Kusudi la Mungu Sasa Linafikia Utimizo Kamili
Kusudi la Mungu la kuiumba dunia lilikuwa ikaliwe na watu wenye furaha wenye kuishi chini ya hali za uadilifu. Ili kuendelea kuishi, ingewapasa wanadamu wazitii sheria za Mungu. Watu wawili wa kwanza hawakutii, wakawa watenda dhambi, wakahukumiwa kufa. Hiyo ikaleta dhambi na kifo kwa watoto wao wote. —Mwanzo 1:27, 28; 2:16, 17; 3:1-19; Warumi 5:12.
Mungu, ambaye jina lake ni Yehova, aliazimu kuyaondoa matokeo ya kutokutii na dhambi katika dunia. Baadaye aliitazama dunia akaona kati ya wanadamu mtu mwaminifu, Abramu, ambaye jina lake Yeye alibadili likawa Abrahamu. Mungu alimwahidi Abrahamu kwamba wazao wake wangekuwa taifa kubwa na kwamba kupitia taifa hilo Mungu angetoa mbegu ambayo kupitia hiyo jamaa zote za dunia zingejibariki zenyewe. —Mwanzo 12:1-3; 18:18, 19; 22:18; Zaburi 83:18; Waebrania 11:8-16.
Karibu na mwisho wa karne ya 16 K.W.K., wazao wa mjukuu wa Abrahamu yaani Yakobo, au Israeli, walikuwa wamekuwa makabila 12 wakiishi katika utumwa Misri. Yehova aliwakomboa Waisraeli hao kutoka Misri akawafanya kuwa taifa. Kupitia Musa kwenye Mlima Sinai aliwapa Torati kuwa katiba yao ya kitaifa. Yehova alikuwa Mfalme wao, Hakimu wao, na Mpaji-Sheria wao. Taifa hilo la Israeli likawa watu wateule wa Mungu, mashahidi wake, waliotengenezwa watimize kusudi lake. Kupitia wao Masihi angekuja, ambaye angesimamisha ufalme wa milele kwa faida ya watu wa mataifa yote. —Kutoka 19:5, 6; 1 Mambo ya Nyakati 17:7-14; 1 Wafalme 4:20, 25; Isaya 33:22; 43:10-12; Warumi 9:4, 5.
Baada ya karne 15, au karibu miaka 2,000 iliyopita, Mungu alimtuma Mwanaye mzaliwa wa pekee kutoka mbinguni kuja duniani, ili azaliwe na Mariamu, bikira kijana Myahudi. Yeye aliitwa jina Yesu na alitazamiwa kuurithi Ufalme ambao Mungu alimwahidi baba yake Daudi. Akiwa na umri wa miaka 30, Yesu alibatizwa na Yohana Mbatizaji akaanza kutangaza Ufalme wa Mungu. Kwa kuponya wagonjwa, alionyesha jinsi Ufalme huo unaokuja ungebariki wanadamu. Kupitia mifano, alieleza jambo ambalo wangetakiwa kufanya wote ambao wangetaka uzima wa milele. Kisha Yesu akauawa juu ya mti, uhai wake mkamilifu wa kibinadamu ukawa ukombozi kwa wanadamu. —Mathayo 1:18-24; 3:13-16; 4:17-23; 6:9, 10; sura 13; 20:28; Luka 1:26-37; 2:14; 4:43, 44; 8:1; Yohana 3:16; Matendo 10:37-39.
Yesu alikuwa ameeleza kwamba Ufalme wa Kimasihi ulitazamiwa kusimamishwa wakati ujao uliokuwa mbali sana, kwenye umalizio wa mfumo wa mambo. Wakati huo yeye angekuwapo bila kuonekana katika mbingu akiwa Mfalme anayetawala na angejulisha kuwapo kwake kwa kuelekeza fikira zake kwenye dunia. Matukio ya ulimwengu yanaonyesha kwamba tumekuwa tukiishi katika wakati huo tangu mwaka 1914. Kama Yesu alivyotabiri, habari njema za Ufalme zinahubiriwa katika dunia yote kuwa ushuhuda kwa mataifa yote. Matokeo ni kwamba watu kutoka mataifa yote wanakusanywa upande wa Ufalme wa Mungu. Hao watauokoka mwisho wa mfumo wa mambo uliopo na kupata uzima wa milele duniani chini ya Ufalme wa Kimasihi. —Mathayo, sura 24 na 25; Ufunuo 7:9-17.
Makanisa mengi yanadai kuwa yanafanya mapenzi ya Mungu leo. Lakini wewe unaweza kulitambuaje kundi la Kikristo la kweli? Ni kwa kuyachunguza Maandiko juu ya kundi la Kikristo la karne ya kwanza kisha kwa kuona ni nani leo wanaofuata kiolezo kile kile.
• Ni sehemu gani ambayo Abrahamu na Israeli walikuwa nayo katika utimizo wa kusudi la Mungu?
• Yesu alitimiza nini kwa huduma yake na kifo chake?
• Ni matukio gani yaliyotabiriwa kutia alama ya wakati wetu wa sasa?