Ni Jambo Gani Limewapata Vijana Wetu?
Wameitwa “kizazi kilichopotea,” “kizazi kilichonyang’anywa haki zake,” “kizazi chenye kung’ang’ania sana mambo yake,” “kizazi chenye kuahirisha-ahirisha mambo” na “vitoto visivyo na nyuma wala mbele.” Hao ni kina nani? Ni matineja wa leo. Wanafanya nini hata wastahili kupewa majina hayo, na kwa sababu gani?
NI JAMBO la kawaida kwa vijana kutenda mambo kwa njia isiyoeleweka na wazee wao. Muda wote wa historia imekuwa hivyo. Lakini vijana wa leo wanaelekea kuwa tofauti na vijana wa zamani. Watu wazima wanalalamika kwamba ubora wa mambo, kanuni za juu, matazamio mema na tumaini, ambazo ni sifa zinazoshirikishwa na vijana kwa kawaida, zimemalizika kabisa katika matineja wengi. Inaonekana ni kama wameacha kuwa na imani katika wakati ujao.
Lakini je! hilo ni jambo la kushangaza? Ni watu wazima wangapi walio na imani katika wakati ujao? Ni mtu gani angeweza kuwa na tumaini hakika, kwa sababu ya mashaka yanayosababishwa na infuleshoni, mashindano ya kutengeneza silaha za nyukilia, mweneo wenye uharibifu wa uchafu katika hewa, maji, ardhi na kadhalika, ongezeko linalozidi kuonekana wazi la watu kuwa washupavu katika siasa za ulimwengu na ongezeko kubwa ajabu la njaa ulimwenguni, la uhalifu na tabia chafu za namna zote? Labda hali ya kuutumaini huu mfumo wa mambo imekwisha kabisa katika wengi wetu, kwa hiyo je! tunaweza kuwalaumu vijana?
Saa Mark Oliphant, mtaalamu mwenye kuchunguza nguvu za nyukilia, alisema hivi: “Vijana si wapumbavu. Wanahisi uovu ulio katika hali ya hewa hata kama hawaelewi sababu ya mambo kuwa hivyo. Wanachukizwa na wakati ujao wao wenye mashaka ya kiuchumi na matatizo ambayo kizazi cha sasa kinawaletea. Wanajisikia kwamba elimu yao haihusiani na mahitaji yao, kwa maana haiwapi uhakikisho kamili wa cho chote, wala kazi wala utamaduni wenye kuwatosheleza.” Halafu, akionyesha ukosefu wake mwenyewe wa kuwa na imani katika wakati ujao, yeye akaonya hivi: “Inazidi kuwa wazi kwamba viwango vya ubora wa kibinadamu visipoinuliwa vipite vile vya kibiashara, ustaarabu kama tuujuavyo unaweza kuangamizwa na elimu ile ile ambayo ndiyo iliyoutokeza.”
Ndiyo, ikiwa inakuwa lazima matineja (vijana) wa leo waishi kulingana na wakati ujao ambao watu wazima wanawafanyizia, hali yao si ya kutamanika. Basi wao wanatendaje kwa sababu hiyo?
Vijana Wanatenda Kivyao Pia
Wengine wanatenda kwa njia zinazopita kiasi kujiondoa kabisa katika mfumo wenyewe. Wanajitia katika madhehebu kidini zinazofanya mambo ya kiajabu, wanakuwa mahipi (wenye kuchoshwa na maisha na kuishi watakavyo). Au wanakimbilia matumizi mabaya ya dawa za kulevya na unywaji mwingi wa pombe. Fujo za hivi majuzi zilizosababisha uharibifu mkubwa wenye kuletwa na vijana katika Ujeremani, Netherlands, Uswisi na Uingereza zilitoa ushuhuda zaidi wa kwamba vijana hawana hali ya kutosheka. Wenye kuleta msiba mkubwa zaidi ni wale wanaojiua ili waepuke mikazo ya siku hizi au mashaka ya wakati ujao. Katika United States (Amerika) ripoti fulani zinafanya tendo la kujiua liwe ndilo kisababishi cha pili chenye kueneza zaidi vifo kati ya matineja.
Vijana wengine wanasitawisha falsafa ya kutaka kujipatia vitu sasa hivi tuu, si kesho. “Vijana katika shule yetu,” alisema kijana wa miaka 15 katika Australia, “wanasema hawadhani mfumo huu utaendelea kuwapo kwa muda wa miaka 10 inayokuja. . . . Lo lote utakalo kufanya maishani, afadhali ulifanye upesi.” Jambo hilo linafanya wengine waahirishe mambo waliyoahidi kutimiza, wakatae kuwa na watoto au hata kuoa au kuolewa na hivyo waepuke ‘kunaswa katika mtego’ wa kiuchumi na “kupoteza uhuru wao.” Wanadai wawe na wakati wa kujifanyia ‘ukuzi wa kibinafsi,’ wapate raha zaidi na kuepuka mtindo wo wote wa maisha ya kujiwekea miradi ya kutimizwa muda mrefu unaokuja.
Halafu iko ile njia inayotumiwa na wanafunzi waliohojiwa kwenye Chuo Kikuu cha Oxford katika Uingereza. Wao walikiri kwamba hawayaoni mambo kama yalivyo hasa. Wao wanaona ufisadi katika mifumo yote—ya kibepari, ya Kikomunisti na ya kiujamaa. Kwa kuwa hawana njia iliyo bora, wanaamua kiupuzi kujipatia faida nyingi kama wawezavyo kutokana na mfumo wanaoishi ndani yake. Kwa kuwa huwezi kuubadili ulimwengu, ni afadhali uutumie ulimwengu wenyewe.’ Hiyo ndiyo nia yao.
“Mwaka wa 1950,” anasema Graham Turner mwandikaji wa habari fupi za magazetini, “wakati nilipokwenda huko Oxford, kulikuwako Imani nyingi sana . . . sasa . . . Oxford ni ua wa makaburi yenye ndoto zilizokosa kutimia na yenye waungu walioshindwa kutimiza miradi yao. Mahali ambapo, miaka mitano tu iliyopita, ilionekana kwamba jambo lo lote lingewezekana, sasa hata watu wanaotazamia mema wakati ujao zaidi ya wenzao wanatarajia kwamba ubora wa mambo utapungua.”
Je! Kuna Lo Lote Linaloweza Kufanywa?
Je! wewe unaweza kuelewa sababu gani vijana wengi sana wanatenda mambo kama “kizazi kilichopotea”? Ikiwa wewe ni mzazi mwenye watoto matineja, je! unajua namna ya kuwasaidia katika hizi nyakati zenye magumu? Labda wewe mwenyewe ni tineja. Ikiwa ndivyo, je! umepata njia ya kuishi katika mfumo wa mambo unaoendelea kubomoka-bomoka bila ya kukubali uwe na maoni ya kupuza mambo kwa sababu sasa umegundua ukweli wa matatizo yanayoendelea? Je! kuna nafasi yo yote ya kuona mambo namna yalivyo hasa na kuwa na tumaini? Gazeti litakalofuata linaweza kukusaidia ujibu maulizo hayo.
[Sanduku katika ukurasa wa 23]
Maoni na Kanuni za Wengi Leo
William Shannon mwandikaji wa habari fupi za magazetini aliandika juu ya maoni na kanuni ambazo ulimwengu unawatia vijana moyo wawe navyo, na matokeo yake:
“Maoni Mapya ya Kilimwengu yalitia ndani kujulisha watoto katika umri mdogo sana namna ya kuvuta bangi, dawa kali-kali za kulevya, pombe na kufanya ngono. . . Wasichana wa miaka 13 na 14 wanaokataa kufanya ngono wanalaumiwa kuwa ‘baridi-baridi.’ Wavulana wa umri uo huo wanaokataa kujaribu bangi au pombe wanadhihakiwa kuwa waoga. . . .
“Matokeo maovu yake yanaweza kuonekana leo katika takwimu za matukio mengi sana ya wenye kujiua, na sasa kujiua ndiyo namba mbili kati ya mambo yenye kusababisha zaidi kifo kati ya watu wa umri wa miaka 13 mpaka 24 na jambo hili linatukia mara mbili ya lilivyokuwa likitukia mwongo mmoja wa miaka iliyopita. Matokeo hayo maovu yanaweza kuonekana pia katika ongezeko kubwa sana la magonjwa ya kisonono na kaswende, mazoea ya kutumia dawa za kulevya, na matumizi ya pombe kati ya vijana.”—The Detroit Free Press.