhusu karibu kila namna ya habari na mapendezi ya kibinadamu—yameujaza ulimwengu, yote yakidai uangalifu wetu. Namna gani fungu la mtangazaji wa kibiashara—“mpiga-tarumbeta bure,” kama alivyofafanuliwa vema? Katika kitabu chake Information Anxiety, mtungaji Richard S. Wurman aonelea: “Mashirika ya utangazaji wa kibiashara yametangaza vita dhidi ya hisi zetu kwa matangazo mengi ya kibiashara ambayo yanadai kuangaliwa, kusikiwa, kunuswa na kuguswa.” Wanasisitiza kuwa wahitaji bidhaa ya karibuni zaidi, bidhaa iliyofanyizwa upya karibuni zaidi, ili uwe na vitu kama majirani wako.
Mwanasaikolojia aliye pia mtafiti wa kijamii Mwaustralia Dakt. Hugh MacKay alisema kwamba ‘ulimwengu unajazwa na habari na watu wanakaribishwa kuingia katika mstari-kasi katika barabara kuu ya habari.’ Tatizo, kama vile Dakt. MacKay aonavyo, ni kwamba ongezeko kubwa la karibuni la habari na programu za mambo ya karibuni katika redio na televisheni, pamoja na ongezeko kubwa la habari za mifumo ya kompyuta, zimetokeza ulimwengu ambao wengi huitikia habari za vyombo vya habari ambazo kwa hakika ni sehemu tu ya kiwakilishi cha mambo ya hakika na matukio, si habari kamili.
Habari Ni Nini?
Neno la msingi la Kilatini informare lina maana ya kufanyiza mata, kama vile mfinyanzi hufanyiza udongo. Wasomaji wengi watakumbuka vizuri wakati, si zamani sana, ambapo habari ilikuwa ni orodha tu ya mambo ya hakika au data ikitueleza kinaganaga kama vile nani, wapi, nini, lini, au vipi. Hakukuwa na lugha au msamiati maalumu wa habari. Kile tu tulichohitaji kufanya ni kuomba kupata habari au kuitafuta sisi wenyewe.
Lakini miaka ya 1990 ikaja, na watu wamebuni maneno mapya mengi sana yanayohusiana na habari hivi kwamba maneno hayo yenyewe yaweza kutokeza vurugu. Leo ulimwengu umejawa na infomania—itikadi ya kwamba yule aliye na habari nyingi zaidi ana faida zaidi kuliko wengine wasioweza kuzipata kwa urahisi na kwamba habari, si njia ya kupata mambo tena bali yenyewe ndiyo jambo kuu.
Kichaa hiki kinaongezewa na furiko la mifumo ya uwasiliano, kama vile mashine za faksi, simu ya mkononi, na kompyuta za kibinafsi, zifikiriwazo na wengine kuwa ishara na utambulishi wa hii enzi ya habari. Ni kweli kwamba kufaa, kasi, na nguvu za kompyuta zimefanya habari ziwe zenye kufikika kuliko wakati mwingine wowote—hivi kwamba Nicholas Negroponte, wa Taasisi ya Tekinolojia ya Massachusetts, asema: “Kutumia kompyuta hakuhusu tena kompyuta. Kwahusu kuishi.” Tokeo ni kwamba habari na tekinolojia zinazoziwasilisha zimekuja kuthaminiwa kupita kiasi, katika visa fulani kustahiwa sana, na watu wengi sana katika sehemu zote za dunia. Habari za televisheni na programu za mambo ya karibuni zaidi huonwa kuwa kweli kabisa, huku mambo mengi yasiyo ya muhimu yakimwagwa kupitia vipindi vya mazungumzo ya televisheni na kumezwa na umma ambao mara nyingi si wenye kuchambua na ulio wenye kudanganyika upesi.
Kwa sababu enzi ya habari imebadili namna tunavyoishi na kufanya kazi, hiyo imefanya watu wengi leo wateseke kutokana na “hangaiko la habari” kwa njia moja au nyingine. Hangaiko la habari ni nini hasa? Waweza kujuaje ikiwa umeathiriwa? Je, kuna lolote uwezalo kufanya kulihusu?
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 3]
Tufe kwenye ukurasa wa 3, 5, na 10: Mountain High Maps® Copyright © 1997 Digital Wisdom, Inc.