Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w86 12/1 kur. 3-7
  • Uhuru wa Kidini Washambuliwa Katika Ugiriki

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Uhuru wa Kidini Washambuliwa Katika Ugiriki
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kuharibu Uhuru na Sifa
  • Mashambulizi na Kukamatwa
  • Akili ya Zile Zamani Zenye Giza
  • Je! ni Tengenezo la “Kisiri”?
  • Walio Wakristo ni Nani?
  • Je! Wao ni “Wapinga Kristo”?
  • Je! ‘Wanaendeleza Utawala wa Kiyahudi Duniani’?
  • Mafundisho Yasiyo ya Kibiblia
  • Unga Mkono Demokrasi Katika Ugiriki
  • Kanisa Othodoksi la Kigiriki—Dini Iliyogawanyika
    Amkeni!—1996
  • Mashahidi wa Yehova Watetewa Katika Ugiriki
    Amkeni!—1997
  • “Vitu vya Kuchukiwa na Mataifa Yote”
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Habari Njema za Ufalme Zitahubiriwa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
w86 12/1 kur. 3-7

Uhuru wa Kidini Washambuliwa Katika Ugiriki

JE! WEWE unathamini uhuru? Watu walio wengi wanauthamini. Wanataka kuwa huru wawe na maoni tofauti juu ya mambo kama siasa, uchumi, na dini, wakiwa ndani ya mipaka ya sheria na utengemano, bila shaka. Kwa upande mwingine, kutesa mtu kwa sababu ya maoni yake kunaleta akilini lile Baraza la Kuhukumu Wazushi wa Kidini la karne ya kumi na tano.

Jambo hilo linahusianaje na Ugiriki, nchi yenye sura nzuri iliyo katika mashariki ya Mediterania? Katika taifa hilo, mna hali ya ajabu isiyopatana na uhuru wa kidemokrasi.

Kuharibu Uhuru na Sifa

Ugiriki umeitwa kwa muda mrefu “mahali ilipozaliwa demokrasi.” Kwa kweli, katika 1975 Ugiriki ilitwaa Katiba ya kidemokrasi kuwapa watu uhakika kamili wa kuwa na mauhuru ambayo wanathamini. Na serikali ya Ugiriki inajitahidi kuyaunga mkono mahakikisho hayo.

Ijapokuwa hivyo, kuna wale katika Ugiriki wanaojaribu kuharibu mauhuru hayo na wanaoharibu vibaya sana sifa ya Ugiriki ulimwenguni pote. Watu hao wasio na utaratibu wamechochea na kuongoza makundi ya watu wenye ghasia mbaya sana washambulie raia Wagiriki wenye amani, wamekaza maafisa ili wawakamate na kuwafunga gerezani, na wamejitahidi kuwanyima mauhuru Wagiriki hao wanaoshika sheria. Jambo hilo limeendelea kwa miaka mingi sasa, ijapokuwa mahakikisho ya kikatiba.

Kwa sababu gani hayo yote yametukia? Ni nani wanaotendwa hayo? Ni nani wanaoyatenda hayo? Acha magazeti katika Ugiriki yakuambie wewe jambo fulani juu ya hali iliyoko.

Mashambulizi na Kukamatwa

Katiba ya Ugiriki inatangaza kwamba “Wagiriki watakuwa na haki ya kukusanyika kwa amani na bila kuwa na silaha.” Inatangaza pia kwamba “uhuru wa dhamiri ya kidini hauwezi kuharibiwa,” na inaongezea hivi: “Dini zote zinazojulikana zitakuwa huru na desturi zao za ibada zitafanywa bila kuzuiliwa na zitakuwa chini ya ulinzi wa sheria.”

Basi, siku ya Jumapili, Juni 15 ya mwaka huu, mamia ya Mashahidi wa Yehova walikutana kwa amani kwenye jumba moja la sinema katika Larisa, Ugiriki. Wao walikuwa kule ili kujifunza Biblia na kuzungumza njia za kufanyia maendeleo matumizi ya kanuni zayo za Kikristo katika maisha zao za kila siku.

Hata hivyo, angalia yaliyotukia. Gazeti la kule linaloitwa I Larisa liliripoti hivi: “Mamia ya watu, hasa washiriki wa matengenezo ya mji wetu [ya Kanisa la Orthodoksi la Ugiriki], yakiongozwa na mapadri kadha, walianza kukusanyika, na wakaanza kuonyesha hawakuwataka wale waliokuwa katika jumba la sinema​—Mashahidi wa Yehova zaidi ya 700, umati huo ulionekana kama ulikuwa karibu kuingia ndani la jumba hilo la sinema likasimamishe kusanyiko hilo.”

Jambo hilo liliendelea kwa karibu muda wa saa tatu. Hatimaye kundi hilo la watu wenye ghasia lilitawanywa na polisi wengi. Hasira ya mapadri wenye kuchochea kundi hilo la watu wenye ghasia ilijulishwa na gazeti la Larisa Eleftheria lilipotaja maneno haya ya padri wa Orthodoksi ya Ugiriki: “Safari ile nyingine meya atakapowapa [Mashahidi] jumba la sinema, sisi tutachukua makolego yetu na kuvunja-vunja kila kitu!” Na askofu mmoja alitaja hadharani kwamba alivikubali vitendo vya kundi la watu hao wenye ghasia.

Katika gazeti la Larisa I Alithia, mwandikaji Sarantos Vounatsos alionyesha ghadhabu yake juu ya kitendo hicho cha mapadri. Yeye alisema kwamba hali ya akili ya kundi hilo la watu wenye ghasia ilikuwa kama ile ya umati wa watu waliopiga makelele wakitaka Yesu auawe, wakipaza sauti: “Acha atundikwe!” Juu ya kundi la watu wenye ghasia katika Larisa, yeye aliandika hivi: “‘Kiongozi’ wao alikuwa [padri] mwenye makelele mengi sana! Yeye alitoa vitisho, akakufuru, akahubiri kwa njia ya kujionyesha, na mahali pamoja . . . akawapa wote waliokuwa ndani ilani ya dakika tano waondoke katika jumba la sinema . . . ‘ama sivyo tutaingia na kuvunja-vunja vichwa vyao.’”

Makala hiyo ya gazeti ilimwelekezea padri huyo maneno na kusema hivi: “Je! wewe ungetaka kujitwika mwenyewe vitendo vya mafarisayo? Haya basi, jihadhari, kwa sababu ukiendelea hutakuwa tena na rehema wala neema [ya Mungu], wala hata yetu sisi.”

Mateso hayo si kisa kimoja tu. Kumekuwa na mamia ya matendo ya kukamata waamini wasio wa dini ya Orthodoksi katika miaka michache iliyopita “kutia na Mashahidi wa Yehova 890 katika 1983 tu,” likasema gazeti The Wall Street Journal. Na mwaka huu, likaripoti gazeti la Athens Eleftherotipia, padri mmoja alishambulia Shahidi wa miaka 76, Vasili Kapeleri, na hatimaye Kapeleri akafa kutokana na jambo hilo.

Akili ya Zile Zamani Zenye Giza

Asili ya tatizo lenyewe ni mapadri wa Kanisa la Orthodoksi la Ugiriki. Kwa kuwa hiyo ndiyo dini kuu katika Ugiriki, mapadri wanahisi kwamba Mashahidi wa Yehova hawana haki ya kuwapo. Kwa hiyo wao wanajaribu kunyima Mashahidi mauhuru yao kwa kuwatendea ghasia, kuwashambulia, kuwafunga gerezani, na kukaza mahakama. Mapema mwaka huu, upinzani wa mapadri ulifanya mahakama ya Krete inyime Mashahidi msimamo unaokubaliwa kisheria.

Katika muhtasari wa kesi iliyotajwa mahakamani, Kanisa la Orthodoksi lilidai kwamba Mashahidi wa Yehova si “dini inayojulikana sana na yenye kutambuliwa,” nao “hawawezi kwa kufaa kuitwa Wakristo.” Kwa hiyo Kanisa hilo linashikilia kwamba Mashahidi hawapaswi kuwa na haki ya kupata majengo yao wenyewe ya ibada wala haki yo yote ya kuongea pamoja na wengine juu ya dini. Lakini akili ya namna hiyo ni ya zile zamani zenye giza. Inaonyesha ile roho ya Baraza la Kuhukumu Wazushi wa Kidini, wala si ile ya ‘mahali pa uzaliwa wa demokrasi.’

Mashahidi wa Yehova hawajaribu kunyima Kanisa la Orthodoksi haki ya kuwa na makanisa yalo na kuhubiri mambo ambayo linataka. Lakini katika kipindi hiki cha kisasa, je! Kanisa hilo linapasa kulazimisha kila mtu mwingineye yote afuate maoni yalo ya kidini? Na hasa katika jamii ya kidemokrasi ambamo mna namna nyingi mbalimbali za maoni? Jambo hilo halifanywi katika demokrasi nyingine ya Magharibi.

Katika sehemu zote za ulimwengu, Mashahidi wa Yehova wanatambuliwa kisheria kuwa dini ya Kikristo. Serikali zenye maoni yanayotofautiana ya kisiasa zinawapa wao haki za kisheria za kujenga mahali pa ibada na kuendelea kushika imani zao. Kwamba wao ni dini ya Kikristo ya mataifa yote inaweza kuonekana kutokana na uhakika wa kwamba wao wana wahudumu watendaji zaidi ya milioni tatu, huku wengine milioni tano wakihudhuria mikutano yao. Nao wamepangwa kitengenezo katika makundi 50,000 katika nchi zaidi ya mia mbili.

Kwa hiyo ni upuuzi mapadri kudai kwamba Mashahidi wa Yehova si ‘dini ya Kikristo inayojulikana.’ Mwelekeo wa mapadri unaleta aibu kwa sifa ya serikali ya Ugiriki iliyo ya kidemokrasi. Huo pia unawakebehi mamilioni ya Mashahidi ulimwenguni ambao ni Wakristo wenye kujitoa sana na wanaojua kwamba wengi wa waamini wenzao wamekwisha kuuawa kwa ajili ya imani yao.

Je! ni Tengenezo la “Kisiri”?

Jambo linalolingana na hilo kwa upuuzi ni dai la Kanisa hilo lililofanywa katika mahakama ya Krete kwamba Mashahidi wa Yehova ni tengenezo la “kisiri.” Kanisa hilo lilisema: “Imani zenyewe za Mashahidi wa Yehova hazijulikani kwa ukamili wala hazifunuliwi peupe . . . Wao hawana ‘nyumba za sala’ wala mahali pengine pa hadharani pa ibada ambapo mtu ye yote anaweza kuingia kwa uhuru. Wala desturi zao za ibada hazijapata kamwe kufunuliwa kwa ukamili.”

Hata mtu ye yote asiyefahamiana sana na Mashahidi wa Yehova anajua kwamba mashtaka hayo ni ya uwongo kabisa. Mafundisho yao yanapigwa chapa ili mtu ye yote ayachungue, na mikutano yao inakuwa wazi kwa watu wote wenye utaratibu, bila malipo. Kwa kweli, Mashahidi wanafundisha mamilioni ya watu Biblia katika nyumba zao katika sehemu zote za ulimwengu ili wawafahamishe imani hizo! Na afisi za matawi ya Mnara wa Mlinzi ulimwenguni pote zinakaribisha maelfu ya wageni kila juma.

Lakini hapa pana kinyume cha maneno. Kwa sababu gani Mashahidi katika Ugiriki hawawezi kukutana katika “nyumba za sala”? Kwa sababu wamenyimwa haki za kuzijenga! Kwa kuwa wao wamenyimwa majumba hayo, wanalazimika kukutana katika nyumba za faragha. Na ndipo Kanisa linasema kwamba wao wanafanya mikutano ya siri ati! Hata hivyo, katika sehemu zote za ulimwengu Mashahidi wa Yehova wamejenga maelfu ya majengo makubwa kwa ajii ya ibada. Lakini hawawezi kufanya hivyo katika Ugiriki.

Hivyo, wewe unaweza kuelewa kwa njia nzuri zaidi sababu inayofanya madai ya Kanisa yawe, kama vile John Manoledakis, Profesa wa Sheria za Adhabu kwenye Chuo Kikuu cha Thesalonike katika Ugiriki, alivyoeleza, “si ya kujipendekeza hata kidogo kwa madhumuni yaliyokusudiwa ya Kanisa [Orthodoksi la Ugiriki] wala kwa ufahamu wa kundi la kanisa hilo.”

Walio Wakristo ni Nani?

Katika karne ya kwanza, Yesu na wafuasi wake ndio walioteswa, wakatendwa ghasia, wakafungwa gerezani, na kuuawa. Watesi wao wakuu walikuwa nani? Viongozi wa kidini wa wakati huo.

Kwa mfano, angalia lililotukia wakati Yesu alipofufua Lazaro kutoka kwa wafu: “Wakuu wa makuhani na Mafarisayo . . . walifanya shauri la kumwua [Yesu].” Bila kuridhika na jambo hilo, “wakuu wa makuhani wakafanya shauri la kumwua Lazaro naye; maana kwa ajili yake wengi katika Wayahudi walijitenga, wakamwamini Yesu.” Na kwa kumaliza, “wakuu wa makuhuni na wazee [wa kidini] wakawashawishi makutano ili wamtake Baraba na kumwangamiza Yesu.”​—Yohana 11:47, 53; 12:10, 11; Mathayo 27:20.

Si ajabu kwamba Yesu aliwaambia wao hivi: “Ole wenu, waandishi na Mafarisayo, wanafiki! kwa kuwa mmefanana na makaburi yaliyopakwa chokaa, nayo kwa nje yaonekana kuwa mazuri, bali ndani yamejaa mifupa ya wafu, na uchafu wote. Vivyo hivyo ninyi nanyi, kwa nje mwaonekana na watu kuwa wenye haki, bali ndani mmejaa unafiki na maasi.” (Mathayo 23:27, 28) Pia, mara nyingi viongozi wa kidini walichochea wengine dhidi ya wafuasi wa Yesu.

Yesu hakuagiza Wakristo mahali po pote watese, wafunge gerezani, washambulie, wala wafanye ghasia dhidi ya wale waliokataa kukubaliana nao. Hivyo, katika karne ya kwanza Wakristo walio wa kweli ndio walioteswa wala wao hawakuwa ndio watesi. Watesi walikuwa ni viongozi wa kidini na wale waliochochewa nao. Ndivyo ilivyo leo katika Ugiriki.

Je! Wao ni “Wapinga Kristo”?

Kanisa Orthodoksi la Ugiriki lilidai hivi pia: “Si kwamba tu Mashahidi wa Yehova hawawezi kwa kufaa kuitwa Wakristo, ndiyo kusema, wafuasi Wakristo, bali kwa kinyume, wao ni . . . wapinga Kristo.”

Biblia inasema nini juu ya “mpinga Kristo”? Kwenye 1 Yohana 2:22 inasemwa hivi: “Ni nani aliye mwongo ila yeye akanaye ya kuwa Yesu ni Kristo? Huyo ndiye mpinga Kristo, yeye amkanaye Baba na Mwana.”

Hivyo, uhakika ulio wazi wa Neno la Mungu lililoongozwa na roho yake ni kwamba mpinga Kristo hakubali Yesu. Lakini Mashahidi wa Yehova wanamkubali! Wao wanaamini Yesu kwa bidii nyingi ya moyoni na kufuata mafundisho yake! Kwa kweli, hakuna mtu anayeweza kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova bila kukubali Yesu kuwa Mwana wa Mungu aliye wa kimungu, aliyeshuka chini kutoka mbinguni, akatundikwa mtini na kufufuliwa, na kurudi mbinguni.

Kwa hiyo mtu ye yote anayesema kwamba Mashahidi wa Yehova ni “wapinga Kristo” amepashwa sana habari zisizo za kweli, amepofushwa na maoni ya ubaguzi, au ana makusudio maovu.

Je! ‘Wanaendeleza Utawala wa Kiyahudi Duniani’?

Dai jingine linaloshikiliwa na Kanisa Orthodoksi ni kwamba Mashahidi wa Yehova wanaendeleza utawala wa Kiyahudi duniani. Kanisa hilo linatangaza hivi: “Kusudi lao halisi linalofichwa lisionekane wazi, ambalo linawekwa siri kabisa lisijulikane na walio wengi wa wenye kulifuata, ni kusimamisha ‘Ufalme wa Kiyahudi wa Kitheokrasi Ulimwenguni Pote’ kituo chao kikuu cha shughuli kikiwa katika Yerusalemu.”

Waulize mamilioni ya Mashahidi kama wao wanaamini hivyo! Hakuna hata mmoja wao anayeamini hivyo. Ingawa wakati mmoja wengine walifikiri kwamba unabii fulani-fulani huenda ukawa ulihusu Palestina halisi katika karne hii, maoni hayo yaliachiliwa mbali zaidi ya miaka 50 iliyopita!

Andiko la Mithali 4:18 linasema kwamba ‘njia ya wenye haki ni kama nuru ing’aayo, ikizidi kung’aa.’ Nuru hiyo ya maarifa yenye kuongezeka, inayotiwa nguvu na utimizo wa unabii wa Biblia, inaonyesha waziwazi kwamba Jamhuri ya Israeli ya kisasa haitamkubali kamwe Yesu Kristo kuwa ndiye Masihi. Hivyo, kusema kwamba Mashahidi hao Wakristo wanaendeleza ufalme wa Kiyahudi duniani wenye kituo kikuu katika Yerusalemu ni upuzi mwingine. Badala ya hivyo, wao wanaendeleza utawala wa kimbingu wa Ufalme wa Mungu, kama vile Yesu alivyofundisha.​—Mathayo 4:17; 6:10.

Mafundisho Yasiyo ya Kibiblia

Kati ya mambo yaliyotumiwa na viongozi wa kidini kuchochea wengine dhidi ya Mashahidi wa Yehova ni uhakika wa kwamba Mashahidi hawakubali mafundisho fulani ya Kanisa. La kwanza kabisa kati ya haya ni lile la Utatu. Lakini kwa sababu gani kutoyakubali kuwe na uhusiano wo wote na matumizi ya demokrasi katika Ugiriki? Kwa sababu gani iwe lazima kila mtu aamini Utatu ili afurahie uhuru wa mambo ya kiraia huko?

Mashahidi wa Yehova hawaukatai uungu wa Yesu. Wao wanakubali yale ambayo Yohana 1:1 husema juu yake, kwamba yeye ni “mungu.” (NW) Ijapokuwa hivyo, Kanisa linasema kwamba Yesu si “mungu” tu bali kwamba yeye ndiye Mungu mwenye nguvu zote, aliye sehemu ya watu (nafsi) watatu ambao wote pamoja wamekuwapo kwa umilele, wote pamoja wanalingana katika uwezo.

Biblia, Neno la Mungu lililoongozwa kwa roho yake, halifundishi hivyo. Badala ya hivyo, linasema waziwazi hivi: “Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee.” (Yohana 3:16) Hakuna wakati wo wote Yesu alipodai kuwa Mungu mwenye nguvu zote. Yeye alisema ndiye “Mwana pekee wa Mungu.” Mtu akiyasoma Maandiko bila upendeleo atathibitishiwa hivyo.​—Yohana 3:18; 10:34-36.

Mara nyingi Yesu alisema: “Mwana hawezi kutenda neno mwenyewe ila lile ambalo amwona Baba analitenda.” “Mimi sikushuka kutoka mbinguni ili niyafanye mapenzi yangu, bali mapenzi yake aliyenipeleka.” “Mafunzo yangu si yangu mimi, ila ni yake yeye aliyenipeleka.” “Baba ni mkuu kuliko mimi.” Na Neno la Mungu linaongeza hivi: “Mwana mwenyewe naye atatiishwa chini yake [Mungu].”​—Yohana 5:19; 6:38; 7:16; 14:28; 1 Wakorintho 15:28.

Hivyo Utatu haupatani na Maandiko. Basi, ulitoka wapi? Ulichaguliwa ufuatwe kwenye Baraza la Nisea katika 325 W.K. wakati waasi-imani walipotunga wazo la kipagani lililokuwa limetoka katika Misri ya kale na Babuloni. Ni kama vile mwanahistoria Will Durant alivyotoa maoni katika kichapo The Story of Civilization: Part III: “Ukristo haukuharibu upagani; ulichagua kuufuata . . . Kutoka Misri yakaja mawazo ya utatu wa kimungu.” Na The New Encyclopcedia Britannica kinasema hivi: Wala neno Utatu wala fundisho hilo linalosemwa waziwazi sana halionekani katika Agano Jipya . . . Fundisho hilo lilisitawi pole kwa pole kwa muda wa karne kadha na kupitia mabishano mengi.”

Ijapokuwa hivyo, ikiwa Kanisa Orthodoksi linataka kuamini Utatu, lina haki ya kufanya hivyo. Lakini halina haki katika nchi ya kidemokrasi kutesa Mashahidi wa Yehova, kufanya uchochezi watendwe ghasia na kukamatwa na kunyimwa uhuru wa mambo yao kwa sababu wao hawauamini Utatu.

Unga Mkono Demokrasi Katika Ugiriki

Katiba ya Ugiriki iko wazi: “Uhuru wa dhamiri ya kidini hauwezi kuharibiwa. . . . Dini zote zinazojulikana zitakuwa huru na desturi zao za ibada zitafanywa bila kuzuiliwa na zitakuwa chini ya ulinzi wa sheria.”

Mashahidi wa Yehova, wanaojulikana sana na waliopewa utambuzi wa kisheria kati ya mataifa yote, wanaunga mkono kanuni hizo za kidemokrasi. Wao wanataka Ugiriki, pia, uziunge mkono, wala usiache kanisa lo lote lilazimishe wengine wafuate akili yalo ya Baraza la Kuhukumu Wazushi wa Kidini kwa kutesa wale wasiokubaliana na maoni yalo.

Viongozi wa kidini wa Kanisa Orthodoksi la Ugiriki ingewafaa watii shauri la mwalimu wa sheria wa karne ya kwanza, Gamalieli. Kwa viongozi wa kidini waliokuwa wakitesa wafuasi wa Kristo, yeye alisema: “Nawaambia, Jiepusheni na watu hawa, waacheni; kwa kuwa shauri hili au kazi hii ikiwa imetoka kwa binadamu, itavunjwa, lakini ikiwa imetoka kwa Mungu hamwezi kuivunja; msije mkaonekana kuwa mnapigana na Mungu.”​—Matendo 5:34-39.

Katika pindi iyo hiyo, wafuasi Wakristo wa Yesu Kristo walisema hivi: “Ni lazima sisi tutii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.” Hivyo ndivyo pia Mashahidi Wakristo wa Yehova leo wanavyoona mambo. Hivyo ndivyo wao watakavyoendelea kufanya katika Ugiriki hata kama viongozi wa kidini watadai nini.​—Matendo 5:29, NW.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Petro na mitume wale wengine waliwaambia viongozi wa kidini wa siku zao hivi: “Ni lazima sisi tutii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki